Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • br78 kur. 3-5
  • Wao Ni Nani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wao Ni Nani?
  • Mashahidi wa Yehova Katika Karne ya 20
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINA LAO
  • Wao Ni Nani?
    Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini?
  • Mashahidi wa Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Jina la Mungu na “Agano Jipya”
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova Katika Karne ya 20
br78 kur. 3-5

Wao Ni Nani?

Mashahidi wa Yehova wanataka ufahamiane nao zaidi. Labda umekutana nao wakiwa majirani na wakiwa wafanya kazi wenzako au katika shughuli zozote za maisha ya kila siku. Labda umewaona barabarani, wakitoa magazeti yao kwa wapitaji. Au labda umesema kifupi nao mlangoni pako.

Kwa hakika, Mashahidi wa Yehova wanapendezwa na wewe na hali njema yako. Wanataka wawe marafiki wako na kukuambia mengi zaidi juu yao wenyewe, imani zao, tengenezo lao, na maoni yao juu ya watu na ulimwengu tunamoishi sote. Ili watimize kusudi hilo wamekutayarishia broshua hii.

Mashahidi wa Yehova wanafanana na watu wengine kwa njia nyingi. Wana matatizo yao​—ya kiuchumi, ya kimwili na ya kimoyoni. Wanakosea mara nyingine, maana si wakamilifu, si wenye kupuliziwa roho ya Mungu, wala si wasioweza kukosea kwa usemi. Lakini wanajaribu kujirekebisha kutokana na makosa ya zamani na kwa kujifunza Biblia kwa bidii ili wafanye masahihisho yanayotakwa. Wamejiweka wakfu kwa Mungu wafanye mapenzi yake, na wanajitahidi kutimiza wakfu huo. Wanatafuta mwongozo wa Neno la Mungu na wa roho takatifu yake katika utendaji wao wote.

Ni jambo la umaana mkubwa kwao kutegemeza imani zao juu ya Biblia si juu ya makisio ya kibinadamu tu wala itikadi za kidini. Wanahisi kama alivyohisi mtume Paulo aliposema hivi akiwa na upulizio wa Mungu: “Acheni Mungu apatikane kuwa wa kweli, ingawa kila mwanadamu apatikana kuwa mwongo.” (Warumi 3:4, New World Translation) Kwa habari ya mafundisho yanayotolewa kuwa kweli ya Kibiblia, wanaunga mkono kabisa mwendo uliofuatwa na Waberoya walipomsikia mtume Paulo akihubiri: “Walilipokea neno kwa bidii iliyo kubwa zaidi sana ya akili, wakiyachunguza kwa uangalifu Maandiko kila siku waone kama mambo hayo yalikuwa hivyo.” (Matendo 17:11, NW) Mashahidi wa Yehova huamini kwamba mafundisho yote ya kidini yamepasa yafanyiwe uchunguzi huo ili kuona kama yanapatana na Maandiko, hata kama fundisho linatolewa na wao au na mtu mwingine. Wanakukaribisha​—wanakusihi—​ufanye hivyo katika mazungumzo yako pamoja nao.

Kutokana na hayo ni wazi kwamba Mashahidi wa Yehova huamini Biblia ni Neno la Mungu. Huviona vitabu 66 vilivyomo kuwa vimepuliziwa na Mungu na ni sahihi kihistoria. Ile sehemu ambayo watu wengi huiita Agano Jipya wao huirejezea kuwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na Agano la Kale huliita Maandiko ya Kiebrania. Hutegemea Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki pia, na huyachukua jinsi yalivyo isipokuwa mahali ambapo semi au hali zaonyesha waziwazi kwamba ni za kitamathali au mfano. Wanaelewa kwamba unabii mwingi wa Biblia umetimizwa, mwingine unaendelea kutimizwa, na bado mwingine unatazamiwa kutimizwa.

JINA LAO

Mashahidi wa Yehova ati? Ndiyo, hivyo ndivyo wanavyojirejezea wenyewe. Ni jina linaloeleza mambo mengi, kuonyesha kwamba wanatoa ushahidi juu ya Yehova, Uungu wake, na makusudi yake. “Mungu,” “Bwana,” na “Muumba”—kama vile “Rais,” “Mfalme,” na “Jemadari”—ni vyeo vinavyoweza kutumiwa kuhusu watu mbalimbali mashuhuri. Lakini “Yehova” ni jina la kibinafsi na hurejezea Mungu mweza yote na Muumba wa ulimwengu wote mzima. Hilo laonyeshwa katika Zaburi 83:18: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, Ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”—Union Version ya Kiswahili ya United Bible Societies ya 1952.a

Jina Yehova (au Yahweh, kama Jerusalem Bible ya Roma Katoliki na wasomi fulani wa kisasa wanavyopendelea) huonekana karibu mara 7,000 katika Maandiko ya Kiebrania ya awali. Biblia nyingi hazilionyeshi kuwa hivyo, bali badala yalo hutumia “Mungu” au “Bwana.” Lakini, hata katika Biblia hizo kwa kawaida mtu anaweza kujua mahali ambapo Maandiko ya Kiebrania ya awali hutumia Yehova, kwa sababu mahali hapo maneno yaliyoandikwa badala ya jina hilo yako kwa herufi kubwa, zilizo nene na ndogo, kama hivi: MUNGU, BWANA. Tafsiri kadha za kisasa hutumia ama jina Yehova ama jina Yahweh. Kwa sababu hiyo, New World Translation inasomwa hivi katika Isaya 42:8, “Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu.”

Simulizi la Kimaandiko ambalo Mashahidi wa Yehova hutumia kwa jina lao liko katika sura ya 43 ya Isaya. Hapo tamasha ya ulimwengu inaonwa kuwa drama ya mahakamani: Vijimungu vya mataifa vinakaribishwa vitokeze mashahidi wavyo ili vithibitishe kesi zavyo za uadilifu vinazojidai kuwa nazo au viwasikie mashahidi wa upande wa Yehova na kukiri ile kweli. Humo Yehova ajulisha rasmi watu wake hivi: “Nyinywi mu mashahidi yangu anena Jehova, na mtumishi wangu ambae nimemtagua: illi mpate jua na kuniamini, na kufahamu kuwa mimi ndiye; kabula sijakuwapo mimi hakuumbwa Mngu awae yote, wala baada yangu hatakuwapo mwengine. Mimi, naam, mimi ni Jehova; tena zaidi ya mimi hapana mwokozi.”​—Isaya 43:10, 11, The Old Testament in Swahili (Mombasa), chapa ya 1949.

Yehova Mungu alikuwa na mashahidi duniani wakati wa maelfu ya miaka kabla ya Kristo. Baada ya kutoa orodha ya baadhi ya watu hao wenye imani katika Waebrania sura ya 11, Waebrania 12:1 husema: “Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu.” Yesu alisema hivi mbele ya Pontio Pilato: “Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli.” Yeye anaitwa “Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli.” (Yohana 18:37; Ufunuo 3:14) Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Nyinyi mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu nyinyi, na nyinyi mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Yudea yote na katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”​—Matendo 1:8, New World Translation.

Kwa sababu hiyo, leo watu zaidi ya 4,000,000 wanaotangaza habari njema za Ufalme wa Yehova kupitia Kristo Yesu katika mabara zaidi ya 200 wanahisi ni kwa kufaa wanajirejezea kuwa Mashahidi wa Yehova.

[Maelezo ya Chini]

a Manukuu ya Biblia katika broshua hii ni kutoka tafsiri hii, isipokuwa imetaarifiwa vingine.

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Wanapendezwa na wewe

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Wamejiweka wakfu wafanye mapenzi ya Mungu

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Wanaamini Biblia ni Neno la Mungu

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Jina la kibinafsi la Mungu katika Kiebrania cha kale

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Jina hilo kama linavyohusishwa na drama ya mahakamani

[Picha katika ukurasa wa 4]

Mashahidi zaidi ya 4,000,000 katika mabara zaidi ya 200

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki