Je! Uponyaji wa Imani Hukubaliwa na Mungu?
“LEO tumeona mambo ya ajabu”! Naam, watazamaji walivutiwa. Mtu mwenye kupooza vibaya alikuwa ameponywa mbele ya macho yao. Mponyaji alimwambia mtu huyo: “Ondoka, ujitwike kitanda chako, ukaende zako nyumbani kwako.” Na mtu huyo akafanya vivyo hivyo! Hakuwa mwenye kupooza tena. Si ajabu kwamba wale waliokuwapo ‘walianza kumtukuza Mungu’! (Luka 5:18-26) Ni wazi sana kwamba uponyaji huo uliofanywa na Yesu Kristo karibu miaka 2,000 iliyopita, ulikuwa na kibali cha Mungu.
Namna gani leo? Je! uponyaji wa kimuujiza bado ni uwezekano mzuri kwa wale wasioweza kuponywa kitiba? Yesu alifanya maponyo ya kimuujiza. Waponyaji wa imani leo hudai kuwa wanamwiga. Je! twapaswa kuonaje madai yao?
Uponyaji wa imani hufafanuliwa kuwa “njia ya kutibu magonjwa kwa sala na kuzoea imani katika Mungu.” Encyclopœdia Britannica hukubaliana hivi: “Historia ya uponyaji wa imani katika Ukristo ilianza na ule utumishi mbalimbali wa kibinafsi wenye kustaajabisha wa Yesu na mitume wake.” Naam, Yesu alifanya maponyo yenye kutokeza. Je! waponyaji wa imani leo hufanya miujiza kama yeye alivyofanya?
Imani—Je! Ni Takwa?
Kulingana na Black’s Bible Dictionary, Yesu “alikazia [imani] kuwa takwa la miujiza yake ya uponyaji.” Lakini je, ilikuwa hivyo? Je! Yesu alitaka kwa lazima kwamba mtu mgonjwa awe na imani kabla ya kumponya? Jibu ni la. Imani ilihitajiwa kwa upande wa mponyaji lakini si kwa lazima kwa upande wa mtu aliyekuwa mgonjwa. Pindi moja wanafunzi wa Yesu walishindwa kumponya mvulana mwenye kifafa. Yesu alimponya mvulana huyo na baadaye akawaambia wanafunzi wake sababu kwa nini walikuwa wameshindwa kumponya. “Akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu.”—Mathayo 17:14-20.
Kulingana na Mathayo 8:16, 17, Yesu ‘aliwaponya wote waliokuwa hawawezi.’ Ni kweli, watu hao walikuwa na kadiri fulani ya imani katika Yesu iliyowafanya wamkaribie. (Mathayo 8:13; 9:22, 29) Katika visa vingi walihitaji kuja na kumwomba kabla ya yeye kuwaponya. Hata hivyo, hakuna ungamo lolote la imani lililohitajiwa ili muujiza huo ufanywe. Pindi moja Yesu alimponya mwanamume kilema ambaye hata hakumjua Yesu. (Yohana 5:5-9, 13) Usiku aliokamatwa, Yesu alirudisha sikio lililokatwa la mtumishi wa kuhani mkuu, ingawa mwanamume huyo alikuwa mmoja wa wale katika kikundi cha maadui wa Yesu waliokuja kumkamata. (Luka 22:50, 51) Kwa kweli, katika pindi nyingine, Yesu hata aliwafufua wafu!—Luka 8:54, 55; Yohana 11:43, 44.
Yesu angeweza kufanyaje miujiza ya jinsi hiyo? Kwa sababu alitegemea roho takatifu, au kani ya utendaji ya Mungu. Hiyo ndiyo iliyofanya maponyo, si imani ya watu mmoja mmoja waliokuwa wagonjwa. Ukisoma masimulizi katika Gospeli, utaona pia kwamba maponyo yaliyofanywa na Yesu yalitimizwa bila vitendo vya kuvutia. Hakukuwa vitendo vya kuvutia uangalifu au kuchezea hisia-moyo za watu isivyofaa. Zaidi ya hayo, haidhuru ni ugonjwa gani, Yesu hakushindwa kamwe. Alifanikiwa sikuzote, naye hakutoza kamwe malipo.—Mathayo 15:30, 31.
Maponyo ya Ki-Siku-Hizi Ni Sawa na Yale ya Yesu?
Ugonjwa ni tatizo baya sana, na wakati unapotokea, sisi kiasili hutafuta kitulizo. Lakini, namna gani ikiwa tunaishi mahali ambapo “watu, hasa walio maskini, hutendewa na wafanyikazi wa afya wenye ujuzi kana kwamba wao ni vitu tu na si kama viumbe wa kibinadamu”? Hiyo ndiyo hali aliyoona daktari mmoja katika nchi moja ya Amerika ya Kilatini. Na namna gani ikiwa tunaishi mahali ambapo, sawa na nchi iyo hiyo, ‘ni asilimia 40 tu ya madaktari wa kitiba walio na ujuzi unaofaa wa kufanya kazi yao’?
Haishangazi kwamba wengi, wakikosa la kufanya, huona uponyaji wa imani kuwa ndilo angalau jambo linalostahili kujaribiwa. Hata hivyo, maponyo ambayo waponyaji wa imani hudai kufanya yamebishaniwa. Kwa mfano, kadirio la watu 70,000 walihudhuria mkutano katika São Paulo, Brazili, ambako waponyaji wawili ‘walikanyaga kwa miguu mamia ya miwani iliyotupwa na wasikilizaji, wakiwaahidi wenye miwani hiyo walioamini, kurudishwa kwa uwezo wao wa kuona vema.’ Mmoja wa waponyaji hao alikiri kwa unyoofu katika mahoji kwamba: “Siwezi kusema kwamba wale wagonjwa wote tunaowaombea wataponywa. Inategemea imani yao. Mtu akiamini, yeye ataponywa.” Yeye alilaumu kushindwa kokote kwa kuponywa juu ya ukosefu wa imani kwa upande wa mgonjwa. Lakini, kumbuka kwamba, kama tulivyoona mapema, Yesu alilaumu kule kushindwa kuponya juu ya ukosefu wa imani kwa upande wa yule afanyaye uponyaji!—Marko 9:37-42.
Mponyaji mwingine aliahidi kuponya kansa na kupooza. Ni nini lililotukia? Kulingana na gazeti Veja, “kwa wazi, ahadi hiyo haikutimizwa.” Na ebu sikiliza njia ambayo mwanamume huyo alijiendesha mwenyewe: “Muda wa karibu saa mbili, [mponyaji huyo wa imani] alitumbuiza wasikilizaji kwa mahubiri, sala, kulia kwa nguvu, kuimba—hata kupiga kwa ngumi, kwa kusudi la kuondosha roho waovu waliokuwa ndani ya miili ya waaminifu. Mwishowe, alitupa tai yake na kitambaa chake cha mkono kuelekea wasikilizaji wenye furaha nyingi sana na akapitisha sahani ili kukusanya ‘michango ya hiari.’” Yesu na mitume wake hawakuomba kamwe pesa kwa ajili ya maponyo ya kimuujiza, nao hawakushiriki kamwe katika vitendo vya kuvutia uangalifu wa watu.
Kwa wazi, basi, waponyaji hao wa ki-siku-hizi hawafanyi lile Yesu alilofanya. Na ni vigumu kuona kwamba Mungu angekubali lile wanalofanya. Lakini, je, yeye hukubali maponyo yoyote ya kimuujiza leo? Au je, kuna njia yoyote ambayo imani yetu inaweza kutusaidia wakati sisi au wapendwa wetu tunapokuwa wagonjwa?