Maisha Duniani—Je! Ni Safari ya Kupitia Tukielekea Mbinguni?
JE! SAYARI yetu ni mahali pa kuzaliwa tu, kuishi miaka michache ya taabu halafu, ikiwa sisi ni wema, kuiacha twende kwenye maisha ya raha nyingi ya milele mbinguni—au, ikiwa sisi ni wabaya, twende kwenye maisha ya motoni mahali pa mateso? Kwa habari ya dunia yenyewe, je, utakuja wakati itakapoteketezwa iwe kaa?
Viongozi wengi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wangesema ndiyo. Je! wewe unakubaliana na maoni hayo? Lakini, je, Biblia inasema nini juu ya dunia na kusudi la Mungu la kuumba wanadamu juu yayo? Zaburi 115:16 inajibu moja kwa moja hivi: “Mbingu ni mbingu za [Yehova], bali [dunia] amewapa wanadamu.”
Tukiweka kando mafundisho yote ya kidini yasiyo na msingi na tukiangalia maandishi ya Biblia tunaambiwa kwamba tangu mwanzo wa maisha ya mwanadamu duniani Mungu alifanya watu wawili wa kwanza kwa mfano na sura Yake. (Mwanzo 1:26-28) Hakuna dokezo hata kidogo kwamba kusudi la Mungu kwao lilikuwa kwamba wao na watoto wao hatimaye wangekufa na kwenda mbinguni au mahali pengine. Kwa kadiri ambavyo wangetimiza mgawo wao waliopewa na Mungu wa ‘kuzaana, waongezeke, na kuijaza dunia,’ polepole dunia ingejawa na watoto wao.
Mahali pa pekee, bustani ya Edeni, palitayarishwa na Mungu hata kwamba wanadamu wa kwanza wakawa na makao makamilifu. Maandishi yanasema: “[Yehova] Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.” (Mwanzo 2:8, 15) Ingepanuliwa kama ilivyohitajiwa, mpaka dunia yote hatimaye iwe Paradiso yenye chakula kitamu sana na cha afya kisicho na mwisho na vitu vingine.
Dunia hiyo ingekuwa zaidi ya makao ya muda au safari ya kupitia watu wakielekea kwenye maisha mengine. Jambo hilo linaonyeshwa wazi na maneno ya Mungu yanayofuata halafu aliyomwambia Adamu: “[Yehova] Mungu akamwagiza huyo mtu, akisema, Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.”—Mwanzo 2:16, 17.
Walipojaribiwa na Ibilisi, Hawa halafu Adamu walikosa kutii amri hiyo nao wakapokea adhabu ya haki ya Mungu, kifo. Lakini jiulize mwenyewe, ‘Ingekuwaje kama hawangekosa kutii?’ Maelekeo ya waziwazi ni kwamba wangeendelea kuishi—bila kufa kamwe. Ndiyo, Adamu na Hawa wangalikuwa wangali hai leo, wakiwa na afya na furaha kamili.
Namna Gani Juu ya Wakati Ujao wa Dunia?
Albert Barnes, katika kichapo chake Notes on the New Testament, anaeleza kwa muhtasari imani ya ujumla ya Jumuiya ya Wakristo kuhusu wakati ujao wa dunia. Kuhusu 2 Petro 3:10, mwelezaji huyo aliandika:
“Dunia pia, na kazi zilizomo, itateketezwa. Yaani, ziwe ni kazi za Mungu au mwanadamu—uumbaji wote wa majani na wanyama, na minara yote, miji, makao ya kifalme, kazi za wenye akili sana, michoro, sanamu, vitabu, ambavyo wanadamu wamefanya.”
Kama ilivyotajwa hapo, maoni katika Jumuiya ya Wakristo kwa muda mrefu yamekuwa ni kwamba wakati utakuja ambapo dunia haitakuwa tena makao ya wanadamu au kitu cho chote kilicho hai. Sayari yetu, kwa maoni ya wengi wanaoenda kanisani, itakuwa imekwisha kutimiza kusudi yalo, kwa maana kulingana na wao dunia ni mahali pa kujaribiwa tu penye kuongoza ama mbinguni au kwenye moto wa mateso.
Lakini, kufikia hapa ungefanya vema kufikiria hivi, Je! kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia na wanadamu lilibadilika wakati Adamu na Hawa walipofanya dhambi? Utaona kwamba hakuna ye yote anayeweza kuonyesha kifungu cha maneno hata kimoja katika Biblia kinachosema hivyo, Tofauti yake, miaka mingi baada ya watu wawili wa kwanza kufanya dhambi, nabii Isaya aliongozwa na roho ya Mungu aandike hivi:
“Maana [Yehova], aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.” Isaya alitaja maneno ya Yehova kwamba: “Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote.” (Isaya 45:18; 46:10) Pia mtunga zaburi aliandika juu Yake: “Uaminifu wako upo kizazi baada ya kizazi, umeiweka nchi, nayo inakaa.”—Zaburi 119:90.
Waweza kuona Biblia inataja kwamba Mungu alipoiumba dunia, aliifanya iwe ya kudumu katika anga na kwamba kusudi lake la hakika la kuiumba lilikuwa ikaliwe na watu. Kusudi hilo halijabadilika. Mungu atahakikisha kwamba kusudi lake litatimizwa kikamili.
Lakini je, Biblia haionyeshi kwamba watu wengine wataenda mbinguni? Ndiyo, Biblia inafundisha kwamba hesabu ndogo itaenda mbinguni kwa kusudi la pekee. Mungu hahitaji wanadamu mbinguni; wala hana lazima ya kuwapeleka mbinguni ili awape furaha ya milele. Kama ingekuwa hivyo, kwa sababu gani hakuwaumba wakiwa mbinguni, na kuondolea mbali taabu na msukosuko wote ambao wamepatwa nao wakiwa duniani?
Hata hivyo, Adamu na Hawa walichagua kutokumtii Mungu, kwa kutumia uwezo wao wa kujiamulia aliokuwa amewapa viumbe wenye akili, Mungu alichukua hatua ya mara moja ili kuhakikisha kwamba kusudi lake kwa dunia na wanadamu wenye kuishi juu yake lingetimizwa. Mambo yote hayakufunuliwa kwa wanadamu mpaka baada ya karne nyingi kupita. Lakini iko wazi kutokana na ufunuo wa kile ambacho Biblia inaita “siri takatifu” kwamba hapo kwa hapo Mungu alitokeza kusudi lake zuri ajabu la kukomboa wanadamu. Hayo yalikuwa “kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu,” yaani, kabla Adamu na Hawa hawajaweza kuzaa watoto ambao wangeweza kukombolewa, kama vile mwana wao mwaminifu Habili.—Warumi 16:25, NW; Waefeso 1:4.
Ni wazo dogo tu la kusudi hilo lililotolewa wakati ahadi ilipotolewa kwamba “uzao” ungezaliwa na “mwanamke” fulani na kwamba “uzao” huo ungeponda kichwa cha “nyoka,” na kuleta faraja kutokana na matatizo yaliyoletwa na uasi. (Mwanzo 3:14, 15) Kama vile ua zuri sana linavyochanua pole kwa pole, habari zaidi juu ya “uzao” huo zilifunuliwa hatua kwa hatua hata ikawa kwamba, baada ya Yesu kuja, maana ya “siri takatifu” hiyo ikawa wazi kabisa. Ndiyo, Mungu alijulisha kwamba “uzao” huo ungekuwa ni Mwanaye mzaliwa wa pekee na washiriki 144,000 ambao “wamenunuliwa katika wanadamu.” Pamoja na Kristo wataufanyiza Ufalme, au serikali mpya ya kuitawala dunia.—Ufunuo 14:3, 4; Wagalatia 3:16, 26-29.
Mungu hakutangulia kuandika majina ya watu ambao wangetwaliwa kutoka duniani waende mbinguni ili wawe washiriki wa serikali hiyo, lakini alitangulia kuandika kwamba kikundi hicho kingekuwapo kwa kupatana na mapenzi yake ya kimungu. Wale ambao wangechaguliwa wawe washiriki wacho, Mungu angeamua baadaye ni nani, baada ya Mwanaye kuja duniani na kufungua njia ya kuwa na uhai wa kimbingu.
Baada ya hiyo “siri takatifu” kufunuliwa kikamili, mtume Paulo, akiwa mmoja wa wale waliochaguliwa kwenda mbinguni, angeweza kuwaandikia hayo wengine waliokuwa na tumaini kama hilo. Kuhusu fadhili zisizostahilika alizoonyesha Mungu kwa kufanya hivyo, Paulo alisema:
“Alizifanya hizo ziwe tele kutuelekea sisi katika hekima yote na akili nzuri, kwa kuwa alitujulisha siri takatifu ya mapenzi yake. Ni kulingana na furaha yake njema aliyokusudia ndani yake mwenyewe kwa ajili ya usimamizi katika utimilifu wa nyakati zilizowekwa, yaani, kuvikusanya tena vitu vyote pamoja katika Kristo, vitu vilivyomo mbinguni na vitu vilivyomo duniani. Naam, katika yeye, ambaye sisi pia tuligawiwa katika umoja naye tuwe warithi, kwa sababu tulitangulia kuagizwa rasmi [si kama watu mmoja mmoja bali kama kikundi cha hesabu kamili iliyowekwa] kulingana na kusudi lake yeye anayetenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.”—Waefeso 1:8-11, NW; Ufunuo 14:1-4.
Je! Dunia Itateketezwa?
Lakini namna gani maneno ya Petro kwamba “mbingu za sasa na [dunia] zimewekwa akibakwa moto”? (2 Petro 3:7) Kwa wazi haiwezi ikawa Petro anazungumza juu ya mbingu na dunia za halisi ambazo Biblia inasema zitabaki milele. (Mhubiri 1:4) Mungu hana sababu ya kukomesha mbingu anamokaa, wala viumbe vyote halisi vya kimbingu. Na dunia mviringano yenyewe haijampa sababu yo yote ya kuiharibu, yajapokuwa yale ambayo watu wamefanya kwa kuiharibu na kuichafua sura. Yehova mwenyewe anatuambia kwamba dunia ilipoumbwa ikiwa ya namna yake ya pekee na uzuri, wana wake wa kimbingu ‘waliimba pamoja, wakapiga kelele kwa furaha.’—Ayubu 38:4-7.
Kusudi zima la Mungu la kukusanya hesabu teule iwe mbinguni ni kutimiza mapenzi yake duniani, ndiyo, kutimiza sala ambayo imesemwa kwa muda mrefu, “Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:10) Zaidi ya hayo, Yesu, akitaja Zaburi 37:10, 11, alitia maneno haya katika Mahubiri yake ya Mlimani yajulikanayo sana: “[Wenye furaha ni] wenye upole; maana hao watairithi [dunia]. (Mathayo 5:5) Unaweza kuona wazi-wazi kutokana na maneno hayo kwamba Yesu hakuwa na maoni kwamba dunia ilikuwa safari ya kupitia tukiwa tunaelekea mbinguni. Ingawa “kundi dogo” litaurithi utawala juu ya dunia kwa muda fulani, ahadi ya Yesu inapanuka pia kutia ndani mabilioni yote ya wanadamu watakaokuwa na urithi wa kidunia. (Luka 12:32; Ufunuo 7:9, 10) Hiyo haitakuwa kwa muda mfupi tu wa maisha ya huzuni, kama tunayoyajua wakati huu, bali kwa umilele katika furaha!
Petro anapotaja “mbingu” zitakazoteketezwa, anasema juu ya “mbingu” za mfano. Hizo ni serikali zinazotawala watu ambao ndio wanaoifanyiza “dunia.” Ni kama kitabu Cyclopcedia cha McCIintock na Strong kinavyosema:
“Po pote tamasha ya njozi ya kiunabii inapokuwa, mbingu zinafananisha . . . mkusanyo wote wa mamlaka zinazotawala, ambazo, kuhusiana na raia katika dunia, ni mbingu za kisiasa, zikiwa juu na zikitawala raia hao, kama vile mbingu halisi zilivyo juu na zinavyotawala dunia.”—Kit. 4, uku. 122.
Mamlaka za kiserikali ambazo zimefanyizwa na wanadamu wasio wakamilifu na mara nyingi wanadamu wenye kuonea zitaondolewa mbali katika “siku ya Yehova,” kama Petro alivyotaja. Mahali pazo patachukuliwa na “mbingu mpya” ambazo washiriki wazo watakuwa ni Yesu Kristo na hesabu ile yenye kipimo ya wale watakaoenda mbinguni ili kuufanyiza Ufalme huo ulio serikali. Ndiyo sababu Petro aliandika hivi: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:12, 13, NW.
Kuhusu wale ambao ni washiriki wa “mbingu mpya,” serikali hiyo mpya ya kimbingu juu ya dunia, Biblia inasema: “Mwenye furaha na mtakatifu ni ye yote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; kifo cha pili hakina mamlaka juu ya hao, lakini watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye kwa hiyo miaka elfu.”—Ufunuo 20:6, NW.
Watatawala juu ya nani? Kwa wazi raia juu ya dunia—ama sivyo mstari huo haungekuwa na maana yo yote. “Dunia” ya kale itafikia mwisho wake, kama kwamba kwa moto, wakati watu waovu na mashirika yao watakapokomeshwa, na kuacha jamii “mpya” ya kidunia peke yake. Wakati uhalifu, uvunjaji wa sheria na uasi yatakapokuwa mambo yaliyokwisha kupita, na wakati afya kamili na furaha isiyo na kikomo vitakapokuwa urithi wa kila mtu aliye hai, kweli kweli hiyo itakuwa jamii “mpya” ya watu, “dunia mpya”!
Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba ahadi hizo za Mungu zitatimizwa.
[Blabu katika ukurasa wa 22]
Kristo atatawala akiwa Mfalme juu ya mamilioni ya raia za kibinadamu wenye kufurahia Paradiso ya kidunia iliyorudishwa
[Picha katika ukurasa wa 21]
Mungu aliweka Adamu na Hawa wapi na alikusudia waishi wapi?