Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 169-uku. 176
  • Majaliwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Majaliwa
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Ujuzi wa Kimbele, Agizo la Kimbele
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Je! Mungu Amekuandikia Yatakayokupata?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Je! Ajali Huongoza Wakati Wako Ujao?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Je, Unaweza Kuamua Wakati Wako Ujao Utakuwaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 169-uku. 176

Majaliwa

Maana: Tukio lisiloepukika na mara nyingine huwa baya. Majaliwa ni imani ya kwamba matukio yote yanaamuliwa na mapenzi ya Mungu au na nguvu fulani zilizo kubwa kuliko za mwanadamu, kwamba ni lazima kila tukio litendeke kwa sababu limeamuliwa hivyo mapema. Hilo si fundisho la Biblia.

Je, kila mtu ameamuliwa mapema “wakati wa kufa”?

Imani hiyo ilienea sana kati ya Wagiriki na Waroma. Kulingana na hadithi za Wagiriki za kipagani, Majaliwa walikuwa miungu watatu wa kike waliosokota uzi wa uzima, waliamua urefu wake, kisha wakaukata.

Andiko la Mhubiri 3:1, 2 linasema kuhusu “wakati wa kufa.” Lakini, ili kuonyesha kwamba huo si wakati ulioamuliwa mapema kwa ajili ya mtu fulani, andiko la Mhubiri 7:17 linashauri hivi: “Usiwe mwovu kupita kiasi, wala kuwa mpumbavu. Kwa nini ufe kabla ya wakati wako?” Andiko la Methali 10:27 linasema: “Miaka ya waovu itafupishwa.” Na andiko la Zaburi 55:23 linaongeza hivi: “Nao watu wenye hatia ya damu na wadanganyifu, hawataishi nusu ya siku zao.” Basi, andiko la Mhubiri 3:1, 2 linamaanisha nini? Andiko hilo linazungumzia tu hali yenye kuendelea ya maisha na kifo katika mfumo huu wa mambo usio mkamilifu. Kuna wakati ambapo watu wanazaliwa na wakati ambapo wanakufa—kwa kawaida wakiwa na umri wa miaka 70 au 80. Mara nyingine wao hufa mapema kabla ya kufikia umri huo, au wanaishi kwa muda mrefu zaidi.—Zab. 90:10; ona pia Mhubiri 9:11.

Ikiwa wakati na jinsi ya kufa kwa mtu vingekuwa vimewekwa wakati wa kuzaliwa au kabla ya hapo, hakungekuwa na uhitaji wa kuepuka hatari au kujali afya, na kutii maonyo ya usalama hakungebadili hesabu ya watu wanaokufa. Lakini je, unaamini kwamba uwanja wa mapigano wakati wa vita ni salama kama vile nyumbani kwa mtu aliye mbali sana na uwanja huo wa vita? Je, wewe unajali afya yako au huwapeleka watoto wako kwa daktari? Kwa nini, kwa wastani, wavutaji wa sigara hufa miaka mitatu au minne mapema kuliko watu wasiovuta sigara? Kwa nini ni watu wachache ambao hufa kwenye misiba wakati abiria wanapojifunga mikanda ya usalama na madereva wanapotii sheria za barabarani? Kwa wazi, kutii maonyo huleta faida.

Je, kila jambo linalotukia “ni mapenzi ya Mungu”?

2 Pet. 3:9: “Yehova . . . ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (Lakini si wote wanaoitikia subira yake. Kwa wazi, si “mapenzi ya Mungu” wakati watu fulani wanapokosa kutubu. Linganisha na Ufunuo 9:20, 21.)

Yer. 7:23-26: “Niliwaamuru [Israeli] neno hili, nikisema: ‘Tiini sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu, nanyi mtakuwa watu wangu; na mtembee katika njia yote ambayo nitawaamuru ninyi, ili iwe vema kwenu.’ Lakini hawakusikiliza . . . Niliendelea kuwatumia ninyi watumishi wangu wote manabii, nikiamka mapema kila siku na kuwatuma. Lakini hawakunisikiliza, nao hawakutega sikio lao, bali waliendelea kufanya shingo yao kuwa ngumu.” (Kwa wazi, ubaya uliotukia katika Israeli haukuwa “mapenzi ya Mungu.”)

Marko 3:35: “Yeyote yule anayefanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu na dada yangu na mama yangu.” (Ikiwa lolote alilofanya mtu ni “mapenzi ya Mungu,” basi kila mtu angekuwa na uhusiano pamoja na Yesu ambao anaeleza hapa. Lakini aliwaambia wengine: “Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi.”—Yoh. 8:44.)

Kwa nini mambo mengi yasiyoelezeka hutukia?

Mhu. 9:11: “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Hivyo, si kwa sababu ya lolote linalotazamiwa katika maisha ya mtu, bali huenda mtu akapatwa na msiba kwa sababu ya tukio lisilotazamiwa.)

Je, wanadamu wanawajibika kwa sababu ya magumu yanayowapata wao wenyewe na wanadamu wengine?

Rom. 5:12: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Sisi sote tumerithi kutokamilika kutoka kwa Adamu, pamoja na maelekeo ya kufanya makosa.)

Mhu. 8:9: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”

Met. 13:1: “Mwana ni mwenye hekima palipo na nidhamu ya baba.” (Yale ambayo wazazi hufanya yana uvutano mkubwa kwa maisha ya watoto wao.)

Gal. 6:7: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” (Pia Methali 11:17; 23:29, 30; 29:15; 1 Wakorintho 6:18)

Je, kuna viumbe wenye nguvu kuliko wanadamu ambao pia huwasababishia wanadamu matatizo?

Ufu. 12:12: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Pia Matendo 10:38)

Je, Mungu hujua na kupanga mapema kila jambo?

Isa. 46:9, 10: “Mimi ni Mungu wala hakuna Mungu mwingine, wala yeyote kama mimi; Yeye anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa; Yeye anayesema, ‘Shauri langu mwenyewe litasimama, na kila jambo ambalo ni mapenzi yangu nitafanya.’” (Yeye hujulisha kusudi lake, hupanga mapema mambo fulani kuhusiana na kutimizwa kwa kusudi hilo, naye ana nguvu zote za kuhakikisha kwamba hayo yatatimizwa.)

Isa. 11:1-3: “Tawi litatoka katika kisiki cha Yese; na kutoka katika mizizi yake chipukizi litazaa. [Yesu alizaliwa katika ukoo wa Yese.] Na roho ya Yehova itatua juu yake, . . . naye atakuwa na shangwe katika kumwogopa Yehova.” (Yehova angeweza kutabiri hayo kumhusu Mwanawe akiwa na uhakika kwa sababu Yeye alikuwa ametazama mwelekeo na mwenendo wake akiwa mbinguni tangu mwanzo wa uumbaji.) (Kwa habari ya kuwapo kwa Yesu kabla ya kuwa binadamu, ona ukurasa 435, chini ya kichwa “Yesu Kristo.”)

Kum. 31:20, 21: “Nitawaleta [taifa la Israeli] katika nchi ambayo nimewaapia mababu zao, inayotiririka maziwa na asali, nao hakika watakula na kushiba na kunenepa na kuigeukia miungu mingine, nao kwa kweli wataitumikia na kunitendea bila heshima na kulivunja agano langu. Na itatukia kwamba wakati ambapo misiba mingi na taabu zitawajia, wimbo huu [unaosimulia jinsi walivyotenda kwa sababu ya kukosa kuthamini kibali cha Mungu] lazima pia utashuhudia mbele yao, . . . kwa maana najua vema mwelekeo wao wanaousitawisha leo kabla sijawaingiza katika nchi niliyowaapia.” (Ona kwamba uwezo wa Mungu wa kufahamu matokeo ya mwenendo wao haukumaanisha kwamba yeye ndiye aliyesababisha jambo hilo wala haukumaanisha kwamba ndivyo alivyowatakia, bali kwa kutegemea waliyokuwa wakitenda angeweza kuona mapema matokeo. Vivyo hivyo, kwa kutegemea mambo yanayoonekana, mtu anayetabiri hali ya hewa anaweza kutabiri hali ya hewa kwa usahihi mkubwa, lakini haimaanishi kwamba yeye ndiye anayeisababisha wala kwamba hayo ndiyo mapenzi yake.)

Je, uwezo wa Mungu wa kujua na kupanga matukio mapema unathibitisha kwamba yeye hufanya hivyo kuhusiana na matendo yote ya viumbe vyake vyote?

Ufu. 22:17: “Yeyote anayesikia na aseme: ‘Njoo!’ Na yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.” (Uchaguzi wa mtu haujapangwa mapema; kila mtu anapaswa kujichagulia.)

Rom. 2:4, 5: “Wewe unadharau utajiri wa fadhili zake na uvumilivu wenye subira na ustahimilivu, kwa sababu hujui kwamba sifa ya fadhili za Mungu inajaribu kukuongoza wewe kwenye toba? Lakini kulingana na ugumu wako na moyo wako usiotubu unajiwekea mwenyewe akiba ya ghadhabu katika siku ya ghadhabu na ya kufunuliwa kwa hukumu ya uadilifu ya Mungu.” (Mtu halazimishwi kufuata mwendo fulani ulioamuliwa mapema. Lakini kila mtu anatozwa hesabu kwa yale anayofanya.)

Sef. 2:3: “Mtafuteni Yehova, ninyi nyote mlio wapole wa dunia . . . Utafuteni uadilifu, utafuteni upole. Huenda mkafichwa katika siku ya hasira ya Yehova.” (Je, Mungu mwenye haki na upendo anaweza kuwatia watu moyo watende yaliyo mema, kwa kutazamia thawabu, ikiwa anajua kwamba wamepangiwa mapema wasifaulu?)

Mfano: Mwenye redio anaweza kusikiliza habari za ulimwengu. Kwa kuwa tu kwamba anaweza kusikiliza kituo fulani cha redio haimaanishi kwamba anakisikiliza. Ni lazima kwanza afungue redio kisha atafute kituo hicho cha redio. Vivyo hivyo, Yehova ana uwezo wa kujua matukio mapema, lakini Biblia inaonyesha kwamba yeye anautumia uwezo huo kwa kuchagua na kwa busara, akiheshimu inavyofaa uhuru wa kuchagua ambao amewapa wanadamu.—Linganisha na Mwanzo 22:12; 18:20, 21.

Mungu alipomuumba Adamu, je, alijua kwamba Adamu angefanya dhambi?

Mungu aliwaambia Adamu na Hawa hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.” “Pia Yehova Mungu akamwekea mtu amri hii: ‘Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.’” (Mwa. 1:28; 2:16, 17) Je, unaweza kuwatia moyo watoto wako waanze mradi wenye matumaini mazuri wakati ujao, ukijua tangu mwanzoni kwamba hawatafaulu? Je, utawaonya juu ya madhara, huku ukijua kwamba tayari umepanga kila jambo hivi kwamba hawawezi kuepuka msiba? Je, ni jambo linalopatana na akili, basi, kudai kwamba Mungu anaweza kufanya hivyo?

Mt. 7:11: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo nzuri, je, Baba yenu aliye mbinguni hatawapa hata zaidi vitu vyema wale wanaomwomba?”

Ikiwa Mungu alipanga na kujua mapema dhambi ya Adamu na matokeo yote, ingemaanisha kwamba kwa kumuumba Adamu, Mungu alikusudia kuanzisha uovu wote ambao wanadamu wametenda. Yeye angekuwa ndiye Chanzo cha vita vyote, uhalifu wote, ukosefu wote wa adili, ukandamizaji wote, uwongo wote, unafiki wote, magonjwa yote. Lakini Biblia inasema waziwazi: “Wewe si Mungu anayependezwa na uovu.” (Zab. 5:4) “Mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia.” (Zab. 11:5) ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) “[Yule aliyewekwa na Mungu kuwa Mfalme Masihi] ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri, nayo damu yao itakuwa na thamani machoni pake.” (Zab. 72:14) “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) “Anapenda uadilifu na haki.”—Zab. 33:5.

Je, Mungu alipanga mapema mambo ambayo yangewapata Yakobo na Esau?

Mwa. 25:23: “Naye Yehova akamwambia [Rebeka]: ‘Mataifa mawili yamo tumboni mwako, na vikundi viwili vya mataifa vitatenganishwa kutoka tumboni mwako; na kikundi kimoja cha taifa kitakuwa chenye nguvu kuliko kile kingine, na mkubwa [Esau] atamtumikia mdogo [Yakobo].’” (Yehova aliweza kusoma chembe za urithi za mapacha hao ambao hawakuwa wamezaliwa. Huenda alifikiria jambo hilo alipokuwa akiona mapema sifa ambazo kila mmoja wa wavulana hao angesitawisha kisha akatabiri matokeo. [Zab. 139:16] Lakini hapa hakuna chochote kinachoonyesha kwamba aliwapangia mapema maisha yao yote au kwamba alipanga mapema jinsi ambavyo kila tukio maishani mwao lingetimia.)

Je, Yuda Iskariote alipangiwa mapema kumsaliti Yesu?

Zab. 41:9: “Mtu mwenye kuwa na amani nami, ambaye nimemtegemea, ambaye alikuwa akila mkate wangu, amekiinua kisigino chake dhidi yangu.” (Ona kwamba unabii huo hautaji waziwazi ni yupi kati ya rafiki za Yesu ambaye angemsaliti. Yehova alijua kwamba Ibilisi alimtumia Ahithofeli mshauri wa Daudi amsaliti, Naye aliongoza habari hizo ziandikwe kwa sababu ilionyesha jinsi Ibilisi alivyotenda kazi na mambo ambayo angefanya wakati ujao. Si Mungu bali ni “Ibilisi . . . [aliyeweka] ndani ya moyo wa Yuda Iskariote, mwana wa Simoni, amsaliti [Yesu].” [Yohana 13:2] Badala ya kuupinga, Yuda aliukubali uvutano huo wa kishetani.)

Yoh. 6:64: “Tangu mwanzo Yesu alijua . . . ni nani angemsaliti.” (Si tangu mwanzo wa uumbaji, wala tangu wakati wa kuzaliwa kwa Yuda, bali “tangu mwanzo” wa matendo yake ya udanganyifu. Linganisha na Mwanzo 1:1, Luka 1:2, na 1 Yohana 2:7, 13, ambapo katika kila moja la maandiko hayo neno “mwanzo” linatumiwa kulingana na maana inayohusika. Ona pia Yohana 12:4-6.)

Je, mtume Paulo hasemi kwamba Wakristo ‘wameagizwa kimbele’?

Rom. 8:28, 29: “Tunajua kwamba Mungu hufanya kazi zake zote zishirikiane pamoja kwa ajili ya mema ya wale wanaompenda Mungu, wale ambao wameitwa kulingana na kusudi lake; kwa sababu wale aliowapa utambuzi wake wa kwanza pia aliwaagiza kimbele wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili awe mzaliwa wa kwanza kati ya ndugu wengi.” (Pia Efe. 1:5, 11) Hata hivyo, andiko la 2 Petro 1:10 linawaambia watu haohao: “Fanyeni hata zaidi yote mnayoweza ili kufanya mwito na kuchaguliwa kwenu kuwe hakika kwa ajili yenu wenyewe; kwa maana mkiendelea kufanya mambo hayo hamtashindwa hata kidogo.” (Ikiwa mtu mmoja-mmoja alipangiwa mapema apate wokovu, haingewezekana ashindwe, bila kujali alilotenda. Kwa kuwa kila mtu anahitajika kufanya bidii, lazima iwe ni jamii iliyoagizwa kimbele. Mungu alikusudia kwamba jamii nzima ifuate kielelezo kilichowekwa na Yesu Kristo. Hata hivyo, wale waliochaguliwa na Mungu wawe sehemu ya jamii hiyo, ni lazima wawe waaminifu ikiwa kweli wataifikia thawabu iliyowekwa mbele yao.)

Efe. 1:4, 5: “[Alituchagua] katika muungano naye [Yesu Kristo] kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu, ili tuwe watakatifu na bila dosari mbele zake katika upendo. Kwa maana alituagiza kimbele ili tufanywe kuwa wana kwake kupitia Yesu Kristo, kulingana na upendezi mwema wa mapenzi yake.” (Inafaa kuangaliwa kwamba, katika Luka 11:50, 51, Yesu alilinganisha “kuwekwa msingi wa ulimwengu” na wakati wa Abeli. Abeli ndiye mwanadamu wa kwanza aliyekuwa na kibali cha Mungu katika maisha yake yote. Kwa hiyo, Mungu alifanyiza kusudi lake la kuleta “uzao” ambao ungeandaa ukombozi baada ya uasi katika Edeni lakini kabla ya kuchukuliwa mimba kwa Abeli. [Mwa. 3:15] Mungu alikusudia kwamba wale wa kushirikiana na Uzao mkuu, Yesu Kristo, wangekuwa kikundi cha wafuasi wake waaminifu ambao wangeshiriki pamoja naye katika serikali mpya juu ya dunia, Ufalme wa Masihi.)

Je, nyota na sayari huongoza matukio katika maisha yetu au hutoa ishara ambazo tunapaswa kupima tunapofanya maamuzi?

Unajimu ulitoka wapi?

“Unajimu wa nchi za magharibi unaweza kufuatwa na kuonekana kwamba ulitokana na nadharia na mazoea ya Wakaldayo na Wababiloni wa miaka ya 2000 K.W.K.”—The Encyclopedia Americana (1977), Buku la 2, uku. 557.

“Unajimu ulitegemea mawazo mawili ya Babiloni: ukanda wa nyota, na uungu wa sayari za mbinguni .  . . . Wababiloni waliamini sayari zina uvutano kama ule ambao mtu angetazamia kutoka kwa mungu wake.”—Great Cities of the Ancient World (New York, 1972), L. Sprague de Camp, uku. 150.

“Katika Babilonia na vilevile katika Ashuru, ufalme uliotokana moja kwa moja na utamaduni wa Babiloni . . . unajimu uko katika dini rasmi ukiwa mojawapo ya njia kuu mbili zilizotumiwa na makuhani . . . katika kutambua mapenzi na kusudi la miungu, njia nyingine ni kupitia uchunguzi wa ini la mnyama wa dhabihu. . . . Miendo ya jua, mwezi na sayari tano ilionwa kuwa inawakilisha utendaji wa miungu mitano inayohusika, pamoja na Sini, ambaye ni mungu-mwezi, na Shamashi, ambaye ni mungu-jua, katika kutayarisha matukio duniani.”—Encyclopædia Britannica (1911), Buku la Pili, uku. 796.

Muumba wa wanadamu analionaje zoea hilo?

Kum. 18:10-12: “Asipatikane ndani yako yeyote . . . anayefanya uaguzi, mwenye kufanya uchawi au yeyote anayetafuta ishara za bahati au mlozi . . . Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.”

Aliwaambia Wababiloni hivi: “Na wasimame, sasa, na kukuokoa, wanaoabudu mbingu, watazamaji wa nyota, ambao kwenye miezi mipya wanajulisha habari za mambo yatakayokuja juu yako. Tazama! Wamekuwa kama majani makavu. . . . Wale ambao umefanya kazi pamoja nao kama wachawi wako tangu ujana wako. Kwa kweli watatanga-tanga, kila mmoja kwenda katika eneo lake mwenyewe. Hakutakuwa na yeyote wa kukuokoa.”—Isa. 47:13-15.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki