Mungu
Maana: Mkuu Kuliko Wote, ambaye jina lake la pekee ni Yehova. Maneno ambayo lugha ya Kiebrania inatumia kumaanisha “Mungu” yanatoa wazo la nguvu, pia fahari, adhama, na utukufu. Kuna miungu ya uwongo, ambayo ni tofauti na Mungu wa kweli. Baadhi ya miungu hiyo imejifanya yenyewe kuwa miungu; mingine imefanywa vitu vya kuabudiwa na wale wanaoitumikia.
Je, kuna sababu nzuri za kuamini kwamba kuna Mungu?
Zab. 19:1: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake.”
Zab. 104:24: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima. Dunia imejaa vitu ulivyotokeza.”
Rom. 1:20: “Sifa zake ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa.”
Gazeti New Scientist lilisema: “Watu wa kawaida wanaendelea kuwa na maoni kwamba wanasayansi ‘wameikana’ dini. Kulingana na maoni hayo, kwa ujumla wanasayansi hawatazamiwi kuwa waamini; wanaamini kwamba Darwin aliondoa kabisa uwezekano wa kuwapo kwa Mungu; na kwamba mfululizo wa mavumbuzi ya kisayansi na ya kitekinolojia tangu wakati huo yameondoa uwezekano wa ufufuo wowote. Maoni hayo ni yenye makosa kabisa.”—Mei 26, 1977, uku. 478.
Mwanachama wa French Academy of Sciences alisema: “Utaratibu wa kiasili haukubuniwa na akili ya mwanadamu wala kuanzishwa na nguvu fulani zenye fahamu. . . . Kuwako kwa utaratibu kunaonyesha kwamba lazima kuwe na akili fulani yenye kupanga mambo. Akili hiyo si ya mtu mwingine bali ni ya Mungu.”—Dieu existe? Oui (Paris, 1979), Christian Chabanis, akimnukuu Pierre-Paul Grassé, uku. 94.
Wanasayansi wametambua elementi zaidi ya 100 za kemikali. Muundo wa atomu zake unaonyesha uhusiano tata wa hesabu kati ya elementi hizo. Jedwali ya elementi huonyesha ubuni ulio wazi. Haiwezekani kwamba ubuni huo wenye kustaajabisha ulijitokeza wenyewe tu.
Mfano: Tunapoona kamera, redio, au kompyuta, tunakubali haraka kwamba bila shaka vitu hivyo vimefanyizwa na mbuni mwenye akili. Basi, je, lingekuwa jambo linalopatana na akili kusema kwamba vitu tata zaidi—jicho, sikio, na ubongo wa mwanadamu—havikufanyizwa na Mbuni mwenye akili?
Ona pia ukurasa wa 390-392 chini ya kichwa “Uumbaji.”
Je, kuwako kwa uovu na kuteseka kunathibitisha kwamba hakuna Mungu?
Fikiria mifano hii: Kwa kuwa visu vimetumiwa kuua watu, je, hilo linathibitisha kwamba hakuna mtu aliyevitengeneza? Ndege zinapotumiwa kuangusha mabomu wakati wa vita, je, hilo linathibitisha kwamba hakuna mtu aliyezitengeneza? Je, kinachomletea mwanadamu msiba si jinsi vitu hivyo vinavyotumiwa?
Je, si kweli kwamba magonjwa mengi yanatokea kwa sababu ya mazoea mabaya ya maisha ya mwanadamu mwenyewe na kwa kujiharibia mwenyewe na wengine mazingira? Je, vita vinavyopiganwa na wanadamu si kisababishi kikubwa cha kuteseka kwa wanadamu? Je, si kweli pia kwamba, huku mamilioni wakiteseka kwa kukosa chakula, kuna chakula cha ziada katika nchi nyingine, hivi kwamba mojawapo ya matatizo ya msingi ni pupa ya wanadamu? Mambo yote hayo yanathibitisha, si kwamba hakuna Mungu, bali kwamba wanadamu kwa kusikitisha wanatumia vibaya dunia na uwezo wao waliopewa na Mungu.
Je, kweli Mungu anajali yanayotupata sisi wanadamu?
Ndiyo, anajali! Fikiria uthibitisho: Biblia inatuambia kwamba Mungu alimpa mwanadamu mwanzo mkamilifu. (Mwa. 1:27, 31; Kum. 32:4) Hata hivyo, ili wanadamu waendelee kuwa na kibali cha Mungu, walipaswa kumtii Muumba wao. (Mwa. 2:16, 17) Ikiwa mwanadamu angetii, angeendelea kuishi maisha makamilifu—bila ugonjwa, bila kuteseka, bila kifo. Muumba angempa mwanadamu mwongozo unaohitajiwa na angetumia uwezo Wake kumlinda mwanadamu asipate msiba wowote. Lakini mwanadamu alikataa mwongozo wa Mungu; akachagua kujitawala mwenyewe. Kwa kujaribu kufanya jambo ambalo hakukusudiwa kamwe kufanya, yeye mwenyewe amejiletea msiba. (Yer. 10:23; Mhu 8:9; Rom. 5:12) Hata hivyo, kwa miaka mingi Mungu amekuwa akitafuta kwa subira wale ambao wana nia ya kumtumikia kwa sababu wanampenda yeye na njia zake. Yeye anaweka mbele yao nafasi ya kupata baraka zote ambazo wamenyimwa kwa sababu ya kutokamilika na utawala mbaya wa wanadamu. (Ufu. 21:3-5) Uandalizi ambao Mungu alifanya kupitia Mwanawe ili kuwakomboa wanadamu katika dhambi na kifo ni uthibitisho mzuri wa upendo mkuu wa Mungu kwa wanadamu. (Yoh. 3:16) Pia Mungu ameweka wakati atakapowaharibu wale wanaoiharibu dunia naye atawafanya wale wanaopenda uadilifu waishi kupatana na kusudi lake la kwanza.—Ufu. 11:18; Zab. 37:10, 11; ona pia vichwa “Kuteseka” na “Uovu.”
Je, Mungu ni mtu halisi?
Ebr. 9:24: “Kristo . . . aliingia mbinguni kwenyewe, ili sasa aonekane mbele za uso wa Mungu kwa ajili yetu.”
Yoh. 4:24: “Mungu ni Roho.”
Yoh. 7:28: “Yule aliyenituma ni halisi,” akasema Yesu.
1 Kor. 15:44: “Ikiwa kuna mwili wa nyama, kuna wa roho pia.”
Je, Mungu ana hisia kama za watu walio hai?
Yoh. 16:27: “Baba mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu mmenipenda na mmeamini kwamba mimi nilitoka nikiwa mwakilishi wa Baba.”
Isa. 63:9: “Wakati wa taabu zao zote hilo lilimtaabisha. . . . Katika upendo wake na katika huruma yake yeye mwenyewe aliwakomboa.”
1 Tim. 1:11: “Mungu mwenye furaha.”
Je, Mungu alikuwa na mwanzo?
Zab. 90:2: “Kabla ya kuzaliwa kwa milima, au kutokezwa kwa dunia na nchi yenye kuzaa kana kwamba kwa maumivu ya kuzaa, tangu wakati usio na kipimo mpaka wakati usio na kipimo wewe ni Mungu.”
Je, hilo linapatana na akili? Akili zetu haziwezi kulifahamu kikamili. Lakini hiyo si sababu halali ya kulikataa. Fikiria mifano: (1) Wakati. Hakuna mtu anayeweza kusema wakati ulianza lini. Na ni kweli kwamba, hata ingawa maisha yetu hukoma, wakati haukomi. Sisi hatulikatai wazo la wakati kwa sababu kuna mambo fulani kuuhusu ambayo hatufahamu kikamili. Badala yake, sisi tunautegemea maishani mwetu. (2) Anga. Wataalamu wa nyota hawaoni mwanzo na mwisho wa anga. Kadiri wanavyoendelea kuuchunguza ulimwengu, ndivyo wanavyoona hauna mwisho. Hawapingi uthibitisho huo; wengi husema anga haina mwisho. Kanuni hiyohiyo inaweza kutumiwa kuhusu kuwako kwa Mungu.
Mifano mingine: (1) Wataalamu wa nyota hutuambia kwamba joto la jua katika kiini chake ni digrii 15,000,000 Selsiasi. Je, tunapinga wazo hilo kwa sababu hatuwezi kufahamu kikamili joto jingi namna hiyo? (2) Wanatuambia kwamba galaksi yetu ya Kilimia ni kubwa sana hivi kwamba nuru inayosafiri mwendo wa zaidi ya kilometa 300,000 kwa sekunde moja ingechukua miaka 100,000 kuivuka. Je, akili zetu kweli zinaufahamu umbali huo? Hata hivyo tunakubali jambo hilo kwa sababu uthibitisho wa sayansi unaliunga mkono.
Ni jambo gani linalopatana na akili zaidi—kwamba ulimwengu uliumbwa na Muumba aliye hai, mwenye akili? au kwamba ulitokea wenyewe tu kutokana na chanzo kisicho hai bila mwelekezo wenye akili? Watu fulani wanakubali maoni hayo ya mwisho kwa sababu kukubali vingine kungemaanisha kwamba wangelazimika kukubali kwamba kuna Muumba ambaye sifa zake hawawezi kuzifahamu kikamili. Lakini inajulikana sana kwamba wanasayansi hawafahamu kikamili utendaji wa chembe za urithi zilizo katika chembe hai na zinazoamua jinsi chembe hizo zitakavyokua. Wala hawajaelewa kikamili jinsi ubongo wa mwanadamu unavyofanya kazi. Hata hivyo, ni nani anayeweza kusema kwamba vitu hivyo haviko? Je, kwa kweli tutarajie kuelewa kila jambo kumhusu Mtu aliye mkuu sana hata akaweza kutokeza ulimwengu mzima, pamoja na ubuni wake wote ulio tata na wenye ukubwa wa kustaajabisha mno?
Je, ni muhimu kulitumia jina la Mungu?
Rom. 10:13: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.”
Eze. 39:6: “Watu watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.”
Yesu alimwambia Baba yake hivi: “Nimewajulisha [wafuasi wake wa kweli] jina lako nami nitalijulisha.”—Yoh. 17:26.
Ona pia ukurasa wa 425, 426, chini ya “Yehova.”
Maadamu tuna dini fulani, je, Mungu tunayemtumikia ni muhimu?
1 Kor. 10:20: “Vitu ambavyo mataifa huvitoa dhabihu wao huvitoa dhabihu kwa roho waovu, na si kwa Mungu.”
2 Kor. 4:4: “Mungu wa mfumo huu wa mambo amezipofusha akili za wasioamini, ili nuru ya habari njema yenye utukufu juu ya Kristo, aliye mfano wa Mungu, isipenyeze mwangaza.” (Hapa Ibilisi anaitwa “mungu.” Ona 1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:9.)
Mt. 7:22, 23: “Wengi wataniambia [Yesu Kristo] siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya matendo mengi yenye nguvu katika jina lako?’ Na hata hivyo nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.” (Mtu kudai kuwa Mkristo si uhakikisho wa kwamba anamtumikia Mungu wa kweli kwa njia inayokubalika.)
Ona pia ukurasa wa 59, 60, chini ya kichwa “Dini.”
Ikiwa Yehova ndiye “Mungu wa pekee wa kweli,” Yesu ni “Mungu” wa aina gani?
Yesu mwenyewe alimwita Baba yake “Mungu wa pekee wa kweli.” (Yoh. 17:3) Yehova mwenyewe alisema: “Zaidi yangu hakuna Mungu.” (Isa. 44:7) Mtume Paulo aliandika kwamba, kwa Wakristo wa kweli, “kuna Mungu mmoja aliye Baba.” (1 Kor 8:5, 6) Kwa hiyo Yehova ni wa pekee; hakuna mwingine aliye na cheo kama chake. Yehova ni tofauti kabisa na vitu vyote ambavyo huabudiwa kama vile sanamu, wanadamu waliofanywa kuwa miungu, na Shetani. Wote hao ni miungu ya uwongo.
Katika Maandiko Yesu anaitwa “mungu,” hata “Mungu Mwenye Nguvu.” (Yoh. 1:1; Isa. 9:6) Lakini haitwi popote kuwa Mweza-Yote, kama Yehova alivyo. (Mwa. 17:1) Yesu anasemwa kuwa ni “mng’ao wa utukufu wake [Mungu],” lakini Baba ndiye Chanzo cha utukufu huo. (Ebr. 1:3) Yesu hatafuti kwa vyovyote cheo cha Baba yake. Yeye alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Luka 4:8) Yeye yuko “katika umbo la Mungu,” na Baba ameamuru kwamba “katika jina la Yesu kila goti lipigwe,” lakini yote hayo yanafanywa “kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Flp. 2:5-11; ona pia ukurasa wa 430-434.
Mtu Akisema—
‘Mimi siamini Mungu’
Unaweza kujibu hivi: ‘Je, umekuwa na maoni hayo sikuzote? . . . Kabla ya kufikia uamuzi huo, je, ulichunguza uthibitisho fulani ambao ulikusadikisha?’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Jambo hilo linanipendeza sana nami nimelifikiria sana. Haya ndiyo mambo yaliyonisaidia: . . . (Katika ukurasa wa 215, ona kichwa kidogo “Je, kuna sababu nzuri za kuamini kwamba kuna Mungu?” Pia ona ukurasa wa 390-392, chini ya “Uumbaji.”)’
Au unaweza kusema: ‘Je, unamaanisha kwamba huamini kuna Muumba, au umeona unafiki mwingi katika makanisa hivi kwamba huamini yale wanayofundisha?’ Ikiwa ni kwa sababu ya unafiki, unaweza kuongezea: ‘Kuna tofauti kubwa kati ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo na Ukristo wa kweli. Ni kweli kwamba Jumuiya ya Wakristo imewakandamiza watu, lakini Ukristo haujawakandamiza watu. Jumuiya ya Wakristo imepigana vita, lakini Ukristo haujafanya hivyo. Jumuiya ya Wakristo imeshindwa kutoa mwongozo mzuri wa maadili, lakini Ukristo haujashindwa. Neno la Mungu, Biblia, haliungi mkono Jumuiya ya Wakristo. Kinyume chake, linailaumu Jumuiya ya Wakristo.’
Pia unaweza kusema: ‘Nimekuwa na mazungumzo mazuri pamoja na wengine wenye maoni kama yako. Baadhi yao walisema kwamba hawawezi kuelewa kwa nini kuna Mungu na bado kuna kuteseka na uovu mwingi ulimwenguni. Je, hayo ndiyo maoni yako? (Ikiwa ndivyo, tumia habari katika ukurasa wa 216, 217, chini ya kichwa kidogo “Je, kuwako kwa uovu na kuteseka kunathibitisha kwamba hakuna Mungu?”)’
‘Mimi naamini tu kitu ninachoweza kuona, nami sijamwona Mungu kamwe’
Unaweza kujibu hivi: ‘Siku hizi watu wengi huamini hivyo. Na kuna sababu ya maoni hayo. Tunaishi katika jamii inayofuatilia mali za kimwili. Lakini wewe ni mtu anayependa uhakika, sivyo.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Je, kuna vitu fulani ambavyo hatuwezi kuona kwa macho yetu lakini tunaamini kwamba viko kwa kuwa tuna sababu nzuri za kuamini hivyo? Namna gani hewa tunayopumua? Huenda tukaihisi kunapokuwa na upepo. Tunaweza kujua inapojaa katika mapafu yetu, hata ingawa hatuioni. Kwa sababu tunaona matokeo, kuna sababu nzuri ya kuamini kwamba ipo, sivyo?’ (2) ‘Na hatuwezi kuziona nguvu za uvutano. Lakini tunapoangusha kitu fulani tunaona uthibitisho kwamba nguvu za uvutano zinatenda kazi. Wala hatuoni harufu, lakini pua yetu inainusa. Hatuwezi kuona mawimbi ya sauti, lakini masikio yetu yanayasikia. Kwa hiyo tunaamini vitu tusivyoweza kuona—maadamu kuna sababu nzuri ya kufanya hivyo, sivyo?’ (3) ‘Je, kweli kuna uthibitisho kwamba Mungu asiyeonekana yuko? (Tumia habari iliyo katika ukurasa wa 215, 216, chini ya kichwa kidogo “Je, kuna sababu nzuri za kuamini kwamba kuna Mungu?”)’
‘Mimi nina maoni yangu mwenyewe kumhusu Mungu’
Unaweza kujibu hivi: ‘Ninafurahi kusikia kwamba umelifikiria jambo hilo na kwamba unamwamini Mungu. Hebu nikuulize, Una maoni gani kumhusu Mungu?’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Nina hakika unatambua kuwa ni muhimu kuhakikisha kwamba lolote tunaloamini linapatana na yale ambayo Mungu mwenyewe anasema. Je, nikuonyeshe wazo moja tu katika Biblia kuhusu jambo hilo? (Zab. 83:18)’