Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • tp sura 3 kur. 22-33
  • Je! Dini za Ulimwengu Zinatoa Uongozi Unaofaa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Dini za Ulimwengu Zinatoa Uongozi Unaofaa?
  • Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Dini za Ulimwengu Zinasaidia kuendeleza Adili?
  • Matokeo ya Kulikataa Neno la Mungu
  • Mwisho wa Dini za Ulimwengu Wakaribia
  • Sababu kwa Nini Dini ya Kilimwengu Itaisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Ibada Ambayo Mungu Anakubali
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Jinsi Dini za Uwongo Zinavyopotosha Ukweli Kumhusu Mungu
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Je, Dini Zote Humpendeza Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
tp sura 3 kur. 22-33

Sura 3

Je! Dini za Ulimwengu Zinatoa Uongozi Unaofaa?

1. Ni maulizo gani ya maana yanayoulizwa hapa juu ya dini za ulimwengu?

“DINI imekuwa mojapo kani zilizo kuu zaidi katika historia,”28 ndivyo kilivyoeleza The World Book Encyclopedia. Lakini je! dini za ulimwengu zimekuwa kani ya kweli kwa amani na usalama? Je! zimewafunza wafuasi wazo kwamba upendo wa kidugu unapasa upite mipaka ya kitaifa na tofauti za watu wa rangi mbalimbali? Pia, je! makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, Katoliki, Protestanti, na Othodoksi, yamethibitisha madai yao kwamba yanamfuata Yesu Kristo akiwa “Mwana-Mfalme wa Amani”? Au hasa yamechangia chuki inayohatarisha wakati ujao wa mwanadamu? Kuyachunguza maandishi kutatoa jibu lenye kushangaza.

2. Vyanzo mbalimbali vinatuambia nini juu ya maandishi ya kihistoria?

2 Kuhusiana na jambo hili, Parade Magazine lilisema: “Historia inawafunza masomo wale wanaotaka kujifunza. Somo moja la msingi ni kwamba mapambano yanayotegemea dini na tofauti za kimadhehebu sikuzote ndiyo makali zaidi, yenye kuendelea muda mrefu zaidi na ndiyo magumu zaidi kutatua.”29 Na kama vile Chicago Tribune lilivyoeleza: “Kila dini kuu inahubiri amani na udugu na rehema, hata hivyo baadhi ya makatili yaliyo makubwa zaidi na yasiyoweza kuvumilika katika historia yametendwa katika jina la Mungu.”30 Akiwa na mambo hayo hakika ya kihistoria akilini, mhariri wa gazeti C. L. Sulzberger anauliza hivi kwa kufaa: “Hata ingawa habari hii huenda ikawa yenye kuchukiza kadiri gani, je! haipasi kutambuliwa kwamba kwa kuongezea visababishi vingine—kutaka kuhifadhi ufalme, fahari ya rangi ya ngozi, moyo wa kutaka vita—dini imesitawi kuwa tisho linalozidi kuwa kubwa zaidi kwa uhai wa kibinadamu?”31

3. Historia ya karne yetu ya 20 inafunua nini juu ya zoea lenye kuaibisha la dini?

3 Ndiyo, historia ina madoa ya damu ya ugomvi unaoungwa mkono na dini. Katika karne hii yetu peke yayo, wakati wa vile vita vya ulimwengu viwili na baadaye, tumeshuhudia zoea lenye kuaibisha la washiriki wa dini wakiuana—Mkatoliki akiua Mkatoliki, Mprotestanti akiua Mprotestanti, Mwislamu akiua Mwislamu, na wengineo. Na makasisi katika pande mbili zenye kupingana, wajapokuwa wa dini moja, walibariki askari ambao karibuni wangekuwa wakiua ndugu zao wa kidini.

4. (a) Kwa sababu gani makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ndiyo yenye kulaumika zaidi? (b) Tahariri moja inasema nini juu ya vita?

4 Yenye kulaumika zaidi katika jambo hili ni makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Kwa sababu gani? Kwa sababu yanadai kwamba yanamwakilisha Mungu wa Biblia na Mwanaye Yesu Kristo, aliyesema: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Hata hivyo mauaji yaliyo mabaya zaidi yametokea pale pale penye moyo wa Jumuiya ya Wakristo. Kama ilivyotangaza tahariri moja katika gazeti Waterloo Courier la Iowa: “Wala Wakristo hawajachukizwa sana juu ya kupigana vita na Wakristo wengine. Kama wangechukizwa, vingi vya vita vilivyopigwa kwa bidii katika Ulaya havingetukia kamwe. . . . Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na ya Pili, ambavyo viliweka rekodi iliyo kubwa zaidi ya zote ya Wakristo kuua Wakristo wenzao, havingetukia kamwe.”32

5. (a) Biblia inawaambia nini waziwazi wale wanaomtumikia Mungu kweli kweli? (b) Ni ulizo gani ambalo lazima washiriki wa kanisa wakabiliane nalo kuhusu kanisa lao wenyewe?

5 Biblia inasema wazi kuhusu jambo hili: Wale ambao kweli wanamtumikia Mungu wanaambiwa ‘watafute amani na kuifuata sana,’ ‘wafue panga zao ziwe majembe,’ na ‘wasijifunze vita tena kamwe.’ (1 Petro 3:11; Isaya 2:2-4) “Tupendane sisi kwa sisi; si kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu [Shetani Ibilisi], akamwua ndugu yake.” (1 Yohana 3:10-12) Lakini wafuasi wa dini ya ulimwengu huu wanaendelea kuwaua ndugu zao, kama alivyofanya Kaini, nao makasisi wao wamewaunga mkono wale wanaofuatia mwendo huo. Hivyo, ikiwa wewe ni mshiriki wa dini, jiulize: ‘Kama kila mtu duniani angalikuwa mshiriki wa dini yangu, je! vita vingalikuwa vimekoma na dunia hii sasa ingalikuwa mahali pa amani ya kweli?’

6. Hali iliyogawanyika na ya kivita ya dini za ulimwengu inathibitisha nini?

6 Hali iliyogawanyika na ya kivita ya dini za ulimwengu inathibitisha kwamba Mungu haziungi mkono. Jambo hili linaweza kuwashangaza wale wanaofikiria kwamba ni lazima dini zote ziwe ni nzuri kwa kuwa zinajidai kumwakilisha Mungu. Hata hivyo Biblia inaonyesha waziwazi kwamba “Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Inaonyesha pia kwamba kuna dini ya kweli na dini ya uwongo pia. Na inaeleza kwamba ni ibada ile tu ambayo msingi wayo ni ukweli, isiyo na unafiki, inayoungwa mkono na Mungu.—Mathayo 15:7-9; Yohana 4:23, 24; Tito 1:16.

7. (a) Ni neno gani ambalo Biblia inatumia kueleza juu ya dini za ulimwengu? (b) Zinashtakiwa hatia gani?

7 Kwa sababu dini za ulimwengu zimejifanya zenyewe ziwe kama malaya kwa kusudi la mapato ya kisiasa, kibiashara, na kijamii, Biblia inazifananisha na kahaba. Ikieleza juu ya “kahaba” huyo, inasema: “Katika yeye ilipatikana damu ya . . . wote ambao wamechinjwa duniani.” (Ufunuo 17:1-6; 18:24, NW) Ndiyo, dini za ulimwengu huu zimebeba hatia nzito sana ya damu kuhusiana na machinjo yote ya historia ya ulimwengu! Kwa sababu hiyo zitatoa jibu.

8. Maneno ya Yesu kuhusu “viongozi vipofu” yanatumikaje leo?

8 Ni wazi kwamba dini yo yote yenye mazoea yaliyo tofauti na Biblia haiwezi kufaulu kuwaongoza wanadamu kwenye amani na usalama wa kweli. Ndiyo sababu Yesu alisema hivi kuhusu viongozi wa kidini wa uwongo katika siku zake: “Hao ni viongozi vipofu wa vipofu. Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili.” (Mathayo 15:14) Vivyo hivyo, dini za ulimwengu za leo ni “viongozi vipofu” katika habari ya vita na katika sehemu nyinginezo muhimu za maisha pia.

Je! Dini za Ulimwengu Zinasaidia kuendeleza Adili?

9, 10. (a) Kwa sababu gani kushikamana na viwango vya kweli vya adili ni jambo la maana kwa amani na usalama? (b) Kama inavyofundishwa katika Biblia, ni nini kinachosaidia kuendeleza adili hizo?

9 Je! ye yote aweza kufurahia amani ya kweli pamoja na jirani zake au usalama wa kweli ikiwa viwango vya kweli vya adili havidumishwi? Mahali ambapo hapana viwango hivyo, uwongo, wivi, uzinzi na mazoea yanayofanana na hayo ni ya kawaida. Kwa upande mwingine, upendo wa kweli wa jirani wapaswa uendeleze adili.

10 Biblia inaeleza maoni ya Mungu kuhusu adili katika njia hii: “Ampendaye mwenzake ameitimiza sheria. Maana kule kusema, Usizini, Usiue, Usiibe, Usitamani; na ikiwapo amri nyingine yo yote, inajumlishwa katika neno hili, ya kwamba, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Pendo halimfanyii jirani neno baya.”—Warumi 13:8-10.

11, 12. (a) Je! mtu asiyeshikamana na viwango vya adili anaweza kutazamia kufurahia amani pamoja na Mungu? (b) Ni nani kwa kufaa anayeviweka viwango hivyo?

11 Hata hivyo, jambo la maana zaidi ya hilo, je! wewe waamini kwamba ye yote aweza kuwa na amani pamoja na Mungu, akiwa na uhakikisho wa kupata kibali na ulinzi Wake, ikiwa hajizoezi viwango vya adili vya Mungu? Je! ungeweza kumheshimu Mungu asiyewataka wale wanaodai kumtumikia wawe na maadili hayo?

12 Ili Mungu atake viwango vyake vifuatwe sana, ingempasa aeleze waziwazi viwango hivyo. Amefanya hivyo katika Neno lake, Biblia. (2 Timotheo 3:16, 17) Kusema kwamba imempasa kila mtu ajitungie viwango vyake mwenyewe vya adili na kuongozwa navyo kungekuwa sawasawa na kusema kwamba imempasa kila mtu ajitungie sheria zake mwenyewe za barabarani na kuongozwa nazo. Unajua matokeo yangekuwa nini. Kwa kufaa Biblia inaonyesha kwamba kuna njia moja tu inayoleta kibali cha Mungu. Kama alivyosema Yesu, barabara nyingine zote zinaongoza tu kwenye uharibifu.—Mathayo 7:13, 14; Luka 13:24.

13-15. (a) Ni maulizo gani kuhusu adili yanayohitaji kuulizwa kuhusu washiriki wa kanisa la mtu mwenyewe? (b) Biblia inasema ni jambo gani linapasa lifanywe juu ya mshiriki wa kundi anayeendelea kuvunja sheria za Mungu? (c) Je! linafanywa katika makanisa?

13 Je! hasa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanategemeza viwango vya adili vya Mungu na hivyo kuiwekea mfano sehemu ile nyingine yote ya ulimwengu? Maisha za wengi ambao ni washiriki wa makanisa hayo zinafunua nini? Je! wewe ni mshiriki wa kanisa fulani? Basi jiulize: ‘Kama watu wote duniani wangeishi kama washiriki wa dini yangu wanavyoishi, je! hiyo ingekomesha uhalifu, mazoea ya kibiashara yasiyo ya unyofu, ugomvi, na ukosefu wa adili kingono?’

14 Biblia inaonya kwamba “chachu kidogo huchachua donge zima” na kwamba “mashirika mabaya yanaharibu mazoea yenye mafaa.” (Wagalatia 5:9; 1 Wakorintho 15:33, NW) Kwa sababu hii inawaamuru pia Wakristo “msichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye. . . . Ninyi mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.”—1 Wakorintho 5:11-13.

15 Kweli, huenda mtu akapiga hatua mbaya kisha apate nafuu. Lakini namna gani wale wanaofanya zoea la mambo hayo? Ikiwa watu hao wanajidai kumtumikia Mungu, wao ni wanafiki. Bila shaka wewe wauchukia sana unafiki, na Biblia inaonyesha kwamba Mungu pia auchukia na wale wanaouzoea. (Mathayo 23:27, 28; Warumi 12:9) Basi, namna gani dini yako? Je! inafuata amri ya Biblia ya ‘kuwaondoa’ wale wanaoendelea kuvunja sheria za Mungu na wasioonyesha toba ya kweli? Au je! inawaacha watu hao wabaki katika msimamo mwema, hivyo wakihatarisha wengine? Je! inasema kwa mdomo tu juu ya adili na kumbe inajifanya haioni makosa, au hata kuyaachilia yaendelee?—Mathayo 15:7, 8.

16. (a) Viongozi wa kidini wengi wanasema nini siku hizi juu ya mwenendo wa kingono? (b) Biblia inasema nini juu ya mwenendo wa namna hiyo?

16 Viongozi wa kidini zaidi na zaidi wanasema kwamba uasherati, uzinzi, na ugoni-jinsia-moja si mbaya kwa lazima. Lakini hawapatani na anavyofikiri Mungu. Neno lake linaeleza hivi waziwazi: “Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi.”—1 Wakorintho 6:9, 10.

Matokeo ya Kulikataa Neno la Mungu

17-19. (a) Mtume Paulo aliionaje Biblia? (b) Viongozi wa kidini wengi leo wanaionaje Biblia?

17 Sababu ya msingi inayofanya dini za ulimwengu huu ziwe katika hali iliyogawanyika, iliyochafuka ni kwamba zinakataa sheria za Mungu kama zinavyopatikana katika Neno lake, Biblia. Kwa kweli, viongozi wa kidini wengi wanaikataa Biblia kuwa Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho. Hata hivyo, mtume Paulo aliyeongozwa kwa roho alitangaza: “Andiko lote liliongozwa na Mungu.” (2 Timotheo 3:16, NW) Pia Paulo alituhimiza tuikubali Biblia “si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu.” (1 Wathesalonike 2:13) Hapana shaka kwamba Yehova Mungu, Muumba Mwenye Nguvu Zote wa ulimwengu wote mzima wenye ajabu za kutisha, angeweza kubuni kitabu na kuhakikisha kwamba kinadumisha ukamilifu wacho kwa muda wa karne zote!

18 Hata hivyo, New Catholic Encyclopedia inasema: “Maneno mengi ya Biblia si ya kweli yakichunguzwa kulingana na maarifa ya kisasa ya sayansi na historia.”39 Akiandika katika U.S. Catholic, kasisi mmoja alisema kwamba kuumbwa kwa dunia hakungeweza kutokea katika njia ambayo imeelezwa katika Mwanzo. Na kuhusu usimulizi wacho wa uumbaji wa kibinadamu, alisema: “Jamii ya kibinadamu haikuanza kwa njia hiyo.”40 Askofu Mwepiskopali alisema: “Biblia ina makosa, ina mambo yasiyo sahihi na yenye kupingana. Basi inaeleweka ni kwa nini makanisa makubwa ya Kikristo hayaioni Biblia kuwa isiyoweza kukosea.”41 Katika Uingereza, askofu Mwanglikana aliueleza ufufuo wa Kristo kuwa “kiinimacho cha kutumia mifupa.”42

19 Hivyo, viongozi wa kidini wengi ama wanaidharau Biblia ama hawafundishi wafuasi wao kuiheshimu na kufuata sheria za Mungu zilizomo. Hiyo ni moja ya sababu kuu zinazofanya kuwe na ukosefu wenye kushangaza wa kujua Neno la Mungu katika sehemu zote za Jumuiya ya Wakristo. Mwelezaji mambo ya kidini, M. J. McManus aliandika hivi kuhusu wahudhuriaji wa kanisa: “Si mielekeo mingi katika dini inayotisha sana kuharibu matengenezo ya dini katika miaka ya muda wa tangu 1980 kwa kadiri ambavyo inatishwa kuharibiwa na ukosefu wenye kusikitisha wa maarifa ya Biblia.” Alisema kwamba “Biblia inabaki kama maandishi ya kigeni, ambayo hayasomwi” kwa waenda-kanisani walio wengi.43

20, 21. Matokeo yamekuwa nini kwa kuyakataa mafundisho ya Biblia?

20 Matokeo ya yote haya yamekuwa nini? Je! dini za ulimwengu zimeonyesha kwamba zinaweza kudharau mafundisho ya Biblia na bado zitokeze amani au maadili mazuri miongoni mwa washiriki wazo? Tofauti na hilo, hali zinazidi kuwa mbaya duniani pote. Mataifa yenye dini zisizo za Kikristo yanazidi kuwa mahali penye msukosuko, mgawanyiko, ufisadi wa kisiasa, na maadili yenye kuharibika. Lakini Jumuiya ya Wakristo hasa kwa muda mrefu imekuwa ndiyo yenye kupatwa zaidi sana na uhalifu, ukosefu wa adili, uzoevu wa dawa za kulevya, ugomvi unaohusu rangi ya ngozi, na vita. Imetukia tu kama lilivyotabiri Neno linalotegemeka la Mungu: “Wamelikataa Neno la [Yehova, NW]; wana akili gani ndani yao?”—Yeremia 8:9.

21 Ushuhuda unaopatikana hauwezi kukanwa. Unathibitisha kwamba dini za ulimwengu huu si kani ya kweli ya kuleta amani na usalama. Na zimewaacha wafuasi wazo bila kujua tumaini lililo la kweli—Ufalme wa Mungu. Yote haya, basi, yanamaanisha nini?

Mwisho wa Dini za Ulimwengu Wakaribia

22, 23. Ni jambo gani ambalo Biblia inasema kwamba litakuja juu ya dini za uwongo za ulimwengu huu?

22 Yesu Kristo alisema: “Kila pando asilolipanda Baba yangu wa mbinguni litang’olewa.” (Mathayo 15:13) Tunda baya ambalo limetokezwa na dini za ulimwengu huu lathibitisha kwamba hizo si pando la Mungu. Hivyo, Biblia inatabiri uharibifu unaokuja wa mifumo yote ya uwongo ya ibada.

23 Akisema juu ya mifumo hii ya kidini chini ya ‘Babeli Mkuu’ wa mfano aliye kama kahaba, Mungu anasema hivi juu ya milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo: “Dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake. . . . mapigo yake yatakuja katika siku moja, mauti, na huzuni, na njaa, naye atateketezwa kabisa kwa moto. Kwa maana [Yehova, NW] Mungu aliyemhukumu ni mwenye nguvu.”—Ufunuo 18:2, 5-8.

24. Uharibifu huu utakujaje, na utatoka chanzo gani?

24 Angalia kwamba uharibifu huo utakuja kwa ghafula yenye kushangaza, kama “katika siku moja.” Kwa mshangao na fadhaa ya watu wengi, dini ya uwongo itaharibiwa, iangamizwe, na mataifa yale yale ya kisiasa ambayo imefanya ukahaba nayo kwa muda mrefu.—Ufunuo 18:10-17, 21; 17:12, 16.

25. (a) Watu wanaotaka kibali cha Mungu wanahimizwa katika Ufunuo 18:4 wafanye nini? (b) Ni jambo gani linalopasa kumsukuma mtu achukue hatua hiyo?

25 Kwa hiyo mwito wa kimungu ni: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.” (Ufunuo 18:4) Kuchukua hatua hiyo kunamaanisha kwamba mtu anaiona dini ya uwongo kama Mungu aionavyo. Inamaanisha kwamba mtu huchukizwa nayo kwa sababu ya matunda yayo mabaya, unafiki wayo, na ushirikina wayo. Anapaswa ahisi uchukivu mwingi kwa jinsi dini ya uwongo imemsingizia Mungu mbele ya wanadamu na kwa jinsi imechangia kutaabika na kuonewa kwa watu. (Warumi 2:24; Yeremia 23:21, 22) Ukitambua hilo, utaondoa utegemezo wote kutoka kwa dini za namna hiyo, kwa njia hiyo uonyeshe kwamba unaunga sana mkono hukumu ya Mungu juu yazo.

26. (a) Kwa kuongezea, ikiwa mtu anataka kujifurahisha amani na ulinzi wa Mungu ni lazima apate nini? (b) Imempasa mtu atafute watu wa namna gani wakati anapotaka kupata wale wanaozoea ibada ya kweli?

26 Hata hivyo, kuondoka tu hakutoshi. Lazima uitafute na kuipata ibada ya kweli isiyo na unafiki, itakayokuletea wewe amani na ulinzi wa Mungu wakati uharibifu uliotabiriwa utakapokuja. Lazima wale wanaoshiriki katika ibada hiyo ya kweli wawe watu ambao wamekwisha ‘kufua panga zao kuwa majembe, wasijifunze vita tena kamwe.’ (Isaya 2:4) Lazima wawe watu wanaoliamini Neno la Mungu na wanaoishi kulingana nalo, wakiliacha liwe kani yenye kuongoza katika maisha zao. (Zaburi 119:105) Lazima waonyeshe upendo wa kweli usio na unafiki kwa wanadamu wenzao. (Yohana 13:35; Warumi 13:8) Je! kuna ibada ya namna hiyo leo? Mamilioni wameipata miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Wanajulikana ulimwenguni pote kwa kushikamana sana na sheria za Mungu zinazopatikana katika Biblia. Na amani na usalama wanaojifurahisha hata sasa unashuhudia ukweli na uwezo wa Neno la Mungu.

27. Ni jambo gani utakaloweza kuona mwenyewe kwa kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme lao?

27 Mashahidi wa Yehova wanahangaikia sana hali yenye hatari ambamo dini ya uwongo imewaingiza watu. Wao wanajitahidi kwa moyo mweupe kulitanguliza Neno la Mungu katika maisha zao. Unakaribishwa uhudhurie mikutano yao katika Jumba la Ufalme lao la mahali penu na kujichunguzia mwenyewe ni kwa kadiri gani wanaonyesha tunda la roho ya Mungu na kujifurahisha amani na usalama ambao tunda hilo linaleta. Vilevile utaona namna wanavyojifunza na kutumia mambo ambayo Mungu anataka kutoka kwa wale watakaookoka uharibifu unaokuja waishi katika Mfumo Mpya wake chini ya utawala wa Ufalme wake wa kimbingu.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

Viongozi wa kidini zaidi na zaidi wanakubali yale ambayo Biblia inayalaumu ikiyaita ukosefu wa adili, kama vile inavyoonyeshwa na sampuli hizi za vichwa na vihabari:

“Wakati Yale Ambayo Ni Mabaya Yatakapokuwa Mema Viongozi wa Kidini Watatuambia.” “[Kanisa la Uingereza] sasa linaacha mfano walo wa kikale wa kushikamana na kanuni za adili. Ngono kabla ya ndoa, ikifanywa pamoja na mwenzi mmoja au zaidi, . . . kuanzia sasa itakubaliwa kiadili.”—Alberta Report.33

“Mapasta Wakimya Kuhusu Ngono Inayofanywa Kabla ya Ndoa.” “Mapasta wa Amerika wamekosa kuhubiri juu ya ngono inayofanywa kabla ya ndoa . . . Wana hofu kwamba watawapoteza wengine wa wanamitaa wao. Isaya alijua juu ya makuhani wa aina hii. Katika Sura 1 ya kitabu chake, anataja maneno ya Bwana akisema hivi juu yao, ‘Nitaficha macho yangu nisiwaone; hata ingawa mwafanya sala nyingi, mimi sitasikiliza; mikono yenu imejaa damu.’”—Telegraph, North Platte, Nebraska.34

“Uzinzi Katika Maoni Yaliyorahisishwa Zaidi.” “Kasisi Mwingereza . . . aliwagutusha watu alipotangaza hadharani maoni ya Kanisa yenye kupunguza uzito wa Amri ya Saba. . . . ‘Mwelekeo wetu ni kuwa waangalifu badala ya kuhukumu,’ akasema.”—The Sunday Times, Perth, Australia.35

“Wayunitaria Wakubali Ndoa ya Wagoni-Jinsia-Moja.”—The New York Times.36

“Jeshi la kazi la Kanisa Umoja la Kanada limeunga mkono kuagizwa rasmi kwa wagoni-jinsia-moja wenye kutenda wawe wahudumu.”—The Toronto Star.37

“Halalisheni Umalaya—Ndio Utatuzi wa Utakatifu.”—Tahariri ya monsinya Mkatoliki katika Philadelphia Daily News.38

[Picha katika ukurasa wa 25]

Viongozi wa kidini wameitia damu mikono yao kwa kuunga mkono madikteta

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki