Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w88 6/1 kur. 10-15
  • Yesu Kristo Mwana Mpendwa wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yesu Kristo Mwana Mpendwa wa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Si ‘Mungu Mwana’ bali “Mwana wa Mungu”
  • Baba Ni Mkubwa Kuliko Mwana
  • Roho Takatifu—Ni Mtu au Ni Kani ya Utendaji?
  • Je! Sikuzote Mungu Ni Mkubwa Kuliko Yesu?
    Je, Uamini Utatu?
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • “Mungu wa Pekee wa Kweli” Ni Nani?
    Amkeni!—2005
  • Je! Umepata Kujiuliza?
    Amkeni!—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
w88 6/1 kur. 10-15

Yesu Kristo Mwana Mpendwa wa Mungu

‘Sauti ikatoka mbinguni ikisema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.’​—MATHAYO 3:17.

1, 2. (a) Ni ukweli gani ulio rahisi ambao Biblia inafundisha kuhusu Mungu mweza yote na Yesu Kristo? (b) Dini za Jumuiya ya Wakristo zinafundisha nini?

YESU KRISTO alibatizwa akiwa na miaka 30 kwa kuzamishwa majini. Alipokuja juu toka majini, sauti kutoka mbinguni ilisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” (Mathayo 3:17) Sauti hiyo ilikuwa sauti ya Mungu. Katika pindi nyingine, akisali kwa Mungu, Yesu alisema: “Baba, ulitukuze jina lako.” Na Yesu alipokuwa amekwisha kusema hivyo, “sauti [ya Mungu] ikaja kutoka mbinguni, Nimelitukuza, nami nitalitukuza tena.”​—Yohana 12:28.

2 Kutokana na masimulizi haya, hata mtoto anaweza kuelewa kwamba uhusiano uliopo kati ya Mungu mweza yote na Yesu Kristo ulikuwa ule wa baba na mwana mpendwa wake, watu wawili walio tofauti. Hata hivyo, ukweli huu wa Biblia ulio rahisi unakanwa na dini za Jumuiya ya Wakristo. Wao wanasisitiza kwamba Yesu Kristo mwenyewe ni Mungu Mweza Yote, mtu wa pili katika Utatu, mtu wa tatu akiwa ni roho takatifu.

3. Mvurugo kuhusu fundisho la kidini la Utatu unaonyeshwa jinsi gani?

3 Fundisho hilo limesababisha mvurugo mkubwa miongoni mwa watu wa dini za Jumuiya ya Wakristo, hiyo ikiwa ndiyo sababu moja inayofanya New Catholic Encyclopedia iite Utatu fumbo. Kweli kweli, unasababisha mvurugo hata miongoni mwa viongozi wa kidini, kwa maana ensaiklopidia hiyo hiyo inasema hivi pia: “Kuna walimu wachache wa theolojia ya Utatu katika seminari za Roma Katoliki ambao hawajasumbuliwa wakati mmoja au mwingine na swali hili, ‘Lakini mtu anaweza kuhubiri juu ya Utatu jinsi gani?’ Na ikiwa swali hilo ni dalili ya mvurugo kwa upande wa wanafunzi, labda hilo ni dalili la mvurugo huo huo kwa upande wa maprofesa wao.”

4. Ni nini fundisho rasmi la makanisa kuhusu Utatu?

4 Fundisho hilo la kidini lenye kuvuruga ndilo itikadi kuu ya dini ya Katoliki na Protestanti. The Catholic Encyclopedia inataarifu hivi: “Utatu ndilo neno linalotumiwa kuonyesha fundisho kuu la kidini la dini ya Kikristo . . . Hivyo, katika maneno ya Imani ya Athanasio: ‘Baba ni Mungu, Mwana ni Mungu, na Roho Takatifu ni Mungu, na bado hakuna Miungu watatu ila mmoja.’” Vivyo hivyo, katika kesi ya mahakama iliyowahusu Mashahidi wa Yehova katika Ugiriki, Kanisa Orthodoksi la Ugiriki lilisema: “Fundisho la kidini la msingi la Ukristo, ambalo katika hilo Wakristo wote wanakiri kuwa wanaitikadi . . . Bila kujali farakano au mfumo wa itikadi, ni . . . Utatu, kwamba Mungu ni Mmoja katika watu watatu.” Kanisa Orthodoksi la Ugiriki hilo lilitaarifu hivi pia: “Wakristo ni wale ambao wanamkubali Kristo kuwa Mungu.” Ilisema kwamba wale ambao hawakubali Utatu si Wakristo bali ni wazushi.

5, 6. Kwa sababu gani ni jambo la maana sana kujua ukweli kuhusu jambo hili?

5 Hata hivyo, ikiwa fundisho hili la “msingi” la Utatu la Jumuiya ya Wakristo si la kweli, ikiwa ni la uwongo, basi kinyume kingekuwa kweli. Wakristo wa kweli wangelikataa. Wale ambao wameasi imani ya Kikristo wangelishikilia. Matokeo yangekuwa nini kwa kikundi cha pili? Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, “ufunuo wa Yesu Kristo, aliopewa na Mungu” tunasoma hivi kuhusu wale ambao hawastahili uhai wa milele katika Ufalme wa Mungu: “Huko nje wako mbwa, na wachawi, na wazinzi, na wauaji, na hao waabuduo sanamu, na kila mtu apendaye uongo na kuufanya.”​—Ufunuo 1:1; 22:15.

6 Kwa sababu ya umaana walo, sisi twapaswa tufahamishwe lilikobuniwa wazo hili la Utatu na kwa sababu gani lilibuniwa. Ni nani hasa anayeliunga mkono? Elimu ya Biblia ya ki-siku-hizi inasema nini juu yalo? Lakini kabla ya kuzungumzia mambo haya, na tuchunguze zaidi yale ambayo Neno la Mungu lenyewe lililovuviwa linasema.​—2 Timotheo 3:16, 17.

Si ‘Mungu Mwana’ bali “Mwana wa Mungu”

7. Funzo la unyofu la Biblia linafunua nini kwa habari ya Yesu?

7 Yesu mwenyewe hakudai kamwe kuwa Mungu mweza yote. Usomaji wo wote wa Biblia kwa unyofu bila kushikilia mawazo ya kimbele kuhusu Utatu utathibitisha hilo. Mathalani, kwenye Yohana 3:16, Yesu alisema: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee.” Mistari miwili baadaye, Yesu alisema tena kwamba yeye alikuwa “Mwana pekee wa Mungu.” (Yohana 3:18) Wayahudi walipomshtaki Yesu kwamba amekufuru, yeye alijibu: “Je! yeye ambaye Baba alimtakasa, akamtuma ulimwenguni, ninyi mnamwambia, Unakufuru; kwa sababu nalisema, Mimi ni Mwana wa Mungu?” (Yohana 10:36) Yesu hakusema kwamba yeye alikuwa ‘Mungu Mwana’ bali alikuwa “Mwana wa Mungu.”

8. Ni ushuhuda gani ambao afisa mmoja wa jeshi na wale waliokuwa naye walitoa?

8 Yesu alipokufa, hata askari Warumi waliokuwa wakisimama karibu walijua kwamba Yesu hakuwa Mungu. “Basi yule akida, na hao waliokuwa pamoja naye wakimlinda Yesu, walipoliona tetemeko la nchi na mambo yaliyofanyika, wakaogopa sana, wakisema, Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Mathayo 27:54) Wao hawakusema, ‘huyu alikuwa Mungu’ au ‘huyu alikuwa Mungu Mwana,’ kwa sababu Yesu na wanafunzi wake walifundisha kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, si Mungu mweza yote katika umbo la kibinadamu.

9, 10. Ni ushuhuda gani wenye nguvu unaotolewa katika zile Gospeli kwa habari ya uhusiano ulioko kati ya Mungu na Yesu?

9 Mungu mwenyewe alishuhudia kwamba Yesu alikuwa Mwana mpendwa wake, kama alivyoandika mwandikaji wa Biblia Mathayo wakati Yesu alipobatizwa. (Mathayo 3:17) Waandikaji wengine wa Biblia waliandika vivyo hivyo. Marko aliandika: “Na sauti ikatoka mbinguni, Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa wangu; nimependezwa nawe.” (Marko 1:11) Luka alisema: “Sauti ikatoka mbinguni, Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa wangu, nimependezwa nawe.” (Luka 3:22) Na Yohana Mbatizaji aliyembatiza Yesu alishuhudia hivi: “Nami nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu [Yesu] ni Mwana wa Mungu.” (Yohana 1:34) Kwa hiyo Mungu mwenyewe, waandikaji wote wanne wa Gospeli, na Yohana Mbatizaji wanataarifu waziwazi kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu. Na muda fulani baadaye, wakati wa kugeuzwa umbo kwa Yesu, jambo linalofanana na hilo lilitukia: “Sauti [ya Mungu] ikatoka katika wingu, ikisema, Huyu ni Mwanangu, mteule wangu, msikieni yeye.”​—Luka 9:35.

10 Katika masimulizi haya, je! Mungu alikuwa akisema kwamba yeye alikuwa mwana wake yeye mwenyewe, kwamba yeye alijipeleka mwenyewe, na kwamba yeye alipendezwa na yeye mwenyewe? La, Mungu Baba, Muumba, alikuwa akisema kwamba yeye alikuwa amepeleka Mwana wake Yesu, mtu aliye peke yake, afanye kazi ya Mungu. Kwa sababu hiyo, katika Maandiko yote ya Kigiriki maneno “Mwana wa Mungu” yanatumiwa kuelekeza kwa Yesu. Lakini hakuna wakati hata mmoja tunapoona maneno ‘Mungu Mwana,’ kwa kuwa Yesu hakuwa Mungu mweza yote. Yeye alikuwa Mwana wa Mungu. Wao ni watu wawili tofauti, na hakuna “fumbo” la kitheolojia linaloweza kubadili ukweli huo.

Baba Ni Mkubwa Kuliko Mwana

11. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba Mungu alikuwa mkubwa wake?

11 Yesu alijua kwamba yeye hakuwa sawa na Baba yake lakini kwa vyo vyote alikuwa katika cheo cha chini. Yeye alijua kwamba alikuwa Mwana mpendwa aliyekuwa na upendo wenye kina kirefu sana kwa Baba yake. Hiyo ndiyo sababu mara kwa mara, Yesu alisema maneno kama yafuatayo: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda.” (Yohana 5:19) “Kwa kuwa mimi sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka.” (Yohana 6:38) “Mafunzo yangu si yangu mimi, ila ni yake yeye aliyenipeleka.” (Yohana 7:16) “Mimi namjua [Mungu], kwa kuwa nimetoka kwake, naye ndiye aliyenituma.” (Yohana 7:29) Anayepeleka ndiye mkubwa. Anayepelekwa ndiye mdogo, mtumishi. Mungu ndiye anayepeleka. Yesu ndiye anayepelekwa. Wao si sawa. Kama alivyoeleza Yesu: “Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka.”​—Yohana 13:16.

12. Ni kielezi kipi kinachoonyesha cheo cha chini cha Yesu kwa Baba?

12 Jambo hili linaonyeshwa wazi pia katika kielezi alichotoa Yesu. Yeye alimfananisha Baba yake, Yehova Mungu, kuwa mwenye shamba aliyesafiri ng’ambo na akaacha shamba lile chini ya uangalizi wa wakulima—ambao bila shaka wanafananisha viongozi wa kidini Wayahudi. Kwa wakati, mwenye shamba alipeleka mtumwa akapate matunda fulani kutoka katika shamba lile la mizabibu, lakini wakulima walimpiga mtumwa huyo na kumpeleka mikono mitupu. Kisha mwenye shamba akapeleka mtumwa wa pili, na jambo lile lile likatukia. Alipeleka mtumwa wa tatu, naye akatendwa vile vile. Kisha mwenye shamba [Mungu] akasema: “Nitamtuma mwanangu [Yesu], mpendwa wangu; yamkini watamheshimu yeye.” Lakini wakulima hao wafisadi wakasema: “Huyu ndiye mrithi; haya, na tumwue, ili urithi uwe wetu. Wakamtupa nje ya shamba la mizabibu, wakamwua.” (Luka 20:9-16) Tena, jambo hili linaonyesha wazi kwamba Yesu yu chini ya Baba, alipelekwa na Baba ili afanye mapenzi ya Baba.

13. Ni taarifa gani za Biblia zilizo wazi zinazoonyesha kwamba Mungu alikuwa mkubwa wa Yesu?

13 Yesu mwenyewe alisema hivi: “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Twapaswa tuitikadi Yesu, kwa kuwa kwa hakika yeye alijua ukweli kuhusu uhusiano wake na Baba yake. Mtume Paulo pia alijua kwamba Mungu alikuwa mkubwa kwa Yesu, na akasema hivi: “Ndipo Mwana [Yesu] mwenyewe naye atatiishwa chini . . . [ya] Mungu.” (1 Wakorintho 15:28) Jambo hilo linaonwa zaidi katika taarifa ya Paulo katika 1 Wakorintho 11:3: “Kichwa cha Kristo ni Mungu.” Yesu alikubali kwamba yeye alikuwa na Mungu mkubwa alipowaambia wanafunzi wake: “Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu.”​—Yohana 20:17.

14. Ni maandiko gani mengine ya Biblia yanayoonyesha kwamba Yesu hakuwa Mungu mweza yote?

14 Yesu alitaja ukubwa wa Mungu wakati mama ya wawili wa wanafunzi alipoomba kwamba wanawe waketi mmoja kulia na yule mwingine kushoto kwa Yesu wakati alipokuja katika Ufalme wake. Yeye alijibu: “Lakini kuketi mkono wangu wa kuume na mkono wangu wa kushoto, sina amri kuwapa.” (Mathayo 20:23) Kama Yesu angekuwa Mungu mweza yote, yeye angekuwa na amri kuwapa. Lakini hakuwa na amri. Baba yake ndiye aliyekuwa na amri ya kuwapa. Vivyo hivyo, alipokuwa akisimulia unabii kuhusu umalizio wa mfumo huu wa mambo, Yesu alitaarifu hivi: “Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba.” (Marko 13:32) Kama Yesu angalikuwa Mungu mweza yote, angalijua siku hiyo na saa ile. Lakini hakujua kwa sababu yeye hakuwa Mungu Mwenye kujua Yote. Yeye alikuwa Mwana wa Mungu naye hakujua kila kitu ambacho Baba yake alijua.

15. Yesu alipokaribia kufa, yeye alijitiisha chini ya Mungu jinsi gani?

15 Yesu alipokaribia kufa, yeye alijitiisha chini ya Baba yake kwa kusali hivi: “Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Yesu alikuwa akisali kwa nani? Je! alikuwa akisali kwake mwenyewe? La, alikuwa akisali kwa Baba yake aliye Mbinguni. Jambo hili linaonyeshwa wazi kwa kusema kwake hivi: “Walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” Halafu, wakati wa kifo chake, Yesu alilia akipaaza sauti: “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?” (Marko 15:34) Yesu alikuwa akilia kwa kupaazia nani sauti? Je! alikuwa akijipaazia yeye mwenyewe? La, yeye alikuwa akipaaza sauti kwa Baba yake aliyekuwa Mbinguni.

16. Ni jinsi gani kifo na ufufuo wa Yesu unavyoonyesha kwamba yeye mwenyewe hangeweza kuwa Mungu mweza yote?

16 Baada ya Yesu kufa, yeye alikuwa kaburini siku zipatazo tatu. Ni nani aliyemfufua? Kwa kuwa alikuwa mfu, yeye hangeweza kujifufua mwenyewe. Na ikiwa hakuwa amekufa kweli kweli, basi hangaliweza kulipia ukombozi kwa dhambi ya Adamu. Lakini yeye alikufa hakika, naye hakuwapo kwa siku zipatazo tatu. Mtume Paulo anatuambia ni nani aliyemfufua Yesu: “Mungu alimfufua, akiufungua uchungu wa mauti.” (Matendo 2:24) Mungu mkubwa, Mweza Yote, alifufua aliye mdogo, Mwana wake mpendwa, Yesu, kutoka kwa wafu. Ili kutoa kielezi: Wakati Yesu alipomfufua Lazaro kutoka kwa wafu, ni nani aliyekuwa mkubwa? Yesu alikuwa mkubwa, kwa kuwa angeweza kumrudisha Lazaro kutoka kwa wafu. (Yohana 11:41-44) Ilikuwa vivyo hivyo Mungu alipomfufua Yesu. Mungu alikuwa mkubwa, kwa kuwa angeweza kumrudisha Yesu kutoka kwa wafu.

17. Ni ithibati gani nyingine iliopo inayoonyesha kwamba Yesu hakuwa Mungu?

17 Kwa kadiri iwezekanavyo Yesu hangeweza kuwa Mungu yeye mwenyewe, kwa kuwa Yesu aliumbwa na Mungu. Angalia jinsi Emphatic Diaglott ya Benjamin Wilson inavyoeleza Kitabu cha Ufunuo sura ya 3, mstari 14: “Mambo haya asema Amina, yule shahidi mwaminifu na wa kweli [Yesu], mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” Hali moja na hiyo, Wakolosai 1:15, 16 inasema hivi kwa habari ya Yesu: “Naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi . . . vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake.” Hivyo katika mbingu Mungu mweza yote alimuumba Mwana wake moja kwa moja kisha “katika yeye” au “kwa njia yake,” akaumba vitu vingine, sawa na vile mfanya kazi stadi anavyoweza kufanyiwa kazi na mfanya kazi aliyezoezwa. Vitu vilivyoumbwa “kwa njia yake” havitii ndani Yesu mwenyewe, kwa kuwa Mungu tayari alikuwa amemuumba. Hivyo, yeye anaitwa “mzaliwa wa kwanza,” ‘wa pekee.’ Mtoto anapokuwa mzaliwa wa kwanza, wa pekee, hiyo haimaanishi kamwe kwamba mtoto huyo ni sawa na baba. Sikuzote hiyo inamaanisha kwamba kuna nyutu mbili tofauti zinazohusika, baba na mwana.

Roho Takatifu—Ni Mtu au Ni Kani ya Utendaji?

18. Biblia inafundisha nini kuhusu roho takatifu?

18 Namna gani kuhusu anayedhaniwa kuwa mtu wa tatu katika Utatu, roho takatifu, inayosemekana kuwa na uwezo ule ule, nguvu, na umilele wa Baba na Mwana? Hakuna mahali po pote katika Biblia ambapo roho takatifu inatajwa pamoja na Mungu na Kristo kuwa inalingana nao. Mathalani, katika pindi ya ubatizo wa Yesu, Marko 1:10 inaonyesha kwamba roho takatifu ilishuka chini juu ya Yesu “kama hua,” si katika umbo la kibinadamu. Roho takatifu haikuwa mtu wa aina fulani akishuka juu ya Yesu lakini ilikuwa kani ya utendaji ya Mungu. Uwezo huo kutoka kwa Mungu ulimwezesha Yesu awaponye wagonjwa na kuwafufua wafu. Kama Luka 5:17 inavyosema katika Diaglott: “Uwezo wenye Nguvu wa Bwana [Mungu] ulikuwa juu yake [Yesu] ili aponye.” Baadaye, katika Pentekoste, mitume pia walipewa uwezo kutoka kwa Mungu ili waponye na kufufua wafu. Je! jambo hilo liliwafanya wawe sehemu ya “kichwa cha mungu” fulani? La, wao walikuwa tu wamepewa uwezo kutoka kwa Mungu, kupitia kwa Kristo, ili wafanye mambo ambayo kwa kawaida wanadamu hawangefanya.

19. Kwa sababu gani haiwezekani roho takatifu iwe mtu wa tatu katika Utatu?

19 Kani hiyo hiyo ya utendaji inatajwa katika Waefeso 5:18, NW, ambapo Paulo anashauri hivi: “Endeleeni kujazwa na roho.” Vivyo hivyo, Matendo 7:55, NW inasema kwamba Stefano alikuwa “amejaa roho takatifu.” Na katika Pentekoste, wafuasi wa Yesu “wote wakajazwa roho takatifu.” (Matendo 2:4 NW) Je! mwanadamu anaweza kujazwa na mtu mwingine? La, lakini anaweza kujazwa na uwezo unaotoka kwa Mungu. Roho takatifu hiyo ndiyo kani ile ile ambayo Mungu alitumia kuumba ulimwengu wote mzima. Kama Mwanzo 1:2, NW inavyosema: “Kani ya utendaji ya Mungu ilikuwa ikienda huku na huku juu ya uso wa maji.”

20. Ni njozi gani aliyoona Stefano inayoonyesha zaidi kwamba Utatu si wa kweli?

20 Baada ya Yesu kufufuliwa, Stefano aliona njozi ya mbingu na “akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu.” (Matendo 7:55) Hivyo, watu wawili waliotengwa walionekana katika mbingu: (1) Mungu na (2) Yesu Kristo aliyefufuliwa. Hakuna roho takatifu inayotajwa katika njozi hii kwa sababu haikuwa mtu wa tatu wa Utatu. Roho takatifu, ikiwa kani ya utendaji ya Mungu, ingetoka kwa Mungu lakini si ikiwa kiumbe kilichotengwa. Hiyo ndiyo sababu Stefano aliona watu wawili tu, si watatu.

21, 22. (a) Ensaiklopidia ya kidini inakubali nini kwa habari ya roho takatifu? (b) Ni mambo gani yatakayotiwa ndani katika makala yetu inayofuata?

21 Kwa habari ya roho takatifu, New Catholic Encyclopedia inakubali hivi: “Hakika [A]gano la [K]ale haliwazii roho ya Mungu kuwa mtu, wala katika maana halisi ya kifalsafa, wala katika maana ya watu wa ukoo wa Shemu. Roho ya Mungu ni uwezo wa Mungu tu. Ikiwa nyakati fulani inaonyeshwa kuwa mbali na Mungu, ni kwa sababu pumzi ya Yahweh inatenda kama umbo.” Pia inataarifu hivi: “Maandiko mengi ya A[gano] [J]ipya yanafunua roho ya Mungu kuwa kitu, si mtu; hii inaonekana hasa katika usawa wa roho na uwezo wa Mungu.”

22 Kwa sababu ya mambo yote haya ya hakika, fundisho hili la kidini lenye “msingi” wa Utatu la Jumuiya ya Wakristo haliwezi kuwa la kweli. Neno la Mungu lenyewe linakanusha dai hilo. Linaonyesha wazi wazi kwamba Yehova Mungu ndiye Baba mwenye upendo na kwamba Yesu Kristo ndiye Mwana wake mpendwa, Mwana ambaye alikuwa na upendo sana kwa Baba yake hivi kwamba alikuwa na nia ya kutii mpaka kifo. Hata hivyo, watu fulani wanabisha kwamba kuna maandiko ambayo yanaonekana kuwa yanaunga mkono Utatu, hivyo katika makala yetu inayofuata, tutachunguza mengine yayo. Pia, tutazungumza kwa nini fundisho hili la kidini limekuwa sehemu ya muhimu ya Jumuiya ya Wakristo, na lilikobuniwa.

Wewe Ungejibu Jinsi Gani?

◻ Biblia inafundisha nini juu ya Mungu na juu ya Yesu?

◻ Maandiko yanaonyesha uhusiano wa Baba na Mwana jinsi gani?

◻ Ni maandiko fulani yapi ya Biblia yanayoonyesha kwamba Mungu ni mkubwa kuliko Yesu?

◻ Kwa sababu gani roho takatifu haiwezi kuwa sehemu ya Utatu?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Yesu alitangaza: “Baba ni mkuu kuliko mimi”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki