Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • tp sura 16 kur. 175-186
  • Uchaguzi Unaohakikishia Uzima Katika Amani na Usalama wa Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uchaguzi Unaohakikishia Uzima Katika Amani na Usalama wa Kweli
  • Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Imani Iliyo Hai
  • Kutubu na Kugeuka
  • Kufanya Tangazo la Waziwazi la Wokovu
  • Kuutunza Sana Uhusiano Wako na Mungu
  • Jinsi Wewe Unaweza Kuona Amani ya Kimungu kwa Ukamili Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Ubatizo na Uhusiano Wako Pamoja na Mungu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Mambo Ambayo Lazima Ufanye Ili Uishi Milele
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Kufanye Kumtumikia Mungu Milele Kuwe Lengo Lako
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
Pata Habari Zaidi
Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
tp sura 16 kur. 175-186

Sura 16

Uchaguzi Unaohakikishia Uzima Katika Amani na Usalama wa Kweli

1. Tukifanya uchaguzi ufaao, tunaweza kupata amani na uhakika gani sasa?

LO! NI furaha kama nini kuwa na kusudi halisi la kuishi, kujua unakoelekea! Na lo! ni amani ya akili na ya moyo ya namna gani inayoletwa na uhakika wa kwamba hakuna mwendo mwingine ulio bora zaidi ambao ungeweza kufuata! Wewe unaweza kupata amani na uhakika huo, ukifanya sasa uchaguzi ufaao tu.

2. Kuja kwetu kumjua Yehova na makusudi yake kunatusaidiaje kwa habari ya matazamio yetu juu ya maisha?

2 Ushuhuda wote unaonyesha wazi kwamba hatuwezi kuutumainia ulimwengu huu kuwa chanzo cha amani na usalama wa kweli. Mifumo ya kibiashara, kidini, na kisiasa, kutia na Umoja wa Mataifa pamoja na matangazo yake ya ‘amani na usalama,’ haiwezi kuileta. Basi, Biblia inatuelekeza sisi kwa Yehova Mungu kama Chanzo cha pekee cha amani na usalama wa kweli. Kwa kumjua yeye na makusudi yake kwa wanadamu tunafahamu sababu ya kuwapo kwetu duniani na sababu ya mambo kuwa kama yalivyo leo. Tunajifunza juu ya suala kubwa linalohusu enzi kuu ya ulimwengu wote mzima wa Yehova, na namna lilivyo na matokeo kwa kila mmoja wetu. Tunajifunza kupima ufaaji na hekima ya miradi yetu, na tunapata viwango vya adili vya kuishilia ambavyo vinategemeka. Tunapoelekewa na ugonjwa, uzee, au kifo, tunakuwa na tumaini lenye kufariji la kupata uzima katika mfumo mpya wenye uadilifu na afya, hata kwa kufufuliwa kutoka kwa wafu, ikiwa hilo litahitajiwa kabisa.

3. Kwa sababu gani Yehova ndiye ambaye imetupasa tuweke matumaini yetu yote kwake?

3 Basi, si ajabu kwamba Isaya 26:4 inasihi: “Mtumainini BWANA [Yehova, NW] sikuzote, maana BWANA YEHOVA ni mwamba wa milele.” Kwa kuwa ni asiyebadilika, mwenye nguvu zote, na wa milele, kweli kweli Yehova ndiye imetupasa tuweke matumaini yetu yote kwake. Je! wewe unataka kufurahia mwongozo na ulinzi wake, si kwa wakati huu tu, bali pia kwa wakati wote ujao katika Mfumo Mpya wake ulioahidiwa? Ikiwa ndivyo, ni lazima ufanye nini?

4. Ili tupate upendeleo wa Yehova, tunahitaji nini, na ni nini kinachotuwezesha tukipate?

4 Wanadamu kwa ujumla wametenganishwa na urafiki wa Mungu kwa sababu ya dhambi ya wazazi wetu wa kwanza. Lakini Mungu amefungua njia ya upatanisho na urafiki pamoja naye kupitia dhabihu ya Mwanaye. (2 Wakorintho 5:19-21; Waefeso 2:12, 13) Hata hivyo, haitoshi kwetu sasa kusema tu tunautaka urafiki wa Mungu.

5. Kichocheo cha kusudio letu katika kutafuta urafiki wa Yehova kinapasa kuwa nini?

5 Imetupasa tuwe wenye nia, hata wenye shauku, kumthibitishia kwamba tunautaka urafiki huo, tena tunautaka kwa kusudio linalofaa. Kwa mfano, je! tunautafuta urafiki wa Yehova kama njia ya kuokokea maafa tu? Ikiwa tutapata msimamo unaofaa pamoja na Mungu, jambo hilo haliwezi kuwa kwa kipindi hiki cha uharaka tu kabla ya hukumu yake wala ili kuokoka tu “dhiki kubwa” inayokuja. (Mathayo 24:21, 22) Lazima liwe ni kwa wakati wote utakaokuja. Ni upendo wa kweli tu utakaotupa sisi kichocheo cha kusudio hilo. Ili tuweze kuonyesha weupe wa tamaa yetu ya kutaka urafiki wake, katika Neno lake Yehova ameweka mambo fulani ambayo lazima kila mmoja wetu ayafanye ili apatanishwe naye.

Imani Iliyo Hai

6. Ili tumpendeze Mungu, ni lazima tuwe na uhakika gani juu yake?

6 Yehova ni Mungu wa ukweli. Kwa hiyo tunaweza kuwa na uhakika kamili katika ahadi zake. Kwa kweli, “pasipo imani haiwezekani kumpendeza yeye vema, kwa maana yeye anayemkaribia Mungu yampasa aamini kwamba yuko na kwamba anakuwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii nyingi.” (Waebrania 11:6, NW) Ikiwa una imani hiyo, basi unajua kwamba kila alifanyalo Mungu lina kusudi la uadilifu, na kwamba sikuzote yeye anazifikiria faida zetu bora. Unaweza ukaona kutokana na kazi zake za kuumba, na kutokana na Neno lake lililoandikwa, kwamba yeye si mwenye hekima yote na mwenye uwezo wote tu bali pia ni Mungu wa fadhili za upendo. Bila shaka, yeye hataondoka kamwe katika viwango vyake vyenye uadilifu. Hata hivyo, ingawa sisi ni watu wasio wakamilifu na tunafanya makosa, ikiwa tunapenda uadilifu, yeye ana njia ya kushughulika nasi itayozitokeza baraka.

7. Kuwa na uhakika katika ufaaji wa matendo ya Yehova na hekima yake kutatulindaje?

7 Hivyo, tupatapo sahihisho kutoka kwa Mungu, tutajua kwamba ni kwa ajili ya masilahi yetu ya milele. Tutakuja kumtumaini Yehova kama vile mwana au binti anavyomtumaini baba mwenye upendo, mwenye hekima, na mwenye nguvu. (Zaburi 103:13, 14; Mithali 3:11, 12) Tukiwa na imani hiyo, hatutatilia shaka hekima ya mashauri yake wala ufaaji wa njia zake, hata ingawa huenda tusifahamu mambo fulani vizuri kabisa kwa muda. Kwa njia hiyo tunajiweka miongoni mwa wale ambao mtunga zaburi anaeleza juu yao hivi: “Wana amani nyingi waipendao sheria yako, wala hawana la kuwakwaza.”—Zaburi 119:165; Mithali 3:5-8.

8. (a) Kwa sababu gani imani peke yake haitoshi? (b) Imani inapasa itusukume kwenye tendo gani linalotajwa kwenye Matendo 3:19?

8 Lakini “imani pasipo matendo imekufa,” linaonyesha Yakobo 2:26. Imani ya kweli inasukuma mtu kwenye tendo. Na mojapo mambo ya kwanza ambalo imani inasukuma mtu kutenda ni lile ambalo mtume Petro alihimiza: “Tubuni . . . [mgeuke], ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake BWANA [Yehova, NW].” (Matendo 3:19) Hiyo inamaanisha nini?

Kutubu na Kugeuka

9. (a) Toba ya kweli ni nini? (b) Tunahitaji kutubia nini?

9 Katika Biblia, toba inamaanisha badiliko la akili lenye kufuatana na majuto ya moyoni kwa ajili ya njia ya maisha ya zamani au matendo mabaya. (2 Wakorintho 7:9-11) Lakini ikiwa tunataka tuzifurahie “nyakati za kuburudishwa” zilizoahidiwa kutoka kwa Mungu, hatuwezi kutubia matendo mabaya ya wakati uliopita tu. Badala yake, lazima tuonyeshe toba kwa sababu tunakubali kwamba asili yetu yenyewe ni yenye dhambi kwa sababu sisi ni watoto wa Adamu. Kama vile mtume Yohana anavyosema: “Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe . . . twamfanya [Mungu] kuwa mwongo wala neno lake halimo mwetu.” (1 Yohana 1:8, 10) Imetupasa tumwakilishe Muumba wetu ifaavyo, tukionyesha ‘mfano wake na sura yake.’ Hata hivyo dhambi iliyorithiwa inatuzuia tusifanye hivyo kwa njia kamilifu. Kwa sababu hiyo, ‘tunaikosa shabaha,’ ambayo ndiyo maana ya neno “dhambi” katika Biblia.—Mwanzo 1:26; Warumi 3:23.

10, 11. (a) Sisi tunawiwa uhai na nani, na kwa sababu gani? (b) Kwa hiyo, inatupasa tuwe tukitumia maisha zetu kwa njia gani?

10 Kwa hiyo tunauhitaji msamaha wa Mungu. (Mathayo 6:12) Tunajua kwamba yeye anatuwia uhai wetu kama Muumba wetu. Lakini sasa tunajifunza kwamba kupitia dhabihu ya Mwana wa Mungu, wanadamu ‘walinunuliwa kwa thamani’ kubwa pia. Haitupasi tuwe “watumwa wa wanadamu,” wala hata wa tamaa zetu wenyewe za ubinafsi. (1 Wakorintho 7:23) Hata hivyo, kabla hatujajifunza ukweli na kuukubali je! sivyo sisi sote tulivyokuwa?—Yohana 8:31-34.

11 Je! wewe unaithamini katika moyo wako zawadi ya Mungu ya Mwanaye na yale ambayo amefanya kupitia Kristo ili kuandaa njia ya kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo? Basi kwa uhakika utajutia kwa weupe wa moyo kushindwa ko kote kwa wakati uliopita kutumia maisha yako kwa kumtii Muumba wako. Hiyo itakusukuma kwenye toba ya moyoni kwa sababu ya kuwa ulifuata mwendo wa maisha kama ule wa ulimwengu, usiopatana na mapenzi na makusudi ya Mungu.—Matendo 17:28, 30; Ufunuo 4:11.

12. Mtu mwenye kutubu anaonyeshaje kwamba yeye ameukataa kweli kweli mwendo wake wa kwanza?

12 Toba hiyo ya kweli inaongoza kwenye ‘kugeuka,’ ambayo ndiyo maana ya neno “kuongoka.” Mtu anayetubu kweli kweli hajuti tu kwa kuwa alitumia maisha yake vibaya. Yeye anaukataa mwendo huo mbaya na anakuja kuzichukia kikweli njia zake mbaya. Anaonyesha hivyo kwa ‘kugeuka’ na kufanya “matendo yanayopatana na kutubu,” akiyapatanisha maisha yake na mapenzi ya Mungu.—Matendo 26:20; Warumi 6:11.

13. (a) Ni nini maana ya taarifa ya Yesu kwamba lazima wafuasi wake ‘wajikane wenyewe’? (b) Ni kwa sababu gani tunajitoa kabisa kwa Yehova kwa njia hiyo, na hiyo inakuwa na matokeo gani juu ya maisha zetu?

13 Sehemu ya kutubu huku na kugeuka inatia ndani kufanya kule ambako Yesu alikuita ‘kujikana wenyewe.’ (Mathayo 16:24) Yaani, hatuishi tena kulingana na tamaa zetu wenyewe tu za ubinafsi bila kujali mapenzi na makusudi ya Mungu. Badala yake, tunakubali kwamba Yehova Mungu ana haki kamili juu ya uhai wetu kwa sababu ndiye Muumba wetu na Mnunuzi wetu kupitia dhabihu ya ukombozi ya Mwanaye. Kama vile Biblia inavyoeleza jambo hilo, sisi ‘si mali yetu wenyewe; maana tulinunuliwa kwa thamani.’ (1 Wakorintho 6:19, 20) Kwa hiyo, badala ya kutumia vibaya uhuru wetu mkubwa ambao ukweli ulitufungulia wazi, tunajitoa kwa ukamili tufanye mapenzi ya Mungu. (Wagalatia 5:13; 1 Petro 2:16) Nasi tunafanya hivyo, si kwa sababu tu inafaa, bali kwa sababu tunampenda Yehova Mungu kwa ‘moyo wetu wote mzima, nafsi, akili na nguvu.’ (Marko 12:29, 30, NW) Kwa kweli hiyo inahitaji kila mmoja wetu aishi maisha ya wakfu kwa Mungu. Badala ya kuwa mzigo, mwendo huo unatuwezesha tufurahie maisha kwa njia tusiyopata kamwe kuyafurahia.—Mathayo 11:28-30.

Kufanya Tangazo la Waziwazi la Wokovu

14. (a) Wakati mtu anapoukubali uenyeji halali wa Yehova juu yake, anaweza kuelezaje Mungu jambo hilo? (b) Imempasa atamani kufanya nini zaidi, kama inavyoonyeshwa katika Warumi 10:10?

14 Ni jambo jema tueleze Mungu katika sala kwamba tunaamini maandalizi yake, tukiukubali uenyeji wake juu yetu. Lakini tunaweza na tunapaswa tutake kuendeleza zaidi elezo letu la imani, kama vile Warumi 10:10 inavyotuambia: “Kwa moyo mtu huamini apate uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la waziwazi la wokovu.” Elezo hilo la “waziwazi” la imani yetu katika Yehova na maandalizi yake linapasa litoke kwa furaha katika moyo uliojawa na uthamini. Kufanya tangazo hilo kunatia ndani kutoa maisha yetu wakfu kwa Yehova kufanya mapenzi yake na kuonyesha wakfu huo kwa ubatizo wa maji.

15. Kwa sababu gani inatupasa tufikirie ubatizo wa maji kwa uzito?

15 Wakati Yesu Kristo alipoanza huduma yake ya waziwazi, alimwaambia Yohana Mbatizaji amzamishe majini. Biblia inaripoti kwamba wakati huo Yesu alimwambia Mungu: “Nimekuja niyafanye mapenzi yako.” (Waebrania 10:9; Zaburi 40:7, 8) Yesu aliagiza kwamba wale wote wanaokuwa wanafunzi wake wanapaswa pia wabatizwe. Wewe ni mwanafunzi wa aina hiyo? Basi ubatizo wako majini utakuwa “tangazo la waziwazi” la jambo hilo.—Mathayo 28:19, 20.

16. (a) Unaweza kuamuaje kama uko tayari kubatizwa? (b) Waangalizi wanasaidiaje watu mmoja mmoja katika tayarisho lao kwa ubatizo?

16 Ni pendeleo kubwa kuwa shahidi aliye wakfu na aliyebatizwa wa Yehova, Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima. Sasa jikumbushe tena yanayotiwa ndani katika hilo: Kwa upendo Yehova amekufungulia njia ili wewe upate urafiki wake. Lakini ili uupate, ni lazima uwe na imani, kuamini kweli kweli kwamba Biblia ndilo Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. (2 Timotheo 3:16, 17) Lazima pia ujizoeze imani katika dhabihu ya ukombozi ya Yesu kama njia pekee ambayo kwayo unaweza kupata msimamo unaokubalika pamoja na Mungu. (Matendo 4:12) Unahitaji kuthamini tegemeo lako juu ya Yehova na kumtolea maisha yako ufanye mapenzi yake, si kwa miaka michache tu, bali milele. Mwendo wa namna hiyo unatia ndani kuwa “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16; 1 Yohana 2:15, NW) Lazima uwe umekwisha kuacha mazoea yo yote yanayotofautiana na viwango vya uadilifu vya Mungu na uwe ukifanya mambo anayoyaamuru Mungu kama ushuhuda wa kwamba umetubu na ‘kugeuka.’ Je! wewe umebadili akili yako hivi kwamba sasa unayaona maisha kwa njia hiyo? (Warumi 12:1, 2) Ikiwa ndivyo, Biblia inakutia moyo ufanye “tangazo la waziwazi” la imani hiyo. Hatua ya kwanza ingekuwa kufikia mmoja wa waangalizi wa kundi la Mashahidi wa Yehova katika eneo lako umjulishe unavyohisi. Yeye atafanya mpango wa kurudia pamoja nawe mafundisho ya msingi ya Biblia ili ujitayarishe kwa ubatizo.

17. Kwa kutumia Biblia, onyesha jinsi ni lazima sisi tuendelee kufanya ‘tangazo la waziwazi la imani yetu.’

17 Hatua ya ubatizo haitakuwa ndiyo mwisho wa kufanya kwako ‘tangazo la waziwazi la imani yako.’ Kama Mkristo aliyejitoa wakfu kwa Yehova Mungu, utataka kutangaza tumaini lako kwa kueleza maoni yako mwenyewe katika kusanyiko la watu wote, ‘ukimhimidi katika kundi lililo kubwa.’ (Zaburi 35:18; 40:9, 10, NW) Vilevile utataka kushiriki katika kazi ya pekee ya “tangazo la waziwazi” ambayo Yehova anagawia wote ambao wanataka kumtumikia—kuhubiri habari njema za Ufalme katika ulimwengu wote na kufanya wanafunzi wa watu wa mataifa yote.—Mathayo 24:14; 28:19.

Kuutunza Sana Uhusiano Wako na Mungu

18. Funzo la kibinafsi ni la maana kadiri gani katika kuhakikisha kwamba uhusiano wa mtu na Yehova utadumu?

18 Sasa, basi, unaweza kuhakikishaje kwamba uhusiano wako na Mungu ukiisha kupatikana utakuwa wenye kudumu milele katika amani na usalama wenye furaha? Kwanza, utataka uendelee kukua katika maarifa ya kumjua yeye. Kupitia funzo la kibinafsi utapata furaha ya kweli katika kupata hazina za hekima ambazo zimewekwa akibani katika Neno la Mungu. Unaweza kuwa kama mtu ambaye Zaburi 1:2, 3 (NW) inaeleza hivi juu yake: “Kupendezwa kwake ku katika sheria ya Yehova, na katika sheria yake husoma kwa sauti ndogo mchana na usiku. Naye hakika atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.” Ndiyo, kupata maarifa ya kumjua Mungu, na kuyatumia, kutakuwezesha utembee katika “njia za kupendeza sana” na katika ‘mapito ya amani,’ kwa maana kutakupa hekima ya kuelekeana na matatizo yote ya maisha. (Mithali 3:13, 17, 18) Kiu yako kwa maarifa hayo ya Biblia sasa itaonyesha kwamba wewe unafaa kwa ajili ya uzima katika Mfumo Mpya wa Mungu, kwa sababu wakati huo ‘dunia itajawa na kumjua BWANA [Yehova, NW], kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

19. Kwa sababu gani kuhudhuria mikutano kwa ukawaida ni jambo la lazima katika maisha ya watu wa Yehova?

19 Jambo jingine unalohitaji sana ni kuhudhuria mikutano kwa ukawaida pamoja na watumishi wengine wa Yehova. Huko utapata kichocheo cha kweli uwe na upendo na kazi nzuri, upate kitia-moyo cha kuendelea kuvumilia katika uhusiano unaofaa ulio nao pamoja na Mungu. (Waebrania 10:23-25) Ushirika wenye kupendeza wa kijamaa walio nao watumishi wa Yehova unatoa ushuhuda wenye kutia nguvu kwamba amani na usalama ulioahidiwa kwa Mfumo Mpya wa Mungu ni mambo halisi.—Zaburi 133:1; 1 Wakorintho 14:26, 33.

20. Wanaume wazee katika kundi wanaweza kutusaidiaje katika nyakati za upinzani na ugumu wa kibinafsi?

20 Katika kundi unaweza kupata manufaa kutokana na uandalizi mwingine wa upendo. Yesu, ‘Mchungaji Mwema,’ ana ‘wachungaji wadogo’ duniani. Hao ndio waangalizi, au wanaume wazee kiroho, wanaotunza “kondoo” zake. Wao ni uvutano wenye nguvu katika kuendeleza amani na usalama miongoni mwa watu wa Mungu waliokusanywa kuwa kundi ulimwenguni pote. (1 Petro 5:2, 3) Wanaume hao wanakuwa “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:1, 2) Ndiyo, katika nyakati zenye dhoruba ya mikazo na mashaka kwa sababu ya upinzani wa kilimwengu au magumu ya kibinafsi, hao wanaume wazee kiroho wanaweza kusaidia kweli kweli kwa imani yao ya kimwamba na ushikaji wao imara wa Neno la Mungu. Wanaweza kukutolea wewe mashauri yenye kuburudisha na kitia-moyo.

21. Ni nini kitakachotuzuia tusiyaruhusu kamwe makosa ya kutokamilika kwa wengine yauharibu uhusiano wetu na Yehova?

21 Ni kweli kwamba makosa ya kutokamilika kwa kibinadamu yataonekana wazi, hata miongoni mwa watumishi wa Mungu. Sote tunafanya makosa kila siku. (Yakobo 3:2) Lakini je! tutajiacha tukwazwe na makosa ya kutokamilika kwa wengine na kuacha jambo hilo liharibu uhusiano wetu na Yehova Mungu? Kwa kuwa hata sisi tunakosa, je! tusionyeshe wengine msamaha ule ule tunaojitakia wenyewe? (Mathayo 6:14, 15) Ikiwa tutajithibitisha wenyewe kuwa raia wastahilio uzima katika Mfumo Mpya wa Mungu wenye amani, ni lazima tuuonyeshe sasa uwezo wetu wa kuchukuliana na wengine katika amani. Hatuwezi kumpenda Mungu bila ya kuwapenda pia ndugu na dada zetu wa kiroho ambao Kristo alifia.—1 Yohana 4:20, 21.

22. Sala inapasa iwe na sehemu gani katika maisha zetu?

22 Uhusiano wako na Mungu ufaao unakupa pendeleo jingine kubwa: kumfikia Mungu kwa sala ukiwa na uhakikisho wa kwamba yeye anakusikia. Ulitunze sana pendeleo hilo na kulitumia kila siku, siku nzima. Matatizo yatatokea. Huenda makosa yako mwenyewe yakakusumbua. Hata hivyo Biblia inashauri hivi: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

23. Tunapoelekewa na majaribu na taabu kwa sababu ya imani yetu, ni nini kitakachotusaidia tuvumilie?

23 Kwa kuchagua kumtumikia Yehova Mungu, Chanzo cha kweli cha amani na usalama, na kuweka tumaini lako katika Mfumo Mpya wake, utakuwa umefanya mwanzo mzuri. Sasa, kama Biblia inavyosema, ‘unahitaji uvumilivu, ili kwamba, ukiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu, upate kupokea utimizo wa ahadi.’ (Waebrania 10:36, NW) Kwa kuwa umezionja baraka za kuwa na uhusiano ufaao pamoja na Yehova Mungu, piga moyo konde usiuache kamwe. Usiziache kamwe raha za muda tu za ulimwengu zikupotoe. Yajapokuwa majaribu makali kutokana na ulimwengu ulio adui, kumbuka kwamba hayo ni ya muda tu. Zikilinganishwa na baraka ambazo Yehova atawapa wale wanaompenda yeye, taabu hizo zaonekana kama si kitu.—2 Wakorintho 4:16-18.

24. (a) Leo sisi tuna sababu ya kufurahia nini hasa? (b) Kama vile mtunga zaburi, inatupasa tuhisije sikuzote juu ya Yehova na uhusiano wetu naye?

24 Uendelee kutembea katika mwendo wa kujitolea Mungu, ukiwa na uhakika kwamba hiyo ndiyo njia bora zaidi ya maisha sasa na kwamba itaongoza kwenye uzima wa milele katika Mfumo Mpya wa Mungu. (1 Timotheo 4:8) Ufurahie ushuhuda wa kukaribia kwa huo Mfumo Mpya na amani na usalama wa milele utakaoletwa nao. Unapoendelea kujenga uhusiano wako na Yehova, sikuzote hisi kama alivyohisi mtunga zaburi aliyeongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Mungu ndiye mwamba wa moyo wangu na fungu langu kwa wakati usiojulikana. Kwa maana, tazama! wale wale wanaojitenga nawe watatoweka. Wewe utamnyamazisha bila shaka kila mtu anayekuacha kwa uovu. Lakini kwa habari yangu mimi, kumkaribia Mungu kwanifaa. Katika Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu ndimo nimeweka kimbilio langu, nipate kuzitangaza kazi zako zote.”—Zaburi 73:26-28, NW.

[Picha katika ukurasa wa 181]

Kufanya tangazo la waziwazi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki