Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jt kur. 19-21
  • Njia Wanazotumia Kuhubiri Habari Njema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Njia Wanazotumia Kuhubiri Habari Njema
  • Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUHUBIRI KUPITIA MFANO WAO
  • Njia Wanazotumia Wakuambie Habari Hizo
    Mashahidi wa Yehova Katika Karne ya 20
  • Ni Nani Wanaohubiri Habari Njema?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • “Habari Njema Lazima Zihubiriwe Kwanza”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Makundi Yametengenezwa kwa Ajili ya Kuhubiri Ufalme wa Mungu
    Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini?
jt kur. 19-21

Njia Wanazotumia Kuhubiri Habari Njema

WAKRISTO wameamriwa ‘wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ lakini hiyo haimaanishi kwamba wanapaswa kutumia mkazo wala kugeuza imani za wengine kwa nguvu. Utume wa Yesu ulikuwa ‘kuwahubiria wanyenyekevu habari njema,’ “kuwaganga waliovunjika moyo,” “kuwafariji wote waliao.” (Mathayo 28:19; Isaya 61:1, 2; Luka 4:18, 19) Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufanya hivyo kwa kuzitangaza habari njema za Biblia. Kama nabii Ezekieli wa kale, Mashahidi wa Yehova leo hujaribu kutafuta wale “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika.”—Ezekieli 9:4.

Njia bora zaidi wanayotumia ili wawaone wale wanaosumbuliwa na hali za sasa ni kwa kwenda nyumba kwa nyumba. Kwa njia hiyo wanajitahidi kihakika wafikie umma, kama vile Yesu alivyofanya alipoanza “kusafiri kutoka jiji hadi jiji na kutoka kijiji hadi kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.” Wanafunzi wake wa mapema walifanya vivyo hivyo. (Luka 8:1; 9:1-6; 10:1-9) Leo, mahali inapowezekana, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kutembelea kila nyumba mara kadhaa kwa mwaka, wakitaka kuzungumza na mwenye nyumba kwa dakika chache juu ya habari fulani ya kwao au ya ulimwengu wote yenye kupendeza au kuhangaisha. Huenda andiko moja au mawili yakatolewa yazungumzwe, na mwenye nyumba akipendezwa, huenda Shahidi akafanya mpango wa kurudi wakati unaofaa ili kuzungumza zaidi. Biblia na vitabu vinavyoeleza juu ya Biblia hutolewa, na mwenye nyumba akitaka, funzo la Biblia la nyumbani huongozwa bila malipo. Mamilioni ya mafunzo hayo ya Biblia yenye kusaidia watu huongozwa kwa ukawaida pamoja na watu mmoja-mmoja na familia ulimwenguni kote.

Njia nyingine ya kuwaambia wengine “habari njema ya ufalme” ni kupitia mikutano inayofanywa katika Majumba yao ya Ufalme. Mashahidi huongoza mikutano humo kila juma. Mkutano mmoja ni hotuba ya watu wote juu ya habari yenye kupendeza ya karibuni, ukifuatwa na funzo la habari au unabii wa Biblia, kwa kutumia gazeti la Mnara wa Mlinzi kuwa chanzo cha habari. Mkutano mwingine ni shule ya kuzoeza Mashahidi wawe watangazaji bora zaidi wa habari njema, ukifuatwa na sehemu ya kuzungumzia kazi ya kutoa ushahidi katika eneo la kwao. Pia, mara moja kwa juma Mashahidi hukusanyika katika nyumba za faragha, wakiwa vikundi vidogo, ili wajifunze Biblia.

Watu wote wanakaribishwa kuhudhuria mikutano hiyo yote. Hakuna sadaka zinazokusanywa wakati wowote. Mikutano hiyo hunufaisha watu wote. Biblia yasema hivi: “Na acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” Funzo la kibinafsi na kufanya utafiti ni mambo ya lazima, lakini kukutana na wengine huchangamsha: “Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.”—Waebrania 10:24, 25; Mithali 27:17.

Pia Mashahidi hutumia vizuri fursa za kuzungumza juu ya habari njema wanapokutana na watu wengine katika shughuli zao za kila siku. Huenda ni maneno machache ya kuongea pamoja na jirani au pamoja na msafiri mwingine katika basi au ndege, mazungumzo marefu zaidi pamoja na rafiki au mtu wa ukoo, au mazungumzo pamoja na mfanyakazi mwenzi wakati wa chakula cha mchana. Mwingi wa ushahidi aliotoa Yesu alipokuwa duniani ulikuwa wa aina hiyo—alipokuwa akitembea kando ya bahari, alipokuwa ameketi kando ya kilima, alipokuwa akila chakula nyumbani kwa mtu fulani, wakati wa arusi, au akisafiri katika mashua ya kuvulia samaki katika Bahari ya Galilaya. Alifundisha katika masinagogi na hekaluni Yerusalemu. Popote alipokuwa, alipata nafasi za kuzungumza juu ya Ufalme wa Mungu. Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuzifuata hatua zake kwa njia hiyo pia.—1 Petro 2:21.

KUHUBIRI KUPITIA MFANO WAO

Hakuna yoyote ya njia hizo za kukuambia habari njema ingekuwa ya maana kwako ikiwa mwenye kukuambia hafuati mwenyewe mambo anayokufundisha. Kusema jambo moja na kufanya kinyume ni unafiki, na unafiki wa kidini umeondoa mamilioni mbali na Biblia. Biblia hailaumiwi kwa haki. Waandishi na Mafarisayo walikuwa na Maandiko ya Kiebrania, lakini Yesu aliwashutumu vikali kuwa wanafiki. Alisema juu ya kusoma kwao Sheria ya Musa, kisha akaongeza kuwaambia wanafunzi hivi: “Mambo yote wawaambiayo nyinyi, yafanyeni na kuyashika, lakini msifanye kulingana na vitendo vyao, kwa maana wao husema lakini hawafanyi.” (Mathayo 23:3) Mkristo kuwa kielelezo cha maisha mema, husadikisha zaidi kuliko saa nyingi za kuhubiri. Hivyo ndivyo wake Wakristo waliokuwa na waume wasioamini walivyoambiwa hivi: “Wapate kuvutwa bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kuwa mashahidi wa kujionea mwenendo wenu ulio safi kiadili.”—1 Petro 3:1, 2.

Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hujaribu kupendekeza habari njema kwa wengine kwa njia hii pia: kwa kuwa vielelezo vyema katika mwenendo wa Kikristo wanaopendekezea wengine. Wao hujaribu ‘kuwatendea wengine kama vile wangetaka hao wawatendee.’ (Mathayo 7:12) Wao hujaribu kuwa hivyo kwa watu wote, si kwa Mashahidi wenzao, marafiki, majirani, au watu wa ukoo wao tu. Kwa vile si wakamilifu, hawafaulu kabisa kabisa nyakati zote kufanya hivyo. Lakini mioyo yao inataka sana kutendea watu wote mema, si kwa kuwaambia habari njema za Ufalme tu, bali pia kwa kutoa msaada iwezekanapo.—Yakobo 2:14-17.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Hawaii

[Picha katika ukurasa wa 19]

Venezuela

[Picha katika ukurasa wa 19]

Yugoslavia

[Picha katika ukurasa wa 20]

Majumba ya Ufalme, yakiwa yamejengwa ifaavyo, ni mahali pa mazungumzo ya Biblia

[Picha katika ukurasa wa 21]

Katika maisha yao ya familia, na katika shughuli zao na watu wengine, Mashahidi hujaribu kwa moyo mweupe kutenda mambo wanayowafundisha wengine

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki