Sura 38
Je! Yohana Alikosa Imani?
YOHANA Mbatizaji, ambaye amekuwa gerezani kwa karibu mwaka mmoja sasa, apokea ripoti juu ya ufufuo wa mwana wa mjane kwenye mji wa Naini. Lakini Yohana anataka kusikia moja kwa moja kutoka kwa Yesu juu ya umaana wa jambo hilo, kwa hiyo anatuma wawili wa wafuasi wake wakaulize: “Wewe ndiwe Yule ajaye, au tumtazamie mwingine?”
Huenda hilo likaelekea kuwa swali la kushangaza, hasa kwa kuwa Yohana aliona roho ya Mungu ikishuka juu ya Yesu na akasikia sauti ya Mungu ya kibali alipokuwa akibatiza Yesu karibu miaka miwili kabla ya hapo. Huenda swali la Yohana likafanya wengine wakate shauri kwamba imani yake imedhoofika. Lakini hivyo sivyo ilivyo. Yesu hangesifu sana Yohana, kama anavyofanya katika pindi hii, kama Yohana ameanza kutia shaka. Basi, mbona Yohana anauliza swali hilo?
Huenda ikawa Yohana anataka ahakikishiwe tu na Yesu kwamba Yeye ndiye Mesiya. Jambo hilo lingemtia nguvu sana Yohana anaponyong’onyea gerezani. Lakini inaonekana kuna zaidi yanayohusika katika swali la Yohana. Ni wazi yeye ataka kujua kama kuna mwingine atakayekuja, akiwa kana kwamba ni mwandamizi, atakayekamilisha utimizo wa mambo yote yaliyotabiriwa kufanywa na Mesiya.
Kulingana na mambo ya unabiii wa Biblia ambayo Yohana amezoelea, Mpakwa-mafuta wa Mungu atakuwa mfalme, mkombozi. Na bado, Yohana angali amefungwa gerezani, hata miezi mingi baada ya ubatizo wa Yesu. Kwa hiyo ni wazi Yohana anauliza Yesu: ‘Je! kwa kweli wewe ndiwe utakayesimamisha Ufalme wa Mungu katika mamlaka yenye kuonekana, au kuna mwingine tofauti, mwandamizi, ambaye sisi tunapaswa kumngojea atimize mambo yote mazuri ajabu ya unabii yanayohusiana na utukufu wa Mesiya?’
Badala ya kuambia wafuasi wa Yohana, ‘Bila shaka mimi ndiye yule aliyepaswa kuja!’ Yesu aonyesha katika saa iyo hiyo wonyesho wa kustaajabisha kwa kuponya watu wengi magonjwa na maradhi ya aina zote. Halafu aambia wafuasi hao: “Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia; vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakasika, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, maskini wanahubiriwa habari njema.”
Kwa maneno mengine, swali la Yohana huenda likatoa wazo la tazamio la kwamba Yesu atafanya mengi zaidi ya anayofanya, na pengine atamweka huru Yohana mwenyewe. Hata hivyo, Yesu anaambia Yohana asitazamie mengi zaidi ya miujiza ambayo Yesu anafanya.
Wakati wafuasi wa Yohana wanapoondoka, Yesu anageukia umati na kuwaambia kwamba Yohana ndiye “mjumbe” wa Yehova aliyetabiriwa katika Malaki 3:1 na pia ndiye nabii Eliya aliyetabiriwa katika Malaki 4:5, 6. Hivyo yeye anatukuza Yohana kuwa alingana na nabii yeyote aliyeishi kabla yake, akieleza hivi: “Amin, nawaambieni, Hajaondokea mtu katika wazao wa wanawake aliye mkuu kuliko Yohana Mbatizaji; walakini aliye mdogo katika ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye. Tangu siku za Yohana mbatizaji hata sasa ufalme wa mbinguni hupatikana kwa nguvu [ndio mradi ambao kuuelekea watu hukazana, NW].”
Hapa Yesu anaonyesha kwamba Yohana hatakuwa katika Ufalme wa kimbingu, kwa kuwa aliye mdogo huko ni mkubwa kuliko Yohana. Yohana alitayarishia Yesu njia, lakini anakufa kabla Kristo hajatia muhuri lile agano au mapatano, pamoja na wafuasi wake, ili wao wawe watawala wenzake katika Ufalme wake. Hiyo ndiyo sababu Yesu asema kwamba Yohana hatakuwa katika Ufalme wa kimbingu. Badala ya hiyo Yohana atakuwa raia wa kidunia wa Ufalme wa Mungu. Luka 7:18-30; Mathayo 11:2-15.
▪ Kwa nini Yohana auliza kama Yesu ndiye Yule Ajaye au kama mtu mwingine tofauti apaswa kutazamiwa?
▪ Ni unabii gani ambao Yesu anasema kuwa Yohana alitimiza?
▪ Kwa nini Yohana Mbatizaji hatakuwa mbinguni pamoja na Yesu?