Kuchapisha Vitabu vya Biblia Ili Kumsifu Mungu
Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kwa kuhubiri kwao Ufalme wa Mungu kupitia ukurasa ulioandikwa. Tangu mwaka 1920 Watch Tower Society imetumia wafanya kazi wenye kujitolea kutoka kati ya Mashahidi wenyewe ili wafanyize magazeti na vitabu vya kueneza. Hilo limefanywa ili kuhakikisha ufanyizwaji wenye kutegemeka wa vitabu kwa gharama ndogo zaidi iwezekanavyo.
Kwa miaka kama 60, Sosaiti imesitawisha na kupanua ufanyizwaji wayo wa vitabu vya Biblia, kwanza katika Brooklyn kisha katika nchi nyingine. Kazi yote hiyo imefanywa na jamii yenye kuongezeka ya wenye kujitolea.
Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1970 njia za kikawaida za kutayarisha na kuchapa maandishi zilikuwa zikiendelea kuondolewa kwa kupendelea utayarishaji wa kutumia kompyuta, kupanga chapa kwa namna ya kutumia nuru, na uchapaji wa ofseti. Kulikuwa na tatizo la kwamba vifaa vya kibiashara vipatikanavyo vingeweza kushughulikia lugha chache tu. Hata hivyo, Sosaiti ilikuwa tayari inafanyiza vitabu katika lugha karibu 160, na kulikuwako uhitaji wa zaidi.
Hivyo wenye kujitolea waliitwa waje wasitawishe mfumo wa kielektroni wa kupanga chapa katika lugha nyingi. Matokeo yalikuwa yenye kufurahisha. Kulikuwa na mafanikio yaliyohitajiwa ya kiufundi, na mfumo uitwao MEPS, wenye kuingiza maandishi, kutunga, na kupanga chapa, ulisitawishwa. Mfumo huo unaweza kushughulika na lugha karibu 200. Nyingine zaidi zaweza kuongezwa.
Leo uingizaji wa maandishi katika MEPS na vifaa vya chapa, vilivyofanyizwa na Mashahidi wa Yehova, unatumiwa katika nchi 25, na nyingine zinafanyiwa mpango. Wafanya kazi wa kujitolea kutoka nchi hizo wamezoezwa ili waendeshe na kudumisha vifaa hivyo. Sasa Sosaiti inafanyiza magazeti katika lugha zaidi ya 100 katika nchi 36, na katika 5 za nchi hizo vitabu vikubwa na Biblia zinafanyizwa pia.
Ili kufanya kazi hiyo, kunataka watu—waandikaji, watafsiri, wasahihishaji, wachapaji, wajalidi vitabu, na wafanya kazi wa kusafirisha vitabu. Ni lazima wengine washughulike na uandikaji wa barua za kwenda kwenye makundi. Wengine wanatayarisha vyakula, wanasafisha nyumba, wanafua nguo na kuzipiga pasi, na kadhalika. Kazi yote hiyo inafanywa na wafanya kazi wa kujitolea ambao wamejitoa wenyewe katika nchi mbalimbali. Kuzunguka ulimwengu wakati wa mwaka 1985, kulikuwako wafanya kazi wa kujitolea 8,438 wenye kutumikia katika afisi mbalimbali, viwanda, makao, na mashamba mbalimbali.
Watu hao ni akina nani? Ni wanaume na wanawake, waseja na waliofunga ndoa, vijana kwa wazee, wote wakiwa Mashahidi wa Yehova walio wakfu. Wengine wamekuwa katika kazi hii kwa miaka 40, 50, na hata 60. Wanatumia wastani wa angalau saa 44 kila juma wakitimiza migawo yao ya kazi, wakifanya hata wakati wa ziada inapohitajiwa. Nyakati za jioni na za mwisho wa juma zinatumiwa kwenye kuhubiri habari njema nyumba kwa nyumba, na kwenye utendaji mwingine wa kundi.
Kuzunguka ulimwengu wafanya kazi hao wanapewa makao ya kiasi na vyakula kwenye nyumba mojapo za Sosaiti ziitwazo Makao ya Betheli. Kwa kuongeza wanapokea alawansi kidogo ili walipie nauli za kwenda kwenye huduma yao na kiasi kidogo cha mahitaji ya kibinafsi.
Tangu mwaka 1920, wafanya kazi hao wa kujitolea wamefanyiza Biblia, vitabu, magazeti, na vikaratasi zaidi ya bilioni tisa katika lugha karibu 200 vipate kugawanywa ulimwenguni pote. Sasa wanatimiza sehemu yao ili habari njema za milele ziweze kutangazwa kama injili kwa kila taifa na kabila na lugha na jamaa. —Ufunuo 14:6, 7.
• Ni shughuli gani za uchapaji ambazo Watch Tower Society inazo, na kwa sababu gani?
• Ni nani wanaofanya kazi yote hiyo, na wanaishije?
[Picha katika ukurasa wa 24]
Wenye kujitolea wakifanya kazi inayohusiana na ufanyizaji wa vitabu vya Biblia kwenye kiwanda, makao, afisi, na shamba, katika Brooklyn na Wallkill, New York, U.S.A.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Wenye kujitolea wakifanya kazi mbalimbali ambazo kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja zinahusiana na ufanyizaji wa Biblia na vitabu vya Biblia
Hispania
Ujeremani
Finland
Kanada
Denmark
Uswedi
Afrika Kusini
Brazili
Uholanzi
Australia