Sura 1
Ni Nini Kitakachoipata Dunia-Sayari?
1. Wewe unatazamia wakati ujao wa aina gani, na kwa nini?
WEWE ukiwa mmoja wa mabilioni ya watu wanaoishi sasa katika Dunia-sayari, unatazamia nini wakati ujao? Je! ungependa wakati ujao huo uwe maisha ya amani na usalama, kati ya watu wanaopendana kweli kweli? Hilo na mengi zaidi yanaweza kuwa yako. Lakini walio wengi hawatazamii wakati ujao wa jinsi hiyo. Kwa nini?
2, 3. Hatari ya vita ya silaha za nyukilia inaongozaje namna watu walivyo na maoni juu ya wakati ujao?
2 Hatari ya vita ya nyukilia imetokeza mashaka makubwa juu ya kama kutakuwako wakati ujao wo wote kwa sehemu iliyo kubwa sana ya jamii ya kibinadamu. Kombora la atomi lilipotumiwa kwa mara ya kwanza vitani mwaka wa 1945, zaidi ya wanaume, wanawake na watoto 70,000 waliuawa papo hapo. Maelfu wengi zaidi walipata kifo chenye maumivu makali wakati wa siku na miaka iliyofuata. Lakini leo kisehemu kimoja tu cha kombora moja tu kama hilo kina nguvu nyingi za mpasuko zinazolingana na zile za makombora yote yaliyoangushwa wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Kuna makumi ya maelfu ya silaha za nyukilia ambazo zimesambazwa ili zitumiwe mara moja. Bado ulimwengu unatumia siku moja dola kama 2,000,000,000 kwa mashindano ya kuunda silaha zaidi, na jambo hilo linaogopesha sana watu wengi.
3 Lakini namna gani kukiwa na ‘vita ya kutumia silaha chache tu za nyukilia’? Bado matokeo yangekuwa yenye kuogopesha. Kulingana na Carl Sagan, mwanasayansi anayejulikana sana, ikiwa mataifa yangetumia hata sehemu ndogo sana ya silaha zao za nyukilia, “bila shaka ustaarabu wetu wa dunia yote ungeharibiwa. . . . Na inaonekana kuna uwezekano mkubwa wa kuangamia kabisa kwa jamii ya kibinadamu.” Watu wengi wanajaribu kuondoa mataraja hayo katika akili zao. Lakini hiyo haiondoi hatari. Hesabu yenye kuongezeka haraka sana ya wengine wameunda vyama vya waokokaji. Kwa kutumaini kwamba watu fulani wataokoka, wamejenga mahali pa kukimbilia katika maeneo ya upweke na kuweka humo akiba ya chakula na vifaa vya tiba, pia bunduki za kufukuzia wadukizi wasiotakwa.
4. Kwa nini kuharibiwa kwa mazingira kunaonwa kuwa hatari kubwa?
4 Mbali na vita ya nyukilia, wanasayansi wanaonya juu ya uwezekano wa kutokea msiba wa dunia yote kutokana na jinsi mazingira yanavyoharibiwa. Uchafuzi wa hewa tunayovuta ni chanzo cha hangaiko kubwa. Misitu inafyekwa kwa kadiri yenye kuogopesha sana. Hata hivyo misitu ni ya maana sana kwa kufanyizwa oksijeni ya dunia, kufanyizwa mvua na kuzuia mmomonyoko wa udongo. Ardhi ya maana sana ya kukuza mazao inaharibiwa kwa sababu ya ujinga na pupa. Mito na chemchemi za maji zinachafuliwa, na mara nyingi kwa kemikali zenye kuleta kifo. Hata hivyo mali hizo ni za lazima kwa kuendeleza uhai wa kibinadamu.
5, 6. Ni hali gani nyingine zinazozuia watu wasitarajie maisha kuwa yenye usalama na furaha?
5 Huenda ukahisi kwamba, hangaiko la sasa hivi ni uhalifu wenye jeuri unaofanya watu kuwa wafungwa katika nyumba zao wenyewe. Msukosuko wa kisiasa na kijamii unafanya maisha kuwa yenye hatari. Ukosefu wa kazi za kuajiriwa wenye kuenea pote na kupanda sana kwa infuleshoni hutokeza shida na kukata tamaa. Maisha ya nyumbani hayaridhishi watu wengi. Vifungo vya upendo vinavyotazamiwa kufunga jamaa pamoja huwa havipo mara nyingi. Kila mahali mwelekeo wa watu ni “Mimi kwanza!”
6 Basi, mtu anaweza kupata wapi msingi mzuri wa kutarajia kufurahia maisha ya usalama? Ikiwa wakati ujao wetu sisi wakazi wa dunia hii ungetegemea tu yale ambayo wanadamu na mataifa yanayoshiriki lawama la matatizo hayo wanataka na wanaweza kufanya, matazamio hayangekuwa mazuri kweli. Lakini ndivyo ilivyo?
MAMBO YA HAKIKA YASIYOPASA KUPUUZWA
7. (a) Ni ushahidi gani unaoonyesha kwamba Biblia ni Neno la Mungu? (b) Kwa nini ni jambo la maana sana watu wajue yanayosemwa na Biblia?
7 Katika makadirio yao, mara nyingi sana wanadamu hawamfikirii Muumba wa dunia na wa jamii ya binadamu. Lakini tunaweza kujuaje ni nini kusudi Lake? Biblia inatuambia. Mara nyingi Kitabu hicho kinasema kwamba yaliyomo ndani yacho yana mwanzo wa kimungu, yaliongozwa na Mungu. Je! dai hilo ni la kweli? Ikiwa ni la kweli, uhai wako wategemea kukifuata. Kwa sababu jambo hili ni la maana, tunakusihi wewe binafsi uichunguze Biblia. Utaona maneno mengi ya unabii wacho yanayoonyesha kwa kutokeza maarifa yenye maelezo marefu juu ya wakati ujao. Kina hekima isiyolinganika kinapozungumza mambo yaliyo ya maana sana kwa furaha yako idumuyo. Tuna hakika kwamba, ukiufikiria ushahidi pasipo kupendelea upande mmoja, utafahamu kwamba Biblia ingaliweza kutoka tu kwenye chanzo kisicho cha kiasili, kutoka kwa Mungu anayependa wanadamu kweli kweli.a Biblia ina habari ya maana sana inayohusu kuokolewa kwetu katika wakati huu wenye hatari katika historia ya kibinadamu. Kwa kufaa, ndicho kitabu chenye kuenezwa sana kote kote duniani.—Ona 2 Petro 1:20, 21; 3:11-14; 2 Timotheo 3:1-5, 14-17.
8. Biblia inamtambulisha Muumba wa Dunia-sayari kwa jina gani?
8 Mstari wa kwanza wa Biblia unasema ukweli wa msingi kwamba “Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1, Zaïre Swahili Bible)b Ijapokuwa watu fulani wanapendelea kumwacha Mungu bila jina, Biblia haifanyi hivyo. Likimtambulisha Muumba kwa jina, andiko la Mwanzo 2:4 linatupasha habari kwamba “Jehova Mwenyiezi Mngu alizifanya mbingu na nti.” (Kulingana na The Old Testament in Swahili, Mombasa, chapa ya mwaka wa 1949) (Ona pia Mwanzo 14:22, OTSW; Kutoka 6:3, UV; Kutoka 20:11, OTSW.) Hapo mwanzoni sehemu kubwa ya Biblia iliandikwa katika Kiebrania, na katika maandishi ya kwanza kabisa ya Biblia katika Kiebrania jina la binafsi la Mungu linaonekana mara karibu 7,000 likiwa na herufi takatifu nne (יהוה). Watafsiri fulani wanatafsiri herufi hizo kuwa Yahweh, lakini katika Kiswahili namna ya jina hilo inayotumiwa sana na watu wengi ni Yehova.
9. (a) Jina hilo la Mungu lilitoka kwa nani? (b) Jina la Mungu ni lenye umaana gani kwetu sisi? (Yoeli 2:32; Mika 4:5)
9 Jina hilo halikutungwa na wanadamu wenye kuabudu Mungu. Lilichaguliwa na Muumba mwenyewe. (Kutoka 3:13-15; Isaya 42:8) Si jina linalotakwa kutumiwa mara fulani fulani, na mara nyingine kutumia Buddha, Brahma, Allah au Yesu badala yalo. Nabii Musa kwa kufaa alikumbusha taifa la Israeli hivi: “Jua hivi leo, uivike moyoni mwako, ya kuwa Jehova [Kiebrania: יהוה] ndiye Mwenyiezi Mngu, juu mbinguni na katika nti tini: hapana mwenginewe.” (Kumbukumbu la Torati 4:39, The Old Testament in Swahili, Mombasa) Huyo ndiye Mungu ambaye Yesu Kristo aliomba kwa sala, Yeye ambaye alitaja kuwa “Mungu wa pekee wa kweli.” Leo anaabudiwa na watu wenye maarifa kutoka kila taifa duniani.—Yohana 17:3; Mathayo 4:8-10; 26:39; Warumi 3:29.
10. Kwa nini hatari ya vita ya silaha za nyukilia na hasara inayoletwa na uchafuzi haitazuia kusudi la Mungu la kuumba dunia?
10 Kwa kuwa Yehova ndiye Muumba wa dunia, sayari nzima ni yake, na wakati ujao wa dunia umo mikononi mwake. (Kumbukumbu la Torati 10:14; Zaburi 89:11) Matatizo ya wanadamu hayamshindi Mungu kuyaondoa. Taraja la vita ya silaha za nyukilia linaogopesha wanadamu. Lakini ni sheria za nani zinazoongoza mipasuko ya nyukilia inayotukia katika mabilioni yasiyo na hesabu ya nyota kwa kadiri yenye kutia woga sana? Mungu, je, si anayo maarifa na nguvu zinazohitajiwa kuhifadhi uhai katika Dunia-sayari? Hali moja na hiyo, yale matatizo ambayo yamesitawi kwa sababu wanadamu kwa ujinga na choyo chao wamechafua mazingira yao hayatazuia kusudi la Mungu Mweza Yote likose kutimizwa. Yeye aliye na hekima na nguvu zinazohitajiwa kuumba dunia na namna za uhai zenye kuvutia zilizo juu yake anaweza pia kuwapa mwanzo safi yakiwa ndiyo mapenzi yake. (Isaya 40:26; Zaburi 104:24) Basi, ni nini lililo kusudi la Yehova kuhusiana na makao yetu ya sayari?
DUNIA ITAENDELEA KUWAPO KWA MUDA GANI?
11. (a) Wanasayansi fulani wanaamini hatimaye dunia itapatwa na nini? (b) Ni nani anayejua mengi juu ya mambo hayo kuliko wao, na kwa nini?
11 Je! ni kusudi la Mungu kuiharibu dunia na vitu vilivyo hai vyote juu yake? Wataalamu fulani wa nyota wanawaza kwamba hatimaye jua letu litapanuka liwe kubwa kiasi cha kupasuka liifunike dunia. Kuna wale wanaowaza kwamba, kwa sababu ya tabia yenyewe ya ulimwengu mzima unaoonekana, utafika wakati ambao jua halitaangaza tena na dunia haitaendeleza uhai tena. Lakini wanasema kweli? Muumba anasema nini? Yeye aliyefanya kuwe nishati na tungamo? Yeye aliyeanzisha sheria zinazotegemeza uzima wetu?—Ayubu 38:1-6, 21; Zaburi 146:3-6.
12. Maneno ya Mhubiri 1:4 yamehakikishwaje kuwa ya kweli?
12 Yehova alimwongoza Mfalme Sulemani mwenye hekima aandike juu ya muda wa maisha ya mwanadamu ukilinganishwa na muda wa dunia yenyewe. Katika Mhubiri, Sulemani aliandika maneno haya: “Kizazi kinaenda, na kizazi kinakuja, lakini dunia inasimama hata kwa wakati usiojulikana.” Historia ya kibinadamu inashuhudia ukweli wa hilo. Ijapokuwa kizazi kimoja cha wanadamu kimeenda na kingine kikaja, dunia ambayo sisi tunaishi juu yake, inaendelea kusimama. Lakini itaendelea kusimama kwa muda gani? Kulingana na tafsiri halisi ya Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures, itakuwa “kwa wakati usiojulikana.” Hiyo ina maana gani?
13. (a) “Wakati usiojulikana” unaweza kuwa na maana gani? (b) Basi, tunawezaje kuwa na hakika kwamba dunia itadumu milele?
13 Neno la Kiebrania ‘oh·lam΄, ambalo limetafsiriwa hapa kuwa “kwa wakati usiojulikana,” maana yake kwa msingi ni kipindi cha wakati ambacho, kwa maoni ya sasa, hakijulikani au kimefichwa kisionekane lakini ni chenye kuendelea muda mrefu. Hiyo yaweza kumaanisha milele. Je! inamaanisha hivyo katika habari hii? Au usemi huo unaonyesha kwamba labda katika wakati fulani ujao usiojulikana, ambao sasa tumefichwa, dunia itafikia mwisho wayo? Mambo fulani ambayo Biblia inasema yangeendelea “kwa wakati usiojulikana” yalikoma hatimaye. (Linganisha Hesabu 25:13; Waebrania 7:12.) Lakini Maandiko yanahusianisha pia ‘oh·lam΄ na kile ambacho ni cha milele—kwa mfano, Muumba mwenyewe. (Linganisha Zaburi 90:2 na 1 Timotheo 1:17.) Kwa habari ya maana ya usemi huo kuhusiana na dunia, sisi hatuachwi tukiwa na shaka. Katika Zaburi 104:5, New World Translation, tunaambiwa hivi: “Yeye ameweka msingi wa dunia juu ya mahali payo palipoimarishwa; haitafanywa iyumbeyumbe kwa wakati usiojulikana, au milele.”c—Ona pia Zaburi 119:90.
14. Twajuaje kwamba siku fulani dunia haitakuwa jangwa lisilozaa kitu?
14 Kitakachodumu milele si dunia tu isiyozaa kitu. Katika Yeremia 10:10-12, New World Translation, tunapashwa habari hivi: “Kwa ukweli Yehova ni Mungu. . . . Yeye ndiye Mfanyi wa dunia kwa nguvu zake, Yeye anayeithibitisha nchi inayozaa kwa hekima yake, na Yeye ambaye kwa ufahamu wake alizikunjua mbingu.” Angalia kwamba yeye hakuifanya “dunia” tu bali pia aliithibitisha “nchi inayozaa.” Badala ya usemi huo wa mwisho, watafsiri wengi wanatafsiri neno la Kiebrania te·vel΄ kuwa “ulimwengu” tu. Lakini, kulingana na kitabu Old Testament Word Studies cha William Wilson, te·vel΄ maana yake ni “dunia, ikiwa tufe lenye rutuba na linalokaliwa, lenye kukalika, ulimwengu.” Kwa habari ya kusudi la Yehova juu ya hii dunia inayokaliwa, yenye rutuba, Zaburi 96:10, New World Translation, inatangaza kwa kutumainisha hivi: “Yehova mwenyewe amekuwa mfalme. Dunia inayozaa pia inapata kuthibitika imara hata haiwezi kufanywa iyumbeyumbe.”—Ona pia Isaya 45:18.
15. Mambo ya hakika hayo yanapatanaje na ile sala ambayo Yesu alifundisha wafuasi wake?
15 Kwa hiyo Yesu Kristo alifundisha wafuasi wake wasali hivi kwa Mungu kuhusu Dunia-sayari ambayo sisi twaishi juu yake: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.
16. (a) Ni watu wa aina gani watakaoishi duniani wakati huo? (b) “Dunia mpya” inayosemwa na Biblia ni nini?
16 Si mapenzi ya Yehova dunia ikaliwe na watu wasiojali Mwenye dunia na wasiopendana sana. Hapo kale yeye aliahidi hivi: “Watenda mabaya wenyewe watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumainia Yehova ndio watakaoimiliki dunia. Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:9, 29, New World Translation) Watu watakaokuwa katika “dunia inayokaliwa ijayo” ambayo Biblia inasema habari zake, ni wenye kumwogopa Mungu na wanaowapenda wanadamu wenzao kwa moyo mnyofu. (Waebrania 2:5, New World Translation; linganisha Luka 10:25-28.) Kutakuwa na mabadiliko makubwa sana hata Biblia inasema juu ya “dunia mpya”—si tufe tofauti, bali jamii mpya ya kibinadamu itakayoishi katikati ya hali za kiparadiso ambazo Muumba wa wanadamu alikusudia tangu alipoanza uumbaji wake wa kidunia.—Ufunuo 21:1-5, New World Translation; Mwanzo 2:7-9, 15.
17. Kwa nini ni jambo la maana kujifunza sasa matakwa ya Mungu ya kuokokea?
17 Lazima kuimarishwa kwa “dunia mpya” hiyo kutanguliwe na uharibifu mkubwa—uharibifu unaopita cho chote ambacho wanadamu wamepata kuona. Kwa faida ya dunia yenyewe na wote ambao ni wenye shukrani kwa Muumba wayo, yeye atakuja “kuharibu wale wanaoiharibu dunia.” (Ufunuo 11:17, 18, New World Translation) Umekaribia sana wakati Mungu atakapofanya hivyo! Baada ya hapo, je! utapatikana kati ya waokokaji?—1 Yohana 2:17; Mithali 2:21, 22.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kitabu Is the Bible Really the Word of God?, kilichochapishwa na Sosaiti yetu.
b Isipokuwa iwe imeonyeshwa vingine, maandiko ya Biblia yaliyotumiwa katika kitabu hiki yamenakiliwa kutoka Union Version ya Kiswahili.
c Kwa hiyo watunga kamusi fulani wanafahamu neno hili ‘oh·lam΄ lililotumiwa katika Mhubiri 1:4 kuwa na maana ya “milele.” Zaïre Swahili Bible, Revised Standard Version, The Jerusalem Bible, The Bible in Living English, Union Version na Biblia nyingine zinatafsiri hivyo.
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 5]