Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 7/1 kur. 26-30
  • Kuchapa Fasihi ya Biblia Tukiwa Chini ya Marufuku

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuchapa Fasihi ya Biblia Tukiwa Chini ya Marufuku
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Malezi ya Mapema
  • Mabadiliko Makubwa Maishani Mwetu
  • Kupata Tena Vifaa vya Kupigia Chapa
  • Kukabiliana na Ziara za Ghafula
  • Kutosheleza Uhitaji Wetu wa Karatasi
  • Sehemu ya Maana ya Wanawake
  • Migawo na Baraka Zaidi
  • Kutokeza Fasihi za Biblia Ili Zitumiwe Katika Huduma
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kutunza Mali za Bwana-Mkubwa
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • Uthibitisho wa Upendo, Imani, na Utii
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kutembelea Kiwanda cha Pekee cha Uchapishaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 7/1 kur. 26-30

Kuchapa Fasihi ya Biblia Tukiwa Chini ya Marufuku

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MALCOLM G. VALE

“Chapa kitabu Children.” Nilipokea agizo hilo lenye kushangaza kutoka kwa mwangalizi wa tawi wa Mashahidi wa Yehova katika Australia wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, muda mfupi baada ya kitabu hicho kutolewa kwenye mkusanyiko wa St. Louis, Missouri, U.S.A., katika Agosti 10, 1941. Kwa nini agizo hilo lilishangaza?

KAZI yetu ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku katika Januari 1941, kwa hiyo kuchapa hata vichapo vichache kungekuwa kazi ngumu. Isitoshe, Children kilikuwa kitabu chenye kurasa 384 na chenye picha zenye rangi kamili. Vifaa vyetu vya kupigia chapa vilihitaji kufanyiwa maendeleo, kulikuwa na upungufu wa karatasi, na wafanyakazi hawakuwa wamezoezwa kutengeneza vitabu vilivyojalidiwa.

Kabla ya kusimulia jinsi tulivyofanikiwa kuchapa tukiwa chini ya marufuku, acheni niwaambie jinsi nilivyokuja kutumikia kuhusiana na ofisi ya tawi ya Australia nikiwa mwangalizi wa utendaji wa kuchapa.

Malezi ya Mapema

Baba yangu alikuwa na biashara ya kuchapa katika jiji lenye kusitawi la Ballarat, Victoria, nilikozaliwa katika 1914. Kwa hiyo nilijifunza biashara ya kuchapa nikifanya kazi katika kiwanda cha Baba cha kupigia chapa. Nilihusika pia na utendaji wa Church of England, nikiimba katika kwaya ya kanisa na kupiga kengele za kanisa. Hata nilikuwa na taraja la kufundisha shule ya Jumapili, lakini hilo lilinitia wasiwasi.

Sababu ni kwamba nilikuwa na maswali mazito juu ya mafundisho fulani ya kanisa. Hayo yalitia ndani Utatu, moto wa helo, na kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, na hakuna aliyenipa majibu yenye kuridhisha. Pia nilitatanishwa kwamba mara kwa mara, mhudumu wetu alisema kwa hasira juu ya kikundi kidogo cha kidini kilichoitwa Mashahidi wa Yehova. Nilijiuliza kwa nini kikundi kidogo hivyo kingeweza kuhangaisha jiji la watu 40,000.

Jumapili moja, nilikuwa nikisimama nje ya kanisa baada ya mahubiri ya jioni wakati kikundi cha wasichana kutoka Kanisa la Methodist lililokuwa karibu walipopitia hapo. Nilianza urafiki na mmoja wao. Jina lake lilikuwa Lucy, na hatimaye alinialika nyumbani kwake kukutana na wazazi wake. Ebu wazia mshangao wangu nilipopata kujua kwamba mama yake, Vera Clogan, alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Tulikuwa na mazungumzo mengi machangamfu juu ya Biblia, na yale aliyosema yalikuwa na maana kwelikweli.

Baada ya muda mfupi, Lucy na mimi tukaoana, na kufikia 1939 tulikuwa tunaishi Melbourne, jiji kuu la Victoria. Ingawa Lucy alikuwa amekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, mimi sikuwa nimeamua bado. Hata hivyo, Vita ya Ulimwengu 2 ilipoanza katika mwezi wa Septemba wa mwaka huo, nilianza kufikiri kwa uzito juu ya yale niliyokuwa nimejifunza katika Maandiko. Kupigwa marufuku kwa kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Januari 1941 kwa kweli kulinisaidia nifanye uamuzi. Niliweka maisha yangu wakfu kwa Yehova Mungu nikabatizwa muda mfupi baadaye.

Mabadiliko Makubwa Maishani Mwetu

Wakati huo, tulikuwa tukikodi nyumba ya starehe katika Melbourne. Hata hivyo, upesi tulialikwa kuishi katika nyumba yenye Mashahidi wengine kadhaa. Tuliuza fanicha yetu yote ila fanicha ya chumba cha kulala tukahamia hayo yaliyoitwa makao ya mapainia. Niliendelea kufanya kazi nikiwa mchapishaji na hivyo nikaweza kuchangia gharama za kuendesha makao hayo. Waume wale wengine walifanya vivyo hivyo. Kwa hiyo, wake zetu, wangeweza kushiriki katika utendaji wa kuhubiri wakati wote, na sisi wanaume tulijiunga nao katika kazi ya kueneza evanjeli na kwenye mikutano ya Kikristo wakati wa jioni na kwenye miisho-juma.

Upesi baadaye, mke wangu na mimi tulipokea barua kutoka ofisi ya tawi ya Watch Tower Society ikitualika kwenda Sidni. Tuliuza fanicha ya chumba chetu cha kulala tukalipa madeni machache tuliyokuwa nayo, lakini ili kupata fedha za kulipia nauli yetu ya gari-moshi hadi Sidni, tulilazimika kuuza pete ya uchumba ya Lucy!

Kwa sababu ya vizuizi vya wakati wa vita na marufuku iliyowekwa karibuni, Biblia au fasihi ya Biblia visingeweza kuletwa nchini kutoka ng’ambo. Kwa sababu hiyo ofisi ya tawi ya Australia iliamua kuanzisha utendaji wa kuchapa wa kichinichini ili kuendeleza mtiririko wa chakula cha kiroho, na nilialikwa kusimamia kazi hiyo. Nilipendelewa kufanya kazi karibu na Mskochi mmoja, George Gibb, aliyetumikia katika kiwanda cha kupigia chapa cha tawi la Australia kwa miaka 60 hivi.a Huo ndio wakati nilipokea lile agizo: “Chapa kitabu Children.”

Kupata Tena Vifaa vya Kupigia Chapa

Tulikuwa na maono mengi yenye kusisimua, na nyakati nyingine yenye kuhofisha, katika miaka hiyo ya vita yenye matukio mengi. Kwa kielelezo, ili kuanza utendaji wetu wa kuchapa, tulihitaji vifaa. Vile vifaa tulivyokuwa tukivitumia kabla ya hapo ili kuchapa kidogo-kidogo katika miaka ya kabla ya vita vilikuwa vimetwaliwa na wenye mamlaka wa serikali, na sasa kile kiwanda kidogo cha kupigia chapa cha Sosaiti kilikuwa kimefungwa kwa ufunguo na kulindwa. Tungeweza kupataje vifaa hivyo na kuvipeleka hadi mahali palipofaa pa kupigia chapa kichinichini?

Walinzi wenye silaha, waliokuwa wakifanya kazi kwa zamu, walilinda makao ya Sosaiti muda wa saa 24 kwa siku. Hata hivyo, mojawapo kuta za nyuma ulipakana na njia ya reli ya upande ambayo haikutumiwa sana. Kwa hiyo usiku, kwa kutumia njia zilizokumbusha juu ya Ezekieli 12:5-7, baadhi ya wafanyakazi hodari wa Betheli waliingia kupitia ukuta huo kwa kuondoa baadhi ya matofali. Mara walipokuwa ndani, waliyarudisha matofali hayo ukutani ili kuepuka kugunduliwa. Kwa kufanya mashambulio hayo ya usiku kwa kipindi cha karibu majuma mawili, walibomoa kwa uangalifu matbaa ndogo, iitwayo Linotype, na mashine mengine machache. Kisha wakavipitisha nje visehemu-sehemu hivyo kimya-kimya, hata walinzi wakiwapo!

Hatimaye tulipata vifaa zaidi kutoka kwa vyanzo vingine, na upesi tukawa na utendaji wa kupigia chapa wa kichinichini uliokuwa ukiendelea kwa bidii nyingi katika mahali mbalimbali kotekote Sidni. Hivyo, tuliweza kuchapa na kujalidi si kitabu Children tu bali pia vile vitabu vikubwa The New World, “The Truth Shall Make You Free,” na The Kingdom Is At Hand, pamoja na Vitabu-Mwaka vya Mashahidi wa Yehova (Kiingereza) vya 1942, 1943, 1944, na 1945. Kuongezea hayo, wakati wa marufuku wa miaka hiyo ya vita, Mashahidi wa Yehova kotekote Australia hawakukosa kamwe toleo moja la Mnara wa Mlinzi. Hilo lilituhakikishia kwa njia ya kibinafsi sana kwamba mkono wa Yehova si mfupi kamwe.—Isaya 59:1.

Kukabiliana na Ziara za Ghafula

Katika kipindi cha ukaguzi mzito wa wakati wa vita, mashirika ya kibiashara ya kupigia chapa mara nyingi yalitembelewa kwa ghafula na maofisa wa serikali waliokagua yale yaliyokuwa yakipigwa chapa. Kwa hiyo, kiwanda chetu kimoja cha siri cha kupigia chapa kilikuwa na chombo cha kuonyea, kibonyeo kilichokuwa sakafuni kilichoweza kufikiwa kwa urahisi na mpokezi. Wakati mtu yeyote ambaye yeye hakuweza kumtambua au aliyemshuku kuwa ni mkaguzi angepanda ngazi, mpokezi angekifinya kibonyeo hicho.

Kibonyeo kilipofinywa, lilikuwa jambo la ajabu kuona akina ndugu wakiponyoka huku na huku kupitia madirisha! Wafanyakazi waliosajiliwa wakiwa waajiriwa walibaki kuzifunika upesi kurasa zozote za Mnara wa Mlinzi au fasihi nyingine ya Biblia zilizokuwa zimepigwa chapa. Ili kufanya hivyo, wangetumia kurasa zilizopigwa chapa zenye ukubwa uo huo za vichapo vingine vilivyokuwa vikitayarishwa kwa ajili ya wateja wa kibiashara.

Wakati wa ziara moja ya jinsi hiyo, wakaguzi wawili waliketi kwenye kurasa za vitabu vyenye michoro, zilizokuwa bado kwenye karatasi kubwa-kubwa, lakini chini yazo kulikuwa kurasa za magazeti Mnara wa Mlinzi zilizokuwa zimepigwa chapa usiku uliotangulia. Katika kiwanda kingine cha kupigia chapa katika sehemu nyingine ya jiji hilo, tulifanya uchapishaji wa kibiashara wakati wa mchana na kuchapa vichapo vya Mnara wa Mlinzi usiku na kwenye miisho-juma.

Kutosheleza Uhitaji Wetu wa Karatasi

Kupata karatasi za kupigia chapa lilikuwa tatizo kubwa. Hata hivyo, baadhi ya viwanda vikubwa vya kupigia chapa ambavyo havikuhitaji kiasi chavyo chote cha karatasi kwa sababu ya upungufu wa biashara wakati wa vita vilikuwa tayari kutuuzia kiasi chavyo cha ziada—bila shaka ikiwa kwa bei ya juu sana, sikuzote. Lakini kwenye pindi moja, tulipokea karatasi kutoka kwa chanzo kingine.

Meli ya kubebea mizigo iliyokuwa ikija Australia ilikuwa na mzigo mkubwa wa karatasi ya rangi ya kahawia, lakini meli hiyo iliharibika baharini na maji yakaiingia sehemu kubwa ya karatasi hiyo. Mzigo huo mzima ulitolewa kwa mnada, na kwa mshangao wetu ni sisi tu tuliotaka kuinunua. Hiyo ilituwezesha kuinunua kwa bei ya chini sana. Tuliikausha karatasi hiyo juani, hivyo tukaokoa sehemu kubwa yayo, kisha tukaikatakata katika kurasa zilizofaa matbaa yetu.

Tungeweza kutumiaje karatasi ya rangi ya kahawia? Tulifikiri ifaavyo, kwamba wenye kusoma vitabu vyenye picha wangefurahia bado kusoma vichapo vyao vikiwa kwenye karatasi yenye rangi. Hivyo, tulitumia karatasi nyeupe tuliyokuwa tumepewa kwa ajili ya vitabu hivyo vyenye picha ili kuchapa Mnara wa Mlinzi na habari nyingine ya Sosaiti.

Sehemu ya Maana ya Wanawake

Wakati wa miaka ya vita, wanawake wengi Wakristo katika Australia walijifunza utendaji wa kujalidi. Alasiri moja ya kiangazi yenye joto jingi, baadhi yao walikuwa wakifanya kazi peke yao katika gereji ndogo tuliyokuwa tumekodi katika barabara ya ndanindani katika kiunga kimoja cha Sidni. Kwa sababu za usalama, walifunga kila dirisha na mlango. Mikebe ya gundi ilitoa mvuke wenye joto, uliotoa harufu, na joto hilo lilikuwa jingi mno. Kwa hiyo walivua mavazi yao ya nje.

Kwa ghafula, mtu akabisha mlango. Dada hao Wakristo waliitikia wakiuliza huyo alikuwa nani, na ofisa mmoja wa wafanyakazi wa serikali akajibu. Alitoka kwenye idara iliyokuwa na mamlaka ya wakati wa vita ya kuwapeleka watu eneo lolote ambapo wafanyakazi walihitajiwa. Dada hao waliitikia kwa sauti kubwa kwamba hawakuweza kumruhusu aingie kwa sasa kwa sababu walikuwa wakifanya kazi wakiwa na nguo zao za ndani kwa sababu ya joto.

Ofisa huyo alibaki kimya kwa muda mfupi; kisha akasema kwa sauti kubwa kwamba alikuwa na mpango wa kufanya jambo jingine katika eneo hilo. Akasema kwamba angerudi siku ifuatayo ili kufanya ukaguzi wake. Mara iyo hiyo wanawake hao Wakristo walitupigia simu, tukapeleka lori usiku huo ili kuokota kila kitu ambacho kiwanda hicho cha kujalidi vichapo kilikuwa kikifanyia kazi, tukavihamisha hadi mahali pengine.

Wengi wa wale waliohusika katika kazi yetu ya kupigia chapa kichinichini hawakuwa wamefanya biashara ya kuchapa kabla ya hapo, kwa hiyo yale yaliyotimizwa yalikazia akilini mwangu kwamba bila shaka ni roho ya Yehova ndiyo iliyoandaa msaada na mwelekezo uliohitajiwa. Lilikuwa pendeleo kubwa kwangu na kwa mke wangu, Lucy, aliyefanya kazi katika kiwanda cha kujalidi vichapo, kushiriki sehemu katika hayo yote.

Kazi yetu ilisimamiwaje katika nyakati hizo za majaribu? Yule aliyetumikia akiwa mwangalizi wa tawi wa muda wa Mashahidi wa Yehova alikuwa amepokea agizo la kizuizi kutoka kwa serikali, likimtaka aishi katika mji mmoja karibu mwendo wa kilometa 100 kutoka Sidni. Agizo hilo lilimkataza asitoke katika nusukipenyo (radiasi) ya kilometa nane kutoka kitovu cha mji huo. Petroli ilipewa kwa posho ya lita nne kwa gari moja kwa mwezi. Lakini akina ndugu walivumbua chombo chenye ustadi kilichoitwa chombo cha kutokeza gesi—chombo cha chuma nyembamba chenye umbo la mcheduara kilichokuwa na uzito wa karibu nusu tani, kilichoweka kwenye sehemu ya nyuma ya gari. Makaa yalichomwa ndani yacho, yakitokeza kaboni monoksaidi ikiwa fueli. Usiku kadha kila juma, ndugu wengineo wenye daraka na mimi tulisafiri kwa njia hiyo ili kukutana na mwangalizi huyo katika bonde kavu la hori lililokuwa karibu na mji wa uhamisho wake. Hivyo, tungeweza kuzungumzia mambo mengi kabla ya kukijaza tena kile chombo cha kutokezea gesi na kuendesha gari kurudi Sidni katika saa za mapema za asubuhi.

Mwishoni, marufuku juu ya Mashahidi wa Yehova ilikuja mbele ya Mahakama ya Juu ya Australia. Hakimu alijulisha kwamba marufuku hiyo “haikufuata kanuni, ilikuwa yenye kigeugeu, na yenye uonevu” akawaondolea Mashahidi wa Yehova mashtaka yote kabisa juu ya utendaji wa kuchochea ghasia. Mahakama ya Juu yote iliunga mkono uamuzi huo, hivi kwamba tuliweza kuendelea waziwazi na utendaji wetu halali wa Ufalme.

Migawo na Baraka Zaidi

Baada ya vita wengi waliokuwa wamefanya kazi katika utendaji wetu wa kupigia chapa kichinichini waliingia huduma ya upainia. Baadaye wengine wao walienda kwenye Watchtower Bible School of Gilead katika New York. Lucy na mimi tulifikiria mradi huo pia, lakini tukawa wazazi wa binti kitoto na nikaamua kurudia biashara ya kuchapa. Tulisali kwamba Yehova angetusaidia sikuzote tuweke masilahi ya Ufalme kwanza, naye amefanya hivyo. Nilikuja kuhusika katika mgawo mwingine wa kihuduma katika njia ifuatayo.

Nilipokea simu kutoka kwa Lloyd Barry, anayetumikia sasa akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Wakati huo alikuwa mwangalizi asafiriye katika Sidni. Aliniuliza kama nilijua tarehe ya kusanyiko letu lifuatalo. Nilipojibu kwamba nilijua, alisema hivi: “Twataka ushughulikie mipango ya chakula.”

Nikishangaa kwa muda mfupi, nilisema hivi kwa unyonge kidogo: “Lakini sijawahi kamwe kufanya jambo lolote kama hilo maishani mwangu.”

“Basi, Ndugu,” akajibu kwa ucheshi kidogo, “ni wakati ufaao sana kwako kujifunza!” Nilijifunza bila shaka, na niliendelea kuwa na pendeleo la kusimamia utumishi wa chakula, hata kwenye mikusanyiko mikubwa, kwa muda wa zaidi ya miaka 40.

Kwa muda wa miaka iliyopita, kampuni yetu ya uchapishaji wa kibiashara ilipanuka, na hilo likanilazimu nifanye ziara kadhaa za kibiashara za kwenda ng’ambo. Sikuzote niliratibisha ziara hizo na mikusanyiko ya kimataifa iliyofanywa New York City na kwingineko katika United States. Hilo lilinipa fursa ya kutumia wakati pamoja na wale waliokuwa na usimamizi wa idara mbalimbali za mkusanyiko, hasa utumishi wa chakula. Hivyo, niliporudi Australia, niliweza kutumikia mahitaji ya mikusanyiko yetu vizuri zaidi.

Tukiwa tumezeeka, Lucy na mimi nyakati nyingine hujiuliza kama tungaliweza kutimiza zaidi ikiwa tungalizaliwa baadaye kidogo. Kwa upande ule mwingine, tukiwa tumezaliwa katika 1916 na 1914 mmoja mmoja, twaliona kuwa pendeleo kuona unabii mwingi wa Biblia ukitimizwa mbele ya macho yetu. Na tunamshukuru Yehova kwa ajili ya baraka ambayo tumekuwa nayo katika kujifunza pamoja na watu wengi na kuwasaidia wajifunze kweli na kuwaona sasa wakimtumikia wakiwa wahudumu waliobatizwa. Sala yetu ni kwamba tutaweza kuendelea kumtumikia hadi umilele, tukimkiri milele kuwa Mtawala mkuu Mwenye Enzi wa ulimwengu wote mzima.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Septemba 15, 1978, kurasa 24-7.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kiwanda cha kupigia chapa katika Betheli ya Strathfield, 1929-73

George Gibb akiwa amesimama kando ya mojawapo matbaa zilizochukuliwa kutoka katika kiwanda cha kupigia chapa kupitia ukuta wa nyuma

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki