Kuponya kwa Imani—Je! Kunaleta Umizo Lo Lote?
WENYE kuponya kwa imani wanaeleza kwamba uwezo wao wa kuponya haufanyi kazi katika visa vyote. Kama tunavyoweza kuwaza, jambo hilo limetokeza matatizo. Wakati wagonjwa wametegemea kabisa mtu mwenye kuponya kwa imani, na ule mwujiza waliotumaini haukutokea, nyakati nyingine matokeo yanakuwa mabaya zaidi. Katika visa fulani, watu wameuawa na maradhi ambayo pengine yangetibiwa na kufaulu katika njia nyingine.
Inawezekana kwamba kwa kukumbuka kuna tofauti nyingi kati ya maponyo yaliyofanywa na Yesu na maponyo ya imani ya siku hizi jambo hilo, watu wengi wenye kuponya kwa imani wanapendekeza kwamba “wagonjwa” wao waendelee kumwona daktari wao wakati wanapowajia ili waponywe kwa imani. Wanasema wanaona daktari kuwa mwenzi, wala si mshindani, katika kazi ya kuponya. Madaktari wengine wanakubali kwa uangalifu faida zinazoweza kutokeza maono ya moyoni yakitenda juu ya mwili kwa wagonjwa wao katika namna hiyo ya kuponya kwa imani.
Dakt. William A. Nolan, baada ya uchunguzi wa muda mrefu wa kuponya kwa imani, alitaja tatizo jingine. Alipofuatia baadhi ya maponyo yaliyodaiwa, alipata watu wenye uchungu mwingi sana. Watu walikuwa wameambiwa, au walikuwa wamejifanya wasadiki, kwamba walikuwa wameponywa. Walakini baadaye ugonjwa huo ungali ulikuwapo. Magonjwa mengine yalikuwa mabaya zaidi ya hapo mbeleni. Watu wengi waliona kuwa wamedanganywa.
Hata hivyo, vipi kama mtu angefuata shauri la kuendelea kumwona daktari wake wa kibinafsi; na namna gani kama mtu huyo alikuwa tayari akijua kwamba ponyo analotumainia huenda lisitokee? Je! bado si ingestahili kumwendea mtu mwenye kuponya kwa imani—ili pengine ikiwezekana apone? Ili kujibu ulizo hilo, tunahitaji kuangalia sehemu ya kidini ya jambo hilo.
UHUSIANO WA KIDINI
Kuponya kwa imani kunahusiana sana na dini. Waevanjeli na wenye kudai wana karama za kuponya magonjwa wanaona kwamba utendaji wao ‘unawarudisha watu kwa Kristo.’ Je! ndivyo?
Inafaa kuangaliwa kwamba wakati wa utumishi wao huenda watu “wakasema katika lugha” au “wakachinjwa katika roho,” kama wanavyosema—yaani, wanaona namna fulani ya njozi ambayo katika hiyo hawawezi kusonga hata hivyo wanaelekea kujua yanayotendeka kuwazunguka. Kwa kupendeza, mambo hayo yanafanana na vifafa na njozi zinazowapata wale wanadini wengine wenye kuponya kwa imani, makuhani wa uchawi na wachawi wanaotibu.
Ni kweli kwamba “waponyaji wenye uwezo wa roho” wengine wanaona kwamba uponyaji wao ni tofauti na dini. Hata hivyo njia wanazofuata na mambo yanayowapata mara nyingi yanafanana na yale ya wanadini wenye kuponya. Isikose wengine msingi wao ni uchawi au pengine falsafa (filosofia) ya kidini ya nchi za Mashariki.
Je! mambo hayo ya undani ni yenye maana katika karne hii ya 20 yenye uhuru? Ndiyo, mambo hayo ya undani ni ya maana sana tukiyatumia kama msingi wa kukadiri maponyo yaliyofanywa na Yesu Kristo na mitume wake katika siku za kwanza za Ukristo. Tunaona nini tunapochunguza maponyo hayo?
MAPONYO ALIYOFANYA YESU
Kuhusiana na maponyo yaliyofanywa na Yesu hakukuwako “upasuaji wa roho” au “kuchinjwa katika roho.” Wala yeye hakutoa mahubiri yenye kugusa maono ya moyoni kabla ya kufanya maponyo yake. Aliyofanya mara nyingi yalikuwa mambo ya kawaida. Huenda alimgusa mtu mgonjwa au mgonjwa akamgusa, au nyakati nyingine akazungumza tu na mwenye kuugua. Nao waliponywa.—Mt. 8:14, 15 Luka 8:43-48; 17:12-19.
Maponyo yaliyofanywa na Yesu hayakuwa matokeo ya maono ya moyoni juu ya mwili. Mkono ulionyauka hauwezi kuponywa kwa njia hiyo. Hata hivyo yeye aliponya maradhi kama hayo. Yeye aliweza kuponya “ugonjwa na udhaifu wa kila namna.” Hata yeye aliwafufua wafu. (Mt. 4:23; Luka 6:6-11; 8:49-56) Hakukuwa kupata nafuu kidogo tu, wala hakukuwako kushindwa. Maneno kama “kukatishwa tamaa” au “udanganyifu” hayakusikiwa kuhusiana na maponyo ya Yesu. Hata adui zake walikubali kwamba mambo hayo yalitokea. (Yohana 11:47, 48) Kwa sababu gani kuna tofauti hiyo kati ya sasa na wakati huo?
KWA SABABU GANI KUNA TOFAUTI HIYO?
Kwa kuwa hata wengi wanaoponya kwa imani, pamoja na wengine wanakubali kwamba maponyo ya Yesu yalitoka kwa Mungu, je! yaweza kuwa kwamba wenye kuponya leo wanahusiana na chanzo tofauti cha uwezo? Hiyo inawezekana sana, sana-sana tunapoufikiria uhusiano wa wengine wenye kuponya kwa imani na uchawi na mafumbo. Na ni jambo la maana kwamba, kuhusu mazoea hayo Biblia inatuonya hivi: “Asionekane kwako mtu . . . atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu.”—Kum. 18:10, 11.
Huko si kuwaza kwa kidini pasipo sababu. Mahali pake kunatulinda tusichafuliwe na nguvu za pepo waovu—mashetani—ambazo sikuzote zimekuwa zikipinga faida njema za wanadamu. Kuponya kwa imani kwa kisasa pamoja na mafumbo yake ya kichawi, kwa hakika ni tofauti na maponyo yaliyofanywa na Yesu Kristo, kwa kuwa sikuzote aliepuka mavutano hayo.Jambo lo lote linalofanywa chini ya uongozi wa uvutano wa nguvu hizo pasipo shaka litaelekeza kwenye visa vingi vya “kukatishwa tamaa” na “udanganyifu”.
Jambo hilo linalohusu chanzo tofauti cha nguvu linakuwa wazi zaidi tunapotambua kwamba hakuna sababu ya kutazamia kwamba namna iyo hiyo ya maponyo aliyofanya Yesu ingefanywa leo. Kazi ya kuponya ya Yesu na mitume wake ilitimiza kusudi lake.
KWA SABABU GANI YESU ALIPONYA
Wakati rafiki ya mtume Paulo, Timotheo, alipokuwa mgonjwa, Paulo alipendekeza si awekelewe mikono juu bali atumie divai kama dawa. (1 Tim. 5:23) Kwa sababu gani? Kwa sababu Wakristo wa kwanza hawakuiona zawadi ya kuponya kuwa namna ya kuponya. Wala haukuwa mgawo wao kutunza afya ya kimwili ya wanadamu huko nyuma.
Kama Yesu, wao walikuwa wahubiri. Yesu alieleza kusudi lake kuu maishani mwake alipomwambia hivi Pontio Pilato: “Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli.”—Yohana 18:37.
Basi, ni kwa sababu gani yeye aliponya? Kuponya, pamoja na miujiza mingine, kulikuwa ishara. Kulithibitisha kwamba ujumbe wa Kikristo ulitoka kwa Mungu, ulikuwa “kweli.” Mtume Paulo alionyesha jambo hilo alipoandika hivi: “Sisi je! tutaokokaje iwapo tumepuza wokovu mkuu namna hiyo maana ulianza kusemwa kupitia Bwana yetu na tulithibitishiwa huo na watu wale waliomsikia, na ambapo Mungu alijiunga kutoa ushahidi kwa ishara pamoja na vionyesho na kazi kubwa sana mbalimbali.” (Ebr. 2:3, 4, NW) Kwa hiyo, jambo la maana lilikuwa ujumbe wa wokovu wala si miujiza. Miujiza hiyo ilithibitisha tu ukweli wa ujumbe huo. Mara jambo hilo lilipokwisha kuthibitishwa na uhakika wa kwamba Mungu alikuwa akilitumia kundi la Kikristo, zawadi za kimwujiza za roho, kutia kuponya, hazikuhitajiwa tena.—1 Kor. 12:27-13:8.
Walakini namna gani juu ya miujiza inayodaiwa kufanywa leo katika jina la Yesu? Yesu alisema kwamba wengi wangemwambia: “Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?” Nalo jibu la Yesu lingekuwa nini? “Ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.” Yesu hakukana kwamba kazi zenye nguvu hazingefanywa. Lakini kazi hizo hazingefanywa kwa ruhusa yake, ‘katika jina lake.’ Zingefanywa kwa nguvu fulani nyingine; kwa hiyo, zilikuwa za kuvunja sheria.—Mt. 7:21-23.
Kwa upande ule mwingine, Yesu alisema juu ya utendaji wa wafuasi wake wa kweli: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” Vile-vile yeye alisema hivi: “Nendeni... mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu .. . kuwafundisha.” Ndiyo, ushuhuda leo ungekuwa ni kuhubiri na kufundisha, si miujiza kama kuponya.—Mt. 24:14, NW; 28:19, 20, NW.
JIBU BORA
Kwa hiyo, ingawa inatiliwa shaka tu kwamba faida za kumwendea mtu mwenye kuponya kwa imani zaweza kuwapo, hatari zenyewe zipo. Kuna hatari ya kuhusiana na mashetani na uonwe na Yesu kuwa mmoja kati ya ‘watendao maovu.’ Pamoja na hayo kuna hatari ya kukosa jibu bora zaidi ya lile linalotolewa na kuponya kwa imani kwa tatizo la magonjwa ya wanadamu.
Kuna jibu bora—jibu la Mungu mwenyewe, ambalo tunaelezwa juu yalo katika Biblia. Kitabu hicho kilichoongozwa na Mungu hakiahidi kupona magonjwa mara moja. Walakini kinatupa msaada juu ya mambo yanayohusu afya. Kufuata shauri la Biblia linalohusu usafi wa mwili na adili kutatusaidia tuepuke maradhi mengi, kutia maradhi ya kisasa yenye kuenea sana ya kaswende na kisonono na kansa inayoletwa na uvutaji wa sigara. Kusikiliza shauri lake kutatusaidia tuepuke maradhi mengi yanayohusiana na wasiwasi unaoweza kuletwa na kijicho, wivu na hasira kali.—Mit. 14:29, 30; 2 Kor. 7:1; Gal. 5:19-23.
Pamoja na hayo, mtume Paulo anatuonyesha namna tunavyoweza kumtegemea Mungu kabisa katika nyakati za hatari kama vile wakati wa magonjwa. Kufanya hivyo kunaondoa mahangaiko mengi na kuleta “amani ya Mungu inayoshinda mawazo yote.” Kwa hakika amani hiyo ya akili inafanya kuwe na matokeo mazuri ya akili juu ya mwili katika nyakati za magonjwa, bila ya mtu kutegemea uponyaji wa imani.—Flp. 4:6, 7, NW.
Zaidi ya hayo, Biblia inatusisimua kwa kusimulia hali zitakazokuwapo duniani pote baada ya Ufalme, serikali ya kimbinguni ambayo Yesu aliihubiri, kuondoa kabisa mfumo wa mambo (system of things) uliopo wenye choyo na wenye jeuri. Masimulizi hayo ni yenye kusisimua zaidi tunapofahamu kwamba wakati wa kuona yakitimia umekaribia sana.
Mtume Petro alisema kwamba miujiza ya Yesu ilikuwa “ishara” na “vionyesho.” (Matendo 2:22, NW) Ilikuwa “ishara” za ile kweli ya ujumbe wa Yesu, na ilikuwa “vionyesho” vya yale ambayo Yehova Mungu atamwezesha kufanyia wanadamu wakati ufalme wa Mungu utakapofanya mapenzi yake yafanywe katika dunia yote. Ebu wazia kazi ya kuponya na ya kurudisha kwenye hali nzuri itakayofanywa wakati huo!
Kikieleza juu ya matokeo ya utendaji huo wa kuponya wa wakati ujao kitabu cha Ufunuo kinasema hivi: “Mungu atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” Hiyo ni ahadi yenye kutegemeka. Hakutakuwapo kukatishwa matumaini au kudanganywa, kwa kuwa Mungu mwenyewe anasema hivi: “Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.”—Ufu. 21:4, 5.
Je! unahangaishwa na tatizo la magonjwa na kifo? Wengi wetu tunahangaishwa. Basi, kwa sababu gani usizichunguze ahadi hizo za Mungu? Utaona kuwa ni zenye kutegemeka sana na zenye kutosheleza kuliko maponyo ya imani.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Maponyo ya Yesu—
• yametoka kwa Mungu kwa hakika
• yalikuwa yenye matokeo kabisa katika kila kisa
• yalikuwa ya kawaida mara nyingi
• yalikubaliwa kuwa yalifaulu hata na adui zake
• yalikusudiwa yauthibitishe ukweli wa ujumbe wa wokovu
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
Maponyo ya Yesu—
• HAYAKUHUSIANA na uchawi au mafumbo
• HAYAKUFUATANA na mahubiri yenye kugusa maono ya moyoni
• HAYAKUHUSIANA na maono ya ndani yakitenda juu ya mwili au namna fulani ya utibabu
• HAYAKUCHUKUA sehemu ya maana zaidi katika huduma yake
• HAYAKUTABIRIWA yangeigwa katika siku zetu
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kuna tofauti nyingi kati ya maponyo yaliyofanywa na Yesu na maponyo ya imani ya siku hizi