Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 6/98 kur. 3-6
  • Kutunza Mali za Bwana-Mkubwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutunza Mali za Bwana-Mkubwa
  • Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Usimamizi-Nyumba wa Kikristo
  • “Msimamizi-Nyumba Mwaminifu, Mwenye Busara”
  • Badiliko Lakaziwa
  • Mahitaji Mbalimbali ya Kitengenezo
  • Mambo Fulani ya Kufikiria kwa Uangalifu
  • Kutunza Hizo Mali
  • Kutokeza Fasihi za Biblia Ili Zitumiwe Katika Huduma
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kuchapa Fasihi ya Biblia Tukiwa Chini ya Marufuku
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Wewe Ni Msimamizi-nyumba Mwenye Kutegemeka!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Je, Wajua?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—1998
km 6/98 kur. 3-6

Kutunza Mali za Bwana-Mkubwa

1 Katika nyakati za Biblia msimamizi-nyumba aliaminishwa wadhifa mkubwa. Abrahamu alimpa msimamizi-nyumba wake kazi ya kumtafutia mwana wake Isaka mke. (Mwa. 24:1-4) Kwa kweli, msimamizi-nyumba huyo alikuwa na daraka la kuhakikisha nasaba ya Abrahamu inaendelea. Lilikuwa daraka zito kama nini! Si ajabu mtume Paulo alisema: “Kitafutwacho katika wasimamizi-nyumba ni mtu kupatwa akiwa mwaminifu”!—1 Kor. 4:2.

Usimamizi-Nyumba wa Kikristo

2 Pande nyingine za huduma ya Kikristo zafafanuliwa katika Biblia kuwa usimamizi-nyumba. Kwa mfano, mtume Paulo aliwaambia Waefeso juu ya “usimamizi-nyumba wa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu ambao nilipewa kwa ajili yenu.” (Efe. 3:2; Kol. 1:25) Aliona utume wake wa kupelekea mataifa habari njema kuwa usimamizi-nyumba ambao alipaswa kuushughulikia kwa uaminifu. (Mdo. 9:15; 22:21) Mtume Petro aliandikia ndugu zake watiwa-mafuta hivi: “Iweni wakaribishaji-wageni nyinyi kwa nyinyi bila kuguna. Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba walio wema wa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu iliyoonyeshwa katika njia mbalimbali.” (1 Pet. 4:9, 10; Ebr. 13:16) Chochote ambacho Wakristo hao wa karne ya kwanza walikuwa nacho kwa njia ya kimwili kilitokana na fadhili isiyostahiliwa ya Yehova. Kwa hiyo, walikuwa wasimamizi-nyumba wa vitu hivyo na walihitaji kuvitumia kwa njia ya Kikristo.

3 Leo, Mashahidi wa Yehova wana maoni hayohayo kuhusu mambo. Wamejiweka wakfu kwa Yehova Mungu nao huona yote waliyo nayo, yaani, uhai wao, nguvu zao za kimwili, mali zao za kimwili kuwa matunda ya “fadhili isiyostahiliwa ya Mungu iliyoonyeshwa katika njia mbalimbali.” Wakiwa wasimamizi-nyumba wazuri, wanahisi wakiwa na hesabu ya kumtolea Yehova Mungu kwa sababu ya jinsi wanavyotumia vitu hivi. Kwa kuongezea, wamepewa ujuzi juu ya habari njema. Hii pia ni amana ambayo wanatamani kuitumia kwa njia nzuri zaidi iwezekanavyo: kutukuza jina la Yehova na kusaidia wengine wapate ujuzi kuhusu kweli.—Mt. 28:19, 20; 1 Tim. 2:3, 4; 2 Tim. 1:13, 14.

4 Mashahidi wa Yehova wanatimizaje madaraka yao wakiwa wasimamizi-nyumba? Ripoti ya kila mwaka yaonyesha kwamba mwaka jana peke yake, walitumia muda wa saa zaidi ya bilioni moja ulimwenguni pote, wakihubiri “habari njema ya ufalme” na wakaongoza mafunzo ya Biblia nyumbani zaidi ya 4,500,000 na watu wanaopendezwa. (Mt. 24:14) Uaminifu wao wakiwa wasimamizi-nyumba wa Yehova pia ulionyeshwa kwa michango mingi kuelekea kazi ya ulimwenguni pote na kwa kutegemeza Majumba ya Ufalme ya kwao, kwa ukaribishaji-wageni wao kwa waangalizi wasafirio na wengine, na kwa fadhili yao isiyo ya kawaida kwa wale wenye uhitaji—kama vile wahasiriwa wa mapambano ya kivita. Wakiwa kikundi, Wakristo wa kweli wanatunza vizuri mali za Bwana-Mkubwa.

“Msimamizi-Nyumba Mwaminifu, Mwenye Busara”

5 Usimamizi-nyumba huwa si kwa mtu mmoja-mmoja tu, bali pia katika tengenezo lote. Yesu aliliita kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lililo duniani “msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara.” (Luka 12:42) Daraka la huyo “msimamizi-nyumba mwaminifu” ni kuandaa “magawio ya chakula” na kuongoza katika kazi ya kuhubiri habari njema. (Ufu. 12:17) Kuhusiana na hilo, jamii ya msimamizi-nyumba mwaminifu, ikiwakilishwa na Baraza Linaloongoza, ina daraka la kupewa na Mungu la kusimamia vizuri “talanta” za kimwili na za kiroho. (Mt. 25:15) Kwa kupatana na kielelezo cha ‘msimamizi-nyumba mwaminifu,’ mashirika ya ofisi ya tawi mojamoja hujitahidi sana kutumia michango yote ya kifedha kwa njia ifaayo, ili kuendeleza masilahi za Ufalme. Michango hiyo yote inafanywa kwa kutumaini, na “msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara” ana daraka la kuhakikisha kwamba inatumiwa kwa kusudi lake na kwamba inatumiwa kwa hekima, kwa kupunguza gharama, na kwa matokeo mazuri.

6 Kielelezo cha kutumia michango vizuri chaonekana katika ukuzi wa kazi ya uchapaji ya Mashahidi wa Yehova katika karne ya 20. Ugawanyaji wa Biblia na vilevile fasihi za Biblia kama vile magazeti, vitabu, broshua, vijitabu, trakti, na Habari za Ufalme umetimiza daraka kubwa katika kueneza “habari njema” wakati wa hizi “siku za mwisho.” (Mr. 13:10; 2 Tim. 3:1) Nalo gazeti Mnara wa Mlinzi limekuwa chombo kikubwa mno katika kugawanya “chakula . . . kwa wakati ufaao” kwa “watumishi wa nyumbani wa Mungu” na waandamani wao, “umati mkubwa” wa “kondoo wengine.”—Mt. 24:45; Efe. 2:19; Ufu. 7:9; Yn. 10:16.

7 Mwanzoni, fasihi zote za Mashahidi wa Yehova zilitokezwa na wachapaji wa kibiashara. Lakini katika miaka ya 1920, iliamuliwa kwamba ingefaa kwa matokeo zaidi na kwa manufaa ya kiroho ikiwa watumishi wa Yehova wangejichapia wenyewe. Ikianza kwa njia ndogo katika 1920, kazi ya kuchapa ikakua hatua kwa hatua huko Brooklyn, New York, hadi ikawa kubwa mno. Kufikia 1967 vifaa hivyo vya uchapaji vilikuwa na ukubwa wa kutoshea eneo la majengo manne ya jiji. Pia uchapaji ulikuwa ukiendelea katika nchi nyinginezo, lakini katika nchi nyingi kati ya hizo, ulikuwa umekatizwa na Vita ya Ulimwengu ya Pili.

8 Hata iwe uchapaji uliongezeka kadiri gani Marekani, haukuwa mwingi vya kutosha kugawia ulimwengu wote. Kwa hiyo, miaka iliyofuata vita, utendaji wa uchapaji ulianzishwa au ulikuwa tayari ukiendelea katika nchi nyingi, kutia ndani Afrika Kusini, Denmark, Kanada, Ugiriki, Uingereza, Ujerumani Magharibi, na Uswisi. Kufikia miaka ya mapema ya 1970, Australia, Brazili, Finland, Ghana, Japani, Nigeria, na Filipino zilikuwa zimeongezwa kwenye orodha hiyo. Baadhi ya nchi hizi pia zilitokeza mabuku yaliyojalidiwa. Pia miaka ya mapema ya 1970, wamishonari wa Gileadi walifundishwa stadi za uchapaji na kutumwa katika baadhi ya nchi hizi ili kusaidia ndugu wa huko kazi ya uchapaji.

9 Miaka ya 1980, idadi ya nchi ambamo magazeti yalikuwa yakichapwa ilifikia kilele cha 51.a Hayo yalikuja kuwa matumizi mazuri kama nini ya mali ya Bwana-Mkubwa! Huo ulikuwa uthibitisho mkubwa kama nini wa ukuzi wa kazi ya Ufalme! Nao ulikuwa ushuhuda wenye nguvu kama nini wa tegemezo la ukarimu la mamilioni ya Mashahidi wa Yehova mmoja-mmoja ambao ‘walimheshimu Yehova kwa mali yao’! (Mit. 3:9) Hivyo, walijithibitisha wenyewe kuwa wasimamizi-nyumba waaminifu wa yale ambayo Yehova alikuwa amewabarikia katika njia mbalimbali.

Badiliko Lakaziwa

10 Miaka ya 1970 na miaka ya mapema ya 1980, maendeleo makubwa yalifanywa katika tekinolojia ya uchapaji, na Mashahidi wa Yehova walijitwalia mbinu mpya za uchapaji. Hapo awali, walikuwa wametumia mtindo wa kizamani wa matbaa ya kuchapa kama kupiga muhuri. Huo ulibadilika hatua kwa hatua walipoanza kujitwalia matbaa za kisasa za uchapaji. Tokeo ni kwamba, vichapo vyenye kupendeza vinatokezwa vikiwa na picha zenye rangi kamili, badala ya picha zenye rangi mbili (nyeusi na rangi nyingine) ambazo ziliwezekana katika matbaa ya zamani. Zaidi ya hilo, tekinolojia ya kompyuta ilibadili utaratibu wote wa kabla ya kuchapa (utayarishaji kwa ajili ya uchapaji). Mashahidi wa Yehova walisitawisha mfumo uitwao Multilanguage Electronic Phototypesetting System (MEPS), mfumo wa kompyuta ambao sasa hutegemeza uchapaji katika lugha zaidi ya 370 tofauti-tofauti. Hakuna programu za kibiashara zinazolingana na MEPS katika uwezo wake wa kutumika katika lugha nyingi hivyo.

11 Kwa msaada wa tekinolojia ya kompyuta ya MEPS na matumizi ya mavumbuzi kama vile mfumo wa kupeleka barua kupitia kompyuta, maendeleo mengine makubwa yalifanywa katika kuandaa chakula kwa wakati unaofaa. Hapo awali, kwa kutumia tekinolojia ya zamani, magazeti yasiyo ya lugha ya Kiingereza yalikuwa na habari ya miezi kadhaa au mwaka mzima baada ya Kiingereza. Sasa, Mnara wa Mlinzi hutokea wakati uleule katika lugha tofauti-tofauti 115, na Amkeni! katika lugha 62. Hilo lamaanisha kwamba ulimwenguni pote zaidi ya asilimia 95 ya wale wanaohudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma la Mashahidi wa Yehova, hujifunza habari ileile kwa wakati uleule. Hii ni baraka kama nini! Kwa kweli yalikuwa matumizi mazuri ya mali ya Bwana-Mkubwa kuingiza tekinolojia yote hiyo mpya!

Mahitaji Mbalimbali ya Kitengenezo

12 Mifumo hii mipya ilibadilisha mahitaji ya kitengenezo ulimwenguni pote ya utendaji wa kuchapa wa Mashahidi wa Yehova. Matbaa za web hufanya kazi haraka sana kuliko matbaa ya kuchapa kama kwa kupiga muhuri, lakini pia ni ghali sana. Mifumo ya kompyuta inayofanya kazi inayohusiana kama vile, uandishi, utafsiri, uchoraji, na upangaji wa chapa, huku ikiwa na uwezo mwingi kuliko ile mifumo ya zamani, ni ghali sana. Upesi ilionekana kwamba halikuwa jambo la kupunguza gharama kuchapa magazeti katika nchi 51 tofauti-tofauti. Kwa sababu hiyo, katika miaka ya 1990 “msimamizi-nyumba mwaminifu” alichunguza mambo tena. Uamuzi ulikuwa nini?

13 Uchunguzi ulionyesha kwamba ‘vitu vyenye thamani’ vilivyochangwa na Mashahidi wa Yehova na rafiki zao vingetumiwa vema zaidi kama kazi ya uchapaji ingeunganishwa. Kwa hiyo idadi ya ofisi za tawi zenye kuchapa ilipunguzwa. Ujerumani imechukua uchapaji wa magazeti na fasihi za nchi nyingi za Ulaya Mashariki na Magharibi, kutia ndani nchi kadhaa ambazo zimekuwa zikifanya uchapaji wao wenyewe. Italia huandaa magazeti na fasihi kwa ajili ya sehemu za Afrika na kusini-mashariki mwa Ulaya, kutia ndani Ugiriki na Albania. Katika Afrika, uchapaji wa magazeti hufanywa Nigeria na Afrika Kusini tu. Kuunganishwa hukohuko kulitokea ulimwenguni pote.

Mambo Fulani ya Kufikiria kwa Uangalifu

14 Kufikia Julai 1998, uchapaji wa magazeti utakomeshwa katika nchi kadhaa za Ulaya kutia na Austria, Denmark, Ufaransa, Ugiriki, Uholanzi, na Uswisi. Kazi ya uchapaji katika Ulaya itashughulikiwa na Finland, Hispania, Italia, Sweden, Uingereza, na Ujerumani. Katika njia hii, gharama zisizo za lazima zingeepukwa na michango ingetumiwa kwa njia bora kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Iliamuliwaje kwamba nchi kadhaa ziendelee kuwa sehemu za uchapaji na zipi ziache uchapaji? Kupatana na amri yake ya kutunza kwa hekima mali za Bwana-Mkubwa, “msimamizi-nyumba mwaminifu” alikadiria busara ya kuchapa katika kila sehemu.

15 Sababu kubwa ambayo uchapaji ulikomeshwa katika nchi kadhaa na kuunganishwa katika nyingine ilikuwa kufaa kwa hali. Katika nchi moja uchapaji wa fasihi za nchi nyingine ni jambo lenye kufaa zaidi na ni matumizi bora ya vifaa vilivyo ghali sana. Uchapaji sasa wafanywa mahali ambapo gharama ni za chini, vifaa vyapatikana, na vifaa vya upakizi ni vizuri. Hivyo mali za Bwana-Mkubwa zatumiwa vizuri. Bila shaka, kukomesha uchapaji katika nchi fulani hakumaanishi kwamba kazi ya kuhubiri humo itakoma. Bado kutakuwako wingi wa vichapo vilivyochapwa, na mamia ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova katika nchi hizo wataendelea kwa bidii kuambia jirani zao “habari njema ya amani.” (Efe. 2:17) Zaidi ya hilo, huku kurudia kupanga kumetokeza manufaa nyingine.

16 Ili kutaja manufaa moja, matbaa zilizo nyingi za kisasa kutoka Denmark, Ugiriki, Uholanzi, na Uswisi zilipelekwa Nigeria na Filipino. Wafanyakazi walio stadi kutoka nchi za Ulaya walikubali mwaliko wa kwenda pamoja na matbaa hizo ili kuwazoeza wale watakaofanya kazi nazo huko. Kwa sababu hiyo, nchi hizo sasa zinapata magazeti ya hali ya juu ambayo nchi nyingine zimekuwa nayo.

17 Fikiria manufaa nyingine: Gharama ya kuchapa magazeti sasa inachukuliwa na nchi chache ambamo uchapaji bado waendelea. Tokeo ni kwamba, katika nchi ambamo uchapaji umekomeshwa, mali sasa zapatikana kwa makusudi mengine, kama vile kujenga Majumba ya Ufalme na kusaidia kutunza mahitaji ya ndugu zetu katika nchi zilizo maskini zaidi. Hivyo, kutumia kwa uangalifu mali za Bwana-Mkubwa kwamaanisha kwamba maneno ya Paulo kwa Wakorintho yanaweza kutumiwa kwa matokeo zaidi kwa kiwango cha kimataifa: “Sikusudii iwe rahisi kwa wengine, lakini vigumu kwenu; bali kwamba kupitia usawazisho wa ziada yenu sasa hivi ipate kujazia upungufu wao . . . ili usawazisho upate kutukia.”—2 Kor. 8:13, 14.

18 Tokeo la kuunganishwa huku limekuwa kwamba, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni wameungana pamoja zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Hakuna shida yoyote Mashahidi katika Denmark wakichapiwa magazeti yao Ujerumani, ingawa walikuwa wakichapa yao. Wanashukuru kwa utumishi wa ndugu zao Wajerumani. Je, Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani wanaona uchungu kwa sababu michango yao inatumiwa kuandalia Denmark fasihi za Biblia—au Urusi, Ukrainia, na nchi nyingine? La hasha! Wanafurahi kujua kwamba michango ya ndugu zao katika nchi hizi yaweza kutumiwa kwa makusudi mengine ya lazima.

Kutunza Hizo Mali

19 Katika kila Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, kuna sanduku la michango lililotiwa alama “Michango ya Kazi ya Ufalme.” Michango isiyo ya kuombwa-ombwa iliyowekwa katika masanduku hayo inapatikana kwa matumizi wakati wowote inapohitajiwa. “Msimamizi-nyumba mwaminifu” na mashirika ya ofisi ya tawi mojamoja ndio waamuao jinsi ya kutumia michango hiyo. Kwa sababu hiyo, mahali ambapo sheria yaruhusu, fedha zilizowekwa katika sanduku la michango katika nchi fulani zaweza kutegemeza utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingine iliyo kilometa nyingi mbali na hiyo. Michango katika nchi fulani, imekuwa ikitumiwa kuandaa msaada wa dharura kwa waamini wanaoteseka kwa sababu ya vitu kama vimbunga, chamchela, matetemeko ya dunia, na vita vya wenyewe kwa wenyewe. Na michango hiyo yatumiwa kutegemeza wamishonari katika nchi zaidi ya 200.

20 Ikiwa kanuni ya ujumla, katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, mambo ya kifedha hutajwa mara moja tu kwa mwezi—na kwa dakika chache tu. Masahani ya michango hayapitishwi katika Majumba ya Ufalme au katika makusanyiko. Maombi ya fedha hayapelekewi watu. Watu wa kuchangisha fedha hawaajiriwi. Kwa kawaida, gazeti Mnara wa Mlinzi lina makala moja tu kwa mwaka likieleza jinsi wale wanaotaka kutoa michango kwa Watch Tower Bible and Tract Society ili kutegemeza kati ya ulimwenguni pote wanavyoweza kufanya hivyo. Kawaida mambo ya kifedha ya Sosaiti hayatajwi katika Amkeni! Basi je, kazi nyingi mno ya ulimwenguni pote ya kuhubiri habari njema, kujenga Majumba ya Ufalme ya lazima, kutunza wale walio katika utumishi wa wakati wote wa pekee, na kusaidia Wakristo walio na uhitaji imetimizwaje? Yehova amebariki watu wake katika njia ya ajabu kwa roho ya ukarimu. (2 Kor. 8:2) Twachukua fursa hii kushukuru wote ambao wamekuwa wakishiriki ‘kumheshimu Yehova kwa mali yao yenye thamani.’ Wanaweza kuwa na uhakika kwamba “msimamizi-nyumba mwaminifu” ataendelea kutunza mali za Bwana-Mkubwa. Na twasali kwamba Yehova aendelee kubariki mipango yote inayofanywa kwa ajili ya upanuzi wa kazi ya ulimwenguni pote.

[Maelezo ya Chini]

a Katika nchi saba kati ya hizi, uchapaji ulifanywa na makampuni ya kibiashara.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki