Sababu kwa Nini Dini ya Kilimwengu Itaisha
“Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.”—UFUNUO 18:4.
1. (a) Babiloni Mkubwa ameanguka katika njia gani? (b) Tukio hilo limekuwa na matokeo gani kwa Mashahidi wa Yehova?
“BABILONI MKUBWA ameanguka!” Ndiyo, kwa maoni ya Yehova milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli imeanguka. Hilo limekuwa kweli tangu 1919, wakati mabaki ya ndugu za Kristo yalipotoka chini ya uvutano wa Jumuiya ya Wakristo, ile sehemu kuu ya Babiloni ya kifumbo. Tokeo limekuwa kwamba wao wamekuwa huru kushutumu dini isiyo ya kweli na kutangaza utawala wenye uadilifu wa Mungu kupitia Ufalme wa Kimesiya. Katika karne hii yote Mashahidi waaminifu-washikamanifu wa Yehova wamefunua muungano wa dini, ambazo Shetani ametumia ili kudanganya “ulimwengu wote.”—Ufunuo 12:9; 14:8; 18:2; linganisha New World Translation.
Babiloni Mkubwa Ameangukaje?
2. Ni nini iliyo hali ya sasa ya dini za ulimwengu?
2 Hata hivyo, huenda mtu akauliza, ‘Unawezaje kusema kwamba Babiloni ameanguka, ilhali dini yaonekana kusitawi katika nchi nyingi sana?’ Ukatoliki na Uislamu kila mmoja hudai kuwa na waamini zaidi ya bilioni moja. Uprotestanti ungali unasitawi katika zile nchi za Amerika, ambako makanisa mapya huchipuka kila wakati. Mamia ya mamilioni hufuata desturi za Dini ya Buddha na Dini ya Hindu. Lakini ni kwa kadiri gani dini hizi zina uvutano mzuri juu ya mwenendo wa mabilioni hayo ya watu? Je, zimezuia Wakatoliki na Waprotestanti wasiuane katika Ireland Kaskazini? Je, zimeleta amani ya kweli kwa Wayahudi na Waislamu katika Mashariki ya Kati? Je, zimetokeza upatano kati ya Wahindu na Waislamu katika India? Na hivi majuzi, je, zimezuia Waothodoksi wa Serbia, Wakatoliki wa Kroatia, na Waislamu wa Bosnia wasifuatie “utakaso wa kikabila,” uporaji wa mali, kulala wanawake kinguvu, na kuchinjana? Mara nyingi dini ni kibandiko tu, kisetiri chembamba sana kivunjikacho kikiguswa kidogo tu.—Wagalatia 5:19-21; linganisha Yakobo 2:10, 11.
3. Kwa nini dini imo hukumuni mbele za Mungu?
3 Kwa maoni ya Mungu, utegemezo ambao dini inapata kwa halaiki za watu haubadili jambo moja la hakika—dini zote zimo hukumuni mbele za Mungu. Babiloni Mkubwa, kama ionyeshwavyo na historia yake, astahili kuhukumiwa adhabu kwa sababu “dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake.” (Ufunuo 18:5) Katika lugha ya kiunabii Hosea aliandika: “Kwa maana wao hupanda upepo, nao watavuna tufani.” Dini zote zisizo za kweli za Shetani ulimwenguni pote zitaangamizwa kwa sababu ya kusaliti Mungu, upendo wake, jina lake, na Mwana wake.—Hosea 8:7; Wagalatia 6:7; 1 Yohana 2:22, 23.
Ni Lazima Uchague
4, 5. (a) Leo twaishi katika hali zipi? (b) Ni lazima tuyajibu maswali gani?
4 Twaishi katika sehemu ya mwisho ya “siku za mwisho,” na tukiwa Wakristo wa kweli tunajitahidi kuokoka hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5, NW) Wakristo wa kweli ni wakazi wa muda katika ulimwengu wa Shetani, ambao kwa kweli waonyesha utu wake wenye ufisadi akiwa muuaji kimakusudi, mwongo, na mchongezi. (Yohana 8:44; 1 Petro 2:11, 12; Ufunuo 12:10) Tumezingirwa na jeuri, madanganyo, upunjaji, ufisadi, na ukosefu mbaya sana wa adili. Kanuni zimepuuzwa. Raha na ubinafsi ni mambo ya kawaida. Na katika hali nyingi makasisi huruhusu ufisadi wa kiadili kwa kupuuza shutuma ya wazi ya Biblia juu ya ugoni-jinsia-moja, uasherati, na uzinzi. Basi suala ni hili, Je, wewe unategemeza na kuruhusu ibada isiyo ya kweli, au wewe hushiriki kwa bidii katika ibada ya kweli?—Mambo ya Walawi 18:22; 20:13; Warumi 1:26, 27; 1 Wakorintho 6:9-11.
5 Huu ni wakati wa kupepeta. Hivyo, kuna sababu hata zaidi ya kupambanua kati ya ibada isiyo ya kweli na ya kweli. Dini za Jumuiya ya Wakristo zimefanya nini zaidi inayofanya zistahili adhabu sana?—Malaki 3:18; Yohana 4:23, 24.
Dini Isiyo ya Kweli Yashtakiwa
6. Jumuiya ya Wakristo imesalitije Ufalme wa Mungu?
6 Ingawa mamilioni katika Jumuiya ya Wakristo kwa kawaida husema Sala ya Bwana, ambayo kwayo wao husali Ufalme wa Mungu uje, kwa bidii wao wameunga mkono kila wonyesho wa kisiasa, wakipuuza ule utawala wa kitheokrasi. Karne nyingi zilizopita “wakuu” wa Kanisa Katoliki, kama vile Kadinali Richelieu, Mazarin, na Wolsey, walikuwa viongozi wa kilimwengu na mawaziri wa serikali.
7. Mashahidi wa Yehova walifunuaje makasisi wa Jumuiya ya Wakristo zaidi ya miaka 50 iliyopita?
7 Zaidi ya miaka 50 iliyopita, katika kijitabu kiitwacho Religion Reaps the Whirlwind, Mashahidi wa Yehova walifunua kujiingiza kwa Jumuiya ya Wakristo katika siasa.a Yale yaliyosemwa wakati huo yatumika kwa nguvu iyo hiyo leo: “Uchunguzi wenye kufuatia haki wa mwenendo wa makasisi wa kidini wa dini zote utafunua kwamba viongozi wa kidini wa ‘Jumuiya ya Wakristo’ wanashiriki kwa upendezi mwingi katika siasa za ‘ulimwengu huu mwovu wa sasa’ nao wanajiingiza katika mambo ya kilimwengu.” Wakati huo Mashahidi walimchambua vikali Papa Pius 12 kwa ajili ya mikataba aliyofanya pamoja na Hitler Mnazi (1933) na Franco Mfashisti (1941), na pia hali ya papa kubadilishana mabalozi na taifa chokozi Japani katika Machi 1942, miezi michache tu baada ya shambulio baya la Pearl Harbor. Papa alikosa kutii onyo la Yakobo: “Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”—Yakobo 4:4.
8. Kanisa Katoliki ya Kiroma limejiingizaje katika siasa leo?
8 Hali ikoje leo? Papa wangali wanajihusisha katika siasa, kupitia makasisi wao na pia wawakilishi wao wa watu wa kawaida. Papa wa majuzi wameupa kibali Umoja wa Mataifa kwa kuuomba ubandia huo ulete amani ya ulimwengu. Toleo la karibuni la L’Osservatore Romano, gazeti rasmi la Vatikani, lilitangaza kwamba mabalozi wapya saba, “mabalozi kwa Makao ya Papa,” walitoa hati zao kwa “Baba Mtakatifu.” Je, twaweza kuwazia Yesu na Petro wakijihusisha katika mabadilishano kama hayo ya mabalozi? Yesu alikataa kuwekwa mfalme na Wayahudi naye alisema kwamba Ufalme wake haukuwa wa ulimwengu huu.—Yohana 6:15; 18:36.
9. Kwa nini twaweza kusema kwamba dini za Kiprotestanti si bora kuliko zile za Katoliki?
9 Je, viongozi wa Protestanti ni bora kuliko wenzao wa Katoliki? Katika Marekani, dini nyingi za Kiprotestanti zenye kufuata desturi, na Wamormon vilevile, huunga mkono upande fulani wa kisiasa. Lile shirika liitwalo Muungano wa Kikristo limejiingiza kabisa katika siasa za Marekani. Makasisi wengine wa Kiprotestanti huunga mkono upande tofauti wa kisiasa. Nyakati nyingine husahaulika kwamba katika Marekani, wasemaji wa kisiasa kama vile Pat Robertson na Jesse Jackson wangali au walikuwa pia “Maaskofu,” kama ilivyo na mbunge wa Uingereza Ian Paisley wa Ireland Kaskazini. Wao huteteaje misimamo yao?—Matendo 10:34, 35; Wagalatia 2:6.
10. Ni taarifa gani ya wazi iliyotolewa katika 1944?
10 Kama kijitabu Religion Reaps the Whirlwind kilivyouliza katika 1944, ndivyo sisi pia twauliza: “Je, tengenezo lolote lifanyalo mikataba na mamlaka za kilimwengu na kushiriki kabisa katika mambo ya kisiasa ya ulimwengu huu, litafutalo kutumia na kupata ulinzi kutokana na ulimwengu huu . . . laweza kuwa kanisa la Mungu au kumwakilisha Kristo Yesu duniani? . . . Kwa wazi, wanadini wote wenye miradi sawa pamoja na falme za ulimwengu hawawezi kuwakilisha ufalme wa Mungu kupitia Kristo Yesu.”
Roho ya Kaini ya Dini Isiyo ya Kweli
11. Dini isiyo ya kweli ilifuataje kielelezo cha Kaini?
11 Katika historia yote, dini isiyo ya kweli imeonyesha roho ya Kaini aliyemwua ndugu yake Abeli. “Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake. Maana, hii ndiyo habari mliyoisikia tangu mwanzo, kwamba tupendane sisi kwa sisi; si kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu, akamwua ndugu yake. Naye alimwua kwa sababu gani? Kwa sababu matendo yake yalikuwa mabaya, na ya ndugu yake yalikuwa ya haki.” Akishindwa kuvumilia ibada ya ndugu yake iliyokuwa safi na yenye kukubalika kwa Mungu, Kaini alitumia ujeuri—jambo la mwisho ambalo wale wasioweza kueleza sababu za matendo yao huamua kufanya.—1 Yohana 3:10-12.
12. Kuna uthibitisho gani wa kujiingiza kwa dini katika vita na mizozo?
12 Je, mambo ya hakika yaunga mkono shtaka hilo dhidi ya dini isiyo ya kweli? Katika kitabu Preachers Present Arms, mtungaji alisema: “Katika historia ya staarabu, . . . sikuzote kani mbili zimekuwa zikiungana katika muungano wa vitu viwili. Vitu hivyo ni vita na dini. Na, kati ya dini zote za ulimwengu zilizo kubwa, . . . hakuna ile ambayo imejiingiza katika [vita] kuliko [Jumuiya ya Wakristo].” Miaka kadhaa iliyopita, gazeti la habari The Sun la Vancouver, Kanada, lilisema hivi: “Ni udhaifu wa labda dini zote mashuhuri kwamba kanisa hufuata bendera . . . Ni vita gani vilivyopata kupiganwa ambamo Mungu hakudaiwa kuwa katika kila upande wenye kupigana?” Labda umeona uthibitisho wa jambo hilo katika kanisa fulani la kwenu. Mara nyingi mno, bendera za kitaifa huwekwa kwenye altare. Unafikiri Yesu angekuwa mwanajeshi chini ya bendera ipi? Maneno yake yamerudiwa katika karne hizi zote: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu”!—Yohana 18:36.
13. (a) Dini isiyo ya kweli imeshindwaje katika Afrika? (b) Ni ishara gani ya kutambulisha Ukristo aliyotoa Yesu?
13 Dini za Jumuiya ya Wakristo hazijafundisha makundi yazo kweli kuhusu upendo wa kweli wa kidugu. Badala ya hivyo, tofauti za kitaifa na za kikabila huachwa zigawanye washiriki. Ripoti zaonyesha kwamba makasisi wa Katoliki na wa Anglikana walishiriki katika migawanyiko iliyotokeza mauaji ya jamii nzima-nzima katika Rwanda. Gazeti The New York Times liliripoti hivi: “Yale machinjo katika Rwanda yamesababisha Wakatoliki wa Kiroma walio wengi kuhisi wamesalitiwa na viongozi wa kanisa hilo. Mara nyingi kanisa liligawanyika kwa makabila, kati ya Wahutu na Watutsi.” Gazeti lilo hilo pia lilimnukuu kasisi mmoja mishonari wa Katoliki akisema: “Kanisa lilifanya vibaya sana Rwanda katika 1994. Kwa njia fulani Warwanda wengi wamepuuza kanisa. Haliheshimiwi tena.” Hilo ni tofauti kama nini na maneno ya Yesu: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”—Yohana 13:35.
14. Ni rekodi gani ya mwenendo ambayo dini mashuhuri zisizo za Kikristo hutoa?
14 Dini nyinginezo kubwa za Babiloni Mkubwa hazijaweka kielelezo kizuri zaidi. Yale machinjo yenye kuogofya mno ya 1947, India ilipogawanywa, yaonyesha kwamba dini zilizo kuu hazijavumiliana. Jeuri yenye kuendelea ya kijumuiya katika India yathibitisha kwamba watu wengi zaidi hawajabadilika. Si ajabu kwamba gazeti India Today lilikata kauli hivi: “Uhalifu mwingi mkatili zaidi umefanywa kwa jina la dini. . . . Hiyo hutokeza ujeuri mwingi ajabu nayo ni kani yenye kuharibu kabisa.”
“Utofauti Wenye Kutokeza Sana”
15. Ni nini hali ya dini katika ulimwengu wa magharibi?
15 Hata wafafanuzi wa kilimwengu wameona kushindwa kwa dini kusadikisha, kufundisha maadili mema, na kukinza hali ya uulimwengu. Katika kitabu chake Out of Control, aliyekuwa mshauri wa usalama wa kitaifa wa Marekani Zbigniew Brzezinski aliandika hivi: “Ni utofauti wenye kutokeza sana kwamba ushindi mkubwa zaidi wa lile wazo la kwamba ‘Mungu amekufa’ haujatokea katika mataifa ya Kimaksi . . . bali katika jamii za Magharibi za kidemokrasi zenye uhuru, ambazo zimekuza ubaridi wa kiadili. Katika [jamii za Magharibi], uhakika ni kwamba dini imeacha kuwa kani kubwa ya kijamii.” Yeye aliendelea hivi: “Mshiko wa dini katika utamaduni wa Ulaya umepungua kabisa, na Ulaya leo—hata zaidi ya Amerika—hasa ni jamii ya kufuata mambo ya kilimwengu.”
16, 17. (a) Ni shauri gani alilotoa Yesu kuhusu viongozi wa kidini wa wakati wake? (b) Ni kanuni gani nzuri ambayo Yesu alitaja kuhusu matunda?
16 Yesu alisema nini kuhusu viongozi wa kidini wa Kiyahudi wa siku yake? “Waandishi na Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa [kufundisha Torati, ile Sheria]; basi, yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende.” Ndiyo, unafiki wa kidini si jambo geni.—Mathayo 23:2, 3.
17 Matunda ya dini isiyo ya kweli huishutumu. Kanuni iliyotolewa na Yesu yatumika sana: “Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya. Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri. Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni. Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua.”—Mathayo 7:17-20.
18. Jumuiya ya Wakristo ingejidumishaje ikiwa safi?
18 Ikiwa dini za Jumuiya ya Wakristo zingetumia kwa kudhamiria nidhamu ya Kikristo ya kutenga na ushirika, au kuondosha, wale wavunjao sheria wanaodai kuwa washiriki wazo, ni nini lingetokea? Ni nini kingepata wawongo, waasherati, wazinzi, wagoni-jinsia-moja, walaghai, wahalifu, walanguzi wa dawa za kulevya na waraibu, na washiriki wa magenge ya uhalifu wote wasiotubu? Bila shaka, matunda yaliyooza ya Jumuiya ya Wakristo yafanya ifae tu kuharibiwa na Mungu.—1 Wakorintho 5:9-13; 2 Yohana 10, 11.
19. Ni maungamo gani ambayo yamefanywa kuhusu uongozi wa kidini?
19 Baraza kuu la Kanisa la Presbiteri katika Marekani lilikiri hivi: “Tunakabili tatizo kubwa sana na lenye madhara sana. . . . Kati ya asilimia 10 na 23 ya makasisi katika taifa lote wamejihusisha na mwenendo wa kingono au kufanya ngono pamoja na waenda-kanisani, wateja, na wafanyakazi wao, n.k.” Mfanya biashara mmoja wa Marekani alijumlisha hivi jambo hilo vizuri: “Mashirika ya kidini yameshindwa kupitisha maadili yayo, na katika visa vingi, yamekuwa sehemu ya tatizo.”
20, 21. (a) Yesu na Paulo walishutumuje unafiki? (b) Ni maswali gani yanayobaki kujibiwa?
20 Shutuma ya Yesu juu ya unafiki wa kidini ni kweli leo kama ilivyokuwa kweli katika wakati wake: “Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.” (Mathayo 15:7-9) Maneno ya Paulo kwa Tito pia yafafanua hali yetu ya kisasa: “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana; ni wenye machukizo, waasi, wala kwa kila tendo jema hawafai.”—Tito 1:16.
21 Yesu alisema kwamba kipofu akimwongoza kipofu, wote watatumbukia katika shimo. (Mathayo 15:14) Je, wataka kumalizwa pamoja na Babiloni Mkubwa? Au wataka kutembea katika njia zilizonyooka macho yako yakiwa wazi ukafurahie baraka za Yehova? Maswali yanayotukabili sasa ni: Ni dini gani, ikiwa kunayo, inayotokeza matunda ya kimungu? Tunawezaje kutambulisha ibada ya kweli inayokubaliwa na Mungu?—Zaburi 119:105.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., katika 1944; sasa hakichapishwi tena.
Je, Wakumbuka?
◻ Ni nini ulio msimamo wa sasa wa Babiloni Mkubwa mbele ya Mungu?
◻ Dini isiyo ya kweli imeshtakiwa kwa msingi gani?
◻ Dini isiyo ya kweli imeonyeshaje roho ya Kaini?
◻ Yesu alitaja kanuni gani ya kuhukumu dini yoyote?
[Picha katika ukurasa wa 13]
Katika historia yote viongozi wa kidini wamejiingiza katika siasa
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kadinali Mazarin
Kadinali Richelieu
Kadinali Wolsey
Makasisi hawa walikuwa pia viongozi mashuhuri wa serikali
[Hisani]
Kadinali Mazarin na Kadinali Richelieu: Kutoka kitabu Ridpath’s History of the World (Buku 6 na 5 kama wanavyofuatana). Kadinali Wolsey: Kutoka kitabu The History of Protestantism (Buku 1).