Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • pe sura 25 kur. 208-216
  • Upande wa Ulimwengu wa Shetani, au Upande wa Mfumo Mpya wa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Upande wa Ulimwengu wa Shetani, au Upande wa Mfumo Mpya wa Mungu?
  • Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ULIMWENGU WA SHETANI—NI NINI?
  • JINSI YA KUEPUKA KUWA SEHEMU YA ULIMWENGU
  • Kwa Sababu Gani Ni Lazima Wakristo Waendelee Kujitenga na Ulimwengu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Lazima Waokokaji Wawe “Si Sehemu ya Ulimwengu”
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Watawala Katika Makao ya Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Uwe Macho​—Shetani Anataka Kukumeza!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
Pata Habari Zaidi
Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
pe sura 25 kur. 208-216

Sura 25

Upande wa Ulimwengu wa Shetani, au Upande wa Mfumo Mpya wa Mungu?

1. Ni nini kinachohakikisha kwamba wewe uko upande wa mfumo (taratibu) mpya wa Mungu?

JE! WEWE uko upande wa mfumo (taratibu) mpya wa Mungu wenye uadilifu, na unautaka uje? Je! wewe unampinga Shetani, na unataka ulimwengu wake umalizike? Huenda ukasema, Ndiyo, kwa maulizo yote mawili. Lakini, je! hiyo inatosha? Kuna usemi wa zamani wa kwamba matendo yanapaza sauti kuliko maneno. Ikiwa unauamini mfumo mpya wa Mungu, namna unavyoishi ndiyo itakayoonyesha unauamini kweli kweli.—Mathayo 7:21-23; 15:7, 8.

2. (a) Ni mabwana gani wawili tunaoweza kutumikia? (b) Ni nini linaloonyesha sisi ni mtumwa, au mtumishi, wa nani?

2 Ukweli ni kwamba namna unavyoishi inaweza kumpendeza mmoja tu kati ya mabwana wawili. Ama unamtumikia Yehova Mungu ama Shetani Ibilisi. Kanuni inayopatikana katika Biblia inatusaidia tufahamu jambo hilo. Inasema: “Je! ninyi hamjui kwamba ikiwa mnaendelea kujitoa wenyewe kwa mtu ye yote kama watumwa ili mmtii, ninyi ni watumwa wake kwa sababu mnamtii?” (Warumi 6:16, NW) Wewe unamtii nani? Ni mapenzi ya nani utakayofanya? Hata ujibuje, ukizifuata njia zisizo za adili ulimwengu huwezi kuwa unamtumikia Mungu wa kweli, Yehova.

ULIMWENGU WA SHETANI—NI NINI?

3. (a) Ni nani ambaye Biblia inaonyesha ndiye mtawala wa ulimwengu? (b) Katika sala, Yesu alionyeshaje tofauti kati ya ulimwengu na wanafunzi wake?

3 Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu huu.” Mtume Yohana naye alisema kwamba “ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu.” (Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19, NW) Angalia kwamba katika sala kwa Mungu Yesu hakuwahesabu wanafunzi wake kuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani. Alisema: “Mimi nawaombea hao [wanafunzi wake]; siuombei ulimwengu . . . Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:9, 16; 15:18, 19) Kwa maneno hayo ni wazi kwamba Wakristo wa kweli wanapaswa wajitenge na ulimwengu.

4. (a) Katika Yohana 3:16, usemi huu “ulimwengu” unahusu nani? (b) “Ulimwengu” ambao ni lazima wafuasi wa Kristo wajitenge nao ni nini?

4 Lakini Yesu alikuwa akimaanisha nini aliposema “ulimwengu”? Katika Biblia usemi huu “ulimwengu” mara nyingine unamaanisha wanadamu kwa ujumla. Mungu alimtuma Mwanaye atoe uhai wake kuwa ukombozi wa ulimwengu huu wa wanadamu. (Yohana 3:16) Hata hivyo Shetani ameipanga sehemu kubwa zaidi ya wanadamu kwa namna ya tengenezo ili impinge Mungu. Hivyo ulimwengu wa Shetani ni jamii hii ya kibinadamu iliyopangwa kwa namna ya tengenezo, iliyojitenga na tengenezo la Mungu linaloonekana au ikawa nje yake. Huo ndio ulimwengu ambao lazima Wakristo wa kweli wajitenge nao.—Yakobo 1:27..

5. Ni sehemu gani ya ulimwengu iliyo kubwa, nayo inafananishwa na nini katika Biblia?

5 Ulimwengu wa Shetani, yaani, jamii yake ya kibinadamu iliyopangwa kwa namna ya tengenezo, una sehemu mbalimbali zinazohusiana sana. Sehemu moja kubwa ni dini ya uongo. Katika Biblia dini ya uongo inafananishwa na “kahaba mkuu,” au malaya, mwenye jina “BABELI MKUU.” Yeye ni milki ya ulimwengu, kama inavyoonyeshwa na uhakika wa kwamba ana “ufalme juu ya wafalme wa [dunia].” (Ufunuo 17:1, 5 18) Lakini ni nini kinachohakikisha kwamba Babeli Mkuu ni milki ya kidini ya ulimwengu?

6, 7. (a) Ni nini kinachohakikisha kwamba Babeli Mkuu ni milki ya kidini? (b) Dini ya uongo imekuwa na uhusiano gani na serikali za kisiasa?

6 Kwa kuwa “wafalme wa [dunia]” wanasemwa kuwa ‘wanazini naye,’ Babeli Mkuu hangeweza kuwa milki ya ulimwengu ya kisiasa. Na kwa kuwa wale “wafanya biashara” wa dunia wanaosafiri wanasimama wakiwa mbali na kuomboleza uharibifu wake, yeye si milki ya ulimwengu ya kibiashara. (Ufunuo 17:2; 18:15) Walakini, ya kwamba yeye kweli ni milki ya kidini inaonyeshwa na maneno ya Biblia ya kwamba “mataifa yote walidanganywa kwa uchawi” wake.—Ufunuo 18:23.

7 Vilevile unaohakikisha kwamba Babeli Mkuu ni milki ya kidini ni uhusiano wake na “mnyama.” Katika Biblia wanyama hao (wa mwitu) wanafananisha serikali za kisiasa. (Danieli 8:20, 21) Babeli Mkuu anasimuliwa kuwa “ameketi juu ya mnyama mwekundu sana, . . . mwenye vichwa saba na pembe kumi.” Hivyo yeye amekuwa akijaribu kutumia uvutano wake juu ya “mnyama” huyo, au serikali ya ulimwengu. (Ufunuo 17:3) Na ni kweli kwamba katika historia yote dini imejichanganya na siasa, mara nyingi ikiziambia serikali jambo la kufanya. Kweli kweli imekuwa na “ufalme juu ya wafalme wa [dunia].”—Ufunuo 17:18.

8. Ni sehemu gani nyingine kuu ya ulimwengu wa Shetani, nazo zinafananishwaje katika Biblia?

8 Nazo serikali hizo za kisiasa ni sehemu nyingine kubwa ya ulimwengu wa Shetani. Kama tulivyokwisha kuona, katika Biblia zinafananishwa na wanyama. (Danieli 7:1-8, 17, 23) Ya kwamba serikali hizo zilizo kama wanyama zinapata uwezo kutoka kwa Shetani inaonyeshwa na njozi iliyoandikwa na mtume Yohana: “Nikaona mnyama akitoka katika bahari, mwenye pembe kumi, na vichwa saba . . . Yule joka akampa nguvu zake na kiti chake cha enzi.” (Ufunuo 13:1, 2; 12:9) Ushuhuda zaidi unaoonyesha kwamba falme hizo, au serikali, ni sehemu ya ulimwengu wa Shetani ni uhakika wa kwamba Shetani alimshawishi Yesu kwa kumtolea falme hizo. Shetani hangaliweza kufanya hivyo kama hangalikuwa ndiye mtawala wazo.—Mathayo 4:8, 9.

9. (a) Sehemu nyingine ya ulimwengu wa Shetani inaelezwaje katika Ufunuo 18:11? (b) Inafanya na kusitawisha nini, kuhakikisha kwamba Shetani ndiye anayeiongoza?

9 Bado sehemu nyingine iliyo mashuhuri ya ulimwengu wa Shetani ni ule mfumo wa kibiashara wenye pupa na uonezi, unaotajwa katika Ufunuo 18:11 kuwa “wafanya biashara” (wanaosafiri). Mfumo huo wa kibiashara unasitawisha tamaa ya kichoyo katika watu ili wanunue vitu ambavyo unafanyiza, ijapokuwa huenda wasivihitaji na hata wanaweza kuishi vizuri zaidi bila hivyo. Wakati uo huo mfumo huo wa kibiashara wenye pupa unalundika chakula katika mabohari (ghala) na bado unaacha mamilioni ya watu wafe njaa kwa sababu hawana pesa za kununua chakula hicho. Kwa upande mwingine, silaha za kivita zenye uwezo wa kuiangamiza jamii nzima ya kibinadamu zinafanyizwa na kuuzwa ili kujipatia faida. Hivyo mfumo wa kibiashara wa Shetani, pamoja na dini ya uongo na serikali za kisiasa, unasitawisha choyo, uhalifu na vita vyenye kuogopesha.

10, 11. (a) Ni sehemu gani nyingine ya ulimwengu wa Shetani? (b) Kuna maonyo gani ya Biblia juu ya kujiingiza katika sehemu hiyo?

10 Jamii ile ya kibinadamu iliyopangwa kwa namna ya tengenezo chini ya Shetani Ibilisi ni yenye uovu na upotovu kweli kweli. Inapingana na sheria za Mungu za uadilifu, nayo imejaa aina zote za mazoea machafu. Hivyo sehemu nyingine ya ulimwengu wa Shetani inaweza kusemwa kuwa ni njia zayo za maisha ya potovu, machafu. Kwa sababu hiyo Paulo na Petro waliwaonya Wakristo wayaepuke mazoea mabaya ya watu wa mataifa.—Waefeso 2:1-3; 4:17-19; 1 Petro 4:3, 4.

11 Vilevile, mtume Yohana aliukazia uhitaji wa Wakristo kujilinda juu ya tamaa mbaya na uchafu wa ulimwengu. Aliandika hivi: “Msiwe mkipenda wala ulimwengu wala vitu vilivyomo katika ulimwengu. Mtu ye yote akipenda ulimwengu, upendo wa Baba haumo katika yeye; kwa sababu kila kitu kilichomo katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake—hakitokani na Baba, bali chatokana na ulimwengu.” (1 Yohana 2:15, 16, NW) Mwanafunzi Yakobo alisema kwamba ‘mtu ye yote akitaka kuwa rafiki ya ulimwengu, anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu.’—Yakobo 4:4, NW.

JINSI YA KUEPUKA KUWA SEHEMU YA ULIMWENGU

12, 13. (a) Yesu alionyeshaje kwamba ni lazima Wakristo wawe katika ulimwengu? (b) Inawezekanaje kuwa katika ulimwengu lakini usiwe sehemu yake?

12 Maadamu ulimwengu wa Shetani upo, ni lazima Wakristo waishi ndani yake. Yesu alionyesha hilo alipotoa sala hii akimwambia Baba yake: “Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu.” Lakini ndipo Yesu alipoongeza maneno haya juu ya wafuasi wake: “Wao si wa ulimwengu.” (Yohana 17:15, 16) Inawezekanaje kuwa katika ulimwengu wa Shetani lakini usiwe sehemu yake?

13 Ndiyo, unaishi kati ya wale watu ambao ndio jamii ya leo ya kibinadamu iliyopangwa kwa namna ya tengenezo. Watu hao ni pamoja na waasherati, watu wenye pupa na wengine wanaotenda maovu. Huenda ukawa unafanya kazi pamoja nao, unaenda shuleni pamoja nao, kula pamoja nao na kushiriki nao katika shughuli kama hizo. (1 Wakorintho 5:9, 10) Hata inakupasa uwapende, kama Mungu anavyowapenda. (Yohana 3:16) Lakini Mkristo wa kweli hayapendi maovu ambayo watu wanafanya. Yeye hakubali maoni yao, matendo wala miradi yao maishani. Yeye hashiriki dini yao na siasa zao zenye upotovu. Na ijapokuwa ni lazima mara nyingi afanye kazi katika ulimwengu huu wa kibiashara ili apate riziki, yeye hashiriki mazoea ya kibiashara ya udanganyifu; wala mradi wake mkuu maishani si kupata mali. Kwa kuwa yeye yuko upande wa mfumo mpya wa Mungu, anaepuka ushirika mbaya wa wale wanaoishi kwa ajili ya ulimwengu wa Shetani. (1 Wakorintho 15:33; Zaburi 1:1; 26:3-6, 9, 10) Kwa njia hiyo anakuwa yumo katika ulimwengu wa Shetani lakini bado anakuwa si sehemu yake.

14. Ikiwa wewe uko upande wa mfumo mpya wa Mungu, utatii amri gani ya Biblia?

14 Namna gani wewe? Je! unataka kuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani? Au unataka kuwa upande wa mfumo (taratibu) mpya wa Mungu? Ikiwa uko upande wa mfumo mpya wa Mungu utajitenga na ulimwengu, kutia na dini yake ya uongo. Utatii amri hii: “Tokeni kwake [Babeli Mkuu], enyi watu wangu.” (Ufunuo 18:4) Walakini, kutoka katika Babeli Mkuu, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, kunatia ndani mambo mengi zaidi ya kuvunja uhusiano wote na matengenezo ya uongo ya kidini. Vilevile ina maana ya kutoshiriki maadhimisho (sherehe) ya kidini ya ulimwengu.—2 Wakorintho 6:14-18.

15. (a) Badala ya kuadhimisha (kusherehekea) kuzaliwa kwa Yesu, Wakristo waliamriwa waadhimishe nini? (b) Ni nini linaloonyesha kwamba Yesu hangaliweza kuzaliwa katika majira ya baridi? (c) Ni kwa sababu gani tarehe ya Desemba 25 ilichaguliwa iwe siku ya kuadhimisha kuzaliwa kwa Yesu?

15 Krismasi ni sikukuu ya kidini inayojulikana sana leo. Lakini historia inaonyesha kwamba haikuwa sherehe iliyoadhimishwa na Wakristo wa kwanza-kwanza. Yesu aliwaambia wafuasi wake waadhimishe ukumbusho wa kifo chake, si kuzaliwa kwake. (1 Wakorintho 11:24-26) Uhakika ni kwamba, Desemba 25 siyo tarehe ya kuzaliwa kwa Yesu. Haingaliweza kuwa hiyo, kwa kuwa Biblia inaonyesha kwamba wakati wa kuzaliwa kwake wachungaji walikuwa bado malishoni usiku. Hawangalikuwa huko katika majira ya baridi, yenye mvua nyingi. (Luka 2:8-12) Kwa hakika Desemba 25 ilichaguliwa kuwa tarehe ya kuadhimisha kuzaliwa kwa Yesu kwa sababu, kama kitabu The World Book Encyclopedia kinavyoeleza: “Watu wa Roma tayari waliiadhimisha kuwa Sikukuu ya Saturn, wakisherehekea siku ya kuzaliwa kwa jua.”

16. (a) Ni sikukuu gani nyingine yenye kujulikana sana ya kidini iliyokuwa na mianzo isiyo ya Kikristo? (b) Ni kwa sababu gani nzuri Wakristo wa kweli hawaadhimishi Krismasi na 1sta?

16 Ista ni sikukuu nyingine ya kidini inayojulikana sana. Juma Takatifu katika nchi fulani za Latin Amerika inafanana na hiyo. Lakini hata Ista haikuadhimishwa na Wakristo wa kwanza. Mianzo ya hiyo vilevile ilikuwa maadhimisho yasiyo ya Kikristo. Kitabu The Encyclopcedia Britannica kinasema: “Hakuna jambo katika Agano Jipya linaloonyesha kuadhimishwa kwa sikukuu ya Ista.” Hata hivyo, je! kweli kuna faida yo yote kujua Krismasi na Ista si maadhimisho ya Kikristo bali kwa hakika yalianzishwa na waabudu wa miungu ya uongo? Mtume Paulo alionya juu ya kuchanganya mambo ya kweli na mambo ya uongo, akisema kwamba hata “chachu kidogo huchachua donge zima.” (Wa galatia 5:9) Aliwaambia Wakristo fulani wa kwanza kwamba ilikuwa makosa kwao kuadhimisha siku zilizokuwa zimesherehekewa chini ya sheria ya Musa lakini zikawa zimefutwa na Mungu kwa ajili ya Wakristo. (Wagalatia 4:10, 11) Basi ni jambo la maana hata zaidi leo Wakristo wajitenge na sikukuu ambazo Mungu hakusema kamwe kwamba zisherehekewe, ambazo zilitokana na dini ya uongo.

17. (a) Kuna ubaya gani wa sikukuu zinazoheshimu wanadamu wenye sifa au mataifa? (b) Biblia inaonyeshaje mwendo ambao Wakristo wamepaswa kuchukua?

17 Sikukuu nyingine za ulimwengu zinaheshimu watu wenye sifa. Bado nyingine zinaheshimu na kutukuza mataifa au matengenezo ya kilimwengu. Lakini Biblia inaonya juu ya kuwapa wanadamu heshima za kuwaabudu, au kuyatumainia matengenezo ya kibinadamu yatimize mambo ambayo ni Mungu pekee anayeweza kutimiza. (Matendo 10:25, 26; 12:21-23; Ufunuo 19:10; Yeremia 17:5-7) Hivyo sikukuu zinazoelekea kutukuza mwanadamu au tengenezo la kibinadamu hazipatani na mapenzi ya Mungu, nao Wakristo wa kweli hawatashiriki hizo.—Warumi 12:2.

18. (a) Ni vitu gani ambavyo wanadamu wamefanya ili waviheshimu au kuviabudu? (b) Sheria ya Mungu inasema nini juu ya kukipa kitu heshima ya kukiabudu?

18 Vitu vingi vimefanywa na wanadamu ambavyo watu wanaambiwa waviheshimu au waviabudu. Vingine vya hivyo vimefanyizwa kwa chuma au miti. Vingine vimefanyizwa kwa nguo na huenda picha ya kitu fulani cha mbinguni au duniani ikashonwa au kuchorwa juu yavyo. Huenda taifa likatunga sheria inayosema inampasa kila mtu atoe heshima ya kuabudu kitu hicho. Lakini sheria ya Mungu inasema watumishi wa Mungu wasifanye hivyo. (Kutoka 20:4, 5; Mathayo 4:10) Watu wa Mungu wamefanyaje katika hali kama hizo?

19. (a) Mfalme wa Babeli aliamuru kila mtu afanye nini? (b) Ni mfano wa nani ambao Wakristo watafanya vema kufuata?

19 Katika Babeli ya kale Mfalme Nebukadreza alijenga sanamu kubwa sana ya dhahabu na akaamuru kwamba kila mtu aisujudie. ‘Mtu ye yote asiyefanya hivyo,’ akasema, ‘atatupwa katika tanuru inayowaka kwa ukali wa moto.’ Biblia inatuambia kwamba vijana watatu Waebrania, Shadraka, Meshaki na Abednego, walikataa kufanya alivyoamuru mfalme huyo. Kwa sababu gani? Kwa sababu ibada ilihusika, na ibada yao ilikuwa ya Yehova peke yake. Mungu alikubali tendo lao, akawaokoa na hasira ya mfalme. Kwa kweli, Nebukadreza alikuja kuona kwamba watumishi hao wa Yehova hawakuwa hatari kwa Serikali, hivyo akatunga sheria ya kulinda uhuru wao. (Danieli 3:1-30) Je! wewe huvutwi na uaminifu wa vijana hao wa kiume? Je! wewe utaonyesha kwamba kweli uko upande wa mfumo (taratibu) mpya wa Mungu kwa kutii sheria zote za Mungu?—Matendo 5:29.

20. Ni njia gani mbalimbali ambazo Shetani anatumia ili ajaribu kutushawishi tuvunje sheria za Mungu juu ya mwenendo mwema unaohusu ngono?

20 Bila shaka, Shetani hataki sisi tumtumikie Yehova. Yeye anataka tumtumikie yeye. Hivyo anajaribu kutushawishi tufanye anayotaka, kwa kuwa anajua ya kwamba sisi tunakuwa watumwa, au watumishi, wa ye yote tunayetii. (Warumi 6:16) Kwa kutumia njia mbalimbali, kutia ndani televisheni, sinema, namna fulani za kucheza dansi na vitabu vya mambo machafu, Shetani anatia moyo watu wasiooana wafanye ngono, vilevile wafanye uzinzi. Mwenendo wa namna hiyo unafanywa uonekane kuwa unakubalika, hata kuwa wenye kufaa. Walakini, hicho ni kinyume cha sheria za Mungu. (Waebrania 13:4; Waefeso 5:3-5) Na mtu anayeshiriki mwenendo wa namna hiyo anaonyesha hakika kwamba yeye yuko upande wa ulimwengu wa Shetani.

21. Ni mazoea gani mengine ambayo, mtu akiyashiriki, ataonyesha yuko upande wa ulimwengu wa Shetani?

21 Kuna mazoea mengine ambayo ulimwengu wa Shetani umefanya yapendwe na watu wengi lakini yanapingana na sheria za Mungu. Kulewa pombe ni moja la mazoea hayo. (1 Wakorintho 6:9, 10) Zoea jingine ni kujifurahisha kwa kutumia dawa za kulevya kama bangi na heroin, vilevile kutumia tumbako. Vitu hivyo vinaumiza mwili na ni vichafu. Kwa wazi kuvitumia ni kuvunja agizo la Mungu la kwamba “tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho.” (2 Wakorintho 7:1) Kuvuta tumbako vilevile kunaiharibu afya ya wale walio karibu ambao wanalazimika kuvuta ule moshi, hivyo mvutaji wa tumbako anavunja sheria ya Mungu inayosema Mkristo amepaswa kupenda jirani yake.—Mathayo 22:39..

22. (a) Biblia inasema nini juu ya damu? (b) Ni kwa sababu gani kuingiza damu mishipani si tofauti na “kula” damu? (c) Ni nini kinachoonyesha kwamba ‘kujiepusha na damu’ maana yake ni kutokuitia katika mwili wako hata kidogo?

22 Zoea jingine linalopendwa na watu wengi katika sehemu mbalimbali za ulimwengu ni kula damu. Hivyo watu wanakula wanyama wasioondolewa damu vizuri au huenda damu ikaondolewa na kutumiwa katika chakula. Hata hivyo Neno la Mungu linakataza kula damu. (Mwanzo 9:3, 4; Mambo ya Walawi 17:10) Basi, namna gani kutiwa damu mishipani? Huenda watu fulani wakawaza kwamba kutiwa damu mishipani si “kula.” Lakini, je! sivyo ilivyo kwamba mgonjwa anaposhindwa kula chakula kwa mdomo wake mara nyingi daktari anapendekeza alishwe kwa njia ile ile inayotumiwa kumtia mtu damu mishipani? Biblia inatuambia ‘tujiepushe na damu.’ (Matendo 15:20, 29) Hiyo maana yake nini? Kama daktari angekuambia ujiepushe na pombe, je! hiyo ingekuwa na maana ya kwamba haikupasi uinywe tu kupitia kinywa chako bali kwamba ungeweza kuipitisha moja kwa moja katika mishipa yako? Hata kidogo! Vivyo, pia, ‘kujiepusha na damu’ maana yake ni kutokuitia katika mwili wako hata kidogo.

23. (a) Ni uamuzi gani ambao unahitaji kuufanya? (b) Ni nini kitakachoonyesha uamuzi ambao umefanya?

23 Ni lazima umwonyeshe Yehova Mungu kwamba wewe uko upande wa mfumo (taratibu) wake mpya na si sehemu ya ulimwengu huu. Jambo hilo linataka ufanye uamuzi. Uamuzi unaohitaji kufanya ni kumtumikia Yehova, kufanya mapenzi yake. Huwezi kuwa mwenye kusita-sita, kama walivyokuwa Waisraeli fulani nyakati za kale. (1 Wafalme 18:21) Kwa maana ukumbuke kwamba, ikiwa humtumikii Yehova, basi unamtumikia Shetani. Labda wewe utasema uko upande wa mfumo mpya wa Mungu, lakini mwenendo wako unasema nini? Kuwa upande wa mfumo mpya wa Mungu kunatia ndani kuepuka mazoea yote ambayo Mungu analaumu na ambayo hayatakuwa katika mfumo wake mpya wenye uadilifu.

[Picha katika ukurasa wa 209]

Ni ulimwengu gani ambao Yesu hakuombea na ambao wanafunzi wake si sehemu yake?

[Picha katika ukurasa wa 211]

Katika Biblia, dini ya uongo inafananishwa na kahaba mlevi, na serikali ya ulimwengu anayoipanda inafananishwa na mnyama

Maisha ya upotovu ni sehemu ya ulimwengu wa Shetani. Vilevile mfumo wa kibiashara wenye pupa ni sehemu yake mashuhuri

[Picha katika ukurasa wa 213]

Kwa kuwa wakati wa kuzaliwa kwa Yesu wachungaji walikuwa bado malishoni pamoja na mifugo yao usiku, yeye hawezi kuwa alizaliwa Desemba 25

[Picha katika ukurasa wa 214]

Watumishi wa Mungu walikataa kuabudu sanamu iliyosimamishwa na mfalme. Wewe ungefanya nini katika hali inayofanana na hiyo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki