Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ws sura 2 kur. 13-20
  • “Mwana-Mfalme wa Amani” Akabili Har–Magedoni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mwana-Mfalme wa Amani” Akabili Har–Magedoni
  • Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Agano kwa Ajili ya Ufalme Bila Mwisho wa Amani
  • “Mlima wa Megido” wa Mfano
  • Mataifa Yanakusanywa Kwenye Har–Magedoni
  • Kuokoka Katika Upande Wenye Kushinda Katika Har–Magedoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Har-magedoni—Mwanzo Wenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Har-magedoni Lini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”
ws sura 2 kur. 13-20

Sura 2

“Mwana-Mfalme wa Amani” Akabili Har–Magedoni

1, 2. (a) Ni maneno gani yenye kusisimua ambayo Mungu alimwongoza nabii Isaya kusema? (b) Maneno hayo yalianza kutimizwa wakati gani?

KATIKA karne ya nane kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, nabii Isaya aliongozwa na Mungu awaambie watu wa Mungu hivi: “Kwa maana kuna mtoto ambaye amezaliwa kwetu, kumekuwa na mwana ambaye amepewa kwetu sisi; na utawala wa mwana-mfalme utakuja kuwa juu ya bega lake. Na jina lake ataitwa Mshauri wa Ajabu, Mungu Mwenye Nguvu, Baba ya Milele, Mwana-Mfalme wa Amani. Kwa wingi wa utawala wa mwana-mfalme na kwa amani hakutakuwa na mwisho, juu ya kiti cha ufalme cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuusimamisha kwa imara na kuuendeleza kwa njia ya haki na kwa njia ya uadilifu, kuanza sasa na kuendelea na mpaka wakati usiojulikana.”—Isaya 9:6, 7, NW.

2 Maneno hayo yenye kusisimua yalianza kutimizwa katika sehemu ya pili ya mwaka 2 K.W.K. Huo ulikuwa wakati Yesu alipozaliwa akiwa mzao wa Mfalme Daudi, ambaye alikuwa ametawala katika mji wa Yerusalemu juu ya yale makabila 12 ya Israeli.

Agano kwa Ajili ya Ufalme Bila Mwisho wa Amani

3. (a) Ni agano gani ambalo Mungu alifanya na Mfalme Daudi? (b) Ni mzao yupi wa Mfalme Daudi ambaye Yehova amempa jina la cheo “Mwana-Mfalme wa Amani”?

3 Kwa sababu ya bidii ya Daudi kwa ajili ya ibada ya Mungu wa Israeli, Yehova alifanya pamoja naye agano kwa ajili ya Ufalme wa milele katika ukoo wake. (2 Samweli 7:1-16) Agano hilo liliimarishwa kwa kiapo cha Mungu. (Zaburi 132:11, 12) Kulingana na agano hilo, ufalme wa Daudi ungetoa msingi kwa ajili ya ule Ufalme uliokuwa ukija wa yule “Mwana-Mfalme wa Amani.” “Yesu Kristo, mwana wa Daudi,” ndiye aliyepewa na Yehova lile jina la cheo “Mwana-Mfalme wa Amani.”—Mathayo 1:1.

4. (a) Ni nani ambaye akawa mama wa kidunia wa Yesu? (b) Malaika Gabrieli alisema nini kwake juu ya jambo hilo?

4 Mama ya Yesu alikuwa mwanamke ambaye alizaliwa katika ukoo wa kifalme wa Mfalme Daudi. Yeye alikuwa bikira wakati alipochukua mimba ya mwana wake aliyeahidiwa, ambaye angekuwa mrithi wa kudumu wa kiti cha ufalme cha Daudi. Aliichukua mimba hiyo kabla Yusufu hajamchukua awe mke wake. (Mathayo 1:18-25) Yule malaika Gabrieli alikuwa amemwambia Mariamu huyo bikira hivi: “Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na [Yehova] Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho.”—Luka 1:31-33.

5. Nabii Isaya alikuwa ametabiri nini kwa habari ya utawala wa “Mwana-Mfalme wa Amani”?

5 Ndiyo sababu nabii Isaya alitabiri kwa habari ya yule “Mwana-Mfalme wa Amani” kwamba “utawala wake utakuwa mpana katika amani ambayo haina mwisho, kwa ajili ya kiti cha ufalme cha Daudi na kwa ajili ya uweza wake wa kifalme.” (Isaya 9:6, 7, The Jerusalem Bible) Hivyo, kulingana na agano lililofanywa pamoja na Daudi, Ufalme huo ungekuwa serikali ya milele ambayo amani yake haingekuwa na mwisho. Kiti chake cha ufalme lazima kisimame hata “milele”!

6. (a) Ili kutimiza agano la Ufalme, Mungu alifanya nini katika siku ya tatu ya kifo cha Yesu? (b) Ni wakati gani Yesu alianza kutawala akiwa “Mwana-Mfalme wa Amani”?

6 Ili kutimiza agano hili la Ufalme, Mungu Mwenye Nguvu Zote alimfufua Yesu kutoka kwa wafu katika siku ya tatu ya kifo chake cha kufia imani. Hiyo ilikuwa ni siku ya kumi na sita ya mwezi Nisani wa Kiyahudi mwaka wa 33 Wakati wa Kawaida wetu. Akiwa mmoja aliyemwona kwa macho Mwana wa Mungu aliyefufuliwa, mtume Petro alisema kwamba Yesu “aliuawa katika mwili, lakini akafanywa hai katika roho.” (1 Petro 3:18, NW) Mungu Aliye Juu Zaidi alimwinua kwenye mkono Wake mwenyewe wa kuume. Akiwa huko, tangu mwisho wa Majira ya Mataifa, au “nyakati zilizowekwa za mataifa,” mapema mwa Oktoba wa 1914, yeye amekuwa akitawala akiwa ndiye “Mwana-Mfalme wa Amani.”—Luka 21:24, NW.

7. (a) Yesu amekabili nini tangu mwanzo wa utawala wake? (b) Ni nani wanaotangaza Ufalme wa Yesu kwa mataifa yote, na ni katika utimizo wa nini?

7 Tangu mwanzo wa utawala wake wa kimbingu, yeye amekabili ulimwengu wenye uadui, kama ushuhuda unavyoonyeshwa na vita viwili vya ulimwengu ambavyo vilipiganwa juu ya suala la ni nani atakayetawala dunia. Sasa yeye anakabiliana na tengenezo la Umoja wa Mataifa. Kupitia habari njema za Ufalme huo zinazotangazwa na Mashahidi wa Yehova, ambao wanahubiri katika nchi zaidi ya 200, fikira za mataifa yote zinavutwa kwenye ufalme wake wenye kutenda katika mbingu. Huo ni utimizo wa yale yaliyotabiriwa na yule “Mwana-Mfalme wa Amani” mwenyewe, kama tunavyosoma kwenye Mathayo 24:14, NW: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”

8. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba tumeingia sana katika huu “umalizio wa mfumo wa mambo”?

8 Lile suala la utawala wa ulimwengu ni lazima liamuliwe upesi. Sasa, zaidi ya miaka sabini baada ya mwisho wa “nyakati zilizowekwa za mataifa” katika mwaka 1914, tumeingia sana katika huu “umalizio wa mfumo wa mambo.” Kile kizazi cha mwaka 1914 kiliona ule mwanzo wa matukio ya ulimwengu yenye maana kubwa yaliyotabiriwa na Yesu. (Mathayo 24:3-14, NW) Kizazi hicho Yesu alisema, hakingepita kamwe mpaka mambo yote hayo yametimizwa. Kizazi hicho sasa kimekaribia sana kumaliza mwendo wacho.—Mathayo 24:34.

9, 10. (a) Sisi tulipashwaje habari za kiunabii zilizomo kwenye kitabu cha Ufunuo? (b) Ufunuo 16:13, 14, 16 hutabiri nini juu ya Har–Magedoni?

9 Kwa hiyo, ni jambo gani lililopo apa hapa mbele tu, naye yule “Mwana-Mfalme wa Amani” anakabili nini? Yeye mwenyewe alitumiwa kutabiri hayo katika kile kitabu cha mwisho cha Biblia, yaani, Ufunuo, ambacho Mungu alimpa mzee mtume Yohana kupitia kwa malaika. (Ufunuo 1:1, 2) Hilo lilitukia karibu na mwisho wa karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu. Kwenye Ufunuo 16:13, 14, 16, Yesu alimfanya mtume Yohana aelekeze kwenye Har–Magedoni kwa njia hii yenye maana:

10 “Nikaona roho tatu za uchafu zilizofanana na vyura, zikitoka katika kinywa cha yule joka, na katika kinywa cha yule mnyama na katika kinywa cha yule nabii wa uwongo. Hizo ndizo roho za mashetani, zifanyazo ishara, zitokazo na kuwaendea wafalme wa ulimwengu wote, kuwakusanya kwa vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi. Wakawakusanya hata mahali paitwapo kwa Kiebrania Har–Magedoni.”

“Mlima wa Megido” wa Mfano

11. (a) Jina Har–Magedoni linamaanisha nini, na je! kulipata kamwe kuwako mahali pa kijiografia penye kuitwa jina hilo? (b) Kwa sababu gani ule mji wa kale wa Megido ulikuwa na maana kubwa ya kihistoria? (c) Jina hilo Megido lilipata kuwa na maana gani mbili?

11 Lile jina la Kiebrania Har–Magedoni, linamaanisha “Mlima wa Megido.” Hakuna mahali pa kijiografia paitwapo Mlima wa Megido katika nyakati za kale au nyakati za kisasa. Kwa hiyo katika kitabu kama Ufunuo ambacho kinajawa na usemi wa mfano, usemi huo unakuwa na maana ya mfano. Ni lazima huo uwe nini? Basi, ule mji wa Megido, ambao jina lake lamaanisha “kusanyiko la vikosi,” ulikuwa na maana ya kihistoria. Katika historia ya kilimwengu na ya Kibiblia jina hilo liliamsha kumbukumbu za vita vya kukata maneno. Kwa sababu gani? Kwa sababu wakati huo mji huo ulitawala nchi yenye kijia kilichopitia mahali pa kupigia vita panapofaa kati ya Ulaya, Esia na Afrika, nao washambuliaji wangeweza kutolewa mwito wa ushindani kwa njia yenye mafaa na kuzuiwa hapa na wakaaji wa mji huo. Hivyo Megido ukawa na maana mbili—upande mmoja ushinde wenye msiba na upande ule mwingine ushindi wenye utukufu.

12, 13. (a) Mungu wa Biblia alikuja kushirikishwaje na Megido na mto wao ulio karibu wakati wa siku za Mwamuzi Baraka? (b) Wimbo wa ushindi wa Baraka na Debora unaelezaje sehemu ambayo Mungu alishiriki katika ushindi huo?

12 Mungu wa Biblia alikuja kushirikishwa na Megido pamoja na mto Kishoni uliokuwa karibu wakati wa kipindi cha waamuzi Waisraeli. Katika siku za Mwamuzi Baraka na nabii wa kike Debora, Mungu aliwapatia watu wake waliochaguliwa ushindi mkubwa katika ujirani wa Megido. Mwamuzi Baraka alikuwa na wanaume 10,000, hali adui waliokuwa chini ya Jenerali Sisera walikuwa na magari ya vita yenye kukokotwa na farasi 900, mbali na vikosi vya chini. Yehova alijiingiza katika vita kwa ajili ya watu wake waliochaguliwa akaleta mvua yenye furiko iliyoyazuia magari hayo ya farasi yenye kuogopesha ya adui. Katika wimbo wa ushindi ambao Baraka na Debora walimwimbia Mungu baada ya jeshi la Sisera kushindwa kimwujiza, walivuta fikira kwenye sehemu ambayo Mungu alishiriki katika kuwapindua adui hao:

13 “Wafalme walikuja wakafanya vita, ndipo wafalme wa Kanaani walifanya vita. Katika Taanaki, karibu na maji ya Megido; hawakupata faida yo yote ya fedha. Walipigana kutoka mbinguni, nyota katika miendo yao zilipigana na Sisera. Mto ule wa Kishoni uliwachukua, ule mto wa zamani, mto wa Kishoni.”—Waamuzi 5:12, 19-21.

14. Ni maneno gani ya kufunga ya wimbo huo ulioongozwa na Mungu ambayo bila shaka ni sala kuhusu ile vita inayokuja kwenye Har–Magedoni?

14 Bila shaka, yale maneno yaliyoongozwa kwa roho ambayo kwayo Baraka na Debora waliufunga wimbo wao baada ya ushindi huo wa kale kwenye Megido yanatumika kama sala kwa habari ya ile vita inayokuja kwenye Har–Magedoni. Wao waliimba hivi: “Na waangamie vivyo hivyo adui zako wote, Ee [Yehova]. Bali wao wampendao na wawe kama jua hapo litokapo kwa nguvu zake.”—Waamuzi 5:31.a

Mataifa Yanakusanywa Kwenye Har–Magedoni

15. (a) Basi, Har–Magedoni ni mahali pa namna gani? (b) Ni Nini kimojapo cha vyanzo vya maenezi ya kisiasa yenye uchafu yanayowakusanya mataifa kwenye vita katika Har–Magedoni?

15 Kwa hiyo Megido palikuwa mahali ambapo vita vya kukata maneno vilipiganwa. Hivyo, kwa kufaa, Har–Magedoni ungekuwa ni uwanja wa vita ambao katika huo mataifa yote ya ulimwengu wa leo yangepiga miguu kuuelekea chini ya majeshi yenye kuchochea yanayosimuliwa kwenye Ufunuo 16:13, 14. Zile “semi zilizoongozwa na mashetani,” (NW) zinazokusanya mataifa ndiyo yale maenezi ya kisiasa ambayo yanatolewa leo kama mkoromo wa vyura, yenye uchafu kama vile chura alivyo mchafu kulingana na maoni ya Biblia. Kimojapo cha vyanzo vya maenezi ya kisiasa hayo yenye uchafu ni lile “joka kubwa jekundu.” Ufunuo 12:1-9 unatambulisha “yule joka” kuwa Shetani yule Ibilisi.

16. Katika Ufunuo 16:13, yule “mnyama” anafananisha nini?

16 Chanzo kingine cha maenezi ya kisiasi yenye uchafu ni “yule mnyama.” Kwenye Ufunuo 16:13 huyu “mnyama” wa mfano anashirikishwa na yule “joka” wa kiibilisi. Kulingana na Ufunuo 20:10, huyo “mnyama” ataharibiwa milele kwa sababu ya kushirikiana na huyo “joka” wa mfano. Huyo “mnyama” anafananisha mfumo mzima wa kisiasa wa ulimwengu huu ambao “yule joka” ndiye mungu wao. (2 Wakorintho 4:4) Anatia ndani serikali zote mbalimbali za kisiasa za ulimwengu huu.—Linganisha Danieli 7:17; 8:20, 22.

17. Ni nini matokeo ya maenezi ya kisiasa yanayofanana na vyura yanayotoka kwa yule “mnyama”?

17 Mfumo huo wa ulimwengu wa utawala wa kisiasa una maenezi yao ya kisiasa ya kuutofautisha. Nayo maenezi ya kisiasa hayo, yenye mkoromo kama wa vyura, ni usemi ulioongozwa na roho unaotumika pamoja na ule usemi ulioongozwa na roho wa “yule joka” ili kukusanya “wafalme,” au watawala wa kisiasa wa ulimwengu, kwenye “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” itakayopiganwa kwenye Har–Magedoni.

18. (a) Jina Har–Magedoni linaonyesha nini? (b) Mlima ungefananisha nini?

18 Hivyo Har–Magedoni huonyesha hali ya ulimwengu inayohusu vita ya kukata maneno. Inaonyesha ile hali ya upeo wa mambo ya ulimwengu ambayo kwa sababu hiyo watawala wa ulimwengu kwa umoja wanapinga mapenzi ya Mungu, hivi kwamba Mungu analazimika kutenda kwa majeshi yenye kupinga kulingana na kusudi lake. Kwa hiyo wakati ujao utaamuliwa kulingana na matokeo ya mkabiliano huo. Kwenye Megido yenyewe, mahali pale pa kijiografia, hapakuwa na mlima. Lakini, mlima ungefananisha mahali pa kukusanyika penye kutokeza sana ambapo pangeweza kuonekana kwa urahisi kutoka mbali na majeshi yote ya kivita yenye kukusanyika hapo.

19, 20. Jenerali wa majeshi ya Yehova ya kimbingu atatumia mpango gani wa werevu wa vita kwenye Har–Magedoni, na kwa matokeo gani?

19 Kwa miaka kadha Yesu Kristo aliye Jenerali wa majeshi yenye kupiga vita ya Yehova, amekuwa akitazama kukusanyika kwa watawala wa ulimwengu pamoja na majeshi yao yenye kupiga vita kwenye Har–Magedoni. Walakini, yeye hakujaribu kumchagua mfalme ye yote mmoja na majeshi yake ya kivita awapige wakiwa peke yao na hivyo amalize majeshi ya adui kidogokidogo. Tofauti na hilo, yeye anawaruhusu wakati wa kutosha wajikusanye pamoja na kuunganisha majeshi yao yawe jeshi la kivita kubwa zaidi liwezekanalo. Kusudi lake la ujasiri ni kupigana nao wote kwa wakati mmoja!

20 Hivyo, yeye atapata ushindi wenye sifa zaidi juu yao, kwa utukufu wa Amiri-jeshi Mkuu, Yehova Mungu, na kwa kuthibitishwa kwake mwenyewe kuwa, yule “Mfalme wa Wafalme na Bwana wa Mabwana,” asiyepingika.—Ufunuo 19:16, HNWW.

[Maelezo ya Chini]

a Mitajo mingine ya Megido inapatikana kwenye 2 Wafalme 9:27; 23:29, 30; 2 Mambo ya Nyakati 35:22; Zekaria 12:11.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki