Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 69-uku. 74
  • Dunia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Dunia
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Dunia Itachomwa Moto?
    Amkeni!—1997
  • Je, Dunia Itaharibiwa?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Je, Dunia Yetu Itaharibiwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Je, Dunia Itaharibiwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 69-uku. 74

Dunia

Maana: Katika Maandiko, neno “dunia” linatumiwa katika maana zaidi ya moja. Kwa kawaida tunalifikiria kuwa linamaanisha sayari yenyewe, ambayo Yehova aliiumba ikiwa na vitu vya kuendeleza uhai wa binadamu kwa kusudi la kufanya maisha yetu yaridhishe sana. Hata hivyo, tunapaswa kufahamu kwamba neno “dunia” huenda likatumiwa pia kumaanisha, kwa mfano, watu wanaoishi duniani au kikundi cha watu wenye tabia fulani.

Je, sayari ya Dunia sayari itaharibiwa katika vita vya nyukilia?

Kulingana na Biblia, kusudi la Mungu kwa dunia ni nini?

Mt. 6:10: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”

Zab. 37:29: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”

Ona pia Mhubiri 1:4; Zaburi 104:5.

Je, kuna uwezekano kwamba, kwa kuwa mataifa hayajali kusudi la Mungu, huenda yakaiharibu kabisa dunia isiweze kukaliwa?

Isa. 55:8-11: “[Neno la Yehova ni:] Kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo njia zangu zilivyo juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu. . . . Neno langu . . . halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”

Isa. 40:15, 26: “Tazama! [Kwa maoni ya Yehova Mungu] Mataifa ni kama tone kutoka katika ndoo; nayo yamehesabiwa kuwa kama mavumbi membamba juu ya mizani. . . . ‘Inueni macho yenu juu, mwone [jua, mwezi, na mabilioni ya nyota]. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye msukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.’” (Nguvu za nyukilia ambazo mataifa yametengeneza zinawaogopesha wanadamu. Lakini mabilioni ya nyota yana nguvu nyingi zaidi za nyukilia ambazo sisi hatuwezi kuzielewa. Ni nani aliyeumba na kuongoza vitu hivyo vyote vya mbinguni? Je, Yeye hawezi kuyazuia mataifa yasitumie silaha zao za nyukilia kwa njia inayoweza kuzuia kusudi lake? Jambo linaloonyesha kwamba Mungu anaweza kufanya hivyo ni jinsi alivyoharibu majeshi ya Misri wakati Farao alipotaka kuzuia ukombozi wa Israeli.—Kut. 14:5-31.)

Ufu. 11:17, 18: “Tunakushukuru wewe, Yehova Mungu, Mweza-Yote, Yeye aliyeko na aliyekuwako, kwa sababu umechukua nguvu zako kuu na kuanza kutawala ukiwa mfalme. Lakini mataifa wakawa na ghadhabu, nayo ghadhabu yako mwenyewe ikaja, na wakati uliowekwa . . . kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.”

Je, Mungu mwenyewe ataiharibu dunia kwa moto?

Je, andiko la 2 Petro 3:7, 10 (UV) linaunga mkono maoni hayo? “Mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu. . . . Siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea [“zitateketezwa,” ZSB; “itatoweka,” BHN; “zitafunuliwa,” NW].” (Ona: Kodeksi ya Sinaitiko na Vatikani MS 1209, zote mbili zikiwa za karne ya nne W.K., zinasema “zitafunuliwa.” Hati za baadaye, Kodeksi ya Aleksandrino ya karne ya 5 na hati iliyosahihishwa ya Klementina ya karne ya 16 ya Vulgata, zinasema “zitateketea.”)

Je, andiko la Ufunuo 21:1 (UV) linaonyesha kwamba dunia yetu itaharibiwa? “Kisha nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena.”

Ili ufafanuzi wa mistari hiyo uwe sahihi, lazima upatane na muktadha, pamoja na maandiko mengine ya Biblia

Ikiwa maandiko haya (2 Petro 3:7, 10 na Ufunuo 21:1) yanamaanisha kwamba Dunia halisi itateketezwa kwa moto, basi mbingu halisi (nyota na vitu vingine vya mbinguni) pia zitaharibiwa kwa moto. Hata hivyo, maoni hayo ya kijuujuu yanapingana na uhakikisho ulio katika maandiko kama vile Mathayo 6:10, Zaburi 37:29 na Zaburi 104:5, pia Methali 2:21, 22. Zaidi ya hayo, je, moto unaweza kuteketeza jua na nyota ambazo tayari ni moto sana? Kwa hiyo neno “dunia” katika maandiko yaliyotajwa hapo juu bila shaka lina maana tofauti.

Katika Mwanzo 11:1, Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 2:1, 2, Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati 16:31, Zaburi 96:1, n.k., neno “dunia” linatumiwa katika maana ya mfano, likimaanisha wanadamu, jamii ya binadamu. Je, inawezekana kwamba andiko la 2 Petro 3:7, 10 na la Ufunuo 21:1, yana maana hiyohiyo?

Ona kwamba, katika andiko la 2 Petro 3:5, 6 (pia 2:5, 9), hali hiyo inalinganishwa na Gharika ya siku za Noa, ambapo jamii ya binadamu waovu iliharibiwa, lakini Noa na nyumba yake, na pia dunia yenyewe, walihifadhiwa. Vivyo hivyo, andiko la 2 Petro 3:7 linasema kwamba wale watakaoharibiwa ni “watu wasiomwogopa Mungu.” Maoni ya kwamba katika andiko hilo “dunia” inamaanisha jamii ya binadamu waovu yanapatana kabisa na maandiko mengine ya Biblia, kama maandiko yaliyotajwa. Kile ‘kinachofunuliwa’ ni “dunia” ya mfano, au jamii ya binadamu waovu; yaani, Yehova atachoma kana kwamba kwa moto udanganyifu wote, akifichua uovu wa jamii ya binadamu wasiomwogopa Mungu na kuonyesha kwamba wanastahili kuharibiwa kabisa. Jamii hiyo ya binadamu waovu ndiyo pia “dunia ya kwanza,” inayotajwa katika Ufunuo 21:1.

Kwa hiyo, maneno ya Yesu katika Luka 21:33, (“mbingu na dunia zitapitilia mbali, lakini . . . ”) yanaweza kueleweka kuwa ni ya mfano. Vivyo hivyo, andiko la Ufunuo 21:1 linasema kuhusu “mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza.”—Ona pia Mathayo 5:18.

Je, waadilifu watapelekwa mbinguni kisha warudishwe duniani baada ya waovu kuharibiwa?

Je, andiko la Ufunuo 21:2, 3 linaunga mkono maoni hayo? Linasema: “Nikaona pia lile jiji takatifu, Yerusalemu Jipya, likishuka kutoka mbinguni kwa Mungu na limetayarishwa kama bibi-arusi aliyepambwa kwa ajili ya mume wake. Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao.’” (Je, taarifa ya kwamba Mungu “atakaa” pamoja na wanadamu na kwamba “atakuwa pamoja nao” inamaanisha kwamba yeye atakuwa na mwili wa kimwili? Hilo haliwezekani, kwa sababu Yehova alimwambia Musa hivi: “Hakuna mwanadamu anayeweza kuniona na bado aishi.” [Kut. 33:20] Kwa hiyo, basi, wale watakaokuwa sehemu ya Yerusalemu Jipya hawatarudi duniani wakiwa watu wenye mwili. Basi, Mungu ‘atakuwaje pamoja na’ wanadamu, na Yerusalemu Jipya ‘litashukaje kutoka mbinguni’? Bila shaka dokezo moja linapatikana katika andiko la Mwanzo 21:1, linalosema kwamba Mungu ‘alimjia’ Sara, akamjalia kuzaa mwana uzeeni. Andiko la Kutoka 4:31 linatuambia kwamba Mungu ‘aliwajilia’ Israeli kwa kumtuma Musa awe mkombozi. Andiko la Luka 7:16 linasema kwamba kupitia huduma ya Yesu, Mungu ‘alikuja’ kwa watu wake. [Maandiko hayo yametoka katika UV, VB, BHN] Tafsiri nyingine zinatumia maneno Mungu ‘aliwaelekezea fikira’ watu wake [NW] au ‘aliwaangalia,’ [ZSB]. Kwa hiyo maana ya andiko la Ufunuo 21:2, 3 lazima iwe kwamba Mungu ‘atawajilia,’ au atakuwa pamoja na wanadamu kupitia Yerusalemu Jipya la mbinguni, na kupitia hilo baraka zitawajia wanadamu watiifu.)

Met. 2:21, 22, UV: “Wanyofu watakaa katika nchi [“duniani,” NW], na wakamilifu [“waaminifu,” BHN] watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” (Kumbuka andiko hilo halisemi kwamba waaminifu watarudi duniani bali “watadumu ndani yake.”)

Je, kusudi la Mungu la kwanza kwa dunia limebadilika?

Mwa. 1:27, 28: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba. Mungu akawabariki na Mungu akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.’” (Basi Mungu alionyesha kusudi lake la kutaka dunia ijawe na wazao wa Adamu na Hawa wakiwa watunzaji wa paradiso ya duniani pote. Baada ya Mungu kuiumba dunia hii vizuri ili iwe makao ya wanadamu, na kuifanya kuwa ya pekee kati ya sayari zote ambazo mwanadamu amechunguza kwa kutumia darubini na vyombo vya angani, je, Muumba alilitupilia mbali kusudi lake, na kuliacha milele bila kulitimiza kwa sababu ya dhambi ya Adamu?)

Isa. 45:18: “Kwa maana Yehova, Muumba wa mbingu, Yeye Mungu wa kweli, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu, amesema hivi: ‘Mimi ni Yehova, wala hakuna mwingine.’” (Ona pia Isaya 55:10, 11.)

Ikiwa hakuna mtu atakayekufa katika Mfumo Mpya wa Mungu, je, watu wote watatoshea duniani?

Kumbuka kwamba Mungu alipoeleza kusudi lake kwa ajili ya dunia alisema: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.” (Mwa. 1:28) Mungu alimpa mwanadamu uwezo wa kuzaa, na wakati kusudi Lake kuhusu jambo hilo litakapotimizwa Yeye anaweza kufanya uzazi ukome duniani.

Mungu atawapa watu wa aina gani uzima usio na mwisho duniani?

Sef. 2:3: “Mtafuteni Yehova, ninyi nyote mlio wapole wa dunia, ambao mmetenda uamuzi Wake wa hukumu. Utafuteni uadilifu, utafuteni upole. Huenda mkafichwa katika siku ya hasira ya Yehova.”

Zab. 37:9, 11: “Wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia. . . . Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki