Maulizo Yanayoulizwa Mara Nyingi na Watu Wenye Kupendezwa
Maulizo fulani hutokea mara nyingi sana kuliko mengine. Machache ya hayo yamezungumzwa hapa.
Ikiwa Mungu ni upendo, sababu gani anaruhusu uovu?
Mungu huruhusu uovu, na mamilioni duniani wanauzoea kwa makusudi. Kwa mfano, wanatangaza vita, wanaangusha makombora juu ya watoto, wanaichoma dunia, na kusababisha njaa nyingi. Mamilioni huvuta sigara na kupata kansa ya mapafu, huzoea uzinzi na kupata kaswende na kisonono, hunywa pombe kupita kiasi na kupata ugonjwa wa ini, na kadhalika. Kwa kweli watu kama hao hawataki uovu wote ukomeshwe. Wanachotaka tu ni kwamba adhabu zinazotokana na uovu huo ziondolewe. Wanapovuna kile ambacho wamepanda, wanaomboleza wakisema, “Mbona iwe mimi?” Nao humlaumu Mungu, kama Mithali 19:3 inavyosema: “Upumbavu wa mwanadamu mwenyewe unaharibu maisha yake, kisha anamwonea BWANA kinyongo.” (The New English Bible) Na kama Mungu angezuia maovu yao wangepinga wakisema wananyimwa uhuru wao wa kuyafanya!
Sababu kubwa inayomfanya Yehova aruhusu uovu ni ili ajibu dai la Shetani. Shetani Ibilisi alisema Mungu hangeweza kuweka duniani binadamu ambao wangekuwa waaminifu kwake Yeye wakiwa katika mtihani. (Ayubu 1:6-12; 2:1-10) Yehova amemruhusu Shetani abaki ili awe na nafasi ya kuthibitisha dai lake. (Linganisha Kutoka 9:16.) Shetani anaendelea kuleta ole mwingi sasa, ili afanye wanadamu wampinge Mungu, anapojaribu kuthibitisha dai lake. (Ufunuo 12:12) Lakini, Ayubu alishika uaminifu mkamilifu. Ndivyo na Yesu. Wakristo wa kweli sasa wanashika uaminifu mkamilifu.—Ayubu 27:5; 31:6; Mathayo 4:1-11; 1 Petro 1:6, 7.
Mimi ningependa kuamini paradiso ya kidunia ambamo watu wataishi milele, lakini je! hilo si jambo linalosikika kuwa si halisi?
Si kulingana na Biblia. Linasikika kuwa si halisi kwa sababu tu ainabinadamu imeyajua mabaya kwa karne nyingi sana. Yehova aliiumba dunia na kuambia ainabinadamu iijaze wanaume na wanawake waadilifu ambao wangetunza mimea na wanyama wayo na kuhifadhi uzuri wayo badala ya kuiharibu. (Tazama kurasa 12 na 17.) Badala ya paradiso hiyo iliyoahidiwa kusikika kuwa si halisi, hali ya sasa yenye kujaa huzuni ndiyo isiyo ya halisi kuweza kuruhusiwa iendelee. Paradiso itachukua mahali payo.
Kuziamini ahadi hizo si imani bila msingi. “Imani, chanzo chake ni kusikia.” Kwa kujifunza Neno la Mungu, hekima yalo inaonekana wazi na imani inakua.—Warumi 10:17; Waebrania 11:1.
Naweza kuwajibuje watu wanaodhihaki na kusema Biblia ni ngano na si ya kisayansi?
Akiolojia (uchimbuzi wa vitu vya kale) ya Kibiblia yathibitisha mambo mengi ya usahihi wa kihistoria wa Biblia. Sayansi ya kweli inapatana na Biblia. Mambo ya hakika yafuatayo yalikuwa katika Biblia zamani sana kabla hayajavumbuliwa na wasomi wa kilimwengu: mfuatano wa hatua zilizochukuliwa katika kutengenezwa kwa dunia, kwamba dunia ni mviringo, kwamba inaning’inia angani pasipo kitu cha kuegemea, na kwamba ndege huhama.—Mwanzo, sura 1; Isaya 40:22; Ayubu 26:7; Yeremia 8:7.
Kupuliziwa kwa Biblia na Mungu kwaonyeshwa na utimizo wa unabii mwingi. Danieli alitabiri mapema kusimama na kuanguka kwa serikali za ulimwengu, na pia wakati ambapo Mesiya angekuja na kuuawa. (Danieli, sura za 2, 8; 9:24-27) Leo, unabii mwingine mwingi ungali unatimizwa, ukitambulisha hizi kuwa ni “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo, sura 24) Binadamu hana uwezo huo wa kujua mambo kimbele. (Isaya 41:23) Kwa uhakikisho zaidi, ona vitabu vya Watch Tower Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? na Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?
Naweza kuwaje na uwezo wa kujibu maulizo juu ya Biblia?
Ni lazima ujifunze Biblia na kuitafakari, na wakati uo huo umwombe Mungu roho yake ikuelekeze. (Mithali 15:28; Luka 11:9-13) “Mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima,” Biblia yasema, “na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei.” (Yakobo 1:5) Pia, kuna misaada ya kujifunza Biblia inayofaa ambayo unaweza kupata habari kwayo. Kwa kawaida msaada kutoka kwa wengine unahitajiwa, kama wakati Filipo alipojifunza pamoja na yule Mwethiopia. (Matendo 8:26-35) Mashahidi wa Yehova huongoza mafunzo ya Biblia kwa watu wenye kupendezwa katika nyumba zao bila malipo. Jione huru kuomba utumishi huo.
Sababu gani wengi hupinga Mashahidi wa Yehova na kuniambia nisijifunze nao?
Mahubiri ya Yesu yalipingwa, na alisema kwamba wafuasi wake pia wangepingwa. Wengine walipovutwa na fundisho la Yesu, wapinzani wa kidini walijibu vikali wakisema: “Je! ninyi nanyi mmedanganyika? Ni nani katika wakuu amwaminiye, au katika Mafarisayo?” (Yohana 7:46-48; 15:20) Wengi wanaokuambia usijifunze na Mashahidi ama hawajui vizuri habari zao ama wana chuki isiyo na msingi. Jifunze na Mashahidi ujionee mwenyewe kama ufahamu wako wa Biblia utaongezeka au sivyo.—Mathayo 7:17-20.
Sababu gani Mashahidi hutembelea watu walio na dini yao wenyewe?
Kwa kufanya hivyo wanafuata kielelezo cha Yesu. Yeye aliwaendea Wayahudi. Wayahudi walikuwa na dini yao wenyewe, lakini ilikuwa imewapotoa wakaliacha Neno la Mungu kwa njia nyingi. (Mathayo 15:1-9) Mataifa yote yana dini za aina fulani, yawe ni yale yanayoitwa ya Kikristo au yasiyo ya Kikristo. Ni jambo la maana sana watu washikilie imani zinazopatana na Neno la Mungu mwenyewe, na jitihada za Mashahidi kuwasaidia wafanye hivyo zinakuwa wonyesho wa kupenda jirani.
Je! Mashahidi huamini kwamba dini yao tu ndiyo ya kweli?
Yeyote asiyefanya mchezo na dini yake amepaswa afikiri kwamba ndiyo ya kweli. Ama sivyo, sababu gani yeye, awe ni mwanamume au mwanamke, ajishughulishe nayo? Wakristo wanaonywa kwa upole hivi: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana kilicho chema.” (1 Wathesalonike 5:21, New World Translation) Imempasa mtu ahakikishe kwamba imani zake zaweza kuungwa mkono na Maandiko, maana kuna imani moja tu ya kweli. Andiko la Waefeso 4:5 lathibitisha hivyo, likitaja “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.” Yesu hakukubaliana na maoni ya kisasa yenye uzembe ya kwamba kuna barabara nyingi, dini nyingi, zote zikiongoza kwenye wokovu. Badala yake, alisema: “Mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.” Mashahidi wa Yehova huamini kwamba wameiona. Ama sivyo, wangetafuta dini nyingine.—Mathayo 7:14.
Je! wao huamini kwamba ni wao tu watakaookoka?
Sivyo. Mamilioni wengi ambao wameishi katika karne zilizopita na ambao hawakuwa Mashahidi wa Yehova watarudi kufufuliwa wapate nafasi ya kuwa na uhai. Wengi wanaoishi sasa bado wanaweza kukubali kweli na uadilifu kabla ya “dhiki kubwa,” nao watapata wokovu. Isitoshe, Yesu alisema kwamba haitupasi kuhukumiana. Sisi hutazama sura ya nje; Mungu hutazama moyo. Yeye huona bila kukosea na huhukumu kwa rehema. Amemkabidhi Yesu jukumu la kuhukumu, si sisi.—Mathayo 7:1-5; 24:21.
Wale wanaohudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova wanatazamiwa kutoa michango gani ya kifedha?
Kwa habari ya michango ya fedha, mtume Paulo alisema: “Kila mmoja, basi, na atoe kadiri alivyoamua, kwa moyo na wala si kwa huzuni au kwa kulazimishwa, maana Mungu humpenda yule mwenye kutoa kwa furaha.” (2 Wakorinto 9:7, Habari Njema kwa Watu Wote) Hakuna sadaka zinazotozwa kwenye Majumba ya Ufalme wala kwenye majumba ya mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Visanduku huwekwa mahali panapofaa ili yeyote anayetaka atoe mchango. Hakuna mtu anayejua ni kitu gani wanachotoa wale wengine. Wengine wana uwezo wa kutoa zaidi ya wengine; huenda wengine wasiweze kutoa chochote. Yesu alionyesha maoni yanayofaa alipoeleza juu ya kisanduku cha hazina hekaluni katika Yerusalemu na wale waliokuwa wakitoa michango: Jambo la maana ni uwezo na roho ya mtu ya kutoa, si wingi wa fedha.—Luka 21:1-4.
Endapo nawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, je! ningetazamiwa kuhubiri kama wao?
Mtu anapojawa na maarifa ya kujua kuna Paradiso ya kidunia iliyoahidiwa chini ya Ufalme wa Kristo, anataka kuyashiriki pamoja na wengine. Wewe utafanya hivyo pia. Ni habari njema!—Matendo 5:41, 42.
Kufanya hivyo ni njia ya maana ya kuonyesha kwamba wewe ni mwanafunzi wa Yesu Kristo. Katika Biblia, Yesu anaitwa “shahidi aliye mwaminifu na wa kweli.” Alipokuwa duniani alihubiri akisema: “Ufalme wa mbinguni umekaribia,” naye aliwatuma wanafunzi wake wakafanye vivyo hivyo. (Ufunuo 3:14; Mathayo 4:17; 10:7) Baadaye, Yesu aliamuru wafuasi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote . . . kuwafundisha.” Vilevile alitabiri kwamba, kabla ya mwisho, “habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ushahidi kwa mataifa yote.”—Mathayo 28:19, 20; 24:14, New World Translation.
Kuna njia nyingi za kujulisha rasmi habari njema hizi. Mara nyingi kuongea na rafiki na wale tunaojuana nao hutoa nafasi ya kufanya hivyo. Wengine hufanya hivyo kwa kuandika barua au kwa kutumia simu. Wengine wanapeleka kwa posta vitabu vilivyo na habari wanayoona yule wanaojuana naye angependezwa sana nayo. Kwa kutotaka kumwacha yeyote, Mashahidi huenda mlango kwa mlango wakiwa na ujumbe huo.
Biblia ina mwaliko huu wenye uchangamshi: “Roho na Bibi arusi wasema, ‘Njoo!’ kila mtu asikiaye hilo, na aseme, ‘Njoo!’ Kisha, ye yote aliye na kiu na aje; anayetaka maji ya uzima na apokee bila malipo yo yote.” (Ufunuo 22:17, Habari Njema kwa Watu Wote) Kuwaambia wengine juu ya dunia-Paradiso na baraka zayo kwapasa kufanywe kwa moyo wa kupenda, kutoka moyo uliojaa kutaka kushiriki habari njema hizi pamoja na wengine.
Tuna hakika unayo maulizo mengine juu ya Mashahidi wa Yehova na imani zao. Labda baadhi yayo ni yenye kutokeza ubishi. Tungetaka kuyajibu. Nafasi ni ndogo katika broshua hii; hivyo twakualika uwaulize Mashahidi wa kwenu maulizo hayo, ama katika mikutano yao kwenye Jumba la Ufalme au wanapokutembelea nyumbani mwako. Au, labda upeleke maulizo yako kwa Watch Tower Society, kwenye ofisi ya tawi iliyo karibu zaidi na wewe; ona orodha iliyo chini.