Maswali Ambayo Huulizwa Mara Nyingi na Watu Wenye Kupendezwa
Ikiwa Mungu ni upendo, sababu gani anaruhusu uovu?
MUNGU huruhusu uovu, na mamilioni ya watu duniani wanautenda kwa makusudi. Kwa mfano, wanatangaza vita, wanarushia watoto mabomu, wanaichoma dunia, na kusababisha njaa kubwa. Mamilioni ya watu huvuta sigara na kupata kansa ya mapafu, hufanya uzinzi na kupata maradhi yanayopitishwa kingono, hunywa pombe kupita kiasi na kupata ugonjwa wa ini, na kadhalika. Kwa kweli watu kama hao hawataki uovu wote ukomeshwe. Wanachotaka tu ni kwamba adhabu zinazotokana na uovu huo ziondolewe. Wanapovuna kile ambacho wamepanda, wanaomboleza wakisema, “Mbona iwe mimi?” Nao humlaumu Mungu, kama Mithali 19:3 inavyosema: “Upumbavu wa mtu hupotosha njia yake; na moyo wake hununa juu ya BWANA.” Na kama Mungu angezuia maovu yao wangepinga wakisema wananyimwa uhuru wao wa kuyafanya!
Sababu kubwa inayomfanya Yehova aruhusu uovu ni ili ajibu dai la Shetani. Shetani Ibilisi alisema Mungu hangeweza kuweka duniani binadamu ambao wangekuwa waaminifu kwake Yeye wakiwa katika mtihani. (Ayubu 1:6-12; 2:1-10) Yehova amemruhusu Shetani abaki ili awe na nafasi ya kuthibitisha dai lake. (Kutoka 9:16) Shetani anaendelea kuleta ole mwingi sasa, ili afanye wanadamu wampinge Mungu, anapojaribu kuthibitisha dai lake. (Ufunuo 12:12) Lakini, Ayubu alishika uaminifu-maadili. Ndivyo na Yesu. Wakristo wa kweli sasa wanashika uaminifu-maadili.—Ayubu 27:5; 31:6; Mathayo 4:1-11; 1 Petro 1:6, 7.
Mimi ningependa kuamini paradiso ya kidunia ambamo watu wataishi milele, lakini je! hilo si jambo lisiloaminika?
Si kulingana na Biblia. Haiaminiki, kwa sababu tu wanadamu wamepatwa na mabaya kwa karne nyingi sana. Yehova aliiumba dunia na kuambia wanadamu waijaze wanaume na wanawake waadilifu ambao wangetunza mimea na wanyama wake na kuhifadhi uzuri wake badala ya kuiharibu. (Tazama ukurasa wa 12 na 17.) Badala ya Paradiso hiyo iliyoahidiwa kuwa ya ajabu isivyoaminika, hali ya sasa yenye kujaa huzuni ni mbaya sana isiweze kuruhusiwa iendelee. Paradiso itachukua mahali pake.
Naweza kuwajibuje watu wanaodhihaki na kusema Biblia ni ngano na si ya kisayansi?
Kuziamini ahadi hizo si imani bila msingi. “Imani hufuata jambo lisikiwalo.” Kwa kujifunza Neno la Mungu, hekima yake inaonekana wazi na imani inakua.—Waroma 10:17; Waebrania 11:1.
Akiolojia ya Biblia yathibitisha mambo mengi ya usahihi wa kihistoria wa Biblia. Sayansi ya kweli inapatana na Biblia. Mambo ya hakika yafuatayo yalikuwa katika Biblia zamani sana kabla hayajavumbuliwa na wasomi wa kilimwengu: mfuatano wa hatua zilizochukuliwa katika kutengenezwa kwa dunia, kwamba dunia ni mviringo, kwamba inaning’inia angani pasipo kitu cha kuegemea, na kwamba ndege huhama.—Mwanzo, sura ya 1; Isaya 40:22; Ayubu 26:7; Yeremia 8:7.
Kupuliziwa kwa Biblia na Mungu kwaonyeshwa na utimizo wa unabii mbalimbali. Danieli alitabiri mapema kuinuka na kuanguka kwa serikali za ulimwengu, na pia wakati ambapo Mesiya angekuja na kuuawa. (Danieli, sura za 2, 8; 9:24-27) Leo, unabii mwingine mbalimbali ungali unatimizwa, ukitambulisha hizi kuwa ni “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo, sura ya 24) Binadamu hana uwezo huo wa kujua mambo kimbele. (Isaya 41:23) Ili kupata uhakikisho zaidi, ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? na Je, Kuna Muumba Anayekujali?, vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society.
Naweza kujifunzaje kujibu maswali juu ya Biblia?
Ni lazima ujifunze Biblia na kuitafakari, na wakati uo huo uombe roho ya Mungu ikuelekeze. (Mithali 15:28; Luka 11:9-13) “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima,” Biblia yasema, “acheni afulize kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yakobo 1:5) Pia, kuna vichapo vinavyofaa vya kujifunza Biblia vinavyoweza kukupa habari. Kwa kawaida msaada kutoka kwa wengine unahitajiwa, kama wakati Filipo alipojifunza pamoja na yule Mwethiopia. (Matendo 8:26-35) Mashahidi wa Yehova huongoza mafunzo ya Biblia kwa watu wenye kupendezwa katika nyumba zao bila malipo. Usisite kuomba funzo hilo.
Sababu gani watu wengi hupinga Mashahidi wa Yehova na kuniambia nisijifunze nao?
Mahubiri ya Yesu yalipingwa, na alisema kwamba wafuasi wake pia wangepingwa. Wengine walipovutwa na mafundisho ya Yesu, wapinzani wa kidini walijibu vikali wakisema: “Nyinyi hamjaongozwa vibaya pia, ndivyo? Hakuna hata mmoja wa watawala au wa Mafarisayo ambaye ameweka imani katika yeye, ndivyo?” (Yohana 7:46-48; 15:20) Wengi wanaokuambia usijifunze na Mashahidi hawana habari ama wana chuki isiyo na msingi. Jifunze na Mashahidi ujionee mwenyewe iwapo ufahamu wako wa Biblia utaongezeka au sivyo.—Mathayo 7:17-20.
Sababu gani Mashahidi hutembelea watu walio na dini yao wenyewe?
Kwa kufanya hivyo wanafuata kielelezo cha Yesu. Aliwaendea Wayahudi. Wayahudi walikuwa na dini yao wenyewe, lakini ilikuwa imewapotosha wakaliacha Neno la Mungu kwa njia nyingi. (Mathayo 15:1-9) Mataifa yote yana dini za aina fulani, ziwe ni zile zinazoitwa za Kikristo au zisizo za Kikristo. Ni jambo la maana sana watu washikilie imani zinazopatana na Neno la Mungu mwenyewe, na jitihada za Mashahidi kuwasaidia wafanye hivyo ni wonyesho wa kupenda jirani.
Je! Mashahidi huamini kwamba dini yao tu ndiyo ya kweli?
Yeyote anayeichukua dini yake kwa uzito apaswa kuiona kuwa ndiyo ya kweli. Kama sivyo, sababu gani yeye ajishughulishe nayo? Wakristo wanaonywa kwa upole hivi: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana lililo bora.” (1 Wathesalonike 5:21) Imempasa mtu ahakikishe kwamba imani zake zaweza kuungwa mkono na Maandiko, maana kuna imani moja tu ya kweli. Andiko la Waefeso 4:5 lathibitisha hivyo, likitaja “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.” Yesu hakukubaliana na maoni ya kisasa yenye uzembe ya kwamba kuna barabara nyingi, dini nyingi, zote zikiongoza kwenye wokovu. Badala yake, alisema: “Lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” Mashahidi wa Yehova huamini kwamba wameiona. Kama sivyo, wangetafuta dini nyingine.—Mathayo 7:14.
Je! wao huamini kwamba ni wao tu watakaookoka?
Mamilioni ambao wameishi katika karne zilizopita na ambao hawakuwa Mashahidi wa Yehova watafufuliwa wapate nafasi ya kuwa na uhai. Wengi wanaoishi sasa bado wanaweza kukubali kweli na uadilifu kabla ya “dhiki kubwa,” nao watapata wokovu. Isitoshe, Yesu alisema kwamba haitupasi kuhukumiana. Sisi hutazama sura ya nje; Mungu hutazama moyo. Yeye huona bila kukosea na huhukumu kwa rehema. Amemkabidhi Yesu jukumu la kuhukumu, si sisi.—Mathayo 7:1-5; 24:21; 25:31.
Wale wanaohudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova wanatazamiwa kutoa michango gani ya kifedha?
Kwa habari ya michango ya fedha, mtume Paulo alisema: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Hakuna sadaka zinazokusanywa kwenye Majumba ya Ufalme wala kwenye majumba ya mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Masanduku huwekwa mahali panapofaa ili yeyote anayetaka atoe mchango. Hakuna mtu anayejua ni kiasi gani wanachotoa wale wengine wala kama wanatoa. Wengine wana uwezo wa kutoa zaidi ya wengine; huenda wengine wasiweze kutoa chochote. Yesu alionyesha maoni yanayofaa alipoeleza juu ya sanduku la hazina hekaluni katika Yerusalemu na wale waliokuwa wakitoa michango: Jambo la maana ni uwezo na roho ya mtu ya kutoa, si wingi wa fedha.—Luka 21:1-4.
Nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, je! ningetazamiwa kuhubiri kama wao?
Mtu anapopata kujua kuna Paradiso ya kidunia iliyoahidiwa chini ya Ufalme wa Kristo, anataka kuwaambia wengine juu yake. Wewe utafanya hivyo pia. Ni habari njema!—Matendo 5:41, 42.
Kufanya hivyo ni njia ya maana ya kuonyesha kwamba wewe ni mwanafunzi wa Yesu Kristo. Katika Biblia, Yesu anaitwa “shahidi mwaminifu na wa kweli.” Alipokuwa duniani alihubiri akisema: “Ufalme wa mbingu umekaribia,” naye aliwatuma wanafunzi wake wakafanye vivyo hivyo. (Ufunuo 3:14; Mathayo 4:17; 10:7) Baadaye, Yesu aliamuru wafuasi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha.” Vilevile alitabiri kwamba kabla ya mwisho, “habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.”—Mathayo 24:14; 28:19, 20.
Kuna njia nyingi za kutangaza habari njema hizi. Mara nyingi kuongea na rafiki na wale tunaojuana nao hutoa fursa ya kufanya hivyo. Wengine hufanya hivyo kwa kuandika barua au kwa kutumia simu. Wengine hutuma vitabu vilivyo na habari wanayoona yule wanayejuana naye angependezwa sana nayo. Kwa kutotaka kumwacha yeyote, Mashahidi huenda mlango kwa mlango wakiwa na ujumbe huo.
Biblia ina mwaliko huu wenye uchangamshi: “Roho na bibi-arusi hufuliza kusema: “Njoo!” Na acha yeyote anayesikia aseme: “Njoo!” Na acha yeyote anayeona kiu aje; acha yeyote atakaye achukue maji ya uhai bure.” (Ufunuo 22:17) Kuwaambia wengine juu ya dunia iliyo Paradiso na baraka zake kwapasa kufanywe kwa moyo wa kupenda, kutoka moyo unaotaka sana kushiriki habari njema hizi pamoja na wengine.
Tuna hakika kwamba una maswali mengine juu ya Mashahidi wa Yehova na imani yao. Labda baadhi ya masuala yaweza kubishaniwa. Tungependa kuyajibu maswali yako. Nafasi ni ndogo katika broshua hii, hivyo twakuomba uwaulize Mashahidi wa kwenu. Unaweza kufanya hivyo katika mikutano yao kwenye Jumba lao la Ufalme au wanapokutembelea nyumbani kwako. Au, waweza kutuma maswali yako kwa International Bible Students Association, ukitumia anwani inayofaa iliyoorodheshwa hapa chini.