Mafunzo Juu ya Maandiko Yenye Pumzi ya Mungu na Habari ya Msingi Yayo
Maandiko Yenye Pumzi ya Mungu Huleta Mafaa za Milele
1. Pitio letu la “Andiko lote” limefumbua mbele ya macho yetu njozi gani tukufu?
PITIO letu la “kila andiko, lenye pumzi ya Mungu” limefumbua mbele ya macho yetu njozi tukufu ya enzi kuu ya Yehova na kusudi lake la Ufalme. Tumeona kwamba Biblia ndicho Kitabu kimoja, chenye habari moja kuu yenye nguvu—kuondolewa malawama kwa enzi kuu ya Yehova na hatimaye utimizo wa kusudi lake kwa ajili ya dunia kupitia Ufalme wake mikononi mwa Kristo, aliye Mbegu Iliyoahidiwa. Kuanzia kurasa za ufunguzi za Biblia, habari hiyo moja kuu imesitawishwa na kuelezwa katika maandishi yanayofuata, mpaka, katika sura zayo za kumalizia, uhalisi mtukufu wa kusudi tukufu la Mungu kupitia Ufalme wake unafanywa kuwa wazi. Jinsi Biblia ilivyo kitabu chenye kutokeza! Kuanzia na uumbaji wenye kutisha wa mbingu halisi na wa dunia pamoja na uhai wayo wa viumbe, Biblia hutupa simulizi pekee lililopuliziwa na Mungu na lenye uasilia la shughuli za Mungu pamoja na ainabinadamu mpaka wakati wetu na hutuingiza kwenye utimizo kamili wa uumbaji mtukufu wa Yehova wa “mbingu mpya na dunia mpya.” (Ufu. 21:1, NW) Kusudi lake tukufu likiwa limetimizwa kwa ukamili kupitia Ufalme wa Mbegu, Yehova Mungu aonekana katika uhusiano wa Baba mfadhili wa familia ya kibinadamu yenye furaha iliyounganika, ambayo yajiunga na majeshi yote ya kimbingu katika kumsifu na kutakasa jina lake takatifu.
2, 3. Habari kuu inayohusu Mbegu imesitawije kote kote katika Maandiko?
2 Jinsi habari hiyo inayohusu Mbegu inavyositawishwa kwa njia nzuri ajabu kote kote katika Maandiko! Akisema unabii wa kwanza uliopuliziwa na Mungu, Mungu anatoa ahadi ya kwamba ‘mbegu ya mwanamke’ itatia jeraha nyoka katika kichwa. (Mwa. 3:15, NW) Zaidi ya miaka 2,000 yapita, na Mungu amwambia Abrahamu mwaminifu hivi: “Kupitia mbegu yako mataifa yote ya dunia kwa yakini yatajibariki yenyewe.” Zaidi ya miaka 800 baadaye, Yehova atoa ahadi kama hiyo kwa mmoja wa wazao wa Abrahamu, Mfalme Daudi mwaminifu-mshikamanifu, akionyesha kwamba Mbegu huyo angekuwa wa kifalme. Kwa kadiri wakati upitavyo, manabii wa Yehova wajiunga kwa msisimuko katika kutabiri utukufu mbalimbali wa utawala wa Ufalme. (Mwa. 22:18, NW; 2 Sam. 7:12, 16; Isa. 9:6, 7; Dan. 2:44; 7:13, 14) Kisha Mbegu mwenyewe atokea, zaidi ya miaka 4,000 baada ya ahadi hiyo ya kwanza katika Edeni. Huyu, ambaye pia ni ‘mbegu ya Abrahamu,’ ni Yesu Kristo, “Mwana wa Aliye Juu Zaidi,” na kwake yeye Yehova humpa “kiti cha enzi cha Daudi baba yake.”—Gal. 3:16, NW; Luka 1:31-33, NW.
3 Ingawa Mbegu huyo, Mfalme mpakwa mafuta wa Mungu, anatiwa jeraha katika kifo na mbegu ya kidunia ya Nyoka, Mungu anamfufua kutoka wafu na kumkweza kwenye mkono Wake mwenyewe wa kulia, ambako anasubiri wakati wa Mungu ufike wa ‘kuponda kichwa cha nyoka.’ (Mwa. 3:15, NW; Ebr. 10:13; Rum. 16:20) Kisha Ufunuo waleta njozi yote kwenye upeo wayo mtukufu. Kristo aingia katika mamlaka ya Ufalme na kuvurumisha “nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani,” kutoka mbingu mpaka chini duniani. Kwa muda mfupi, Ibilisi aleta ole kwenye dunia na kufanya vita na ‘uzao [mbegu, NW] wa mwanamke uliosalia.’ Lakini Kristo, akiwa ‘Mfalme wa wafalme,’ awapiga mataifa dharuba ya upanga. Yule Nyoka wa awali, Shetani, atiwa ndani ya abiso kisha hatimaye ataharibiwa milele. Kwa upande mwingine, kupitia Yerusalemu Jipya, bibi-arusi wa Mwana-kondoo, mafaa za dhabihu ya Kristo zatumiwa kwa ainabinadamu kwa ajili ya baraka ya familia zote za dunia. Ndivyo, habari kuu iliyo nzuri ajabu ya Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu inavyokunjuliwa mbele yetu katika utukufu wayo wote wenye kusisimua!—Ufu. 11:15; 12:1-12, 17; 19:11-16; 20:1-3, 7-10; 21:1-5, 9; 22:3-5.
KUFAIDIKA NA MAANDISHI HAYO YENYE PUMZI YA MUNGU
4. Twaweza kupataje mafaa iliyo kubwa zaidi kutokana na Maandiko Matakatifu, na kwa nini?
4 Twawezaje kupata mafaa iliyo kubwa zaidi kutoka kwa Maandiko Matakatifu? Twaweza kufaidika kwa kuruhusu Biblia ifanye kazi maishani mwetu. Kwa funzo la kila siku na matumizi ya Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu, twaweza kupata uongozi kutoka kwa Mungu. “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu,” na laweza kuwa nguvu nzuri ajabu kwa ajili ya kutokeza uadilifu maishani mwetu. (Ebr. 4:12) Tukiendelea kujifunza na kufuata miongozo ya Neno la Mungu, tutakuja ‘kuvaa utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.’ Tutafanywa wapya katika kani inayotendesha akili zetu, nasi tutabadilishwa-umbo kwa kugeuza akili zetu, ili tujithibitishie wenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”—Efe. 4:23, 24; Rum. 12:2.
5. Twaweza kujifunza nini kutokana na mtazamo na kielelezo cha Musa?
5 Twaweza kujifunza mengi kwa kuona jinsi watumishi wengine waaminifu wa Mungu wamefaidika kwa kujifunza Neno la Mungu na kulitafakari. Kwa kielelezo, alikuwako Musa, aliyekuwa “mpole zaidi ya wanadamu wote,” ambaye sikuzote alikuwa mwenye kufundishika na mwenye nia ya kujifunza. (Hes. 12:3) Sikuzote twapaswa kuwa na uthamini uo huo wa sala juu ya enzi kuu ya Yehova kama yeye. Musa ndiye aliyesema: “Wewe, Bwana [Yehova, NW], umekuwa makao yetu, kizazi baada ya kizazi. Kabla haijazaliwa milima, wala hujaiumba dunia, na tangu milele hata milele ndiwe Mungu.” Musa aliijua kikamili hekima ya Mungu, kwa maana yeye alitumiwa na Yehova katika kuandika vitabu vya ufunguzi vya Biblia. Kwa hiyo, yeye alielewa umaana wa kutafuta kila siku hekima ya Mungu. Kwa hiyo, yeye alisali kwa Mungu hivi: “Utujulishe kuzihesabu siku zetu, tujipatie moyo wa hekima.” Kwa kuwa “siku za miaka yetu” zaweza kuwa fupi, miaka 70 tu, au 80 tuwapo wenye “nguvu,” sisi tu wenye hekima endapo tunakula karamu Neno lake kila siku, kwa maana ndipo “uzuri wa BWANA [Yehova, NW], Mungu wetu” ‘utatuthibitisha,’ kama ulivyothibitisha Musa mtumishi wake mwaminifu.—Zab. 90:1, 2, 10, 12, 17.
6. Sisi, kama vile Yoshua, twaweza kufanyaje njia yetu ifanikiwe?
6 Jinsi lilivyo jambo la lazima kutafakari kila siku juu ya Neno la Mungu! Yehova alionyesha hilo wazi kwa Yoshua, mwandamizi wake Musa, akimwambia hivi: “Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako. Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana [utatenda kwa hekima, NW].” Je! usomaji wa Yoshua wenye kuendelea wa Sheria ya Yehova ‘ulifanikisha njia yake’? Baraka ya Yehova juu ya shughuli yake yenye moyo mkuu katika Kanaani yatoa jibu.—Yos. 1:7, 8; 12:7-24.
7. Daudi alielezaje uthamini wake kwa ajili ya hekima kutoka kwa Mungu, na uthamini uo huo waelezwaje katika Zaburi 119?
7 Fikiria, pia, Daudi aliye mpendwa, ambaye ni mwingine aliyechukua kuwa hazina kubwa hekima kutoka kwa Yehova. Jinsi alivyoonyesha uthamini wa kutoka moyoni kwa ajili ya “sheria,” “kikumbusho,” “maagizo,” “amri,” na “maamuzi ya kihukumu” ya Yehova! Ni kama Daudi alivyosema hilo: “Hayo ni ya kutamanika zaidi ya dhahabu, ndiyo, zaidi ya dhahabu iliyosafishwa sana; na matamu zaidi ya asali na asali yenye kutiririka ya masega.” (Zab. 19:7-10, NW) Habari hiyo ya kutukuza inapanuliwa na kurudiwa na mtunga zaburi mwingine kwa uzuri wenye kuchochea nafsi katika Zaburi yote ya 119. Tunapojifunza kila siku Neno la Mungu na kuishi kulingana na shauri lalo lenye hekima, daima na tuweze kusema hivi kwa Yehova: “Neno lako ni taa kwa mguu wangu, na nuru kwa njia ya barabara yangu. Vikumbusho vyako ni vya ajabu. Ndiyo sababu nafsi yangu imevishika.”—Zab. 119:105, 129, NW.
8. Ni semi gani za Sulemani tunazopaswa kufanya ziwe zetu wenyewe?
8 Katika siku za uaminifu wake, Sulemani mwana wa Daudi aliishi kulingana na Neno la Mungu, na katika semi zake pia, twaweza kupata maneno yenye kugusa moyo yenye uthamini ambayo twafanya vema kuyafuata. Kupitia usomaji wa kila siku na matumizi ya Biblia, tutakuja kuelewa kikamili kina cha ndani cha maana ya maneno haya ya Sulemani: “Heri [ni mwenye furaha, NW] mtu yule aonaye hekima, na mtu yule apataye ufahamu. Ana wingi wa siku katika mkono wake wa kuume, utajiri na heshima katika mkono wake wa kushoto. Njia zake ni njia za kupendeza sana, na mapito yake yote ni amani. Yeye ni mti wa uzima kwao wamshikao sana; ana heri [furaha, NW] kila mtu ashikamanaye naye.” (Mit. 3:13, 16-18) Funzo la kila siku na utii kwa Neno la Mungu huongoza kwenye furaha iliyo kubwa zaidi sasa, pamoja na uhakikisho wa “wingi wa siku”—uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Yehova.
9. Ni kitia moyo gani tunachoweza kupata kutokana na kielelezo cha Yeremia?
9 Wasio wa kusahauliwa miongoni mwa wale ambao wamethamini na kutii Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu ni manabii waaminifu wa Mungu. Kwa kielelezo, Yeremia alikuwa na mgawo mgumu sana. (Yer. 6:28) Ni kama alivyosema: “Neno la BWANA [Yehova, NW] limefanywa shutumu kwangu, na dhihaka, mchana kutwa.” Lakini yeye alikuwa ameimarishwa sana na mafunzo yake ya Neno la Mungu, na kwa kweli, yeye mwenyewe alitumiwa kuandika vitabu vinne vya Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu—Wafalme wa Kwanza na wa Pili, Yeremia, na Maombolezo. Kwa hiyo, ni nini kilichotukia wakati kuvunjika moyo kulielekea kumlemea Yeremia na akafikiri ataacha kuhubiri ‘neno la Yehova’? Acha Yeremia mwenyewe ajibu: “Moyoni mwangu kumekuwamo kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami nimechoka kwa kustahimili, wala siwezi kujizuia.” Yeye alilazimika kunena maneno ya Yehova, na katika kufanya hivyo, alikuta kwamba Yehova alikuwa pamoja naye “mfano wa shujaa mwenye kutisha.” Tukijifunza na kufuliza kujifunza Neno la Mungu, hata liwe sehemu yetu kabisa kama lilivyokuwa kwa Yeremia, ndipo uwezo wa Yehova usioshindika utakapokuwa nasi vivyo hivyo, nasi tutaweza kushinda kila kipingamizi katika kuendelea kunena juu ya kusudi Lake tukufu la Ufalme.—Yer. 20:8, 9, 11.
10. Maandiko yalitimiza fungu gani katika uhai wa Yesu, naye alisali nini kwa niaba ya wanafunzi wake?
10 Sasa, vipi juu ya kielelezo chetu kikubwa zaidi, “Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu”? Je! yeye alizoeleana na Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu kama vile manabii wote na wanaume wengine waaminifu waliomtangulia? Ni yakini ndivyo, kwa kuwa manukuu yake mengi na mwendo wake wa maisha wa kupatana na Maandiko huonyesha hivyo waziwazi. Ni kwa kuwa na Neno la Mungu akilini kwamba akajitoa mwenyewe kufanya mapenzi ya Baba yake hapa duniani: “Tazama, nimekuja (katika gombo la chuo nimeandikiwa) niyafanye mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; naam, sheria yako imo moyoni mwangu.” (Ebr. 12:2, NW; Zab. 40:7, 8; Ebr. 10:5-7) Kwa hiyo, Neno la Mungu lilitimiza fungu kubwa katika Yehova kutakasa Yesu, au kumweka kando kwa ajili ya utumishi wake. Yesu alisali kwamba wafuasi wake waweze kutakaswa vivyo hivyo: “Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli. Kama vile ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami vivyo hivyo naliwatuma hao ulimwenguni. Na kwa ajili yao najiweka wakfu mwenyewe, ili na hao watakaswe katika kweli.”—Yn. 17:17-19.
11. (a)Petro alikazia nini kwa Wakristo wapakwa mafuta kuhusu Neno la Mungu? (b) Ni kwa nini funzo la Biblia ni lenye maana pia kwa mkutano mkubwa?
11 Wakiwa wametakaswa “kwa ile kweli,” wafuasi wa nyayo za Yesu waliozaliwa kwa roho na kupakwa mafuta lazima ‘wakae katika kweli yake’ kusudi wawe wanafunzi wake kweli kweli. (Yn. 8:31) Kwa hiyo, Petro, akiandikia “wale waliopata imani moja,” alikazia uhitaji wa funzo lenye kuendelea na kutoa uangalifu kwa Neno la Mungu: “Kwa hiyo nitakuwa tayari kuwakumbusha hayo sikuzote, ijapokuwa mnayajua na kuthibitishwa katika kweli mliyo nayo.” (2 Pet. 1:1, 12) Vikumbusho vyenye kuendelea, kama vile vinavyopatikana katika usomaji wa kila siku na funzo la Neno la Mungu, ni vyenye maana pia kwa wote wanaotumaini kuwa wa “mkutano mkubwa” ambao Yohana aliona katika njozi baada ya kueleza juu ya wale 144,000 waliotiwa muhuri wa makabila ya Israeli wa kiroho. Kwa maana wasipofuliza kutwaa maji ya ukweli ya uhai, huo mkutano mkubwa waweza kuendeleaje kwa akili ‘kulia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo’?—Ufu. 7:9, 10; 22:17.
12. Ni kwa nini twapaswa kutafakari daima juu ya Neno la Mungu?
12 Hatuwezi kuepa! Njia ya kupata mafaa kubwa zaidi kutokana na Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu, njia ya kupata wokovu wa kuingia kwenye uhai wa milele, ni kujifunza Maandiko hayo na kuishi kupatana nayo kila siku ya maisha zetu. Ni lazima daima tutafakari juu ya Neno la Mungu, tukiwa na mtazamo ule ule wa sala wenye uthamini kama unavyosemwa na mtunga zaburi: “Nitayakumbuka matendo ya BWANA [Yehova, NW]; naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote.” (Zab. 77:11, 12) Kutafakari juu ya ‘maajabu na kazi’ ya Yehova kutatuchochea sisi pia kuwa watendaji katika matendo mema, tukiwa tunatazamia uhai wa milele. Kusudi la kitabu hiki, “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa,” ni kutia moyo kila mmoja anayependa uadilifu ashiriki katika mafaa za milele na zenye kuridhisha zinazotokana na funzo na matumizi yenye kuendelea ya Neno la Mungu.
KATIKA “NYAKATI ZA HATARI”
13. Tunaishi katika ‘nyakati zipi za hatari’?
13 Kizazi hiki cha ki-siku-hizi ndio wakati wenye hatari zaidi katika historia ya kibinadamu. Kimejawa na uwezekano mbalimbali wenye kutisha. Hakika, yaweza kusemwa kikweli kwamba kuendelea kuwa hai kwenyewe kwa jamii ya kibinadamu ku hatarini. Basi, yafaa sana maneno ya mtume Paulo: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.”—2 Tim. 3:1-5.
14. Kwa sababu ya nyakati hizi, ni shauri gani la Paulo tunalopaswa kutii?
14 Kwa nini ujiepushe na hao? Kwa sababu njia yao ya kumkana Mungu karibuni itamalizikia katika uharibifu! Badala yake, sisi pamoja na wenye mioyo ya ufuatiaji-haki, tugeukie fundisho lenye afya la Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu, tukiyafanya Maandiko hayo kuwa msingi wenyewe wa maisha yetu ya kila siku. Na tutii maneno ya Paulo kwa kijana Timotheo: “Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishiwa.” (2 Tim. 3:14) Ndiyo, ‘kaa’ katika hayo, asema Paulo. Katika kufanya hivyo, ni lazima turuhusu kwa unyenyekevu Maandiko yatufundishe, yatukaripie, yanyooshe mambo kwa ajili yetu, na kututia nidhamu katika uadilifu. Yehova ajua tunayohitaji, kwa maana mawazo yake yako juu zaidi ya mawazo yetu. Kupitia Maandiko yake yaliyopuliziwa na Mungu, yeye hutuambia yaliyo na mafaa kwetu ili tuwe tayari kabisa na wenye uwezo wa kutosha kwa ajili ya kazi njema ya kutoa ushahidi kwa jina lake na Ufalme. Paulo atoa waidha hili lenye kutokeza katika muktadha wa kueleza juu ya “nyakati za hatari” zijazo “siku za mwisho”: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.” Sisi sote na tuokoke hizi nyakati zenye hatari kwa kutii ushauri huo uliopuliziwa na Mungu!—2 Tim. 3:16, 17; Isa. 55:8-11.
15. (a)Ni nini limekuwa tokeo la kutokutii? (b) Ni nafasi gani tukufu imefunguliwa na utii wa Kristo?
15 Utii kwa Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu wapasa kuwa mradi wetu. Ilikuwa kupitia kutokutii neno na amri ya Yehova kwamba mwanadamu wa kwanza aliangukia dhambi na kifo, “na hivyo mauti ikawafikia watu wote.” Kwa hiyo mwanadamu alipoteza nafasi ambayo ingaliweza kuwa yake katika Paradiso ya Kiedeni ya ‘kutwaa matunda ya mti wa uzima, ale, aishi milele.’ (Rum. 5:12; Mwa. 2:17; 3:6, 22-24) Lakini ni kupitia utii wa Kristo na kwa msingi wa dhabihu ya “Mwana-kondoo wa Mungu” kwamba Yehova atasababisha “mto wa maji ya uzima, wenye kung’aa kama bilauri,” utiririke kwa mafaa ya wale wote kati ya ainabinadamu wanaojiweka wakfu Kwake katika utii. Ni kama mtume Yohana alivyouona katika njozi: “Na upande huu na upande huu wa ule mto, ulikuwapo mti wa uzima, uzaao matunda, aina kumi na mbili, wenye kutoa matunda yake kila mwezi; na majani ya mti huo ni ya kuwaponya mataifa.”—Yn. 1:29; Ufu. 22:1, 2; Rum. 5:18, 19.
16. Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu ni yenye mafaa gani ya milele?
16 Kwa mara nyingine njia ya kwenda kwenye uhai wa milele iko wazi kwa ainabinadamu. Basi, wenye furaha ni wale wanaotii andiko hili lililopuliziwa na Mungu: “Basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako; kumpenda BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uzima wako, na wingi wa siku zako.” (Kum. 30:19, 20) Mbarikiwa ni Yehova, Mungu na Baba ya Bwana yetu Yesu Kristo, anayefanya mpango huu mtukufu wa uhai kupitia dhabihu ya Mwana wake na kupitia Ufalme wake wa milele. Jinsi tulivyo na shangwe na shukrani kubwa kwamba twaweza kusoma na kusoma tena, kujifunza na kujifunza tena, na kutafakari juu ya kweli hizo zenye thamani, kwa maana kweli kweli “kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa,” likiongoza kwenye uhai ama katika mbingu au juu ya dunia-paradiso. (Yn. 17:3; Efe. 1:9-11) Ndipo kila jambo litakuwa ni ‘utakatifu kwa Yehova.’—Zek. 14:20; Ufu. 4:8.