Njia Wanazotumia Wakuambie Habari Hizo
Wakristo wameamriwa ‘wakafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ lakini hiyo haina maana inawapasa kutumia mkazo wala kugeuza imani za wengine kwa nguvu. Agizo la Yesu lilikuwa ni ‘kuwahubiri wanyenyekevu habari njema,’ “kuwaganga waliovunjika moyo,” “kuwafariji wote waliao.” (Mathayo 28:19, New World Translation; Isaya 61:1, 2; Luka 4:18, 19) Mashahidi wa Yehova hufanya hivyo kwa kuzitangaza habari njema kutoka Biblia. Kama nabii Ezekieli wa kale, Mashahidi wa Yehova leo hujaribu kutafuta wale “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika.”—Ezekieli 9:4.
Njia bora zaidi wanayotumia ili wawaone wale wanaosumbuliwa na hali za sasa ni kwa kwenda nyumba kwa nyumba. Kwa njia hiyo wanajitahidi kihakika wafikie umma, kama vile Yesu alivyofanya alipokuwa “akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.” Wanafunzi wake wa mapema walifanya vivyo hivyo. (Luka 8:1; 9:1-6; 10:1-9) Leo, mahali inakowezekana, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kutembelea kila nyumba mara nyingi kwa mwaka, wakitaka kuzungumza na mwenye nyumba kwa dakika chache juu ya habari fulani ya mahali pao au ya ulimwengu wote yenye kupendeza au kuhangaisha. Huenda andiko moja au mawili yakatolewa yazungumzwe, na mwenye nyumba akionyesha kupendezwa, huenda Shahidi akafanya mpango wa kurudi wakati unaofaa ili kuzungumza zaidi. Biblia na vitabu vinavyoeleza juu ya Biblia vinatolewa, na mwenye nyumba akitaka, funzo la Biblia nyumbani linaongozwa bila malipo yoyote. Wakati wa 1990 wastani wa mafunzo ya Biblia yapatayo 3,624,091 yaliongozwa kikawaida ulimwenguni pote.
Njia nyingine ya kuwaambia wengine “habari njema za ufalme” ni kupitia mikutano inayofanywa katika Majumba ya Ufalme ya mahali walipo. Mashahidi wanaongoza mikutano humo kila juma. Mkutano mmoja ni mhadhara wa peupe juu ya habari ya sasa yenye kupendeza, ukifuatwa na funzo la habari au unabii wa Kibiblia, kwa kutumia gazeti la Mnara wa Mlinzi kuwa chanzo cha habari. Mkutano mwingine ni shule ya kuzoeza Mashahidi wawe watangazaji bora zaidi wa habari njema, ukifuatwa na sehemu inayoshughulikia kuzungumza juu ya kazi ya kutoa ushahidi katika eneo la kwao. Pia, mara moja kwa juma Mashahidi hukusanyika katika nyumba za faragha, wakiwa vikundi vidogo, ili wajifunze Biblia.
Watu wote wanakaribishwa kuhudhuria mikutano hiyo yote. Hakuna sadaka zinazotolewa wakati wowote. Mikutano hiyo ni yenye kunufaisha wote. Biblia yasema: “Tujitahidi kushughulikiana kwa ajili ya kuongezeana bidii ya kupendana na kutenda mema. Tusiache ile desturi ya kukutana pamoja, kama vile wengine wanavyofanya. Bali tunapaswa kusaidiana kwani, kama mwonavyo, Siku ile ya Bwana inakaribia.” Funzo la kibinafsi na uchunguzi wa habari ni mambo ya lazima, lakini kukutana na wengine ni kuhimizana: “Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.”—Waebrania 10:24, 25, Habari Njema kwa Watu Wote; Mithali 27:17.
Pia Mashahidi hutumia vizuri nafasi za kuzungumza juu ya habari njema wanapokutana na watu wengine katika maisha zao za kila siku. Labda yaweza kuwa maneno machache ya kuongea pamoja na jirani au pamoja na msafiri mwingine katika basi au eropleni (ndege), mazungumzo marefu zaidi pamoja na rafiki au mtu wa ukoo, au mazungumzo pamoja na mfanya kazi mwenzi wakati wa chakula cha mchana. Mwingi wa ushahidi aliotoa Yesu alipokuwa duniani ulikuwa wa aina hiyo—alipokuwa akitembea kando ya bahari, alipokuwa ameketi kando ya kilima, alipokuwa akila chakula nyumbani kwa mtu fulani, wakati wa arusi, au akisafiri katika mashua ya kuvulia samaki katika Bahari ya Galilaya. Alifundisha katika masinagogi na hekaluni Yerusalemu. Popote alipokuwa, alipata nafasi za kuzungumza juu ya Ufalme wa Mungu. Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuzifuata hatua zake kwa njia hiyo pia.—1 Petro 2:21.
KUHUBIRI KWA KIELELEZO
Hakuna yoyote ya njia hizo za kukuambia habari njema ingekuwa ya maana kwako ikiwa mwenye kukuambia hafuati mwenyewe mafundisho anayokupa. Kusema jambo moja na kufanya jingine ni unafiki, na unafiki wa kidini umeondoa mamilioni mbali na Biblia. Biblia hailaumiwi kwa haki. Waandishi na Mafarisayo walikuwa na Maandiko ya Kiebrania, lakini Yesu aliwalaumu vikali kuwa wanafiki. Alisema juu ya kusoma kwao kutoka Sheria ya Musa, kisha akaongeza kuwaambia wanafunzi hivi: “Yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi.” (Mathayo 23:3) Mkristo kuwa kielelezo cha maisha mema, hilo husema mengi zaidi ya saa nyingi za kuhubiri. Jambo hilo waliambiwa wake Wakristo waliokuwa na waume wasioamini: “Wavutwe kwa mwenendo wa wake zao, pasipo lile Neno; wakiutazama mwenendo wenu safi.”—1 Petro 3:1, 2.
Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hujaribu kupendekeza habari njema kwa wengine kwa njia hii pia: kwa kuwa vielelezo vyema katika mwenendo wa Kikristo wanaopendekezea wengine. Wao hujaribu ‘kuwatendea wengine kama vile wangetaka hao wawatendee.’ (Mathayo 7:12) Wao hujaribu kuwa hivyo kwa watu wote, si kwa Mashahidi wenzao, marafiki, majirani, au watu wa ukoo wao tu. Kwa vile si wakamilifu, si nyakati zote wanapofaulu kabisa kabisa kufanya hivyo. Lakini mioyo yao inataka sana kutendea watu wote mema, si kwa kuwaambia habari njema za Ufalme tu, bali pia kwa kutoa msaada iwezekanapo.—Yakobo 2:14-17.
[Blabu katika ukurasa wa 21]
Wavutwe pasipo neno
[Picha katika ukurasa wa 20]
Majumba ya Ufalme, yakiwa yamejengwa kwa kufaa, ni mahali pa mazungumzo ya Biblia
[Picha katika ukurasa wa 22]
Katika maisha yao wenyewe ya familia, na pia katika shughuli zao na watu wengine, Mashahidi hujaribu kwa moyo mweupe kutenda mambo wanayowafundisha wengine