Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w08 4/1 kur. 10-12
  • Je, Dunia Yetu Itaharibiwa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Dunia Yetu Itaharibiwa?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kusudi la Mungu kwa Dunia
  • Biblia Haijipingi
  • Maisha Duniani—Je! Ni Safari ya Kupitia Tukielekea Mbinguni?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kusudi la Mungu Kuelekea Dunia Litatimizwa Karibuni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Dunia
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Ni Nini Kusudi la Mungu kwa Dunia?
    Mungu Anataka Tufanye Nini?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
w08 4/1 kur. 10-12

Je, Dunia Yetu Itaharibiwa?

JE, UMEWAHI kujiuliza, ‘Ni nini kitakachoipata dunia yetu?’ Kwa sababu ya mambo wanayoona yakiipata sayari yetu maridadi, watu wengi wanaamini kwamba dunia yetu huenda ikaharibiwa.

Kwa kweli, matumizi mabaya ya mali za asili zenye thamani, kama vile maji, misitu, na mazingira, yanaharibu dunia. Pia, wanasayansi fulani wanaonya kwamba huenda dunia na uhai wote ulio duniani ukaharibiwa na vitu kama vile kimondo, nyota zinazolipuka, au kupungua kwa nguvu za jua.

Wanasayansi wanaamini kwamba hatua kwa hatua—labda kwa mabilioni ya miaka—dunia itapoteza uwezo wake wa kutegemeza uhai wa wanadamu. Kitabu kimoja (Encyclopædia Britannica) kinaeleza jambo hilo kuwa “mwelekeo usioweza kubadilishwa wa kuharibika.”

Hata hivyo, Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova Mungu hataruhusu dunia yetu iharibiwe au isiweze kukaliwa. Akiwa Muumba, Mungu ana “nguvu zenye msukumo” zisizo na mipaka. Hivyo, anaweza kuendelea kuutegemeza ulimwengu wote milele. (Isaya 40:26) Kwa hiyo, unaweza kuyaamini maneno haya: “[Mungu] ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” “Msifuni, enyi jua na mwezi. Msifuni, enyi nyota zote za nuru. . . . Kwa maana yeye mwenyewe aliamuru, navyo vikaumbwa. Naye huendelea kuvisimamisha milele.”—Zaburi 104:5; 148:3-6.

Kusudi la Mungu kwa Dunia

Mungu hakukusudia kamwe kwamba dunia itumiwe vibaya na kuchafuliwa kama ilivyo leo. Badala yake, Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, naye akawaweka katika bustani maridadi. Bila shaka, Paradiso yao haingebaki maridadi ikiwa haingetunzwa. Mungu aliwapa kazi ya ‘kuilima na kuitunza.’ (Mwanzo 2:8, 9, 15) Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza wakamilifu kazi yenye kupendeza na kuridhisha kama nini!

Lakini kusudi la Mungu kwa dunia lilitia ndani mambo mengi zaidi ya kuitunza bustani hiyo ya kwanza. Alitaka dunia yote ifanywe kuwa paradiso. Hiyo ndiyo sababu Mungu aliwaamuru Adamu na Hawa hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.”—Mwanzo 1:28.

Inasikitisha kwamba kusudi la Mungu lilipingwa na malaika mmoja mwenye kiburi ambaye alikuja kuitwa Shetani. Alitamani sana Adamu na Hawa wamwabudu. Akizungumza kupitia nyoka, Shetani aliwachochea waasi utawala wa Mungu. (Mwanzo 3:1-6; Ufunuo 12:9) Bila shaka, ubinafsi na kukosa kwao kuthamini kulimhuzunisha sana Muumba wetu. Lakini jambo moja ambalo uasi wao haukuweza kufanya ni kubadili kusudi la Yehova Mungu kwa dunia. Anasema hivi: “Neno langu linalotoka katika kinywa changu . . . halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:11.

Yehova ana sababu nzuri ya kuruhusu uasi wa Shetani uendelee mpaka siku zetu. Katika kipindi hicho chote, wanadamu wamejaribu namna mbalimbali za kujitawala, na matokeo yamethibitisha kwamba kinyume na madai ya Shetani, hawawezi kufanikiwa wasipomtegemea Mungu.a—Yeremia 10:23.

Ingawa uasi wa Shetani umesababisha madhara mengi, kwa maelfu ya miaka, Mungu ameendelea kuwabariki wanadamu fulani wanyoofu. Pia, amehakikisha kwamba katika Biblia kuna masimulizi kuhusu matokeo ya kumtii Mungu au kukataa utawala wake. Zaidi ya hayo, Yehova amefanya mambo mazuri ajabu kwa ajili ya wakati wetu ujao. Kwa upendo, amewatayarishia wanadamu Mkombozi kwa kumtuma Mwana wake mpendwa, Yesu Kristo, atufundishe njia bora zaidi ya maisha na atoe uhai wake kwa ajili yetu. (Yohana 3:16) Kwa kuwa Yesu hakustahili kufa, kifo chake kimetumiwa na Mungu kama njia inayofaa kisheria kununua kile ambacho Adamu na Hawa walipoteza, yaani, tarajio la kuishi milele katika paradiso duniani.b Ili kutimiza hilo, Yehova amesimamisha serikali ya kimbingu ili kuwatawala wanadamu, naye amemweka rasmi Mwana wake, Yesu Kristo aliyefufuliwa, awe Mfalme wa Ufalme huo. Mpango huo mzuri sana utahakikisha kwamba kusudi la Mungu kwa dunia limetimizwa.—Mathayo 6:9, 10.

Kwa hiyo, unaweza kuwa na uhakika kabisa katika ahadi hizi zinazopatikana katika Biblia: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia. Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” “‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’ Na Yule aliyeketi juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’”—Zaburi 37:9, 29; Ufunuo 21:3-5.

Biblia Haijipingi

Hata hivyo, huenda watu fulani wakajiuliza, ‘Tunaweza kupatanisha namna gani Maandiko ambayo tumezungumzia na maandiko mengine yanayoonekana kuwa yanazungumzia mwisho wa dunia?’ Acheni tuchunguze mifano fulani. Kuchunguza mifano hiyo kutaonyesha kwamba Biblia haijipingi.

Mapema kabla wanasayansi hawajagundua kwamba vitu vyote vya asili vina “mwelekeo usioweza kubadilishwa wa kuharibika,” mtunga-zaburi wa Biblia aliandika hivi: “Wewe [yaani, Mungu] uliiweka misingi ya dunia zamani za kale, nazo mbingu ni kazi ya mikono yako. Hizo zitaangamia, lakini wewe mwenyewe utaendelea kusimama; nazo zote zitachakaa kama vazi. Utazibadili kama mavazi, nazo zitamaliza zamu yake. Lakini wewe ni yuleyule, nayo miaka yako mwenyewe haitamalizika.”—Zaburi 102:25-27.

Alipoandika maneno hayo, mtunga-zaburi hakuwa akipinga kusudi la Mungu la milele kwa dunia. Badala yake, alikuwa akitofautisha kuwepo kwa Mungu kwa milele na mwelekeo wa kuharibika wa vitu ambavyo Mungu ameumba. Pasipo nguvu za Mungu za milele za kufanyiza vitu upya, ulimwengu—kutia ndani mfumo wa jua ambao tunautegemea kwa ajili ya nuru, nishati, na kuimarisha dunia—utaharibika hatua kwa hatua na hatimaye kuangamia kabisa. Hivyo, ikiachiliwa, dunia yetu ‘itachakaa,’ au itaangamia milele.

Kuna mistari mingine katika Biblia ambayo mwanzoni huenda ikaonekana kuwa inapingana na kusudi la Mungu la awali kwa dunia. Kwa mfano, Biblia inazungumza kuhusu mbingu na dunia ‘zikipitilia mbali.’ (Ufunuo 21:1) Kwa kweli, maneno hayo hayapingi ahadi hii ya Yesu: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Basi Biblia inamaanisha nini inaposema kwamba mbingu na dunia ‘zitapitilia mbali’?

Mara nyingi Biblia inatumia neno “dunia” kwa njia ya mfano kumaanisha jamii ya wanadamu. Kwa mfano, fikiria mstari huu: “Dunia yote iliendelea kuwa na lugha moja na maneno ya namna moja.” (Mwanzo 11:1) Bila shaka, katika mstari huu “dunia” inarejelea watu waliokuwa wakiishi duniani. Mfano mwingine unapatikana katika Zaburi 96:1, inayosema hivi kulingana na King James Version: “Mwimbieni BWANA, dunia yote.” Ni wazi kwamba mstari huu na mistari mingine mingi inatumia neno “dunia” katika njia ya mfano kurejelea watu.—Zaburi 96:13.

Nyakati nyingine Biblia hutumia mbingu au nyota kufananisha mamlaka zinazotawala duniani. Kwa mfano, watawala wenye kukandamiza wa Babiloni walifananishwa na nyota kwa sababu walijiinua juu ya wote waliowazunguka. (Isaya 14:12-14) Kama ilivyotabiriwa, “mbingu” za ufananisho za Babiloni, au watawala, na “dunia,” yaani, watu waliounga mkono utawala huo, zilikomeshwa mwaka wa 539 K.W.K. (Isaya 51:6) Hilo liliwawezesha Wayahudi waliotubu warudi Yerusalemu, ambako “mbingu mpya,” yaani, watawala wapya, walitawala juu ya “dunia mpya,” jamii ya watu waadilifu.—Isaya 65:17.

Ni wazi kwamba maneno ya Biblia kuhusu ‘kupitilia mbali’ kwa mbingu na dunia kunamaanisha mwisho wa serikali za wanadamu zilizopotoka na watu wasiomwogopa Mungu wanaoziunga mkono. (2 Petro 3:7) Hilo litaifungulia njia serikali ya Mungu ya kimbingu ibariki jamii mpya ya wanadamu waadilifu, kwa kuwa “kulingana na ahadi [ya Mungu] tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.

Hivyo, unaweza kuiamini ahadi ya Mungu ya kwamba makao yetu ya kidunia yatadumu milele. Zaidi ya hilo, Biblia inaonyesha yale unayopaswa kufanya ili uishi wakati huo mzuri ajabu dunia yote itakapogeuzwa iwe paradiso. Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Kwa nini usiazimie kuchunguza yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu kitakachoipata dunia na wanadamu? Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukusaidia kufanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa habari zaidi kuhusu kwa nini Mungu ameruhusu mateso, ona ukurasa wa 106-114 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

b Kwa habari zaidi kuhusu kifo cha Yesu cha kidhabihu, ona ukurasa wa 47-56 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Biblia inaonyesha kwamba makao yetu ya kidunia yatadumu milele

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Background globe: NASA/The Visible Earth (http://visibleearth.nasa.gov/); polar bear: © Bryan and Cherry Alexander Photography

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki