Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ijwbq makala 178
  • Yohana Mbatizaji Alikuwa Nani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yohana Mbatizaji Alikuwa Nani?
  • Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jibu la Biblia
  • Kwa nini Yohana Mbatizaji alikuwa mtu wa pekee?
  • Wazazi wa Yohana Mbatizaji walikuwa nani?
  • Ni nani aliyesababisha kifo cha Yohana Mbatizaji?
  • Je, Yohana Mbatizaji na Yesu walikuwa washindani?
  • Yohana Anataka Kusikia Kutoka kwa Yesu
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Je! Yohana Alikuwa na Ukosefu wa Imani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Je! Yohana Alikosa Imani?
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Je, Yohana Mbatizaji Alikuwa Mtu Halisi?
    Habari Zaidi
Pata Habari Zaidi
Maswali ya Biblia Yajibiwa
ijwbq makala 178
Yohana Mbatizaji akibatiza mwanamume mtoni.

Yohana Mbatizaji Alikuwa Nani?

Jibu la Biblia

Yohana Mbatizaji alikuwa nabii wa Mungu. (Luka 1:76) Alizaliwa muda mfupi tu kabla ya mwisho wa karne ya kwanza K.W.K. na aliishi katika karne ya kwanza W.K. Mungu alimtuma ili atayarishe njia kwa ajili ya Masihi, au Kristo. Yohana alifungua njia kwa kuwahubiria Wayahudi wengine ujumbe unaotoka kwa Mungu ili kurudisha mioyo yao kwa Mungu.—Marko 1:1-4; Luka 1:13, 16, 17.

Ujumbe wa Yohana ungewasaidia wasikilizaji wanyoofu kumtambua Masihi aliyeahidiwa ambaye ni Yesu wa Nazareti. (Mathayo 11:10) Yohana aliwasihi wasikilizaji wake watubu dhambi zao na kubatizwa ili kuonyesha kwamba wametubu. (Luka 3:3-6) Kwa sababu aliwabatiza watu wengi, Yohana anaitwa Mbatizaji. Ubatizo muhimu zaidi ambao alifanya ni ule wa Yesu.a—Marko 1:9.

Katika makala hii

  • Kwa nini Yohana Mbatizaji alikuwa mtu wa pekee?

  • Wazazi wa Yohana Mbatizaji walikuwa nani?

  • Ni nani aliyesababisha kifo cha Yohana Mbatizaji?

  • Je, Yohana Mbatizaji na Yesu walikuwa washindani?

  • Kuna wanaume wangapi walioitwa Yohana katika Biblia?

Kwa nini Yohana Mbatizaji alikuwa mtu wa pekee?

Jukumu lake lilitabiriwa mapema: Kupitia kazi yake ya kuhubiri, Yohana alitimiza unabii kumhusu mjumbe wa Yehova. (Malaki 3:1; Mathayo 3:1-3) Alithibitisha kwamba yeye ndiye yule ambaye angekuja “kumwandalia Yehova watu waliotayarishwa”—yaani, alitayarisha njia ili Wayahudi wengine wakubali ujumbe wa mwakilishi mkuu wa Yehova, Yesu Kristo.—Luka 1:17.

Alichotimiza: Yesu alisema kwamba “hajatokea mtu mkuu kuliko Yohana Mbatizaji, lakini mtu mdogo zaidi katika Ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye.” (Mathayo 11:11) Kwa sababu Yohana hakuwa tu nabii bali alikuwa “mjumbe” aliyetabiriwa, hakuna mtumishi wa Mungu aliyekuja kabla yake aliyekuwa mkuu zaidi yake. Maneno ya Yesu yalionyesha pia kwamba Yohana hatakuwa sehemu ya Ufalme wa mbinguni.b Nabii huyu mwaminifu alikufa kabla Yesu hajafungua njia ya kuingia mbinguni. (Waebrania 10:19, 20) Hata hivyo, Yohana atakuwa raia wa Ufalme wa Mungu duniani, akiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso.—Zaburi 37:29; Luka 23:43.

Wazazi wa Yohana Mbatizaji walikuwa nani?

Wazazi wa Yohana walikuwa Zekaria na Elisabeti. Zekaria alikuwa kuhani Myahudi. Yohana alizaliwa kimuujiza kwa sababu mama yake alikuwa tasa, yaani, hakuwa na uwezo wa kuzaa watoto. Mbali na hilo, wazazi wake “walikuwa wamezeeka.”—Luka 1:5-7, 13.

Ni nani aliyesababisha kifo cha Yohana Mbatizaji?

Mfalme Herode Antipa alimkata Yohana kichwa. Alifanya hivyo kwa sababu alichochewa na mke wake, Herodia. Herodia alimchukia Yohana kwa sababu Yohana alikuwa amemwambia Herode, ambaye alidai kuwa Myahudi kwamba ndoa ya Herode na Herodia ilikuwa kinyume na sheria ya Wayahudi.—Mathayo 14:1-12; Marko 6:16-19.

Je, Yohana Mbatizaji na Yesu walikuwa washindani?

Wazo la kwamba walikuwa washindani halipatikani popote katika Biblia. (Yohana 3:25-30) Na hata Yohana alisema kwamba jukumu lake ni kutayarisha njia kwa ajili ya Masihi na si kushindana naye. Yohana alisema: “Nilikuja kubatiza katika maji ili afunuliwe kwa Israeli.” Kisha akaongezea hivi: “Huyo ndiye Mwana wa Mungu.” (Yohana 1:26-34) Basi, Yohana alifurahi sana kusikia huduma aliyofanya Yesu ikisonga mbele.

a Yesu “hakufanya dhambi.” (1 Petro 2:21, 22) Hivyo basi, hakubatizwa kwa sababu alipaswa kutubu bali kwa sababu alikuwa anajitoa ili kufanya mapenzi ya Mungu. Na hilo lilitia ndani kutoa uhai wake kwa ajili yetu.—Waebrania 10:7-10.

b Ona makala yenye kichwa “Ni Nani Wanaoenda Mbinguni?”

Kuna wanaume wangapi walioitwa Yohana katika Biblia?

Biblia inataja wanaume watano walioitwa Yohana.

  1. 1. Yohana Mbatizaji, mwana wa Zekaria na Elisabeti.—Marko 1:4; Luka 1:57-60.

  2. 2. Yohana baba ya mtume Petro.—Yohana 1:42.

  3. 3. Mtume Yohana, ‘mwana wa Zebedayo.’ (Mathayo 10:2) Mtume huyo aliandika Injili ya Yohana; barua ya Kwanza, ya Pili, na ya Tatu ya Yohana; na kitabu cha ufunuo.

  4. 4. Yohana, ambaye pia aliitwa Marko, aliyeandika Injili ya Marko.—Matendo 12:12.

  5. 5. Mtawala Myahudi, ambaye huenda alikuwa mtu wa ukoo wa kuhani mkuu Anasi.—Matendo 4:6.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki