Manufaa ya Habari Njema Katika Jumuiya Yenu
ULIMWENGUNI leo, mara nyingi twasikia maoni haya yakitolewa: “Kanuni za Ukristo hazitumiki. Haziwezi kamwe kutumika katika jamii ya leo yenye mambo magumu.” Lakini, katika mazungumzo fulani yaliyoripotiwa kati ya Mohandas K. Gandhi kiongozi wa Wahindu pamoja na aliyekuwa Mwakilishi wa Uingereza nchini India, Lord Irwin, maoni tofauti sana yalitolewa. Yasemekana kwamba Lord Irwin alimwuliza Gandhi maoni yake kuhusu kinachoweza kutatua matatizo kati ya Uingereza na India. Gandhi alichukua Biblia akafungua sura ya tano ya Mathayo, akasema: “Nchi yako na yangu zitakapopatana juu ya mafundisho yaliyotolewa na Kristo katika Mahubiri haya ya Mlimani, hatutakuwa tumetatua matatizo ya nchi zetu tu, bali pia yale ya ulimwengu mzima.”
Mahubiri hayo yanasema juu ya kutafuta hali ya kiroho na kuwa mwenye tabia pole, mwenye amani, mwenye rehema, mpenda-uadilifu. Yanalaumu sana si uuaji wa kukusudia tu bali pia kukasirikia wengine, si uzinzi tu bali pia mawazo yenye tamaa mbaya. Yanapinga matendo ya talaka za ovyo-ovyo zinazovunja nyumba na kuwataabisha watoto. Yanatuambia hivi: ‘Wapendeni hata wale wasiowapenda ninyi, wenye uhitaji wapeni, acheni kuhukumu wengine bila rehema, watendee wengine kama vile ungetaka kutendewa.’ Ushauri wote huo, ukifuatwa, waweza kuleta manufaa makubwa sana. Kadiri kunavyokuwa watu wengi zaidi katika jumuiya yenu wanaoyatenda, ndivyo jumuiya yenu inavyokuwa bora!
Mashahidi wa Yehova huwahimiza watu wafuate ushauri huo. Biblia inawafundisha kustahi ndoa. Watoto wao wanazoezwa kanuni njema. Umaana wa familia unakaziwa. Familia zenye umoja ni manufaa kwa jumuiya yenu, hata kwa taifa lenu. Historia imejaa vielelezo vya serikali za ulimwengu zilizoanguka wakati vifungo vya kifamilia vilipodhoofika na ukosefu wa adili ukaongezeka. Kadiri watu mmoja-mmoja na familia ambazo Mashahidi wa Yehova wanazivuta kuishi kwa kanuni za Kikristo zinavyokuwa nyingi zaidi, ndivyo makosa, ukosefu wa adili, na uhalifu utakavyopunguka katika jumuiya yenu.
Mojawapo matatizo makubwa yanayokumba jumuiya nyingi na mataifa mengi ni ubaguzi wa rangi. Tofauti na hivyo, mtume Petro alisema: “Nahisi kwamba Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” Naye Paulo aliandika hivi: “Hakuna Myahudi wala Mgiriki, hakuna mtumwa wala mtu huru, hakuna wa kiume wala wa kike; kwa maana nyinyi nyote ni mtu mmoja katika muungano na Kristo Yesu.” (Matendo 10:34, 35; Wagalatia 3:28) Mashahidi wa Yehova wanakubali hilo. Makabila na watu wa rangi zote huishi na kufanya kazi pamoja katika makao yao makuu ya ulimwengu, katika ofisi zao za tawi, na katika makutaniko.
Katika Afrika makabila fulani hayawezi kuchangamana pamoja bila kukosana. Hata hivyo, katika makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova, utaona huko watu wa makabila mengi mbalimbali wakila, wakilala, na kuabudu pamoja kwa upatano kabisa na ushirika mchangamfu. Maofisa wa serikali hustaajabu wanapoona hivyo. Kielelezo kimoja cha tokeo la kuunganisha na Ukristo wa kweli kilitajwa na Amsterdam News la New York la Agosti 2, 1958. Kilichofanya maelezo hayo yatolewe ni kutazama lile kusanyiko la kimataifa lililotangulia kutajwa ambako Mashahidi zaidi ya robo milioni walikusanyika New York City.
“Kila mahali Waafrika, Wazungu na watu wa Mashariki, kutoka tabaka zote maishani na sehemu zote za ulimwengu, walichangamana pamoja kwa furaha na uhuru. . . Mashahidi waabuduo kutoka nchi 120 wameishi na kuabudu pamoja kwa amani, wakawaonyesha Wamarekani jinsi hilo linavyowezekana kwa urahisi. . . . Kusanyiko hilo ni kielelezo bora sana cha kuonyesha jinsi watu wanavyoweza kufanya kazi na kuishi pamoja.”
Huenda watu wengi wakasema kwamba kanuni za Ukristo hazitumiki katika ulimwengu huu wa leo. Lakini, ni jambo gani kuliko hilo ambalo limefanya kazi au litakalofanya kazi? Kanuni za Kikristo zaweza kuwa zenye faida halisi zikitumiwa katika jumuiya yenu sasa, nazo zitakuwa ndio msingi wa kuunganisha ‘mataifa yote, makabila, na vikundi vya watu’ duniani pote chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu utakaotawala wanadamu.—Ufunuo 7:9, 10.
[Blabu katika ukurasa wa 23]
Watu wa jamii zote na wa rangi zote hufanya kazi pamoja
[Blabu katika ukurasa wa 24]
Ukristo unatumika. Ni jambo gani zaidi ya huo ambalo limefaa?