Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 5/1 kur. 16-20
  • Mungu Mwana au “Mwana wa Mungu”?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mungu Mwana au “Mwana wa Mungu”?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Baba Ndiye Mkuu Zaidi?
  • Baada ya Kupaa kwa Yesu
  • Kwenye “Mkono wa Kuume wa Nguvu”
  • Mwana wa Nani?
  • Lile Agano Jipya kwa Ajili ya Wakristo
  • Hali Iliyobadilika
  • Yesu Kristo Mwana Mpendwa wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Je! Sikuzote Mungu Ni Mkubwa Kuliko Yesu?
    Je, Uamini Utatu?
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 5/1 kur. 16-20

Mungu Mwana au “Mwana wa Mungu”?

“Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”—MATHAYO 16:16

1. (a) Washiriki wengi wa makanisa wana maoni gani juu ya Yesu? (b) Ni maelezo gani ya kupendeza ambayo Yesu alitoa juu ya jambo hilo?

JE! YESU alikuwa Mungu? Washiriki wengi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wangejibu kwa kusema ndivyo. Lakini je! wewe ulijua kwamba kuna mtu fulani ambaye Yesu alimwita “Mungu”? Fungua Biblia yako mwenyewe kwenye Yohana 20:17 kisha usome maneno ya Yesu mwenyewe karibu na mwisho wa mstari huo: “Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu.”

2. Ni maelezo gani mengine ya kupendeza ambayo Biblia inatoa juu ya uhusiano ulio kati ya Yesu na Mungu?

2 Kwa muda mfupi, ebu fikiria yule malaika aliyetangazia Mariamu kuzaliwa kwa Yesu. Yeye hakusema mtoto wake angekuwa Mungu, bali kwamba angekuwa “Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Na badala ya kusema, kama wengine wanavyosema, kwamba “Mungu Mwenyewe” ndiye aliyekuja duniani kutoa ukombozi, Maandiko yanasema “Mungu alimtuma Mwanawe” kufanya hivyo.—Wagalatia 4:4, 5; 1 Yohana 4:9,10.

3, 4. Maneno yaliyosemwa na Petro na Yohana Mbatizaji yanakosaje kukubaliana na fundisho la Jumuiya ya Wakristo juu ya Utatu?

3 Yesu aliuliza wanafunzi wake wao waliamini yeye alikuwa nani. Je! Simoni Petro alijibu hivi: “Wewe ni Mungu”? Hapana. Petro alisema: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” Je! Yesu alimsahihisha Petro? Hapana, Yesu alisema: “Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni.”—Mathayo 16:15-17.

4 Waandikaji wa kidini wanamtaja “Mungu Mwana” kwa sababu ya kuamini Mungu ni Utatu. Lakini, Yohana Mbatizaji hakumwita Yesu “Mungu Mwana” bali “Mwana wa Mungu.” Wanafunzi wa Yesu hawakusema, “Wewe ni Mungu Mwana,” bali, “Hakika wewe u Mwana wa Mungu.” Pana tofauti kubwa kati ya maneno hayo.—Yohana 1:34; Mathayo 14:33.

Je! Baba Ndiye Mkuu Zaidi?

5. Ni nini linaloweza kusemwa juu ya cheo cha Yesu cha kimbingu?

5 Biblia inaeleza habari za kuwako kwa Yesu kabla hajawa mwanadamu. Yeye alikuwako kabla ya Abrahamu kuwako, alikuwa pamoja na Baba yake wa kimbingu “kabla ya ulimwengu kuwako,” alikuwa ndiye “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” na kupitia yeye “vitu vyote viliumbwa.” (Yohana 17:5; 8:58; Wakolosai 1:15-17) Yesu “alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya [mti wa mateso]. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina.” Pia Biblia inasema kwamba “Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo... [alimfufua] katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia.”—Wafilipi 2:8, 9; Waefeso 1:17, 20, 21.

6-8. Ni nini mengine kati ya mambo ambayo Yesu alisema juu ya cheo chake kuhusiana na Baba?

6 Hata hivyo Yesu alirudia-rudia kuonyesha utii wa kunyenyekea Baba, wala hakuonyesha usawa naye. Alisema alitumwa na Baba yake, akapewa maagizo na Baba yake, akaamriwa na Baba yake juu ya mambo atakayosema. (Yohana 3:17; 5:36; 6:38; 12:49, 50) Yesu alisema kwamba ‘aliimaliza kazi’ ambayo Baba yake alimpa, na kwamba wafuasi wake “wamejua ya kuwa ndiwe [Baba] uliyenituma.”—Yohana 17:4, 6, 18, 25.

7 Hata adui za Yesu hawakumshtaki juu ya kusema alikuwa Mungu. Bali, walisema alikuwa akijifanya mwenyewe “sawa na Mungu” kwa kumwita Mungu Baba yake. Walitaka kumwua Yesu kwa sababu kama inavyoelezwa vizuri na tafsiri moja inayojulikana sana ya Katoliki ya Roma: “Yeye alisema juu ya Mungu kuwa Baba yake mwenyewe, na kwa hiyo akajifanya mwenyewe mtu aliye sawa na Mungu.” Yesu alisema: “Mimi nawaambia ninyi kwa uzito ulio mkubwa zaidi, Mwana hawezi kufanya kitu akiwa peke yake mwenyewe; yeye anaweza kufanya lile tu analoona Baba akifanya: na lo lote analofanya Baba ndilo Mwana anafanya pia.”-—Yohana 5:18,19, The Jerusalem Bible.

8 Ajapokuwa na cheo kilichotukuzwa sana, Yesu aliwaambia mitume wake hivi: “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Watu wengine wanasema kwamba ilikuwa hivyo kwa sababu tu Yesu alikuwa angali duniani na kwamba sivyo ilivyo tena sasa kwa kuwa amekwisha kupaa mbinguni. Lakini hivyo sivyo Biblia inavyosema.

Baada ya Kupaa kwa Yesu

9. Paulo alionyeshaje tofauti iliyopo kati ya Yesu na Mungu hata baada ya Yesu kufufuliwa?

9 Baada ya Yesu kupaa mbinguni, wafuasi wake waliendelea kufundisha kwamba Baba ndiye mkuu kuliko Mwana. Miaka zaidi ya 20 baadaye, Paulo aliandika juu ya “Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.” (Warumi 15:6) Angalia maneno hayo kwa makini. Paulo anataja Mungu wa Yesu. Paulo anaendelea kuonyesha tofauti hiyo bila ugeugeu, si kati ya Baba na Yesu tu, bali pia kati ya Mungu na Yesu. Anaandika juu ya Mungu na Kristo. Salamu ambayo Paulo aliitumia kama kiwango chake katika barua alizoandika ilikuwa hii: “Neema na iwe kwenu na amani itokayo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo.” (Warumi 1:7; 1 Wakorintho 1:3; 2 Wakorintho 1:2; Wagalatia 1:3; Waefeso 1:2; Wafilipi 1:2) Pia, si kwamba Paulo aliandika Kristo ni Mungu, bali kwamba yeye ni “sura yake Mungu,” na kwa hiyo anamwakilisha yeye kwa ukamilifu. (2 Wakorintho 4:4) Lakini, mtafsiri wa The Living Bible alibadili kifungu hicho kwa sababu ya kuamini kwamba Mungu ni Utatu, akakifanya kiseme “Kristo, ambaye ni Mungu.” Lakini kwa kuwa hivyo sivyo hasa kinavyosema kifungu chenyewe, maelezo ya chini haya yaliongezwa: “Kwa uhalisi, ‘ambaye ndiye mfano wa Mungu.’ ”

10. Ufunuo unaonyeshaje tofauti iliyo kati ya Yesu na Mungu?

10 Kitabu cha Biblia cha Ufunuo hakitofautishi kati ya Yesu na Baba tu, bali pia kati ya Yesu na Mungu. Kinaanza kwa kusema, “Ufunuo wa Yesu Kristo, aliopewa na Mungu.” (Ufunuo 1:1) Miaka zaidi ya 60 baada ya kupaa kwa Yesu, Ufunuo unamtaja Yesu wa kimbingu aliyetukuzwa kuwa akisema: “Yeye ashindaye, nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu . . . Nami nitaandika juu yake jina la Mungu wangu, na jina la mji wa Mungu wangu, huo Yerusalemu mpya, ushukao kutoka mbinguni kwa Mungu wangu, na jina langu mwenyewe, lile jipya.”—Ufunuo 3:12.

11. Tofauti kati ya Yesu na Mungu inaonyeshwaje katika sura ya mwisho ya Biblia?

11 Tofauti hiyo kati ya Mungu na mwana-Kondoo Yesu Kristo inaendelea kuonyeshwa moja kwa moja mpaka kwenye sura ya mwisho ya Biblia, ambapo kile kiti kikuu cha kifalme cha mbinguni cha Yerusalemu Mpya wenye utukufu mwingi sana hakielezwi kuwa kiti cha ufalme cha Utatu wa kuwaziwa tu, bali kuwa “kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 22:1, 3) Hayo si maneno yaliyo magumu kuelewa, isipokuwa kama wewe umefundishwa kujaribu kuyafanya yaseme jambo fulani ambalo hayalisemi.

Kwenye “Mkono wa Kuume wa Nguvu”

12. (a) Yesu alielezaje cheo ambacho angekuwa nacho baada ya kufufuliwa kwake? (b) Andiko la Zaburi 110:1 linaonyeshaje kwamba Yesu si Yehova?

12 Kwa kutafuta sababu ya kumwua Yesu, adui zake hawakuuliza kama yeye alidai kuwa Mungu, bali kama alikuwa ndiye “Kristo, Mwana wa Mungu.” Yeye alijibu: “Wewe umesema; lakini nawaambieni, Tangu sasa mtamwona Mwana wa Adamu ameketi mkono wa kuume wa nguvu, akija juu ya mawingu ya mbinguni.” (Mathayo 26:63, 64) Mapema kabla ya hapo Yesu alikuwa ametaja na kutumia maneno haya ya Daudi kuhusu yeye mwenyewe: “Neno la [Yehova] kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako.” Yesu hakusema alikuwa ndiye Yehova, wala sehemu ya Utatu fulani usiopatana na Maandiko, bali alisema kwamba angekuwa kwenye mkono wa kuume wa Yehova, akingojea kutimia kwa wakati wa Mungu na makusudi yake.—Zaburi 110:1; Mathayo 22:42-44.

13. Stefano aliona nini muda mfupi tu kabla ya kufia imani?

13 Stefano, mtu wa kwanza kufa kwa ajili ya imani yake katika Kristo, alipewa njozi ya Yesu aliyefufuliwa akiwa mbinguni. Je! alimwona Yesu akiwa Mungu, au sehemu ya Utatu fulani? Hapana. Kama vile Yesu na Daudi walivyokuwa wametabiri, alimwona Yesu “mkono wa kuume wa Mungu.” The Living Bible inasema kwamba Stefano alimwona “Yesu Masihi amesimama kando ya Mungu, kwenye mkono wa kuume wake! ”—Matendo 7:55, 56.

14. Njozi ya Danieli inaonyesha nini juu ya “mmoja aliye mfano wa mwanadamu”?

14 Maono makubwa zaidi ya jambo hilo yanapatikana katika njozi ya Danieli yenye utukufu mwingi juu ya yule Mzee wa Siku. Danieli aliandika hivi: “Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye. Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo haitapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa.” (Danieli 7:13,14) Yesu siye aliyekuwa Mzee wa Siku, yaani Yehova Mungu, bali alikuwa Mwana wa Adamu. Na ebu angalia kwamba huyo alipandishwa juu akaletwa mbele ya Baba yake wa kimbingu, ili apokee “mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie.”—Linganisha Mathayo 25:31.

15. Ufunuo unaonyesha kwamba mkutano mkubwa huo ungejua nini?

15 Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinaonyesha wazi kwamba mkutano mkubwa wa kutoka mataifa yote na lugha zote ambao unakuja chini ya utawala wa Kristo ungekuwa watu wanaojua tofauti kati ya Mungu na Mwana-Kondoo Yesu Kristo, kwa maana wanatoa mlio wa sifa wakisema: “Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.” Zaidi ya hilo, wale 144,000 wanaosimama pamoja na Mwana-Kondoo Yesu Kristo juu ya Mlima Sayuni wa kimbingu wanakuwa na “jina lake na jina la Baba yake limeandikwa katika vipaji vya nyuso zao.”—Ufunuo 7:9, 10; 14:1.

Mwana wa Nani?

16. Wayahudi wangeelewa nini wakati Yesu aliposema kwamba Baba yake ndiye yule walimwita Mungu wao?

16 Wayahudi walijua habari za jina la Mungu. Walijua Yesu alikuwa akiongea habari za nani wakati aliposema hivi: “Anitukuzaye ni Baba yangu, ambaye ninyi mwanena kuwa ni Mungu wenu.” (Yohana 8:54) Huyo alikuwa Mungu gani? Hata kama wao wangeendelea au hawangeendelea kulitamka jina lake, waliliona katika nakala zao za Maandiko, lilikuwa katika vitabu vya kukunjwa katika masinagogi yao, nalo liliandikwa kwa herufi za Kiebrania katika tafsiri ya Biblia ya Septuagint ya Kigiriki ambayo waliisoma na kuitumia. (Ona makala inayosema “Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kikristo,” ukurasa wa 8.) Yehova si jina jingine la Yesu. Wakati Yesu alipomwita “Mungu Baba yake mwenyewe” na kujiita mwenyewe “Mwana wa Mungu,” Wayahudi wenye kumsikia wangeelewa kwamba alikuwa akisema yeye ni Mwana wa yule ambaye jina lake liliandikwa kwa zile herufi nne za Kiebrania YHWH. Yeye hakuwa akisema kwamba ndiye Yehova, bali kwamba ndiye Mwana wa Yehova.—Yohana 5:18; 11:4.

Lile Agano Jipya kwa Ajili ya Wakristo

17, 18. (a) Ni mambo gani makuu ambayo wewe unaona katika unabii wa Yeremia juu ya agano jipya, na unabii huo una maana kadiri gani? (b) Mpatanishi wa agano hilo alifanya nini?

17 Unabii mkuu wa Yeremia wa lile agano jipya unaonyesha kwamba si Wayahudi peke yao bali Wakristo pia wangekuwa watu kwa ajili ya jina la Yehova. Ikiwa watafsiri wa Biblia yako walitumia jina la Mungu inavyofaa katika mahali linapoonekana katika Kiebrania cha kwanza kabisa, wewe ungesoma hivi:

“ ‘Tazama! Kuna siku zinazokuja,’ ni tamko la Yehova, ‘na mimi nitamalizia pamoja na nyumba ya Israeli na pamoja na nyumba ya Yuda agano jipya . . . Kwa maana hili ndilo agano ambalo mimi nitamalizia pamoja na nyumba ya Israeli baada ya siku hizo,’ ndilo tamko la Yehova. ‘Mimi nitatia sheria yangu ndani yao, na katika moyo wao mimi nitaiandika. Na mimi nitakuwa Mungu wao, na wao wenyewe watakuwa watu wangu. Na wao hawatafundisha tena kila mmoja mwenzi wake na kila mmoja ndugu yake, wakisema, “Mjueni Yehova! ” kwa maana wote watanijua mimi, kutoka yule aliye mdogo zaidi ya wote hata yule aliye mkuu zaidi ya wote,’ ndilo tamko la Yehova.”—Yeremia 31:31-34, NW.

18 Paulo mtume Mkristo anatumia sura nne za kitabu cha Waebrania (sura 7-10) ili kuzungumza habari ya hilo agano jipya, ambalo Mungu alianzisha pamoja na Israeli wa kiroho. Paulo hatoi wazo la kwamba Kristo ndiye aliyekuwa mfanyizaji wa agano hilo (ambalo lilifanywa halali kupitia damu yake), bali anasema kwamba Kristo alikuwa “mpatanishi” walo. Mwenye kulifanyiza alikuwa ni Yehova Mungu. Juu ya mpatanishi walo, Paulo aliandika hivi: Kristo aliingia... ndani ya mbingu zenyewe, sasa atokee mbele za utu wa Mungu kwa ajili yetu.”—Waebrania 8:6; 9:15, 24, NW.

19. Unabii huo unasema ni nani angekuwa Mungu wa wale walio katika agano jipya la Kikristo?

19 Ni nani ambaye Yeremia anasema angekuwa Mungu wa Wakristo katika agano jipya? Yehova! Ni Yehova aliyesema hivi: “Mimi nitamalizia . . . Mimi nitatia . . . Mimi nitakuwa Mungu wao.” Na unabii huo unasema hivi juu ya Wakristo walio katika agano jipya: “Wote watanijua mimi, kutoka yule aliye mdogo zaidi ya wote hata yule aliye mkuu zaidi ya wote, ndilo tamko la Yehova.” Kwa hiyo wale wote walio kweli kweli katika agano jipya la Kikristo—na pia Wakristo wengine waaminifu wanaoshirikiana nao— wangekuwa ni watu wanaomjua Yehova na kumtumikia! Miaka zaidi ya 400 iliyopita, John Calvin aliandika hivi: “Maneno haya, ‘Jueni Yehova ninyi,’ yanaonyesha viasili vya kwanza vya imani.”—Commentaries on the Book of the Prophet Jeremiah and the Lamentations, kilichotayarishwa na John Calvin, kikatafsiriwa na John Owen, ukurasa wa 136.

Hali Iliyobadilika

20. Wenye kumsikia Yesu walihitaji kujua nini?

20 Katika siku za Yesu wenye kumsikia walimjua Mungu wa Abrahamu, wa Isaka na wa Yakobo. Babu zao wa kale walimwabudu Yehova, na walikuwa na hekalu la Yehova katikati yao. Walichohitaji kuona kilikuwa umaana wa kumheshimu Yesu na kumfuata. Hivyo Yesu alisema kwamba watu wote wanapaswa “wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba. Asiyemheshimu Mwana hamheshimu Baba aliyempeleka.”—Yohana 5:23.

21, 22. (a) Hali hiyo imebadilishwaje ikawa kinyume leo? (b) Ni jambo gani tusilopaswa kamwe kulisahau?

21 Leo hali yenyewe imebadilishwa ikawa kinyume. Washiriki wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wanasema mengi juu ya Mwana lakini wanamsahau “Baba aliyempeleka.” Mungu ndiye aliyemtukuza Yesu, na “alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Wafilipi 2:9-11.

22 Haitupasi kamwe kusahau uhakika huo kama vile wengine wameusahau—kwamba tunapomkiri Yesu tunapaswa kufanya hivyo “kwa utukufu wa Mungu Baba.” Wengi wa viongozi wa kidini wa leo, na basi hata makundi yao, wamemsahau Baba kabisa. Hata hivyo, katika sala aliyopelekea Baba yake wa kimbingu, Yesu alisema: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli mmoja tu.” Lakini hiyo haitoshi. Ni lazima pia tujifunze habari za yule aliyepelekwa na Mungu kisha tumfuate. Hivyo, Yesu aliendelea kusema, “Na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3, NW.—Kutoka w12/1/83.

Maulizo ya Kurudia Kujikumbusha

□ Ni maneno gani ya Kibiblia yanayoonyesha tofauti iliyopo kati ya Yesu na Mungu?

□ Je! maneno ya Yesu ya kwamba “Baba ni mkuu kuliko mimi” yangali na maana ile ile baada ya Yesu kurudi mbinguni?

□ Daudi na Danieli walisema nini yanayotusaidia tuelewe cheo alicho nacho Yesu katika mbingu?

□ Unabii wa Yeremia juu ya agano jipya unaonyesha kwamba Wakristo wa kweli wangejua nini juu ya Mungu?

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

“Mungu Mwana” Ni Wazo Lililotokea Baadaye

Kichapo New Catholic Encyclopedia, buku la 13, ukurasa wa 426, kinasema hivi: “Kuuliza kama A[gano] J[ipya] linaonyesha Yesu kuwa Mungu Mwana” ni ‘kumtafutia Yeye mtajo ambao ulitokezwa baadaye tu.’

Hivyo, Yesu na mitume wake walifundisha kwamba yeye alikuwa “Mwana wa Mungu,” lakini wanakanisa wa baadaye ndio walilitokeza wazo la “Mungu Mwana.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki