Jinsi Imani Iwezavyo Kusaidia Wagonjwa
MASIMULIZI ya maponyo ya kimuujiza katika Biblia hutuhakikishia kwamba Mungu huhangaikia afya njema yetu, nayo huonyesha uwezo wake wa kuponya. Kwa kuwa maponyo hayo ya kimuujiza yalimtukuza Mungu na kuleta shangwe nyingi sana, inafaa kuuliza, Je! zawadi ya uponyaji kupitia roho takatifu bado hutenda kazi?
Jibu la swali hilo ni la—na sababu huenda ikashangaza wengine. Maponyo hayo ya kimuujiza katika karne ya kwanza yametimiza kusudi layo. The Illustrated Bible Dictionary huonyesha kwa usahihi kwamba: “Kusudi la miujiza ya uponyaji lilikuwa la kidini, si la kitiba.” Ni baadhi gani ya makusudi ya kidini yaliyotimizwa na miujiza hiyo?
Kwanza, miujiza ya Yesu ya uponyaji ilitimiza kusudi la kumtambulisha yeye kuwa yule Mesiya. Na baada ya kifo chake, ilisaidia kuthibitisha kwamba baraka ya Mungu ilikuwa juu ya lile kundi jipya la Kikristo. (Mathayo 11:2-6; Waebrania 2:3, 4) Zaidi ya hayo, ilionyesha kwamba ile ahadi ya Mungu ya kuponya ainabinadamu katika ulimwengu mpya ingetimizwa. Inatia nguvu imani yetu kwamba kwa kweli wakati utakuja ambao “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa; watu wakaao humo watasamehewa uovu wao.” (Isaya 33:24) Mara makusudi hayo ya karne ya kwanza yalipotimizwa, miujiza haikuhitajika tena.
Inastahili kuangaliwa kwamba wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza wenyewe walipatwa na maradhi ambayo hayakuponywa kimuujiza. Huo ni ushuhuda wa ziada kwamba utendaji wa uponyaji wa kimuujiza wa Yesu pamoja na ule wa mitume ulikusudiwa ufundishe kweli za maana, si kuandaa utumishi wa kitiba. Alipokuwa akimtolea Timotheo pendekezo la utibabu kwa sababu ya kuwa kwake mgonjwa mara nyingi, Paulo alipendekeza utumizi wa divai kitiba, si uponyaji wa imani. Paulo, aliyefanya miujiza ya uponyaji, hakupata kitulizo chochote kutoka katika ule “mwiba katika mwili” uliokuwa ‘ukimpiga’ daima.—2 Wakorintho 12:7; 1 Timotheo 5:23.
Mitume walipokufa, zawadi ya uponyaji ilipitilia mbali. Paulo mwenyewe alionyesha kwamba hilo lingetukia. Akifananisha kundi la Kikristo na mtoto mchanga, Paulo alisema hivi: “Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto.” Jambo hasa la kielezi chake lilikuwa kwamba zawadi za kimuujiza za roho zilikuwa sehemu ya utoto wa kundi la Kikristo. Zilikuwa “mambo ya kitoto.” Kwa hiyo, alitaarifu hivi: ‘[Zawadi hizo za kimuujiza] zingebatilika.’—1 Wakorintho 13:8-11.
Je! Imani Yaweza Kusaidia Tunapokuwa Wagonjwa?
Hata hivyo, hata kama hatutegemei uponyaji wa imani, kwa hakika inafaa kusali kwa Mungu kumwomba msaada tunapokuwa wagonjwa. Na kwa hakika hakuna kosa lolote ikiwa wengine wanasali kwa ajili yetu. (1 Yohana 5:14, 15) Hakuna mahali ambapo Biblia hutuamuru tuombe ili tupate uponyaji wa imani.a Badala ya hivyo, sisi huomba utegemezo wa Yehova wenye upendo wakati wa majaribu yanayosababishwa na ugonjwa.
Biblia huonyesha lile ambalo walio waaminifu waweza kuomba wanapokuwa wagonjwa inaposema hivi: “BWANA [Yehova, New World Translation of the Holy Scriptures] atamtegemeza alipo mgonjwa kitandani. Katika ugonjwa wake umemtandikia.” (Zaburi 41:3) Kutafakari juu ya Neno la Mungu kutasaidia wale wanaopatwa na ugonjwa wa kihisia-moyo. Mtunga zaburi aliandika hivi: “Ee BWANA [Yehova, NW], fadhili zako zilinitegemeza. Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, faraja zako zaifurahisha roho yangu.”—Zaburi 94:18, 19; ona pia 63:6-8.
Kuongezea hayo, tunahitaji kuonyesha kufikiri kuzuri katika mambo ya afya, na Biblia hutushauri juu ya hilo. Ni afadhali zaidi kuishi kulingana na kanuni za Biblia kuliko kushiriki katika utumizi mbaya wa dawa za kulevya, kuvuta sigareti, kunywa vileo kupita kiasi, au kula kupita kiasi na kisha ugonjwa unapofuata, kugeukia uponyaji wa imani kwa kukata tamaa. Kuomba muujiza wakati mtu anapopatwa na ugonjwa hakuchukui mahali pa mwenendo wenye hekima ili kuponyoka ugonjwa unaoweza kuepukika, kama vile kwa kula chakula chenye kunufaisha mwili ikiwa kinapatikana au kutafuta msaada wa kitiba unaofaa mahali kunapowezekana.
Neno la Mungu hututia moyo pia tusitawishe mitazamo ya akili inayofaa ambayo yaweza kufaidi afya yetu ya kimwili. Kitabu cha Mithali hutushauri hivi: “Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili; bali husuda ni ubovu wa mifupa.” “Moyo uliochangamka ni dawa nzuri; bali roho iliyopondeka huikausha mifupa.” (Mithali 14:30; 17:22) Kusali kupata roho takatifu ili kusitawisha utulivu na shangwe ndani yetu kwaweza tu kuwa na matokeo yenye mafaa juu ya afya yetu ya kimwili.—Wafilipi 4:6, 7.
Namna Gani Uponyaji wa Imani?
Bila shaka, hata kama mtu anaishi maisha yenye afya kadiri hali yake inavyomruhusu, huenda bado akapatwa na ugonjwa. Vipi basi? Je! kuna dhara lolote kwenda kwa mponyaji wa imani kwa tumaini la kuponywa? Naam, kuna dhara. Ni mara chache kwamba waponyaji wa ki-siku-hizi hufanya hivyo bila malipo. Na kutumia pesa kumlipa mponyaji wa imani hali pesa hizo zingeweza kutumiwa kupata msaada wa kitiba kungeweza kutusababishia hasara nyingi. Isitoshe, kwa nini kuwapa pesa watu mmoja mmoja wanaojifaidi wenyewe kwa imani ya watu?
Wengine huenda wakatoa hoja hivi: ‘Kwa hakika, ni lazima uponyaji wa imani uwe na thamani fulani ikiwa hata asilimia ndogo ya wale wanaoenda kwa “waponyaji” huponywa.’ Lakini inabishaniwa kama kwa kweli waponyaji wa imani huponya mtu yeyote kwa njia ya kudumu. Encyclopœdia Britannica hukiri hivi: “Ni uchunguzi mdogo tu wenye kufanywa kwa kupatana na utaratibu mbalimbali usiobadilika ambao umetimizwa juu ya mambo mengi yasiyojulikana katika uponyaji wa imani.”
Hata ikiwa idadi ndogo ya watu yaonekana huponywa, huo si ushuhuda wa kazi ya roho takatifu. Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.” (Mathayo 7:22, 23) Yesu alisema pia kwamba ingawa wengine hawangekubaliwa na Mungu, wangevuta uangalifu kwao wenyewe kwa njia ya ishara: “Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kupoteza, kama yamkini, hata walio wateule.” (Mathayo 24:24) Kwa hakika, waponyaji wa ki-siku-hizi wangeweza kutiwa ndani katika utumizi wa maneno hayo, pamoja na maonyesho yao ya ajabu, kuomba-omba kwao pesa, na madai yao ya kufanya maponyo ya kimuujiza.
Watu kama hao hawafuati nyayo za Yesu. Wao wanamfuata nani basi? Mtume Paulo anatuonyesha anaposema hivi: “Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru. Basi si neno kubwa watumishi wake nao wakijigeuza wawe mfano wa watumishi wa haki, ambao mwisho wao utakuwa sawasawa na kazi zao.” (2 Wakorintho 11:14, 15) Ikiwa waponyaji wa imani hawafanyi yale maponyo wanayodai kufanya, basi wao ni wadanganyi, wanaofuata kijia cha Shetani, “audanganyaye ulimwengu wote.” (Ufunuo 12:9) Lakini vipi ikiwa, wao hufanya maponyo katika visa vilivyo vichache sana? Je! si ni lazima tukate kauli kwamba “miujiza” yao hutokezwa kwa uwezo wa Shetani na roho waovu wake? Naam, ni lazima hali iwe ni hivyo!
Wakati wa Maponyo ya Kweli
Maponyo ya kimuujiza ya Yesu yalifanywa kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu. Yalionyesha kusudi lake la kutatua matatizo yote ya afya ya binadamu. Yehova aahidi “kuwaponya mataifa.” (Ufunuo 22:2) Na yeye hataponya magonjwa tu bali ataondolea mbali kifo. Yohana aeleza kwamba Yesu alikuja “ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Huo utakuwa uponyaji mzuri kama nini! Yesu atafanya tena maponyo kama yale yaliyorekodiwa katika Biblia lakini kwa kadiri kubwa zaidi. Yeye hata atafufua wafu! (Yohana 5:28, 29) Hilo litatukia lini?
Katika ulimwengu mpya wa Mungu, ambao, kulingana na ushuhuda wote, uko karibu sana. Ulimwengu huo mpya, utakaoletwa baada ya uovu wa mfumo huu wa mambo kuondolewa mbali milele, utakuwa baraka ya kweli kwa ainabinadamu yenye moyo unaofaa. Utakuwa ulimwengu bila kuteseka. “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” (Ufunuo 21:4) Hayo ni tofauti kama nini na yale tuonayo leo!
Kwa hiyo, upatwapo na ugonjwa, sali kwa Mungu ili upate utegemezo. Na iwe wewe ni mgonjwa au mwenye afya, jifunze jinsi uhai wa milele bila ugonjwa utakavyowezekana kweli kweli. Jenga imani yako katika ahadi hiyo ya Mungu yenye kutegemeka kwa kujifunza yale marejezeo yayo mengi katika Biblia. Jifunze jinsi kusudi la Mungu kwa habari hiyo linavyokaribia kutimizwa kulingana na ratiba yake mwenyewe ya wakati. Usiwe na shaka lolote, kwani Neno la Mungu hutuhakikishia hivi: “Amemeza mauti hata milele; na Bwana MUNGU [Yehova, NW] atafuta machozi katika nyuso zote.”—Isaya 25:8.
[Maelezo ya Chini]
a Wengine hufikiri kwamba maneno kwenye Yakobo 5:14, 15 huhusu uponyaji wa imani. Lakini muktadha huonyesha kwamba hapo Yakobo anaongea juu ya ugonjwa wa kiroho. (Yakobo 5:15b, 16, 19, 20) Yeye ashauri watu mmoja mmoja wanaokuwa wadhaifu katika imani wawaite wazee ili kupata msaada.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Maponyo ya Yesu ya kimuujiza yalitimiza kusudi layo
[Picha katika ukurasa wa 8]
Yesu atarudia na kuongeza mara nyingi miujiza ya uponyaji