Thamani Yenye Kutumika ya Habari Njema kwa Jumuiya Yenu
Katika ulimwengu huu wa leo mara nyingi twasikia rai hii ikitolewa: “Kanuni za Ukristo hazitumiki. Haziwezi kufanya kazi katika jamii ya leo yenye mambo magumu.” Lakini, katika mazungumzo fulani yaliyoripotiwa kati ya Mohandas K. Gandhi kiongozi wa Wahindu pamoja na aliyekuwa Mwakilishi wa Uingereza katika India, Lord Irwin, maoni tofauti sana yalitolewa. Lord Irwin alimwuliza Gandhi alifikiri ni nini kingetatua matatizo kati ya Uingereza na India. Gandhi alichukua Biblia akafungua sura ya tano ya Mathayo, akasema: “Wakati nchi yako na yangu zitakapopatana juu ya mafundisho yaliyotolewa na Kristo katika haya Mahubiri ya Mlimani, hatutakuwa tumetatua matatizo ya nchi zetu tu, bali pia yale ya ulimwengu mzima.”
Mahubiri hayo yanasema juu ya kutafuta ukiroho na kuwa mwenye tabia pole, mwenye amani, mwenye rehema, mpenda uadilifu. Yanalaumu sana si uuaji wa kukusudia tu bali pia kukasirikia wengine, si uzinzi tu bali pia mawazo yenye tamaa mbaya. Yanapinga matendo ya talaka za ovyo-ovyo zinazovunja nyumba na kufanya watoto wapate taabu. Yanatuambia hivi: ‘Wapendeni hata wale wasiowapenda ninyi, wenye uhitaji wapeni, acheni kuhukumu wengine bila rehema, watendee wengine kama vile ungetaka kutendewa.’ Ushauri wote huo, ukifuatwa, ungeleta manufaa kubwa sana. Kadiri kunavyokuwa watu wengi zaidi katika jumuiya yenu wanaoyatenda, ndivyo jumuiya yenu inavyokuwa bora zaidi!
Mashahidi wa Yehova ni uvutano wa kuelekea upande huo. Biblia inawafundisha kustahi ndoa. Watoto wao wanazoezwa katika kanuni njema. Umaana wa familia unatiliwa mkazo. Familia zenye umoja ni manufaa kwa jumuiya yenu, hata kwa taifa lenu. Historia imejaa vielelezo vya serikali za ulimwengu zilizoanguka wakati vifungo vya kifamilia vilipokosa nguvu na ukosefu wa adili ukaongezeka. Kadiri watu mmoja mmoja na familia ambazo Mashahidi wa Yehova wanazivuta kuishi kwa kanuni za Kikristo zinavyokuwa nyingi zaidi, ndivyo makosa, ukosefu wa adili, na uhalifu utakavyopunguka katika jumuiya yenu.
Mojawapo matatizo yaliyo makubwa yanayosumbua jumuiya nyingi na mataifa ni ubaguzi wa rangi. Tofauti na hivyo, mtume Petro alisema: “Nimetambua kwamba hakika Mungu hana ubaguzi. Mtu wa taifa lo lote anayemcha Mungu na kutenda yaliyo haki anapokelewa naye.” Na Paulo aliandika hivi: “Hakuna tena tofauti kati ya Myahudi na Mgiriki, mtumwa na mtu huru, mwanamume na mwanamke. Nyote ni kitu kimoja katika kuungana na Kristo Yesu.” (Matendo 10:34, 35; Wagalatia 3:28, Habari Njema kwa Watu Wote) Mashahidi wa Yehova wanakubali hilo. Makabila na watu wa rangi zote huishi na kufanya kazi pamoja katika makao makuu yao ya ulimwengu, katika matawi yao, na katika makundi.
Katika Afrika makabila fulani hayawezi kuchangamana pamoja bila kukosana. Hata hivyo, katika makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova, utaona huko watu wa makabila mengi mbalimbali wakila, wakilala, na kuabudu pamoja kwa upatano kabisa na ushirika mchangamfu. Maofisa wa serikali hustaajabu wanapoona hivyo. Kielelezo kimoja cha tokeo lenye kuunganisha la Ukristo wa kweli kilielezwa na Amsterdam News la New York la Agosti 2, 1958. Kilichofanya maelezo hayo yatolewe ni kutazama lile kusanyiko la mataifa yote lililotangulia kutajwa ambako Mashahidi zaidi ya robo milioni walikusanyika katika Jiji la New York.
“Kila mahali Wanegro, weupe na watu wa nchi za Mashariki, kutoka vyeo vyote maishani na sehemu zote za ulimwengu, walichangamana pamoja kwa furaha na uhuru. . . . Mashahidi waabuduo kutoka mabara 120 wameishi na kuabudu pamoja kwa amani, wakawaonyesha Waamerika jinsi hilo linavyowezekana kwa urahisi. . . . Kusanyiko hilo ni kielelezo bora sana cha kuonyesha jinsi watu wanavyoweza kufanya kazi na kuishi pamoja.”
Huenda wengi wakasema kwamba kanuni za Ukristo hazitumiki katika ulimwengu huu wa kisasa. Lakini, ni jambo gani kuliko hilo ambalo limefanya kazi au litakalofanya kazi? Kanuni za Kikristo zaweza kuwa zenye faida halisi kwa jumuiya yenu sasa, nazo zitakuwa ndio msingi wa kuunganisha ‘mataifa yote, kabila, na jamaa’ duniani pote chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu utakaotawala ainabinadamu.—Ufunuo 7:9, 10.
[Blabu katika ukurasa 24]
Mataifa yote na watu wa rangi zote hufanya kazi pamoja
[Blabu katika ukurasa 24]
Ukristo unatumika. Ni jambo gani zaidi ya huo ambalo limefaa?