Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jt kur. 3-5
  • Wao Ni Nani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wao Ni Nani?
  • Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINA LAO
  • Wao Ni Nani?
    Mashahidi wa Yehova Katika Karne ya 20
  • Mashahidi wa Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Jina la Mungu na “Agano Jipya”
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini?
jt kur. 3-5

Wao Ni Nani?

MASHAHIDI WA YEHOVA wanataka uwafahamu vizuri zaidi. Labda umewafahamu wakiwa majirani na wafanyakazi wenzako au umekutana nao katika hali nyinginezo za maisha ya kila siku. Labda umewaona barabarani, wakiwapa wapita-njia magazeti yao. Au labda umeongea nao kifupi mlangoni pako.

Mashahidi wa Yehova wanapendezwa na wewe na hali yako. Wanataka kuwa rafiki zako na kukuambia mengi zaidi juu yao wenyewe, imani yao, tengenezo lao, na maoni yao juu ya watu na ulimwengu tunamoishi sote. Wamekutayarishia broshua hii kwa kusudi hilo.

Mashahidi wa Yehova wanafanana na watu wengine kwa njia nyingi. Wana matatizo ya kawaida—ya kiuchumi, ya kimwili, na ya kihisia-moyo. Wanakosea mara nyingine, maana si wakamilifu, na wanayosema hayapuliziwi na roho ya Mungu moja kwa moja, wala si wasioweza kukosea. Lakini wanajaribu kujirekebisha kutokana na makosa ya zamani nao hujifunza Biblia kwa bidii ili wafanye marekebisho yanayotakiwa. Wamejiweka wakfu kwa Mungu wafanye mapenzi yake, na hujitahidi kutimiza wakfu huo. Wanatafuta mwongozo wa Neno la Mungu na wa roho takatifu yake katika utendaji wao wote.

Kutegemeza imani yao juu ya Biblia wala si juu ya makisio ya kibinadamu tu wala itikadi za kidini ni jambo muhimu kwao. Wana maoni kama ya mtume Paulo aliyesema hivi akiongozwa na Mungu: “Acheni Mungu apate kuonekana kuwa wa kweli, lakini kila binadamu apate kuonekana kuwa mwongo.” (Waroma 3:4, Tafsiri ya Ulimwengu Mpyaa) Kuhusu kweli za Biblia zinazofundishwa, Mashahidi huunga mkono kabisa mwendo uliofuatwa na Waberea walipomsikia mtume Paulo akihubiri: “Walilipokea neno kwa hamu ya akili iliyo kubwa zaidi sana, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo yalikuwa hivyo.” (Matendo 17:11) Mashahidi wa Yehova huamini kwamba mafundisho yote ya kidini yamepasa yachunguzwe hivyo ili kuona kama yanapatana na Maandiko yaliyopuliziwa, hata kama fundisho ni lao au la mtu mwingine. Wanakusihi ufanye hivyo katika mazungumzo yako pamoja nao.

Kutokana na hayo ni wazi kwamba Mashahidi wa Yehova wanaamini Biblia ni Neno la Mungu. Wao huviona vitabu 66 vilivyomo kuwa vimepuliziwa na Mungu na ni sahihi kihistoria. Ile sehemu ambayo watu wengi huiita Agano Jipya wao huiita Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na Agano la Kale wao huliita Maandiko ya Kiebrania. Wao hutegemea Maandiko ya Kigiriki na ya Kiebrania pia, nao huyachukua jinsi yalivyo isipokuwa mahali ambapo semi au hali zaonyesha waziwazi kwamba ni ya kitamathali au mfano. Wanaelewa kwamba unabii mwingi wa Biblia umetimizwa, mwingine unaendelea kutimizwa, na bado mwingine utatimizwa.

JINA LAO

Mashahidi wa Yehova? Ndiyo, hivyo ndivyo wanavyoitwa. Ni jina lenye maana, linaloonyesha kwamba wanatoa ushahidi juu ya Yehova, Uungu wake, na makusudi yake. “Mungu,” “Bwana,” na “Muumba”—kama vile “Rais,” “Mfalme,” na “Jemadari”—ni majina ya vyeo yanayoweza kutumiwa kuhusu watu mbalimbali mashuhuri. Lakini “Yehova” ni jina la kibinafsi nalo ni jina la Mungu mweza yote na Muumba wa ulimwengu wote. Hilo laonyeshwa katika Zaburi 83:18: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”

Jina Yehova (au Yahweh, kama vile Jerusalem Bible ya Katoliki na wasomi fulani wanavyopendelea) huonekana karibu mara 7,000 katika Maandiko ya awali ya Kiebrania. Biblia nyingi hazilitumii, bali hutumia “Mungu” au “Bwana.” Lakini, hata katika Biblia hizo kwa kawaida mtu anaweza kujua mahali ambapo maandishi ya awali ya Kiebrania hutumia Yehova, kwa sababu mahali hapo maneno yaliyoandikwa badala ya jina hilo yameandikwa kwa herufi kubwa, zilizo nene, kama hivi: MUNGU, BWANA. Tafsiri kadhaa za kisasa hutumia Yehova ama Yahweh. Kwa hiyo, New World Translation, inasema hivi katika Isaya 42:8, “Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu.”

Simulizi la Kimaandiko ambalo Mashahidi wa Yehova hutumia kwa jina lao liko katika sura ya 43 ya Isaya. Hapo tamasha ya ulimwengu inaonwa kama drama ya mahakamani: Miungu ya mataifa yaambiwa itokeze mashahidi wao ili ithibitishe madai yao ya uadilifu au iwasikie mashahidi wa upande wa Yehova na kukiri ile kweli. Humo Yehova ajulisha rasmi watu wake hivi: “Nyinywi mu mashahidi yangu anena Jehova, na mtumishi wangu ambae nimemtagua: illi mpate jua na kuniamini, na kufahamu kuwa mimi ndiye; kabula sijakuwapo mimi hakuumbwa Mngu awae yote, wala baada yangu hatakuwapo mwengine. Mimi, naam, mimi ni Jehova; tena zaidi ya mimi hapana mwokozi.”—Isaya 43:10, 11, The Old Testament in Swahili (Mombasa), chapa ya 1949.

Yehova Mungu alikuwa na mashahidi duniani kwa maelfu ya miaka kabla ya kuzaliwa kwa Yesu. Baada ya Waebrania sura ya 11 kuorodhesha baadhi ya watu hao wenye imani, Waebrania 12:1 husema: “Kwa hiyo, basi, kwa sababu tuna wingu kubwa hivyo la mashahidi likituzingira, acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” Yesu alisema hivi mbele ya Pontio Pilato: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” Yeye anaitwa “shahidi mwaminifu na wa kweli.” (Yohana 18:37; Ufunuo 3:14) Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu iwasilipo juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8.

Kwa hiyo, leo watu wapatao 6,000,000 wanaotangaza habari njema za Ufalme wa Yehova kupitia Kristo Yesu katika nchi zaidi ya 230 wanahisi kwamba wanaitwa Mashahidi wa Yehova kwa kufaa.

[Maelezo ya Chini]

a Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanatoka katika Biblia hii, na yale ya Maandiko ya Kiebrania yanatoka katika Union Version, chapa ya 1994.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Wamejiweka wakfu kwa Mungu wafanye mapenzi yake

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Wanaamini Biblia ni Neno la Mungu

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Jina hilo kama linavyohusishwa na drama ya mahakamani

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Mashahidi wapatao 6,000,000 katika nchi zaidi ya 230

[Picha katika ukurasa wa 3]

Wanapendezwa na wewe

[Picha katika ukurasa wa 4]

Jina la Mungu katika Kiebrania cha kale

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki