Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 1/8 kur. 26-27
  • Je, Dunia Itachomwa Moto?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Dunia Itachomwa Moto?
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Mungu Hujali?
  • “Dunia ya Kwanza”
  • “Dunia Mpya”
  • Dunia
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Je, Dunia Itaharibiwa?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Je, Dunia Yetu Itaharibiwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Ni Nini Kitakachoipata Dunia-Sayari?
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 1/8 kur. 26-27

Maoni ya Biblia

Je, Dunia Itachomwa Moto?

KUUNGUZWA katika maangamizi makubwa ya nyukilia, kuunguzwa na jua lenye kuvimba, au kuchomwa na mungu mwenye hasira—huenda namna ya maangamizi ikatofautiana, lakini watu wengi wanasadiki kwamba sayari Dunia, makao ya wanadamu, itaharibiwa katika moto ulao kila kitu, uharibifu mkubwa.

Baadhi ya watu hutaja maandiko ya Biblia ambayo hutabiri moto mkubwa wa kimungu kuwa malipo kwa makosa ambayo wanadamu wamefanyia dunia. Wengine hukubaliana na maoni ya Paul Davies, profesa katika Chuo Kikuu cha Adelaide, Australia, ambaye huandika juu ya yale afikiriayo kuwa uharibifu wa dunia kwa moto usioepukika. Yeye hunadharia katika kitabu chake The Last Three Minutes: “Kadiri jua liendeleavyo kuvimba, litaimeza . . . Dunia katika mzingo wake wenye moto. Sayari yetu itageuka kuwa makaa.” Ukweli ni nini kuhusu hali ya baadaye ya dunia? Tueleweje maandiko ya Biblia ambayo huonekana kutabiri maangamizi ya moto?

Je, Mungu Hujali?

Katika Yeremia 10:10-12 tunaarifiwa: “Bali BWANA ndiye Mungu wa kweli. . . . Ameiumba dunia kwa uweza wake, ameuthibitisha ulimwengu kwa hekima yake, na kwa ufahamu wake amezitandika mbingu.” Mungu aliiumba dunia na kuiweka imara. Hivyo kwa hekima, upendo, na uelewevu, aliitayarisha dunia kwa uangalifu ili idumu kwa wakati usio dhahiri ikiwa makao mazuri ya wanadamu.

Kuhusu uumbaji wa wanadamu uliofanywa na Mungu, Biblia yaripoti: “Mwanamume na mwanamke aliwaumba. Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha.” (Mwanzo 1:27, 28) Alipomaliza kazi yake ya kuumba, aliweza kutangaza waziwazi kwamba “ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Alitaka idumu hivyo. Kama vile wazazi fulani watarajiao mtoto hubuni na kutayarisha chumba cha mtoto anayetazamiwa kuzaliwa, Mungu alipanda bustani nzuri akamweka mwanamume Adamu hapo ili aitunze.—Mwanzo 2:15.

Adamu aliuacha kimakusudi ukamilifu na wajibu wake wa kuitunza dunia. Lakini, je, Muumba aliliacha kusudi Lake? Isaya 45:18 laonyesha kwamba hakuliacha: “Maana BWANA, aliyeziumba mbingu, asema hivi; . . . Aliyeiumba dunia . . . , ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Ona pia Isaya 55:10, 11.) Ingawa mwanadamu aliacha wajibu wake wa utunzi, Mungu aliendelea kutimiza kusudi lake kwa dunia na wakaaji wake. Sheria iliyotolewa kwa taifa la Israeli la kale iliandaa “sabato ya kustarehe kabisa kwa ajili ya hiyo nchi” kila mwaka wa saba. Ilitia ndani sheria za fadhili ambazo zililinda wanyama kwa kadiri fulani. (Mambo ya Walawi 25:4; Kutoka 23:4, 5; Kumbukumbu la Torati 22:1, 2, 6, 7, 10; 25:4; Luka 14:5) Hii ni mifano michache katika Biblia ambayo huonyesha waziwazi kwamba Mungu hujali sana wanadamu, na yote ambayo aliweka chini ya utunzi wa mwanadamu.

“Dunia ya Kwanza”

Hivyo twaweza kupatanishaje maandiko ya Biblia ambayo yaonekana kupingana? Andiko moja kama hilo ni 2 Petro 3:7, ambalo, kulingana na Zaire Swahili Bible, husema: “Lakini mbingu zilizo sasa na dunia, zimewekwa akiba kwa moto kwa neno hili, zikilindwa hata siku ya hukumu na uharibifu wao wasioogopa Mungu.” Jingine ni Ufunuo 21:1, ambalo lasema: “Nami nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali.”

Maneno ya Petro yakichukuliwa kihalisi na sayari Dunia ikiangamizwa na moto halisi, basi mbingu halisi—nyota na magimba mengine ya mbinguni—pia yataharibiwa kwa moto. Hata hivyo, maoni hayo yapingana na uhakika uliopo katika maandiko kama vile Mathayo 6:10: “Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia,” na Zaburi 37:29, NW: “Waadilifu wenyewe watamiliki dunia, nao watakaa milele juu yayo.” Isitoshe, moto ungekuwa na matokeo gani kwa jua na nyota ambazo tayari zina joto jingi sana na hutokeza milipuko ya kinyukilia kwa kuendelea?

Kwa upande mwingine, kwa kawaida Biblia hutumia neno “dunia” katika maana ya mfano. Kwa mfano, Mwanzo 11:1 (ZSB) husema: “Na dunia nzima ilikuwa na lugha moja na usemi mumoja.” Hapa, neno “dunia” hurejezea wanadamu kwa ujumla, au jamii ya wanadamu. (Ona pia 1 Wafalme 2:1, 2; 1 Mambo ya Nyakati 16:31.) Muktadha wa 2 Petro 3:5, 6 hudokeza maana hiyohiyo ya mfano ya “dunia.” Hurejezea siku ya Noa ambapo jamii ya wanadamu waovu waliharibiwa katika Furiko lakini Noa na nyumba yake na pia tufe lenyewe walihifadhiwa. (Mwanzo 9:11) Hali kadhalika, katika 2 Petro 3:7, husema kwamba watu watakaoharibiwa ni “wasiomwogopa Mungu.” Maoni haya yakubaliana na sehemu nyingine za Biblia. Jamii ya watu waovu ambao wamekusudiwa maangamizi ndio “dunia ya kwanza” ambayo pia inarejezewa katika Ufunuo 21:1, lililonukuliwa awali.

Kwa kweli, kama vile baba wa kidunia mwenye kujali atakavyochukua hatua yoyote iwezekanayo kuhakikisha kutoharibiwa kwa nyumba yake, ndivyo Yehova Mungu anavyopendezwa sana na uumbaji wake. Wakati fulani aliwaondoa watu wasio na maadili na waliokuwa waovu kutoka Bonde la Yordani lenye rutuba akawahakikishia watunzaji hao wapya wa bara hilo, ambao walikuwa katika agano naye, kwamba ikiwa wangetunza sheria zake, ‘nchi haingewatapika pia, kwa kuitia unajisi, kwa jinsi ileile ambavyo iliyatapika kwa hakika mataifa yaliyokuwa mbele yao.’—Mambo ya Walawi 18:24-28.

“Dunia Mpya”

Leo, jamii ambayo imepotoka kingono, yenye ukatili wa kijeuri, na yenye ufisadi kisiasa imechafua dunia. Ni Mungu pekee awezaye kuiokoa. Atafanya hivyo hasa. Kwenye Ufunuo 11:18, anaahidi “kuwaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.” Dunia iliyorudishwa na kufanywa upya itakaliwa na watu wenye kuhofu Mungu na wanaowapenda wanadamu wenzao kwa weupe wa moyo. (Waebrania 2:5; linganisha Luka 10:25-28.) Mabadiliko yatakayotokea chini ya Ufalme wa kimbingu wa Mungu yatakuwa makubwa sana hivi kwamba Biblia yasema juu ya “dunia mpya”—jamii mpya ya kibinadamu.

Tusomapo maandiko kama vile Zaburi 37:29 na tuelewapo taarifa ya Kristo katika Mathayo 6:10, tunasadikishwa kwamba wala kani za asili zisizoongozwa wala mwanadamu pamoja na nguvu zake zote za uharibifu hawatakomesha sayari yetu. Hawatazuia kusudi la Mungu. (Zaburi 119:90; Isaya 40:15, 26) Wanadamu waaminifu wataishi duniani katika hali nzuri sana na shangwe isiyo na mwisho. Hiyo ndiyo kweli kuhusu hali ya baadaye ya dunia, kwani hilo ndilo kusudi la Muumba mwenye upendo wa wanadamu, na hilo limekuwa kusudi lake nyakati zote.—Mwanzo 2:7-9, 15; Ufunuo 21:1-5.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki