Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 4/15 kur. 171-231
  • Kuokoka Katika Upande Wenye Kushinda Katika Har–Magedoni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuokoka Katika Upande Wenye Kushinda Katika Har–Magedoni
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • VITA, SI JUU YA MWANADAMU, BALI JUU YA MUNGU
  • ULIZO KATIKA HAR-MAGEDONI
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Faida za Wanadamu Kutokana na Ushindi Katika Har–Magedoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Chanzo cha Taabu ya Wanadamu Chakaribia Kuondolewa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • “Mwana-Mfalme wa Amani” Akabili Har–Magedoni
    Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 4/15 kur. 171-231

Kuokoka Katika Upande Wenye Kushinda Katika Har–​Magedoni

“Wakapaza sauti pamoja: ‘Ushindi kwa Mungu wetu aketiye juu ya kiti cha enzi, na kwa Mwana-Kondoo!’”​—Ufu. 7:10, New English Bible.

1. Ni nini kitakachofuata vita inayokuja katika Har–​Magedoni, nasi twafanya vema tukifanya nini sasa?

AMANI ya miaka elfu itafuata vita ya ulimwengu wote katika uwanja wa vita wa Har–​Magedoni. Litakuwa jambo la kutamanika sana kuiokoka vita hiyo ya mwisho ya taratibu hii ya mambo ya kilimwengu. Wokovu utakuwa ndilo pendeleo lenye furaha la wale watakaokuwa katika upande wenye kushinda. Hii yatoa maoni yaliyo tofauti sana na maoni yenye huzuni sana yanayofikiriwa na watabiri wa kisiasa na wa kijeshi kwamba vita ya ulimwengu ya tatu, ikipigwa kwa silaha za atomiki, haitakuwa yenye ushindi kwa upande wo wote. Pande zote mbili zitashindwa. Utabiri mwingine waonyesha kwamba vita hiyo ya ulimwengu itamaanisha kujiua kwa jamaa ya kibinadamu. Walakini, hatuna haja ya kuogofishwa na mawazo hayo ya kibinadamu. Kutakuwako upande wenye kushinda katika pigano linalokuja katika Har–​Magedoni. Twafanya vema ikiwa sasa twajiunga na upande utakaoshinda bila shaka, tukafurahie baada ya hapo tunda jema la ushindi.

2. Kwa sababu gani kujipanga sasa katika upande wenye kushinda hakutuhitaji tujitie katika siasa zo zote za ulimwengu huu?

2 Katika habari hii hautakuwa ushindi wa chama kimoja cha kisiasa au jamii ya mataifa juu ya chama kingine cha kisiasa au jamii ya mataifa. Hakutakuwa kulazimisha wazo moja la utawala wa kibinadamu juu ya watu walioshindwa wasiotaka kuacha wazo jingine la utawala wa kisiasa. Wala washindi hawatalazimisha washinde kuingia katika kambi moja ya kisiasa inayotia ndani ulimwengu wote wa wanadamu. Jambo kama hilo halileti amani yenye kuendelea duniani wala halileti utii wa nia kwa upande wa washinde. Ushindi utakaopatikana hautakuwa ushindi wa kisiasa, bali utafutilia mbali siasa zote za kibinadamu duniani. Kujipanga kwetu katika upande wenye kushinda kutahitaji kutojitia katika siasa zenye kuleta migawanyiko za ulimwengu huu.

3. Kwa hiyo, ni maulizo gani yanayotupendeza zaidi sana sasa?

3 Uhakika huu wa maana ndio unaoonyesha sehemu ya kuvutia ya vita ya ulimwengu wote inayokuja katika Har–​Magedoni, ingawa leo watu zaidi na zaidi hawapendi kuzungumza wala kuwaza juu ya habari ya vita. Maulizo yanayotupendeza sana ni, Mshindi atapata nini kutokana na ushindi wake? Ushindi utakuwa na maana gani kwa wale ambao kati yetu twajipanga upande wa mshindi? Je! itastahilisha kuokoka kwetu katika Har–​Magedoni?

4. Kama mamlaka moja au zote za kisiasa zingeshinda katika pigano la ulimwengu, mshindi angetupa nini?

4 Kama mamlaka zote za kisiasa za taratibu hii ya mambo zikiupata ushindi zikiwa pamoja au jamii mojawapo ikiupata, twajua itatupa nini kwa sababu ya magumu tuliyoona. Kisingeweza kuwa bora kuliko walichowapa wanadamu tangu kutokea kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza mwaka wa 1914 C.E. Nacho hicho kimekuwa nini? Si kingine ila nyakati zenye magumu, zinazokuwa zenye magumu zaidi na zaidi kwa watu wote. Sababu ya kutumainia hali njema ya ulimwengu inafifia zaidi na zaidi. Sababu ya kutumainia mabaya inaongezeka. Ijapokuwa misaada ya sayansi ya kisasa na ufundi wenye maendeleo na Umoja wa Mataifa kama wakili wa ushirikiano wa mataifa yote, wataalamu wenye busara wa uwekevu wa vifaa vya jamii ya watu, wanafunzi wa mambo ya kijamii na wenye kuchunguza hali za maisha ya kinyumbani wanatuonya kwamba tunakaribia mwisho kamili, mtunga sheria ye yote, mwanasiasa, mkuu wa polisi au mwalimu asijue njia ya kutokea. Zaidi ya haya lazima hasara zenye kutatiza ziongezwe na ushindi katika vita nyingine ya ulimwengu katika maisha za kibinadamu, mali za kimwili na mazingira. Kwa hiyo, yaelekea sana kwamba mamlaka za kisiasa zingekuwa na vitu vibaya zaidi vya kutupa sisi kuliko ambavyo zimetupa tangu mwaka wa 1914 mpaka sasa.

5. Kwa hiyo, lazima nani awe ndiye mshindi atamanikaye katika Har–​Magedoni, na kwa sababu gani hivyo?

5 Kwa hiyo, bila shaka lazima watu wote wenye mioyo minyofu watumainie na kutazamia ushindi katika vita inayokuja katika Har–​Magedoni kama zawadi ya mtu awezaye kutupa wakati ujao ambao tungependa tuokoke tukauone. Mshindi huyo wa kutamanika katika Har–​Magedoni hawezi kuwa mwingine ila Muumba wa mazingira ya kwanza ya kidunia ya mwanadamu, yaani, Mungu mwenyewe. Hili ndilo jambo la busara, kwa maana yahusuyo mazingira ya asili ya mwanadamu yamhusu Mungu. Yahusuyo wanadamu wote yamhusu Mungu.

6. Kutakuwa na uhusiano gani kati ya vita ya ulimwengu wote inayokuja katika Har–​Magedoni na mazingira ya kwanza ya kidunia ya mwanadamu?

6 Mazingira ya kwanza ya mwanadamu hayakuwa pango la kuwazia kama ifundishwavyo na wenye kuendeleza kisio la mageuzi ya mwanadamu. Mambo ya kweli juu ya habari hii ni kwamba mazingira ya kwanza ya asili ya mwanadamu yalikuwa bustani kamilifu, paradiso yenye uzuri wa asili na hali za maisha yenye kupendeza. Kwa hiyo mojawapo la matunda mazuri sana ya ushindi wa kimungu katika Har–​Magedoni litakuwa kuwekwa tena kwa paradiso duniani, lakini katika dunia nzima. Kurudi kwa wanadamu kwenye Paradiso hakuwezekani kwa njia nyingine yo yote ila kwa ushindi wa kimungu katika Har–​Magedoni. Hilo ni mojawapo la mambo yanayotuondolea wazo la kuchukia vita ya ulimwengu wote​—ile itakayokuwa katika Har–​Magedoni.

VITA, SI JUU YA MWANADAMU, BALI JUU YA MUNGU

7. Kwa hiyo, mataifa yote yatakuwa yakipigana na nani, nayo maoni yao wenyewe ni nini juu ya jambo hilo?

7 Je! kuwaza huku kwamaanisha kwamba mataifa yote ya dunia yako karibu kupiga vita juu ya Mungu Muumba katika uwanja wa vita wa Har–​Magedoni? Barabara! Lakini mataifa yanachukia kuambiwa kwamba yanaelekea kwenye mpambano huo na Mungu. Kwa kweli, ingekuwa vigumu kuyasadikisha mataifa ya kisiasa, zaidi yale ya Jumuiya ya Wakristo wenye kufuata dini (Kristendomu), kwamba wao wanajitayarisha sasa kupigana na Mungu wa Biblia Takatifu. Viongozi wa dini wameyahakikishia mataifa ya Jumuiya ya Wakristo sikuzote kwamba sikuzote wao wamempigania Mungu, katika upande wa Mungu, katika vita zote za mataifa yote tangu kuanzishwa kwa Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) katika karne ya nne C.E. Wao wamejiacha waingizwe katika jitihada zao za vita na nia ya kidini kama ile ya Mfalme wa Kirumi Konstantino, ambaye alipiga vita chini ya ishara ya msalaba kabla hajaanzisha Jumuiya ya Wakristo. Konstantino huyu alidai kuona njozi ya kimbinguni ya msalaba wenye kung’aa ukiwa na maneno yenye miali ya mwangaza, “Kwa huu shinda” (katika Kigiriki, En touʹto niʹka), kabla ya kupigana vita ya kukata maneno na adui yake wa kisiasa.

8. Uwanja huo wa vita utakaokuwapo umepewaje jina, nao una eneo kadiri gani?

8 Hata hivyo, Mungu mwenyewe ndiye aonyaye mataifa yote kwamba watakuwa wakipigana na Yeye. Yeye ndiye anayetoa jina la mahali itakapopiganiwa vita mpaka mwisho, yaani, Har–​Magedoni. Lazima uwanja huo wa vita uwe duniani, kwa maana ndipo mataifa wanapojikuta, bila ya njia ya kuokokea kuingia katika anga za juu. Kwa kweli, uwanja huo wa vita watia ndani dunia yote​—jambo litakalofanya isiwezekane mtu ye yote duniani ayaepuke matokeo yake.

9. Kuendelea kwetu kuwa pamoja na mataifa kutaongoza tukapigane na nani, lakini twaweza kutii shauri gani lililoongozwa na Mungu katika Luka 14:31, 32?

9 Huenda mataifa yasijiache yasadiki kwamba Mungu Ndiye watakayekuwa wakipigana naye, lakini namna gani sisi kama watu mmoja mmoja, hata tuwe wa taifa gani? Je! tunafurahia wazo la kupigana na Mungu? Ikiwa sivyo, tutafanyaje, kwa maana sote tumo katika mataifa hayo mbalimbali? Je! tutajiacha tuvutwe kwa werevu na mipango ya hila tukapigane na Mungu tukiwa pamoja na mataifa? Ikiwa sivyo, basi yatupasa tuliendee Neno la Mungu mwenyewe lililoandikwa, Biblia Takatifu, tujue Yeye atuambia tufanye nini. Yafaa tufuate shauri la Mwana wa Mungu, aliyewaonya wanafunzi wake kwa upole wahesabu gharama (bei) ya shughuli zao, akisema hivi: “Kuna mfalme gani, akitaka kwenda kupigana na mfalme mwingine, asiyeketi kwanza na kufanya shauri, kwamba yeye pamoja na watu elfu kumi ataweza kukutana na yule anayekuja juu yake na watu elfu ishirini? Na kama akiona hawezi, hutuma ujumbe kutaka sharti za amani, mtu yule akali mbali.” (Luka 14:31, 32) Vivyo hivyo, je! tutaendelea kusonga na mataifa ya kilimwengu kuelekea kwenye Har–​Magedoni, au tutaomba amani na Mungu sasa bila kukawia?

10. Ni wapi na ni kwa usemi gani wenye kusimulia Mungu asemapo kwamba atapigana na mataifa katika Har–​Magedoni?

10 Twawezaje basi kuondoka katika njia ya kuelekea kwenye Har–​Magedoni tusije tukajipanga huko katika upande wa mataifa? Ni wapi Mungu anapotupasha habari kwamba atapigana na mataifa katika Har–​Magedoni? Ni katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo, sura ya kumi na sita, mstari wa kumi na sita. Mistari inayotangulia yasema kwa unabii namna ambavyo mataifa yangeongozwa kwa maongozi yasiyoonekana yapitayo uwezo wa mwanadamu, yaani, kwa maongozi yenye chuki nyingi ya kishetani, kwenye vita hii isiyo ya kawaida. Akiyasimulia maongozi yenye kumpinga Mungu kama “roho za mashetani” wasioonekana, mwandikaji wa Biblia Yohana Mhubiri wa Injili asema hivi: “Kwa kweli, ni roho za mashetani hizo nazo zafanya ishara, nazo zawaendea wafalme wa dunia yote inayokaliwa na watu, zikawakusanye pamoja kwenye vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenye Nguvu Zote. . . . Zikawakusanya pamoja kwenye mahali paitwapo kwa Kiebrania Har–​Magedoni.” (NW)

11. Katika Kiebrania chenyewe jina la uwanja wa vita lamaanisha nini?

11 Maneno hayo ya unabii yaliandikwa kwanza na Yohana Mhubiri wa Injili katika Kigiriki cha kawaida. Lakini yalipotafsiriwa kwa Kiebrania chenyewe katika karne ya kumi na tisa, mstari wa kumi na sita ulisema hivi: “Wakawakusanya kwenye mahali ambapo Waebrania wanapaita Mlima wa Megido [Har Megiddon].”​—Ufu. 16:16, tafsiri ya Kiebrania ya Salkinson-Ginsburg; pia, ya F. Delitzsch.

12. Kwa hiyo wengine wanadai vita hiyo ya mwisho itapiganiwa wapi, lakini maoni hayo yanatokeza maulizo gani?

12 Watafsiri wengine wa Biblia na viongozi wakuu wa dini watoao matangazo ya radio ulimwenguni pote wamesema kwamba vita inayokuja ya ulimwengu wote itapigwa katika nchi ya Israeli, katika Bonde la Megido, penye magofu ya mji wa kale wa Megido, kwa sababu jina Har–​Magedoni lamaanisha Mlima wa Megido. Kwa kweli, mtalii akizuru magofu hayo leo atasoma ishara ionyeshayo mahali hapo na kusema kwamba ndipo vita ya mwisho itakapopigiwa kulingana na maoni ya watu wengine. Lakini, ingawa bonde hilo lililoko mbele ya kilima cha magofu ya Megido wa kale ni pana, haliwezi kuchukua kusanyiko la majeshi ya wafalme na watawala wa dunia yote inayokaliwa na watu. Na kwa kweli vita ikipigwa huko mbele ya uwanja halisi wa Megido ingeamua ulizo gani? Je! mataifa yasiyo ya Kiyahudi yatapigana na Jamhuri ya Israeli katika Megido kama uwanja wa vita wa dunia yote ulio katikati na ufaao maarifa ya vita, wakiwa na manowari zao, ndege zao za vita, vifaru vyao vya vita, roketi zao za vita zenye kufika mbali na majeshi yao yenye vifaa vya kusafiria? Kwa hiyo ni Jamhuri ya Israeli itakayojikuta katika upande wenye kushinda katika mahali paitwapo Har–​Magedoni?

13. Watu wafanyao matumizi hayo wanadharau uhakika gani juu ya Ufunuo, kama inavyoonyeshwa na matumizi yake ya “mto ule mkubwa Frati”?

13 Wale wachukuao jina Har–​Magedoni au Mlima wa Megido kwa njia halisi wanaleta maulizo kama hayo. Wanaudharau uhakika ustahilio kuangaliwa kwamba kitabu cha Biblia cha Ufunuo kiliandikwa sehemu kubwa kwa usemi wa mfano, kwa matumizi mengi ya ishara au semi za mfano. Kwa mfano, wakati mstari wa kumi na mbili wa sura ii hii ya kumi na sita unapozungumza juu ya pigo la sita la Mungu likimwagwa juu ya “mto ule mkubwa Frati,” haumaanishi kwamba pigo hili la mfano la sita linatimizwa juu ya Mto Frati wa halisi ambao sasa umo katika nchi ya Iraq. Katika nyakati za kale za Biblia, mahali halisi pa mto huo palikuwa mji wa Babeli, iliyoongoza mamlaka ya ulimwengu ya tatu ya historia ya Biblia, Milki ya Kibabeli. Kwa hiyo matumizi ya Mto Frati kama mfano yakaza fikira kwenye milki ya ulimwengu ya dini ya uongo ambayo ingali ipo iitwayo na kitabu cha Ufunuo Babeli Mkuu, ambayo mstari wa kumi na tisa wa sura ii hii ya kumi na sita inataja. Kwa njia ile ile, mstari wa kumi na sita watumia jina Har–​Magedoni kwa njia ya mfano kwa sababu ya kushirikishwa kwalo na mambo ya kihistoria.

14. Jina Megido lilikuwa na maana gani mbili, na kwa sababu gani?

14 Jina Megido ni lenye nguvu sana. Katika historia ya kilimwengu na katika historia ya Biblia jina hilo lilikumbusha habari za mapigano ya kukata maneno. Kwa sababu gani? Kwa maana mji wakati huo ulitawala kipito cha nchi kifaacho kwa maarifa ya vita katikati ya Ulaya, Asia na Afrika, na kwa hiyo washambuliaji wangeweza kuzuiwa hapo kwa kufaa na wakaaji. Kwa hiyo Megido pakawa na maana mbili, maana ya kushindwa kwa upande mmoja kwa njia ya kuhuzunisha na ya ushindi wenye fahari kwa upande ule mwingine.

15. Ni mtu gani hasa akashirikishwa na Megido, na kwa njia gani?

15 Mungu wa Biblia alishirikishwa na mahali hapo, na mto wa karibu wa Kishoni. Mungu huyu alikuwa pamoja na Mwamuzi Yoshua, aliyemrithi nabii Musa, wakati Yoshua alipokuwa anaitiisha Nchi ya Ahadi na kuteka Megido. (Yos. 12:21; 17:11) Wakati wa kipindi cha waamuzi waliomfuata Yoshua, Mungu aliwapa watu wake wateule ushindi mkuu katika ujirani wa Megido. Hii ilikuwa katika siku za Mwamuzi Baraka na nabii wa kike Debora.

16, 17. (a) Pigano hilo halikuwa la maana ndogo kwa nani, na kwa hiyo kulifanywa nini kwa ajili ya Waisraeli? (b) Nani aliyehesabiwa ushindi na Baraka na Debora?

16 Likilinganishwa na idadi na vifaa vitumiwavyo katika mapigano ya kisasa, pigano la huko nyuma lilikuwa jambo dogo, Mwamuzi Baraka alipokuwa na wanaume elfu kumi tu na nabii wa kike Debora, huku Jemadari adui Sisera akiwa na magari 900 ya vita yenye kuvutwa na farasi yakiwa na miundu mikubwa ya kukatia, zaidi ya kuwa na vikosi vya kutembea kwa miguu. Walakini, hilo halikuwa jambo lisilo na maana sana kwa Mungu, kwa maana alijitia piganoni kwa ajili ya watu wake wateule. Yeye peke yake ndiye angaliwezesha mvua kubwa inye katika wakati ufaao hasa, kuleta gharika ya ghafula katika bonde la Mto Kishoni iliyoyakwamisha magari hayo 900 ya adui yenye kuogofya. Katika wimbo wa ushindi ambao Baraka na Debora walimwimbia Mungu baada ya kushindwa kwa mwujiza kwa adui waonezi, wao walikaza fikira kwenye ushirika wa Mungu uliokuwa wa lazima kabisa katika kuwashinda adui, kwa kusema:

17 “Wafalme walikuja wakafanya vita, ndipo wafalme wa Kanaani walifanya vita. Katika Taanaki, karibu na maji ya Megido; hawakupata faida yo yote ya fedha. Walipigana kutoka mbinguni, nyota katika miendo yao zilipigana na Sisera. Mto ule wa Kishoni uliwachukua, ule mto wa zamani, mto wa Kishoni. Ee [nafsi ] yangu, endelea mbele kwa nguvu. Ndipo kwato za farasi zilikanyaga-kanyaga kwa sababu ya kupara-para, kupara-para kwao wenye nguvu. Ulaanini Merozi, alisema malaika wa [Yehova], walaanini kwa uchungu wenyeji wake; kwa maana hawakuja kumsaidia [Yehova], kumsaidia [Yehova] juu ya hao wenye nguvu.”​—Amu. 5:19-23; 4:1-3, 10, 12, 13.

18. Sababu ya kuokoka kwa Debora na Baraka na vikosi vyake yasemwaje katika Waamuzi 4:14-16?

18 Nabii wa kike Debora na Mwamuzi Baraka na mashujaa wenzake wa vita waliliokoka pigano katika upande wenye kushinda katika Megido. Sababu yake yasemwa pia katika masimulizi yaliyomo katika Waamuzi 4:14-16: “Debora akamwambia Baraka, Haya! inuka; maana siku hii ndiyo siku ambayo [Yehova] amemtia Sisera katika mkono wako. Je! [Yehova] hakutoka atangulie mbele yako? Basi Baraka akashuka katika mlima wa Tabori [katika upande wa bonde ulioelekeana na Megido], na watu elfu kumi wakamfuata. [Yehova] akamfadhaisha Sisera na magari yake yote, na jeshi lake lote, kwa makali ya upanga, mbele ya Baraka.” Baada ya hapo lilikuwa jambo jepesi kwa Mwamuzi Baraka na vikosi vyake kuwafuatia adui waliotawanywa na kuwaharibu wote.

19. (a) Maneno ya sala mwishoni mwa wimbo wa Baraka na Debora yanatumika kwa habari ya vita gani inayokuja? (h) Ni jambo gani la maana sana lililoufuata ushindi huo karibu na Megido?

19 Bila shaka maneno yaliyoongozwa na Mungu ambayo Baraka na Debora waliyaimba mwishoni mwa wimbo wao baada ya ushindi huo wa kale katika Megido yatumika kama sala kwa habari ya vita inayokuja katika Har–​Magedoni. Wao waliimba hivi: “Na waangamie vivyo hivyo adui zako wote, Ee [Yehova]. Bali wao wampendao na wawe kama jua hapo litokapo kwa nguvu zake.” (Amu. 5:31) Utimizo wa sala hiyo iliyoongozwa na Mungu wamaanisha wakati ujao wenye matumaini mazuri sana kwa wote wampendao Yehova watakaokuwa katika upande wenye kushinda katika Har–​Magedoni. Jambo la maana katika habari hii ni kwamba, huko nyuma katika siku za Baraka na Debora ‘nchi ilistarehe miaka arobaini’ kama maandishi yatuambiavyo.

20. Ni nini katika siku zetu kinachofananishwa na “mahali paitwapo kwa Kiebrania Har–​Magedoni”?

20 Sasa ni nini kinachofananishwa katika siku zetu na “mahali paitwapo kwa Kiebrania Har–​Magedoni”? Kama vile katika Megido wa kale, panamaanisha hali ya ulimwengu ihusuyo vita ya kukata maneno. Panamaanisha hali hiyo yenye ukatili wa ulimwengu juu ya Mungu inayohitaji ulizo ambalo limetokeza ukatili liamuliwe. Kwa kuwa mwinuko wa nchi wa Megido wa kale ulisimamia kipito cha nchi kutoka bara moja hata nyingine, hivyo Har–​Magedoni yamaanisha hali ya upeo ambayo mambo ya ulimwengu yanafikia ambapo watawala wa kisiasa wanatumia nguvu kwa umoja wapenyeze njia yao na ambapo lazima Mungu achukue hatua akiwa na majeshi yenye kupinga kulingana na kusudi lake Yeye. Kwa hiyo wakati ujao wa ulimwengu wote utaamuliwa na yatakayotokea kutokana na kupambana kwa majeshi maadui.

21. (a) Tukiwa na maoni hayo juu ya Har–​Magedoni, hatutakuwa tukitazama au kutazamia nini? (b) Uchunguzi wetu zaidi wa Maandiko utatuwezesha kufanya nini?

21 Kuwa na maoni hayo yanayolingana na Maandiko juu ya inachomaanisha Har–​Magedoni hasa kutatuzuia tusitazame upande usiofaa na kutotazamia jambo lisilofaa. Hatutakuwa tukitazamia mahali ulipokuwa Megido wa kale katika nchi ya Israeli kulingana na jiografia. Hatutakuwa tukitazamia kuelekeana kwa majeshi yote ya mataifa huko yakiwa na lengo la kuishambulia Jamhuri ya Israeli. Hatutakuwa tukitazamia Wayahudi wote katika Jamhuri ya Israeli wageuzwe wamkubali Yesu wa Nazareti kama Masihi. Hatutaongozwa kuwa na maoni ya kwamba lazima tujipange pamoja na Wayahudi wa asili katika Jamhuri ya Israeli ili kuokoka katika upande wenye kushinda katika Har–​Magedoni. Bali, tutaona kwamba Bonde la Megido, ndiyo, Jamhuri ya Israeli yote, silo ulizo linalohusika. Tutayachunguza Maandiko yote matakatifu yaliyoongozwa na Mungu kwa bidii nasi tutaamua ulizo lenyewe hasa ni nini katika Har–​Magedoni, kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu. Ndipo tutakapojua tutasimama upande gani tupate kuokoka pamoja na washindi katika Har–​Magedoni halisi.

ULIZO KATIKA HAR-MAGEDONI

22. Ni nani wanaosonga leo kuelekea kwenye Har–​Magedoni halisi?

22 Na tusikosee; kuna mwendo wa kuelekea kwenye Har–​Magedoni halisi leo. Tuonapo ni akina nani wanaopiga mwendo kuelekea huko, twaweza kufahamu ulizo ni nini. Na tusome tena Ufunuo 16:14, NW, uliosema kwa unabii ni akina nani ambao wangepiga mwendo kuelekea kwenye Har–​Magedoni katika mahali pa kugeukia katika historia ya ulimwengu wote: “Kwa kweli, ni roho za mashetani hizo nazo zafanya ishara, nazo zawaendea wafalme wa dunia yote inayokaliwa na watu, zikawakusanye pamoja kwenye vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenye Nguvu Zote.”

23. (a) Kwamba kuna vita katika Har–​Magedoni yaonyesha nini, nayo itapiganwa na nani? (b) Basi, ulizo ni nini katika Har–​Magedoni, na kwa kadiri gani?

23 Uhakika wenyewe wa kwamba wanakusanywa pamoja kwenye vita waonyesha kwamba ulizo lahusika. Vita hiyo itapigwa kuliamua ulizo. Kwa kuwa hii ndiyo “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenye Nguvu Zote,” yamaanisha kwamba wako wale walio katika ulizo na Mungu Mwenye Nguvu Zote na watakao kuliamua pamoja na Yeye. Wafanyao ulizo naye na watakao kuamua mambo kwa vita watapoteza nini? Basi, tafadhali kiangalie cheo rasmi cha hawa kwa habari ya dunia yote inayokaliwa na watu. Wao ni watawala wa kisiasa, “wafalme wa dunia yote inayokaliwa na watu.” Falme zao zimo hatarini. Kuchochea kwao vita hii katika Har–​Magedoni ni kwa kusudi la kutetea utawala wao wa kisiasa, ufalme wao, hata kwa kutumia silaha. Kwa hiyo, basi, UFALME ndilo ulizo kuu katika Har–​Magedoni! Si “ufalme” juu ya Uingereza, si “ufalme” juu ya Thailand, si “ufalme” juu ya Sweden, bali “ufalme” juu ya “dunia yote inayokaliwa na watu.”

24. Kwa hiyo, ni maulizo gani yanayotokea juu ya kuacha mambo yakae kama yalivyo?

24 Lakini kwa sababu gani ufalme juu ya dunia yote inayokaliwa na watu ndio uwe ulizo katika Har–​Magedoni? Kwa sababu gani wafalme, marais na watawala wengine wa kisiasa wa dunia wafadhaishwe sasa na serikali yao inayoendelea kuwapo itiliwe mashaka? Ulimwengu wa wanadamu umechukuliana na watawala hawa wa kisiasa kwa muda mrefu sana, kwa kweli, kwa zaidi ya miaka elfu nne au tangu siku za Mfalme Nimrodi wa Babeli katika Mto Frati. Kwa hiyo, sababu gani kielelezo cha kisiasa cha serikali ya kidunia ambacho kimeendelea kuwapo kwa muda mrefu sana kisiachwe kiendelee tu kuwapo, mradi watu wenyewe wana nia ya kuchukuliana nacho au kuwa na uchaguzi wa kidemokrasi mara nyingi sana? Kwa sababu gani watu wasiachwe walau wajichagulie njia yao wenyewe katika habari hii? Sababu gani badiliko la ulimwengu liletwe juu ya utawala wa dunia? Je! ulimwengu haukupatwa na taabu ya kutosha kama ulivyo?

25. (a) Ni maulizo gani yanayotokea juu ya “badiliko” linalotamaniwa na wale waonao ni wakati wake’ (b) Lakini “wafalme wa dunia yote inayokaliwa na watu” wanasisitizia nini, na chini ya uongozi gani?

25 Walakini, watu wengi zaidi na zaidi leo wanasadiki kwamba “wakati wa badiliko umefika!” Lakini badiliko kutoka hali ya ulimwengu ya kiserikali iliyopo kwenda kwenye nini? Pia, je! wao wana umoja juu ya watakalofanya wafanyapo badiliko, nalo hili litafanywaje? Wajapokuwa wana wakili huyo ambaye amekuwapo kwa miaka 29 kwa ajili ya hatua ya mataifa yote, Umoja wa Mataifa, watu waliotiwa wasiwasi hawawezi kuachwa washughulikie kuleta “badiliko” la kitu kinachokubalika kwa wote, kitu kifaacho mahitaji yote ya wanadamu na kitakachoendelea kuwapo wakati wote ujao bila shaka. Zaidi ya hayo, kulingana na Ufunuo, sura ya kumi na sita, mstari wa kumi na nne, watawala wa kisiasa wanaotenda kwa sasa hawataki kabisa badiliko lenye amani. Wanasisitiza juu ya kulazimisha “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenye Nguvu Zote” ipigwe mpaka mwisho. Na majeshi makorofi yampitayo mwanadamu kwa uwezo yanawaunga mkono watawala hawa.

26. Kwa hiyo, lazima nini ipiganwe, na kwa sababu gani watu wengine wasingetaka kuisukumia mbali?

26 Kwa hiyo, lazima vita ipigwe. Haiwezi kuepukwa. Ni watu gani wenye ujuzi, wenye maoni ya Biblia, wangetaka kuisukumia mbali? Wanapendelea ushindi kwa upande ufaao. Wanatazamia kwa shauku badiliko la dunia yote inayokaliwa na watu litakaloifuata vita hiyo ya ulimwengu wote. Wakielekeana na nafasi inayotolewa kwa watu wa kizazi hiki, wao wangependa kuiokoka “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenye Nguvu Zote” na kushiriki katika mapendeleo mazuri sana katika kipindi cha baada ya vita.

27. Kwa sababu ya mambo ya hakika kuna haja gani ya hatua ifaayo sasa, na kwa uongozi na msaada gani?

27 Sasa hakuna hali ya kutokuwamo kwa habari ya vita inayokuja, itakayokuwa ya ulimwengu wote. Hatua ifaayo ni ya lazima sasa kabla vita hiyo haijatokea ili mtu ajikute katika upande wenye kushinda katika Har–​Magedoni. Ni kwa kupatikana akiwa katika upande huo kwa moyo wote tu mtu ye yote duniani awezavyo kuliona badiliko linalohitajiwa kwa haraka sana na uso wa dunia yetu. Yatupasa tuangalie ulizo ni nini na upande ulio wa haki katika ugomvi wenyewe ili tupate uongozi na msaada wa kuchukua hatua ifaayo sasa. Upande huo ndio utakaoshinda!

[Ramani katika ukurasa wa 175]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Mt. Carmel

R. Kishon

Harosheth

Nazareth

Mt Tabor

Kwa msaada wa Yehova, Baraka alilishinda jeshi la Sisera

MEGIDDO

Yoshua alimshinda mfalme wa Megido

Hill of Moreh

Well of Harod

Yehova alimpa Gideoni ushindi akiwa na wanaume 300 juu ya Wamidiani 120,000

[Picha katika ukurasa wa 173]

Mchoro wa mchoraji wa Megido wa kale

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki