Sura 7
Sababu ya Sisi Kuwa Hapa
1.Watu wenye kufikiri wamefikia uamuzi gani?
KWA MUDA mrefu watu wametaka kujua maana ya kuishi hapa duniani. Wamelitazama anga kubwa mno lenye kujaa nyota. Wamestaajabia machweo ya jua yenye rangi ya kupendeza na uzuri wa sehemu za mashambani. Watu wenye kufikiri wamewaza kwamba bila shaka kuna kusudi kuu la kuwako kwa vitu vyote hivyo. Lakini mara nyingi wametaka kujua ni wapi wanapofaa kuwa.—Zaburi 8:3, 4.
2. Ni maulizo gani ambayo watu wameuliza?
2 Wakati fulani maishani watu wengi wanauliza hivi: Je! tunapaswa kuishi muda mfupi tu, tupate tunachotaka katika maisha, kisha tufe? Tunaelekea wapi hasa? Je! kuna mengi tunayoweza kutazamia kuliko muda mfupi tu wa kuzaliwa, kuishi na kufa? (Ayubu 14:1, 2) Kitakachotusaidia tufahamu jambo hilo ni jibu kwa ulizo hili: Tulipataje kuwa hapa?
MAGEUZI {EVOLUTION) AU KUUMBWA?
3. Fundisho la mageuzi linasema nini?
3 Mahali fulani watu wanafundishwa kwa kawaida kwamba kila kitu tunachokiona kilijitokeza chenyewe, kwamba hakikuumbwa. Inasemwa kwamba kwa muda wa mamilioni mengi ya miaka uhai ulijitokeza wenyewe kwa njia ya mageuzi, au ukasitawi kutokana na namna ndogo za vitu vilivyo hai mpaka mwishowe wanadamu wakatokea. Katika sehemu nyingi za dunia wazo hilo la mageuzi linafundishwa kuwa jambo la hakika. Lakini je! ni kweli kwamba sisi tulitokana na mnyama aliye mfano wa nyani aliyeishi mamilioni ya miaka iliyopita? Je! ulimwengu mzima huu ulio mkubwa ulijitokeza wenyewe?
4. Sababu gani tunaweza kuamini kwamba “Mungu aliziumba mbingu na nchi”?
4 Biblia inasema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.” (Mwanzo 1:1) Nayo mambo ya hakika ya sayansi yanakubali kwamba mbingu, pamoja na mabilioni yazo ya nyota, na dunia yetu zilikuwa na mwanzo. Ziliumbwa. Miendo ya nyota na sayari inafuata sana kawaida zilizowekwa hivi kwamba inaweza kujulikana kwa usahihi kabisa zitakuwa zimekwenda na kufika wapi, hata miaka mingi mapema. Nyota na sayari hizo zinasonga katika ulimwengu mzima kulingana na sheria na kanuni za hisabati (elimu ya hesabu). Profesa wa hisabati kutoka Chuo Kikuu cha Cambridge, P. Dirac, alisema, katika gazeti Scientific American: “Labda mtu angeweza kusimulia hali hiyo kwa kusema kwamba Mungu ndiye mhisabati mwenye utaratibu ulio bora sana, naye alitumia hisabati za juu sana katika kuumba ulimwengu mzima.”
5. Mwili wetu wenye nyama unaonyeshaje kwamba sisi tuliumbwa wala hatukutokana na mageuzi?
5 Biblia inasema hivi: “Mjue kwamba Yehova ni Mungu. Ni yeye ambaye amefanyiza sisi, wala si sisi wenyewe.” (Zaburi 100:3, NW) Mwili wetu wa kibinadamu unaonyesha ubuni wa ajabu sana hivi kwamba mwandikaji mmoja wa Biblia alivutwa na moyo wake kumwambia Mungu hivi: “Nitasifu wewe kwa sababu kwa njia yenye kutia hofu mimi nimeumbwa kiajabu. . . . Mifupa yangu hukufichwa wewe wakati mimi niliumbwa kwa siri . . . Macho yako yaliona hata kiinitete cha mimi, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimewekwa katika mwandiko.” (Zaburi 139:14-16, NW) Kitoto kinakua ndani ya mama yacho kwa njia ya ajabu. Gazeti Newsweek lilisema hivi juu ya jambo hilo: “Huo ni mwujiza kabisa.” Kisha likaongeza hivi: “Hakuna njia inayoweza kueleza kwa usahihi kabisa wakati mimba inapofanyika hasa. Hakuna mwanasayansi anayeweza kusimulia ni nguvu gani za ajabu zinazochukua kazi ya kukuza viungo na makumi ya maelfu ya mishipa iliyo katika kiinitete cha mwanadamu.”
6. Sababu gani ni jambo la akili tuamini uumbaji badala ya mageuzi?
6 Ebu ufikirie ulimwengu wetu ulio mkubwa mno, na vilevile mwili wetu wenyewe pamoja na mwundo na ubuni wake wa ajabu. Kuwaza timamu kunapasa kutuambie kwamba mambo hayo hayakujitokeza yenyewe kwa namna ya mageuzi. Yalikuwa na Mbuni, Muumba. Fikiria vitu vingine tunavyoona kutuzunguka. Unapokuwa katika nyumba yako, jiulize hivi: Je! dawati yangu, taa, kitanda, kiti, meza, kuta, au hata nyumba yenyewe, vilijitokeza vyenyewe? Au vilihitaji fundi wa kuvitengeneza? Bila shaka watu wenye akili walivitengeneza! Ni katika njia gani basi, inaweza kudaiwa kwamba ulimwengu wetu ulio na mambo magumu kufahamika na sisi wenyewe hatukuhitaji mtu wa kutufanyiza? Na ikiwa Mungu ndiye aliyetuweka hapa, bila shaka alikuwa na sababu ya kufanya hivyo.
7. (a) Yesu alionyeshaje kwamba aliamini uumbaji? (b) Kuna ushuhuda gani zaidi wa kuonyesha kwamba Adamu alikuwa mtu halisi?
7 Yesu Kristo mwenyewe alisema hivi juu ya mwanamume na mwanamke wa kwanza: “Yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja.” (Mathayo 19:4, 5) Hapo Yesu alitumia maneno ya Mwanzo 1:27 na 2:24 juu ya kuumbwa kwa Adamu na Hawa. Kwa njia hiyo alikuwa akionyesha kwamba masimulizi hayo ya Biblia ni ya kweli. (Yohana 17:17) Vilevile, Biblia inamtaja Henoko kuwa “mtu wa saba baada ya Adamu.” (Yuda 14) Kama Adamu hakuwa mtu halisi, Biblia haingalimtaja katika njia hiyo ya waziwazi.—Luka 3:37, 38.
8. Ni maoni gani juu ya mwanzo wa mtu yasiyofundishwa na Biblia?
8 Watu fulani wanasema kwamba Mungu alitumia njia ya mageuzi ili kuumba mtu. Wanadai kwamba Mungu alimruhusu mtu ageuke-geuke, na alipofikia hatua fulani Yeye (Mungu) akaweka nafsi ndani yake. Lakini wazo hilo halionekani po pote katika Biblia. Badala yake, Biblia inasema kwamba mimea na wanyama viliumbwa ‘kulingana na aina zavyo.’ (Mwanzo 1:11, 21, 24, NW) Na mambo ya hakika yanaonyesha kwamba aina moja ya mmea au mnyama haiwi aina nyingine baadaye. Habari zaidi inayoonyesha kwamba sisi hatukutokana na mageuzi inaweza kupatikana katika kitabu cha Kiingereza Did Man Get Here by Evolution or by Creation (au cha Kifaransa)
NAMNA MUNGU ALIVYOUMBA MTU
9. (a) Biblia inasimuliaje kuumbwa kwa mtu? (b) Ilikuwaje Mungu alipopuliza “pumzi ya uhai” katika vilango vya pua ya mtu?
9 Mungu aliumba mtu kutokana na ardhi ili aishi hapa duniani, kama Biblia inavyosema: “[Yehova] Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) Kwa hayo tunaweza kuona kwamba mtu aliumbwa moja kwa moja na Mungu. Katika tendo la pekee la kuumba, Mungu alimfanya mwanadamu kuwa mtu aliye kamili, mzima. Mungu alipopuliza katika vilango vya pua ya mtu “pumzi ya uhai,” mapafu ya mtu huyo yalijaa hewa. Lakini mengi kuliko hilo yalitimizwa. Kwa njia hiyo Mungu aliupa mwili wa mtu uhai. Hiyo kani ya uhai inaendelezwa, au inafanywa iendelee kufanya kazi, kwa kupumua.
10. Nafsi ya binadamu ni nini, na iliumbwaje?
10 Walakini, angalia uone kwamba hapo Biblia haisemi Mungu alimpa mtu nafsi. Badala yake, inasema kwamba Mungu alipomwanzisha mtu kupumua, huyo “mtu akawa nafsi hai.” Basi mtu huyo alikuwa nafsi, kama vile mtu anayekuwa daktari ni daktari. (1 Wakorintho 15:45) Yale “mavumbi ya ardhi,” ambayo katika hayo mwili wenye nyama umefanyizwa, siyo nafsi. Wala Biblia haisemi kwamba ile “pumzi ya uhai” ndiyo nafsi. Badala yake, Biblia inaonyesha kwamba kuwekwa pamoja kwa vitu hivi viwili ndiko kulikofanya ‘mtu awe nafsi hai.’
11. Ni mambo gani ya hakika inayoyasema Biblia juu ya nafsi ya kibinadamu yanayoonyesha kwamba nafsi haiwezi kuwa ni namna ya kivuli kinachoweza kuishi mbali na mtu?
11 Kwa kuwa nafsi ya mwanadamu ni mtu mwenyewe, basi haiwezi kuwa ni kitu cha namna ya kivuli kinachoishi ndani ya mwili au kinachoweza kuuacha mwili. Kwa urahisi, Biblia inafundisha kwamba nafsi yako ni wewe. Kwa mfano, Biblia inasema juu ya nafsi ikitaka kula chakula cha mwili, ikisema: “Nafsi yako inatamani sana kula nyama.” (Kumbukumbu la Torati 12:20, NW) Vilevile inasema kwamba nafsi zina damu inayotembea katika mishipa yazo, maana inasema juu ya “alama za damu ya zile nafsi za maskini wasio na hatia.”—Yeremia 2:34, NW.
SABABU MUNGU ALIMWEKA MTU HAPA
12. Mungu alikuwa na kusudi gani kwa kuweka wanadamu duniani?
12 Halikuwa kusudi la Mungu Adamu na Hawa wafe baada ya muda mfupi kisha waishi mahali penginepo. Walitakwa wabaki hapa waitunze dunia na vitu vyake vyote vilivyo hai. Kama Biblia inavyosema: “Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” (Mwanzo 1:28; 2:15) Adamu na Hawa, vilevile watoto wote ambao wangezaa, wangaliweza kuwa wenye furaha duniani milele, wakifanya mambo ambayo Mungu alitaka wafanye.
13. (a) Tunawezaje kuwa wenye furaha? (b) Ni nini kitakachozipa maisha zetu maana halisi?
13 Angalia kwamba hapo panasema “Mungu akawabarikia.” Aliwajali kweli kweli watoto wake wa kidunia. Basi akiwa Baba mwenye upendo aliwapa maagizo yaliyokuwa kwa faida yao. Wangeona furaha katika kuyatii. Yesu alijua hayo na kwa hiyo baadaye alisema: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” (Luka 11:28, NW) Yesu alishika neno la Mungu. “Sikuzote mimi nafanya mambo yanayopendeza yeye,” akasema. (Yohana 8:29, NW) Huo ndio ufunguo wa kuonyesha sababu yenyewe ya sisi kuwa hapa. Ni kuwa na maisha zenye furaha kamili kwa kuishi kupatana na mapenzi ya Mungu. Kumtumikia Yehova kutazipa maisha zetu sasa maana ya kweli kweli. Na kwa kufanya hivyo tutajiweka wenyewe katika hali ya kuja kuishi milele duniani katika Paradiso.—Zaburi 37:11, 29.
SABABU TUNAZEEKA NA KUFA
14. Kwa kutokutii amri ya Mungu. Adamu na Hawa walifanya nini?
14 Lakini sote sasa tunazeeka na kufa. Sababu gani? Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, ni kwa sababu ya kuasi kwa Adamu na Hawa. Yehova alikuwa amewawekea jaribu lililoonyesha uhitaji wao wa kumtii Mungu. Alimwambia Adamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Kwa kula kutokana na mti huo, Adamu na Hawa walimgeuzia Baba yao wa kimbingu visogo vyao na kukataa uongozi wake. Walikataa kutii wakachukua kile kisichokuwa mali yao. Wangaliweza kuishi milele kwa furaha katika paradiso bila umaskini wala taabu, lakini sasa wakajiletea wenyewe ile adhabu ya dhambi. Adhabu hiyo ni kutokukamilika na kifo.—Warumi 6:23.
15. Tulipata dhambi yetu kutoka kwa Adamu namna gani?
15 Je! unajua tulivyopata dhambi kutoka kwa Adamu? Adamu alipokwisha kuwa mtu asiyekamilika, alipelekea watoto wake wote hali hiyo ya kutokamilika na kifo. (Ayubu 14:4; Warumi 5:12) Ili usaidiwe kufahamu hali hiyo, ebu fikiria yanayotokea wakati mwokaji mikate anapooka mkate katika kiokeo kilicho na kishimo ndani yake. Alama itaonekana juu ya mikate yote iliyookwa katika kiokeo hicho. Adamu akawa kama kiokeo hicho, na sisi ni kama mikate hiyo. Yeye akawa asiyekamilika alipovunja sheria ya Mungu. Ilikuwa kana kwamba alipata kishimo au alama mbaya. Basi alipozaa watoto, wote wakawa na alama iyo hiyo ya dhambi au kutokamilika.
16, 17. Mmoja wa miujiza ya Yesu unaonyeshaje kwamba magonjwa yameipata jamaa ya kibinadamu kwa sababu ya dhambi?
16 Tunakuwa wagonjwa na kuzeeka sasa kwa sababu ya dhambi hiyo ambayo sote tumepata kutoka kwa Adamu. Mmoja wa miujiza aliyofanya Yesu unaonyesha hivyo. Yesu alipokuwa akifundisha katika nyumba alimokuwa akikaa, kundi kubwa la watu lilikusanyika hata ikawa hakuna mtu mwingine ambaye angeweza kujifinya aingie katika chumba hicho. Wakati wanaume wanne walipoleta mtu aliyepooza akiwa amelala katika godoro (machela) dogo, waliona kwamba hawangeweza kuingia ndani. Basi walipanda kwenye dari, wakatoboa shimo, wakalitelemsha lile godoro dogo lenye mtu aliyepooza mpaka mahali penyewe hasa alipokuwa Yesu.
17 Yesu alipoona imani waliyokuwa nayo, alimwambia mtu huyo aliyepooza: “Umesamehewa dhambi zako.” Lakini baadhi ya watu waliokuwapo hawakudhani Yesu angeweza kusamehe dhambi. Basi Yesu akasema hivi: “Mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi. (hapo amwambia yule mwenye kupooza). Nakuambia, Ondoka, ujitwike godoro lako uende nyumbani kwako. Mara akaondoka, akajitwika godoro lake, akatoka mbele yao wote.”—Marko 2:1-12.
18. Watumishi wa Mungu wanaweza kutazamia wakati ujao wa namna gani?
18 Ebu fikiria uwezo huo wa Yesu unachoweza kumaanisha kwetu! Chini ya utawala wa ufalme wa Mungu, Kristo ataweza kusamehe dhambi za watu wote wanaompenda Mungu na kumtumikia. Hiyo ina maana kwamba maumivu yote na uchungu na magonjwa yote yataondolewa. Hakuna mtu atakayezeeka na kufa wakati wo wote! Lo! hilo ni tumaini zuri kama nini la wakati ujao! Ndiyo, kwa kweli kuna mambo mengi tunayoweza kutazamia kuliko kuzaliwa tu, kuishi kwa muda mfupi tu kisha tufe. Kwa kuendelea kujifunza juu ya Mungu na kumtumikia, tunaweza kweli kweli kuishi milele duniani katika Paradiso.
[Picha katika ukurasa wa 69]
Wengi wanataka kujua maana ya kuishi
[Picha katika ukurasa wa 70]
Je! vitu hivi vilijitokeza vyenyewe, au vilitengenezwa?
[Picha katika ukurasa wa 75]
Masimulizi ya Biblia ya Yesu kuponesha mtu aliyepooza yanaonyesha kwamba watu wanakuwa wagonjwa kwa sababu ya dhambi ya Adamu