Je! Sikuzote Mungu Ni Mkubwa Kuliko Yesu?
YESU hakudai kamwe kuwa Mungu. Kila jambo alilosema juu yake mwenyewe huonyesha kwamba hakujifikiria kuwa sawa na Mungu katika njia yoyote—si katika uwezo, si katika maarifa, si katika umri.
Katika kila kipindi cha kuwako kwake, iwe ni mbinguni au duniani, uneni na mwenendo wake ulionyesha unyenyekeo wa kuwa na cheo kidogo kwa Mungu. Sikuzote Mungu ndiye mwenye cheo kikubwa, Yesu akiwa ndiye mwenye cheo kidogo aliyeumbwa na Mungu.
Yesu Atofautishwa na Mungu
TENA na tena, Yesu alionyesha kwamba yeye ni kiumbe aliye tofauti na Mungu na kwamba yeye, Yesu, ana Mungu aliye juu yake, Mungu ambaye yeye aliabudu, Mungu ambaye yeye aliita “Baba.” Katika sala kwa Mungu, yaani, Baba, Yesu alisema, “Wewe uliye peke yako Mungu wa kweli.” (Yohana 17:3, HNWW) Kwenye Yohana 20:17 alisema hivi kwa Mariamu Magdalene: “Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu.” Kwenye 2 Wakorintho 1:3 mtume Paulo huhakikisha uhusiano huu: “Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.” Kwa kuwa Yesu alikuwa ana Mungu fulani, Baba yake, (Yesu) hangeweza wakati ule ule kuwa ndiye Mungu huyo.
Mtume Paulo hakusita-sita kuwanena Yesu na Mungu kuwa watu walio mbalimbali wakiwa tofauti-tofauti: “Kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, . . . yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo.” (1 Wakorintho 8:6) Mtume Paulo huonyesha tofauti hiyo atajapo “kuwapo kwa Mungu na kwa Kristo Yesu na kwa malaika wateule.” (1 Timotheo 5:21, RS Common Bible) Sawa na vile Paulo anena juu ya Yesu na malaika wenye kutofautiana mmoja na mwenzake mbinguni, ndivyo pia Yesu na Mungu walivyo.
Maneno ya Yesu kwenye Yohana 8:17, 18 yana umaana wa kufikiriwa pia. Yeye ataarifu hivi: “Katika torati yenu imeandikwa kwamba, Ushuhuda wa watu wawili ni kweli. Mimi ndimi ninayejishuhudia mwenyewe, naye Baba aliyenipeleka ananishuhudia.” Hapa Yesu aonyesha kwamba yeye na Baba, yaani, Mungu Mweza Yote, ni lazima wawe ni watu wawili tofauti-tofauti, kwa maana ni jinsi gani nyingine kungeweza kikweli kuwako mashahidi wawili?
Zaidi ya hilo Yesu alionyesha kwamba alikuwa mtu aliye tofauti na Mungu kwa kusema hivi: “Kwa nini kuniita mwema? hakuna aliye mwema ila mmoja, ndiye Mungu.” (Marko 10:18) Kwa hiyo Yesu alikuwa akisema kwamba hakuna aliye mwema kwa kadiri Mungu alivyo, wala hata Yesu mwenyewe. Mungu ni mwema katika njia ambayo humtenganisha na Yesu.
Mtumishi Mnyenyekevu wa Mungu
TENA na tena, Yesu alisema taarifa za jinsi hii: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda.” (Yohana 5:19) “Sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka.” (Yohana 6:38) “Mafundisho ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16, HNWW) Je! mtumi si mkubwa kuliko mtume?
Uhusiano huu waonekana wazi katika kielezi cha Yesu cha shamba la mizabibu. Yeye alimlinganisha Mungu, Baba yake, na mwenye shamba la mizabibu, aliyesafiri ng’ambo na kuliacha katika utunzi wa walimaji, ambao waliwakilisha makuhani Wayahudi. Baadaye mwenyewe alipotuma mtumwa mmoja akachukue baadhi ya matunda ya shamba la mizabibu, walimaji walimpiga mtumwa huyo wakamfukuza mikono mitupu. Halafu mwenyewe akatuma mtumwa wa pili, na baadaye wa tatu, na wote wawili wakatendwa jinsi ile ile. Mwishowe, mwenyewe alisema: “Nitamtuma mwanangu [Yesu], mpendwa wangu; yamkini watamheshimu yeye.” Lakini walimaji hao wafisadi wakasema: “Huyu ndiye mrithi; haya, na tumwue, ili urithi uwe wetu. Wakamtupa nje ya shamba la mizabibu, wakamwua.” (Luka 20:9-16) Hivyo Yesu alitoa kielezi cha cheo chake mwenyewe akiwa ndiye mwenye kutumwa na Mungu akafanye mapenzi ya Mungu, sawa na vile baba hutuma mwana mnyenyekevu.
Wafuasi wa Yesu walimwona sikuzote kuwa mtumishi mnyenyekevu wa Mungu, si kuwa sawa na Mungu. Walisali kwa Mungu juu ya “Mtumishi wako mtakatifu Yesu, uliyemtia mafuta, . . . ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu.”—Matendo 4:23, 27, 30.
Mungu Ni Mkubwa Zaidi Nyakati Zote
PALE pale mwanzoni mwa huduma ya Yesu, alipokuja juu kutoka katika maji ya ubatizo, sauti ya Mungu kutoka mbinguni ilisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye [ambaye nimemkubali, NW].” (Mathayo 3:16, 17) Je! Mungu alikuwa akisema kwamba yeye alikuwa mwana wake mwenyewe, kwamba alijikubali mwenyewe, kwamba alijituma mwenyewe? Sivyo, Mungu Muumba alikuwa akisema kwamba yeye, aliye mkubwa zaidi, alikuwa akimkubali mmoja aliye mdogo zaidi yake, Mwana wake Yesu, kwa ajili ya kazi iliyoko mbele.
Yesu alionyesha ukubwa mwingi zaidi wa Baba yake aliposema hivi: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu amenipaka mafuta nijulishe wazi habari njema kwa maskini.” (Luka 4:18, NW) Kupaka mafuta ni upaji mamlaka au utume wa mtu mkubwa zaidi kwa mtu fulani ambaye hana mamlaka tayari. Hapa Mungu aonekana wazi kuwa ndiye mkubwa zaidi, kwa maana alimpaka Yesu mafuta, akimpa mamlaka asiyotangulia kuwa nayo.
Yesu alielewesha wazi ukubwa mwingi zaidi wa Baba yake wakati mama ya wanafunzi wawili alipoomba kwamba wanae waketi mmoja kulia na mmoja kushoto kwa Yesu aingiapo katika Ufalme wake. Yesu alijibu hivi: “Kwa habari ya viti kwenye mkono wangu wa kulia na kushoto kwangu, hivi si vyangu kukidhi; hivyo ni vya wale ambao wamepewa fungu hilo na Baba yangu,” yaani, Mungu. (Mathayo 20:23, JB) Kama Yesu angalikuwa Mungu Mweza Yote, vyeo hivyo vingalikuwa vyake avitoe. Lakini Yesu hangeweza kuvitoa, kwa maana vilikuwa vya Mungu avitoe, na Yesu hakuwa Mungu.
Sala za Yesu mwenyewe ni kielelezo thabiti cha cheo chake kidogo zaidi. Yesu alipokuwa karibu kufa, alionyesha ni nani aliyekuwa mkubwa zaidi kwake kwa kusali hivi: “Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Alikuwa akisali kwa nani? Je! ni kwa sehemu yake mwenyewe? Sivyo, alikuwa akisali kwa mtu fulani aliye tofauti naye kabisa kabisa, Baba yake, Mungu, ambaye mapenzi yake yalikuwa makubwa zaidi na yangeweza kuwa tofauti na yake mwenyewe, yule Mmoja tu awezaye ‘kuondoa kikombe hiki.’
Halafu, alipokaribia kifo, Yesu alipaaza kilio hiki: “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?” (Marko 15:34) Yesu alikuwa akipaaza kilio kwa nani? Je! ni kwake mwenyewe au kwa sehemu yake mwenyewe? Kwa uhakika, kilio hicho, “Mungu wangu,” hakikutoka kwa mtu aliyejifikiria kuwa Mungu. Na kama Yesu angalikuwa ni Mungu, basi yeye aliachwa na nani? Je! akajiacha mwenyewe? Lingekuwa si jambo la akili. Pia Yesu alisema hivi: “Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu.” (Luka 23:46) Kama Yesu angalikuwa ni Mungu, kwa sababu gani impase kuweka roho yake mikononi mwa Baba yake?
Baada ya Yesu kufa, alikuwa katika ziara (kaburi) kwa sehemu za siku tatu. Kama angalikuwa ni Mungu, basi Habakuki 1:12, NW, lakosea lisemapo: “O Mungu wangu, Mtakatifu wangu, wewe hufi.” Lakini Biblia husema kwamba Yesu alikufa na akawa bila fahamu katika ziara (kaburi). Na ni nani aliyefufua Yesu kutoka kwa wafu? Ikiwa yeye alikuwa mfu kikweli, asingaliweza kujifufua mwenyewe. Kwa upande mwingine, ikiwa hakuwa mfu kihalisi, kifo chake cha kujifanya tu kisingalilipia bei ya ukombozi kwa dhambi ya Adamu. Lakini yeye alilipa bei hiyo kwa ukamili kwa kifo chake cha kweli kweli. Kwa hiyo “Mungu [ndiye] alimfufua [Yesu], akiufungua uchungu wa mauti.” (Matendo 2:24) Aliye mkubwa zaidi, Mungu Mweza Yote, ndiye aliyeinua aliye mdogo zaidi, mtumishi wake Yesu, kutoka kwa wafu.
Je! uwezo wa Yesu kufanya miujiza, kama vile kufufua watu, huonyesha kwamba alikuwa Mungu? Mitume na manabii Eliya na Elisha walikuwa na uwezo huo pia, lakini hiyo haikuwafanya wawe zaidi ya wanadamu. Mungu alitoa nguvu ya kufanya miujiza kwa manabii, Yesu, na mitume ili kuonyesha kwamba Yeye alikuwa anawategemeza. Lakini hiyo haikufanya wowote kati yao wawe sehemu ya Uungu wa wengi.
Yesu Alikuwa na Maarifa Yenye Mipaka
YESU alipotoa unabii wake juu ya mwisho wa mfumo huu wa mambo, alitaarifu hivi: “Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba.” (Marko 13:32) Kama Yesu angalikuwa ni Mwana aliye sehemu sawa ya Uungu, angalijua yale ambayo Baba yake ayajua. Lakini Yesu hakujua, kwa maana hakuwa sawa na Mungu.
Vivyo hivyo, kwenye Waebrania 5:8 twasoma kwamba Yesu “alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata.” Je! twaweza kuwazia kwamba ilikuwa lazima Mungu ajifunze lolote? Sivyo, lakini Yesu alifanya hivyo, kwa maana hakujua kila jambo alilojua Mungu. Na ilikuwa lazima ajifunze jambo fulani ambalo Mungu hahitaji kamwe kujifunza—utii. Mungu halazimiki kamwe kumtii yeyote.
Pia tofauti iliyopo kati ya ajuayo Mungu na ajuayo Kristo ilikuwapo Yesu alipofufuliwa kwenda mbinguni akawe pamoja na Mungu. Angalia maneno ya kwanza ya kitabu cha mwisho cha Biblia: “Ufunuo wa Yesu Kristo, aliopewa na Mungu.” (Ufunuo 1:1) Kama Yesu mwenyewe angalikuwa ni sehemu ya Uungu, je! ingalikuwa lazima apewe ufunuo na sehemu nyingine ya Uungu—Mungu? Kwa uhakika angalijua yote kuuhusu, kwa maana Mungu alijua. Lakini Yesu hakujua, kwa maana hakuwa Mungu.
Yesu Aendelea Kuwa na Cheo Kidogo
KATIKA kuwako kwake kabla ya kuwa binadamu, na pia wakati alipokuwa duniani, Yesu alikuwa na cheo kidogo kwa Mungu. Baada ya ufufuo wake, yeye aendelea kuwa katika cheo kidogo, cha pili.
Wakinena juu ya ufufuo wa Yesu, Petro na wale wenye kuwa pamoja naye waliiambia hivi Sanhedrini ya Kiyahudi: “Mtu huyo [Yesu] Mungu amemtukuza kwa [kwenye, NW] mkono wake wa kuume.” (Matendo 5:31) Paulo alisema hivi: “Mungu alimwadhimisha mno [alimkweza kwenye cheo cha juu zaidi, NW].” (Wafilipi 2:9) Kama Yesu angalikuwa Mungu, Yesu angalikwezwaje, yaani, kuinuliwa kwenye cheo cha juu zaidi ya kile alichokuwa ameonea shangwe hapo kwanza? Tayari angalikuwa amekuwa ni sehemu iliyokwezwa ya Utatu. Ikiwa, kabla ya kukwezwa kwake, Yesu angalikuwa amekuwa ni sawa na Mungu, kumkweza zaidi ya hapo kungalimfanya awe mkubwa zaidi ya Mungu.
Pia Paulo alisema kwamba Kristo aliingia “mbinguni kwenyewe, ili aweze kuonekana katika kuwapo halisi kwa Mungu kwa ajili yetu.” (Waebrania 9:24, JB) Wewe ukienda ukaonekane mbele ya mtu mwingine, wawezaje kuwa ndiwe mtu huyo? Huwezi. Ni lazima uwe mtu tofauti na aliye mbali naye.
Vivyo hivyo, kabla tu ya kupigwa kwa mawe hadi kufa, Stefano mfia-imani ‘alikaza macho yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu.’ (Matendo 7:55) Kwa wazi, yeye aliona watu wawili waliotengeka wakiwa mmoja mmoja—lakini hakuona roho takatifu, hakuona Uungu wa Utatu.
Katika usimulizi kwenye Ufunuo 4:8 hadi 5:7, Mungu aonyeshwa akiwa ameketia kiti-ufalme chake cha kimbingu, lakini Yesu haonyeshwi. Inakuwa lazima yeye afikie Mungu ili kuchukua hati-kunjo kutoka mkono wa kulia wa Mungu. Hii yaonyesha kwamba mbinguni Yesu si Mungu bali yu tofauti naye.
Kwa kuafikiana na yaliyotangulia, Bulletin of the John Rylands Library katika Manchester, Uingereza, hutaarifu hivi: “Katika maisha yake ya kimbingu baada ya kufufuliwa, Yesu huonyeshwa kuwa akidumu na utu wake wa upekee kwa kila kijambo akiwa tofauti tena aliye mbali na uso wa Mungu kama alivyokuwa katika maisha yake duniani akiwa Yesu wa nchini. Akiwa kando ya Mungu na kulinganishwa na Mungu, kweli kweli yeye huonekana akiwa mtu mwingine wa kimbingu katika ua wa kimbingu wa Mungu, sawa na vile malaika walivyokuwa—ingawa akiwa Mwana wa Mungu, yeye yumo katika aina tofauti, na ana daraja lililo juu yao sana.”—Linganisha Wafilipi 2:11.
Bulletin husema hivi pia: “Hata hivyo, lisemwalo juu ya maisha na utendaji wake mbalimbali akiwa Kristo wa kimbingu halimaanishi wala halidokezi kwamba akiwa katika hadhi ya kimungu yeye alingana na Mungu mwenyewe na kwamba ni Mungu kikamili. Bali, kama ionyeshwavyo katika Agano Jipya juu ya sura na huduma yake ya kimbingu twaona mtu aliye tofauti na pia mwenye cheo kidogo kwa Mungu.”
Katika wakati ujao ulio wa milele mbinguni, Yesu ataendelea kuwa mtumishi wa Mungu aliye tofauti na mwenye cheo kidogo. Biblia hueleza jambo hilo hivi: “Hapo ndipo mwisho, [Yesu] atakapompa Mungu Baba ufalme wake . . . Ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote.”—1 Wakorintho 15:24, 28.
Yesu Hakudai Kamwe Kuwa Mungu
MAONI ya Biblia yako wazi. Mungu Mweza Yote, Yehova, si mtu aliye tofauti tu na Yesu bali pia nyakati zote Yeye ni mkubwa kuliko yeye. Sikuzote Yesu huonyeshwa akiwa aliye tofauti na aliye mdogo zaidi, yaani, mtumishi mnyenyekevu wa Mungu. Ndiyo sababu Biblia husema wazi kwamba “kichwa cha Kristo ni Mungu” katika njia ile ile ambayo “kichwa cha kila mwanamume ni Kristo.” (1 Wakorintho 11:3) Na hiyo ndiyo sababu Yesu mwenyewe alisema hivi: “Baba ni mkuu kuliko mimi.”—Yohana 14:28.
Uhakika ni kwamba Yesu si Mungu na hakudai kamwe kuwa hivyo. Jambo hili linatambuliwa na idadi inayoongezeka ya wanachuo. Kama vile Bulletin ya Rylands yataarifu: “Ni lazima uhakika ukabiliwe kwamba utafiti wa Agano Jipya, tuseme, uliofanywa muda wa miaka thelathini au arobaini iliyopita umekuwa ukiongoza idadi inayoongezeka ya wanachuo maarufu wa Agano Jipya kwenye mkataa wa kwamba Yesu . . . kwa uhakika hakujiamini kamwe kuwa Mungu.”
Pia Bulletin hiyo husema hivi juu ya Wakristo wa karne ya kwanza: “Kwa hiyo, wao walipotoa [kwa Yesu] mitajo ya heshima kama kusema Kristo, Mwana wa binadamu, Mwana wa Mungu na Bwana, hizi zilikuwa si njia za kusema kwamba yeye alikuwa Mungu, bali kwamba alifanya kazi ya Mungu.”
Hivyo, hata wanachuo fulani wa kidini hukiri kwamba wazo la Yesu kuwa Mungu hupinga ushuhuda mzima wa Biblia. Humo, sikuzote Mungu ndiye mkubwa zaidi, na Yesu ndiye mtumishi mwenye cheo kidogo.
[Blabu katika ukurasa wa 19]
‘Utafiti wa Agano Jipya umekuwa ukiongoza idadi inayoongezeka ya wanachuo kwenye mkataa wa kwamba kwa uhakika Yesu hakujiamini kamwe kuwa Mungu.’—Bulletin of the John Rylands Library
[Picha katika ukurasa wa 17]
Yesu aliwaambia Wayahudi hivi: “Mimi sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka.”—Yohana 6:38
[Picha katika ukurasa wa 18]
Yesu alipopaaza kilio hivi: “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?” kwa uhakika hakuamini kwamba yeye mwenyewe alikuwa Mungu