Uponyaji
Maana: Kumfanya mtu ambaye amekuwa mgonjwa kimwili, kiakili, au kiroho apate afya njema. Roho ya Mungu iliwawezesha baadhi ya manabii Waebrania waliokuwako kabla ya Ukristo na pia Yesu Kristo na washiriki fulani wa kutaniko la kwanza la Kikristo waponye kimuujiza.
Je, uponyaji wa kimuujiza leo unafanywa kupitia roho ya Mungu?
Je, uwezo wa kufanya miujiza unaweza kutoka chanzo kingine ambacho si Mungu wa kweli?
Musa na Haruni walienda mbele ya Farao wa Misri ili wamwombe awaruhusu Waisraeli waende nyikani kumtolea Yehova dhabihu. Kama uthibitisho wa kwamba anaungwa mkono na Mungu, Musa alimwelekeza Haruni atupe chini fimbo yake nayo ikawa nyoka mkubwa. Muujiza huo ulifanywa kwa nguvu za Mungu. Lakini makuhani wa Misri wenye kufanya uchawi nao wakazitupa chini fimbo zao nazo pia zikawa nyoka wakubwa. (Kut. 7:8-12) Walifanya muujiza wao kwa uwezo wa nani?—Linganisha na Kumbukumbu la Torati 18:10-12.
Katika karne ya 20 uponyaji fulani wa imani unafanywa katika ibada zinazoongozwa na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Kati ya dini zisizo za Kikristo kuna makuhani wa uchawi, walozi, waganga, na wengine wanaoponya pia; mara nyingi wanatumia uchawi na uaguzi. Watu fulani ambao huponya kwa kuchunguza akili husema kwamba uponyaji wao hauna uhusiano na dini. Katika visa hivyo vyote, je, uwezo huo wa kuponya unatoka kwa Mungu wa kweli?
Mt. 24:24: “Makristo wa uwongo na manabii wa uwongo watatokea na kutoa ishara kubwa na maajabu [“miujiza,” NAJ] ili kuwapotosha, ikiwezekana, hata wale waliochaguliwa.”
Mt. 7:15-23: “Jihadharini na manabii wa uwongo . . . Wengi wataniambia siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya matendo mengi yenye nguvu [“miujiza,” UV, BHN, VB] katika jina lako?’ Na hata hivyo nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.”
Je, maponyo ya leo yenye kusisimua yanafanywa kwa njia ileile kama maponyo ya kimuujiza yaliyofanywa na Yesu na wanafunzi wake wa kwanza?
Malipo: “Ponyeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, fukuzeni roho waovu. Mlipokea bure, toeni bure.” (Mt. 10:8) (Je, waponyaji leo wanafanya hivyo—wanatoa bure, kama Yesu alivyoamuru?)
Kiwango cha mafanikio: “Umati wote ulikuwa ukitafuta kumgusa, kwa sababu nguvu zilikuwa zikimtoka na kuwaponya wote.” (Luka 6:19) “Wakawaleta wagonjwa nje hata katika zile njia pana na kuwalaza huko juu ya vitanda na machela, ili, wakati Petro anapopita hapo, angalau kivuli chake kipate kumwangukia mtu fulani kati yao. Pia, umati kutoka kwenye majiji yanayozunguka Yerusalemu ukazidi kuja pamoja, ukiwa umewabeba wagonjwa na wale wenye kutaabika wakiwa na roho wachafu, nao wote wakawa wakiponywa.” (Mdo. 5:15, 16) (Katika siku zetu, je, wote wanaowaendea waponyaji wa kidini au wanaoenda kwenye mahekalu ya kidini wakitafuta kuponywa, huponywa?)
Je, maisha ya wafuasi wa mashirika ambayo “waponyaji” wanashirikiana nayo yanaonyesha kwamba wana roho ya Mungu?
Wakiwa kikundi, je, wanaonyesha waziwazi matunda ya roho kama vile upendo, ustahimilivu, upole, kujizuia?—Gal. 5:22, 23.
Je, kwa kweli wao “si sehemu ya ulimwengu,” wakiepuka kujiingiza katika siasa zote za ulimwengu? Je, wamejiepusha kabisa na hatia ya damu wakati wa vita? Je, wana sifa nzuri kwa sababu ya kuepuka mwenendo usio wa adili wa ulimwengu?—Yoh. 17:16; Isa. 2:4; 1 The. 4:3-8.
Je, leo Wakristo wa kweli wanatambuliwa kwa uwezo wa kuponya kimuujiza?
Yoh. 13:35: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Hivyo ndivyo Yesu alivyosema. Ikiwa tunamwamini kweli kweli, tutatafuta kuona upendo, wala si uponyaji wa kimuujiza, kuwa uthibitisho wa Ukristo wa kweli.)
Mdo. 1:8: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Muda mfupi tu kabla ya kuwaacha mitume wake na kurudi mbinguni, Yesu aliwaambia kwamba hiyo ilikuwa ndiyo kazi ya maana sana ambayo walipaswa waifanye, wala si kufanya uponyaji. Ona pia Mathayo 24:14; 28:19, 20.)
1 Kor. 12:28-30: “Mungu amewaweka watu mbalimbali katika kutaniko, kwanza, mitume; pili, manabii; tatu, walimu, kisha matendo yenye nguvu; kisha zawadi za maponyo; utumishi wenye msaada, uwezo wa kuelekeza, lugha tofauti. Je, wote ni mitume? Je, wote ni manabii? Je, wote ni walimu? Je, wote hufanya matendo yenye nguvu? Je, wote wana zawadi za maponyo?” (Biblia inaonyesha waziwazi kwamba si Wakristo wote wa kweli ambao wangekuwa na zawadi za maponyo.)
Je, andiko la Marko 16:17, 18 halionyeshi kwamba uwezo wa kuponya wagonjwa ungekuwa ishara ya kutambulisha waamini?
Marko 16:17, 18, UV: “Ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.”
Mistari hiyo inaonekana katika hati fulani za Biblia na tafsiri za karne ya tano na ya sita W.K. Lakini haionekani katika hati za Kigiriki za zamani zaidi, kama vile hati ya Sinaitiko na ya Vatikani MS. 1209 ya karne ya nne. Dakt. B. F. Westcott, mtaalamu wa hati za Biblia, alisema kwamba “mistari hiyo . . . si sehemu ya masimulizi ya kwanza bali ni nyongeza.” (An Introduction to the Study of the Gospels, London, 1881, uku. 338) Katika karne ya tano, Jerome, mtafsiri wa Biblia, alisema kwamba “karibu vitabu vyote vya Kigiriki havina fungu hilo.” (The Last Twelve Verses of the Gospel According to S. Mark, London, 1871, J. W. Burgon, uku. 53) New Catholic Encyclopedia (1967) yasema hivi: “Msamiati na mtindo wake unatofautiana sana na sehemu inayobaki ya Injili hiyo hivi kwamba haionekani ni Marko mwenyewe aliyeiandika [yaani, mstari wa 9-20].” (Buku la 9, uku. 240) Hakuna maandishi ya kuonyesha kwamba Wakristo wa kwanza walikunywa sumu au wakawashika nyoka ili kuthibitisha kwamba walikuwa waamini.
Kwa nini Wakristo wa karne ya kwanza walipewa zawadi hizo, kama vile uwezo wa kuponya kimuujiza?
Ebr. 2:3, 4: “Tutaponaje ikiwa tumepuuza wokovu mkuu namna hii kwa kuwa ulianza kusemwa kupitia Bwana wetu nasi tukathibitishiwa na wale waliomsikia, huku Mungu akijiunga katika kutoa ushahidi kwa ishara na vilevile mambo ya ajabu na matendo mbalimbali yenye nguvu na kwa ugawaji wa roho takatifu kulingana na mapenzi yake?” (Huo ulikuwa uthibitisho wenye kusadikisha, kwamba kutaniko la Kikristo, ambalo wakati huo lilikuwa jipya, lilikuwa la Mungu kikweli. Lakini mara tu lilipoimarishwa kikamili, je, ingekuwa lazima kuthibitisha jambo hilo tena na tena?)
1 Kor. 12:29, 30; 13:8, 13: “Je, wote ni manabii? . . . Je, wote wana zawadi za maponyo? Je, wote husema kwa lugha? . . . Upendo haushindwi kamwe. Lakini kama kuna zawadi za kutoa unabii, zitaondolewa mbali; kama kuna lugha, zitakoma . . . Sasa, hata hivyo, inabaki imani, tumaini, upendo, hayo matatu; lakini lililo kubwa zaidi kati ya hayo ni upendo.” (Wakati zilipokuwa zimetimiza kusudi lake, zawadi hizo za kimuujiza zingekoma. Lakini sifa bora ambazo ni tunda la roho ya Mungu bado zingeonyeshwa katika maisha ya Wakristo wa kweli.)
Maadamu mtu ameponywa, jinsi uponyaji huo hufanywa ni muhimu kweli?
2 The. 2:9, 10: “Kuwapo kwa huyo mwasi-sheria ni kulingana na utendaji wa Shetani pamoja na kila tendo lenye nguvu [“kila namna ya miujiza,” BHN] na ishara za uwongo na mambo ya ajabu na pamoja na kila udanganyifu usio wa uadilifu kwa wale wanaoangamia, kuwa malipo kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli ili wapate kuokolewa.”
Luka 9:24, 25: “Yeyote yule anayetaka kuiokoa nafsi [“maisha,” BHN] yake ataipoteza; lakini yeyote yule anayeipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeiokoa. Kwa kweli, mtu anapata faida gani ikiwa anaupata ulimwengu wote lakini aipoteze nafsi yake mwenyewe au apate hasara?”
Kuna tumaini gani la kuponywa kikweli magonjwa yote?
Ufu. 21:1-4: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali . . . ‘Naye [Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’”
Isa. 25:8: “Kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Pia Ufunuo 22:1, 2)
Isa. 33:24: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”
Mtu Akisema—
‘Je, unaamini uponyaji?’
Unaweza kujibu hivi: ‘Yeyote ambaye haamini kwamba Mungu ana uwezo wa kuponya haiamini Biblia. Lakini nina shaka ikiwa watu wanafanya uponyaji kwa njia iliyo sawa leo.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Acha nikusomee andiko moja, na uone ikiwa unatambua zoea lililo tofauti sana leo. (Mt. 10:7, 8) . . . Je, unatambua pia jambo fulani hapa ambalo Yesu alisema wanafunzi wake wangeweza kufanya lakini ambalo waponyaji wa leo wameshindwa kulifanya? (Hawawezi kufufua wafu.)’ (2) ‘Sisi hatuwahukumu watu wengine, lakini ona kwamba andiko la Mathayo 24:24 linataja jambo fulani tunalohitaji kujihadhari nalo.’
Au unaweza kusema: ‘Ninaamini hakika kwamba yale ambayo Biblia inasema kuhusu uponyaji ni ya kweli. Lakini uponyaji wowote unaofanywa katika mfumo huu wa mambo ni wa faida za muda mfupi tu, sivyo? Mwishowe sisi sote hufa. Je, kutakuwa na wakati ambapo kila mtu anayeishi atakuwa na afya njema naye hatakufa kamwe? (Ufu. 21:3, 4)’