Je! Mungu Amekuandikia Yatakayokupata?
WATU wengi wanasadiki kwamba Mungu anatangulia kuandika yatakayompata mtu. Na wana maoni ya uhakika kwamba Biblia inathibitisha hilo ni kweli.
Kwa mfano, wengine huenda wakaelekeza kwenye kisa cha Esau na Yakobo. Walikuwa wangali kwenye tumbo la uzazi wakati Mungu alipotabiri: “Mkubwa atamtumikia mdogo.” (Mwanzo 25:23) Vivyo hivyo, Mungu alitangulia kujua kwamba Samsoni, Yeremia na Yohana Mbatizaji wangefanya kazi za ajabu katika utumishi wake. (Waamuzi 13:3-5; Yeremia 1:5; Luka 1:13-17) Je! hilo halikumaanisha kwamba watu hao mmoja mmoja walikuwa wameandikiwa wokovu wa milele?
Zaidi ya hayo, namna gani Yuda Iskariote? Muda mrefu kabla hajazaliwa, unabii mbali-mbali wa Kimaandiko ulisema juu ya Masihi kusalitiwa. (Zaburi 41:9; 55:12, 13) Hata Biblia inasema kwamba “tangu mwanzo” Yesu Kristo alijua ni nani ambaye angemsaliti.—Yohana 6:64.
Kwa ajili ya mambo hayo yanayotangulia, wewe ungesemaje? Je! Biblia inafundisha kwamba Mungu amekwisha kuandikia wengine wokovu wa milele na wengine laana? Je! Mungu amekwisha kukuandikia yatakayokupata?
Kusema Mungu Amekuandikia Yatakayokupata Ingemaanisha Hivi
Kabla ya kujibu maulizo hayo, fikiria kusema Mungu amekuandikia yatakayokupata ni kusema nini. Kama fundisho hilo lingekuwa ni kweli, ingemaanisha kwamba Mungu alitangulia kujua yote ambayo yangetokea kwa kumuumba mwanadamu—kupotoka kwa Adamu na Hawa, vita, uhalifu, mwenendo usio wa adili, uonezi, kusema uongo, unafiki, maradhi. Kwa kusema maneno, “Na tufanye mtu,” basi, Mungu kwa kukusudia angekuwa anaanzisha mwendo wa uovu! (Mwanzo 1:26) Kwa hiyo, kwa Mungu kuwekea Adamu na Hawa taraja la uzima wa milele kungekuwa ni kisingizio tu. Hali moja na mwaliko wa Biblia, “Yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:17.
Lakini Biblia inasema kwamba Yehova ni Mungu “mwingi wa rehema na kweli.” (Kutoka 34:6) Yeye hangeweza kamwe kutoa kitu alichojua haingewezekana kwa mtu kukipata. Yesu Kristo aliuliza: “Kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? . . . Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?” (Mathayo 7:9-11) Kuongezea hayo, kama Mungu alitangulia kuagiza zamani za kale ni nani hasa angepata wokovu wa milele na ni nani ambaye angeharibiwa milele, kwa sababu gani Biblia inasema kwamba Yehova “huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba”?—2 Petro 3:9.
Kwa hiyo, kusema Mungu ametangulia kuandika yatakayokupata ni kinyume cha yale ambayo Biblia inafundisha hasa juu ya Mungu. ‘Lakini je, kusema maarifa ya Mungu ya wakati ujao yana mpaka si kunatia shaka kwamba yeye si mweza yote?’ huenda ukauliza. Hata kidogo. Katika Tito 1:2, kwa mfano, tunajifunza kwamba ‘Mungu hawezi kusema uongo.’ Lakini je, jambo hilo linatia shaka kwamba Mungu si mweza yote? Hapana, badala yake, linakazia ukweli wa Mungu.
Mtume Paulo alishauri Wakristo waliopewa karama ya unabii hivi: “Zawadi za roho za manabii ni za kuongozwa na manabii. Kwa maana Mungu ni Mungu, si wa kukosa utaratibu, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:32, 33, NW) Manabii hao hawangesema ovyo ovyo bali wangeshiriki ujumbe wao wa kiunabii kwa njia ya utaratibu. Ili kufanya hivyo, kujiweza kungehitajiwa upande wao. Basi, kwa hakika, Mungu anaweza pia kutumia maarifa yake ya kimbele akichagua kufanya hivyo, akiyatumia wakati tu kuna sababu au kusudi la kufanya hivyo.—Linganisha Mwanzo 22:1, 12.
Maarifa ya Kimbele ya Mungu
Miaka 40 tu baada ya kuwatengeneza Waisraeli wawe taifa, Mungu alitabiri kwamba wangevunja agano lake pamoja nao. Hata hivyo, maarifa hayo ya kimbele hayakuwa bila msingi, kwani ukosefu wa taifa hilo kutii uongozi na uasi walo tayari vilikuwa vimetokea. Kwa hiyo, Mungu akasema: “Nayajua mawazo yao wayawazayo, hata sasa kabla sijawatia katika nchi niliyoapa.” (Kumbukumbu la Torati 31:20, 21) Kama ambavyo mjenzi stadi anavyoweza kutabiri jengo lililojengwa kwa vifaa dhaifu litaanguka, ndivyo Yehova angeweza kuona taifa hilo lilikuwa likielekea wapi. Hata hivyo, watu mmoja mmoja, wangeweza na waliitikia na kujifaidi kwa mashauri yaliyotolewa na manabii wa Mungu.—Yeremia 21:8, 9; Ezekieli 33:1-20.
Hali moja na hiyo Yesu Kristo alitabiri kuhukumiwa kifo kwa viongozi wa kidini walioitwa waandishi na Wafarisayo. (Mathayo 23:15, 33) Hata hivyo, hiyo haikumaanisha kwamba kila Farisayo au mwandishi alikuwa anaelekea Gehena. Mtume Paulo mwenyewe hapo awali alikuwa Farisayo mwenye bidii sana!—Matendo 26:4, 5.
Ni kweli kwamba Mungu alitabiri mwendo wa watu fulani mmoja mmoja, kama vile Yakobo na Esau. Lakini hiyo haikuwa kuwaandikia mambo yatakayowapata. Katika kisa cha Esau na Yakobo, ni kwamba tu Mungu alitangulia kujua ni vikundi gani vya kitaifa vilivyo wazao wao vingetawala vile vingine. (Mwanzo 25:23-26) Hata hivyo, hakuna kidokezo kwamba Mungu alikuwa ameandika mambo yasiyoweza kubadilika ambayo yangewapata kwa umilele. Sehemu kubwa ya mwelekeo na tabia ya mtoto yaelekea inaamuliwa na mambo yenye kuhusiana na chembe za urithi. Huenda Yehova akawa alikuwa amechunguza chembe za urithi walizokuwa nazo Esau na Yakobo ili aamue ni mwana gani ambaye angetawala mwenzake.—Linganisha Zaburi 139:14-16.
Hali moja na hiyo, Yehova alitumia maarifa yake ya kimbele kuhusiana na Samsoni, Yeremia na Yohana Mbatizaji. Maarifa hayo ya kimbele, hata hivyo, hayakutoa uhakikisho kwamba wangeendelea kuwa waaminifu mpaka kifo chao. Pia Mungu alitabiri kwamba mmoja wa wana wa Daudi angeitwa Sulemani na kwamba Sulemani angetumiwa kujenga hekalu. (1 Mambo ya Nyakati 22:9, 10) Hata hivyo, Sulemani, aliasi imani katika miaka ya baadaye ya maisha yake.—1 Wafalme 11:4, 9-13.
Lakini namna gani Yuda Iskariote? Je! mwendo wa usaliti wa mmoja wa wanafunzi wa Yesu haukuwa umetabiriwa waziwazi kimbele? Ndiyo, lakini unabii haukutaja ni mwanafunzi yupi angekuwa msaliti. Hakika, vipi kama Yesu alikuwa amejua kwamba Yuda angekuwa ndiye msaliti? Basi kwa Yesu kumweka rasmi Yuda awe mtume kungalimfanya Yesu awe ‘mshiriki’ wa dhambi za msaliti huyo. (Linganisha 1 Timotheo 5:22.) Pia Mungu mwenyewe angekuwa amezishiriki, kwa kuwa kabla ya kuchagua Yuda, Yesu alisali kwa Yehova kwa bidii nyingi.—Luka 6:12-16.
Hata hivyo, Yehova ‘hakukosa kujua fikira za Shetani.’ (Linganisha 2 Wakorintho 2:11.) Yeye alijua kwamba Shetani Ibilisi alikuwa ametangulia kutumia rafiki wa karibu wa mwanamume mmoja awe msaliti, kama alivyokuwa amefanya katika kisa cha rafikiye Daudi, Ahithofeli. Kwa hiyo, ilikuwa ni Shetani, wala si Mungu, aliyemtia “Yuda, mwana wa Simoni Iskariote, moyo wa kumsaliti” Yesu Kristo. (Yohana 13:2; 2 Samweli 15:31) Badala ya kupinga uongozi wa kishetani, Yuda aliruhusu dhambi imshinde nguvu. Na hatua fulani ilipofika Yesu aliweza kusoma moyo wa Yuda na kwa hiyo akatabiri kusalitiwa kwake. (Yohana 13:10, 11) Kwa hiyo Yesu alijua Yuda angemsaliti “tangu mwanzo” wa Yuda kutenda kwa njia ya hila wala si “tangu mwanzo” wa Yesu kufahamiana naye.—Yohana 6:64.
Waliotangulia Kuagizwa Rasmi na Mungu
Kwa hiyo kutumia kwa Mungu maarifa ya kimbele hakuongozwi kamwe na tamaa fulani ya muda tu. Mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo wapakwa-mafuta wenzake: “Tulitangulia kuagizwa rasmi kulingana na kusudi lake yeye [Yehova Mungu] anayetenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.” (Waefeso 1:11, NW) Tangu wanadamu walipoanguka katika dhambi, limekuwa kusudi la Mungu kutetea jina Lake kupitia Ufalme Wake. Kwa kusudi hilo, nyakati nyingine Mungu ametumia uweza wake atangulie kuona wakati ujao. Kwa mfano, yeye alitangulia kuagiza rasmi kwamba kungekuwako jamii ya warithi-washirika pamoja na Yesu Kristo katika Ufalme, ijapokuwa watu mmoja mmoja ni lazima wawe waaminifu ili wawe sehemu ya jamii hiyo.—2 Petro 1:10, 11.
Ukiwa unajua fundisho la Biblia lililo wazi juu ya jambo hilo unaweza kusaidika uwe na maoni yanayofaa juu ya wakati ujao. Mungu hatangulii kukuandikia yatakayokupata. Badala yake, unaweza kutumia hiari ambayo Yehova Mungu amewapa viumbe walioumbwa “kwa mfano wake.” (Mwanzo 1:27) Unaweza kufanya uchaguzi wa hekima na kwa moyo wote ukubali toleo la Yehova Mungu la uzima wa milele.—Yohana 17:3.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kama Mungu alijua kwamba Adamu na Hawa walikuwa wamehukumiwa kushindwa, kuwawekea uzima wa milele mbele yao kungalikuwa ni kisingizio cha ukatili
[Picha katika ukurasa wa 6]
Ni wakati gani Yesu alijua kwamba Yuda angemsaliti?