Sura 58
Ile Mikate na Ile Chachu
UMATI mkubwa umemiminika ukamjia Yesu katika Dekapoli. Wengi wamekuja umbali mkubwa kwenye jimbo hilo ambalo sana-sana linakaliwa na Mataifa ili wamsikilize na kuponywa udhaifu wao. Wao wameleta vikapu vikubwa, au makanda, ambavyo kwa desturi wao wanatumia kuchukulia vyakula vya kutumia wakati wanaposafiri kupitia maeneo ya Mataifa.
Hata hivyo, hatimaye, Yesu anaita wanafunzi wake na kusema: “Mimi nahisi sikitiko kwa ule umati, kwa sababu tayari ni siku tatu ambazo wao wamebaki karibu nami nao hawana kitu cha kula; nami nikiwaambia waende zao kwenye makao yao wakiwa wanafunga, wao wataishiwa nguvu wakiwa barabarani. Kweli kweli, baadhi yao wametoka mbali sana.”
“Ni kutoka wapi mtu yeyote ataweza katika mahali hapa palipo peke yapo kutosheleza watu hawa kwa mikate?” wanafunzi wanauliza.
Yesu anauliza: “Ni mikate mingapi mliyo nayo nyinyi?”
“Saba,” wanajibu, “na samaki wadogo wachache.”
Akiwaagiza watu wakae chini, Yesu anachukua mikate na samaki wale, anatoa sala kwa Mungu, anaimega, na kuanza kuwapa wanafunzi wake. Wao, nao, wanawapa watu wale, nao wote wanakula mpaka wanashiba. Baada ya hapo, wakati masazo yanapookotwa, kuna vikapu saba vya kuchukulia maandalizi ambavyo vimejaa, hata ingawa wanaume karibu 4,000, na pia wanawake na watoto, wamekula!
Yesu anaruhusu umati huo uende zao, aingia ndani ya mashua pamoja na wanafunzi wake, na kuvuka kwenda kwenye ufuo wa magharibi wa Bahari ya Galilaya. Hapa Mafarisayo, wakati huu wakiwa wameandamana na washiriki wa lile farakano la Masadukayo, wanajaribu kushawishi Yesu kwa kumuuliza aonyeshe ishara kutoka mbinguni.
Akijua jitihada zao za kumshawishi, Yesu anajibu: “Wakati jioni inapoingia nyinyi mna desturi ya kusema, ‘Itakuwa hali ya hewa iliyo nzuri kiasi, kwa maana anga lina wekundu-moto’; na asubuhi, ‘Itakuwa hali ya hewa iliyo ya kipupwe na mvua-mvua leo, kwa maana anga lina wekundu-moto, lakini lenye kuonekana la utusi-tusi.’ Nyinyi mwajua kufasiri sura ya anga, lakini zile ishara za nyakati nyinyi hamwezi kufasiri.”
Kufuata hilo, Yesu anawaita wao kuwa kizazi kiovu na kizinifu na kuwaonya kwamba, kama vile alivyokuwa ametangulia kuambia Mafarisayo, hakuna ishara watakayopewa isipokuwa ile ishara ya Yona. Akiondoka, yeye na wanafunzi wake wanaingia katika mashua na kuelekea Bethsaida katika ufuo wa kaskazini-mashariki mwa Bahari ya Galilaya. Wakiwa njiani wanafunzi wanagundua kwamba wamesahau kuleta mikate, kwa kuwa miongoni mwao mna mkate mmoja tu.
Akifikiria akilini mkabiliano wake wa karibuni pamoja na Mafarisayo na Masadukayo wenye kuunga mkono Herode, Yesu anaonya kwa upole hivi: “Endeleeni kuweka macho yenu yakiwa yamefunguka, jihadharini na ile chachu ya Mafarisayo na ile chachu ya Herode.” Kwa wazi ule mtajo wa chachu wafanya wanafunzi wafikiri kwamba Yesu anarejeza kwenye lile jambo la kusahau kwao kuleta mikate, hivyo wanaanza kuhojiana juu ya jambo hilo. Kwa kuona kutoelewa kwao, Yesu anasema: “Kwa sababu gani nyinyi mnahojiana juu ya kutokuwa na mikate?”
Hivi majuzi, Yesu alikuwa ameandaa kimuujiza mikate kwa ajili ya maelfu ya watu, akifanya muujiza huo wa mwisho labda siku moja au mbili tu kabla ya hapo. Inawapasa kujua kwamba yeye hahangaikii ukosefu wa mikate halisi. “Je! nyinyi hamkumbuki,” yeye anawakumbusha, “wakati mimi nilipoimega ile mikate mitano kwa ajili ya wale wanaume elfu tano, ni vikapu vingapi vyenye kujaa vipande-vipande ambavyo nyinyi mlichukua?”
“Kumi na viwili,” wanajibu.
“Wakati mimi nilipomega ile saba kwa ajili ya wale wanaume elfu nne, ni vikapu vingapi vya kuchukulia maandalizi vyenye kujaa vipande-vipande mlichukua?”
“Saba,” wanajibu.
“Je! bado nyinyi hamwipati maana?” Yesu anauliza. “Inakuwaje nyinyi hamng’amui kwamba mimi sikusema nanyi juu ya mikate? Bali jihadharini na ile chachu ya Mafarisayo na Masadukayo.”
Mwishowe wanafunzi wanaipata maana. Chachu, kitu ambacho kinasababisha uchachishaji na kufanya mkate uumuke, lilikuwa neno ambalo lilitumiwa kuonyesha ufisadi. Kwa hiyo sasa wanafunzi wanafahamu kwamba Yesu anatumia neno la ufananisho, kwamba yeye anawaonya wawe macho dhidi ya “lile fundisho la Mafarisayo na Masadukayo,” fundisho ambalo lina matokeo yenye kufisidi. Marko 8:1-21; Mathayo 15:32–16:12, NW.
▪ Kwa nini watu wanatembea wakiwa na vikapu vikubwa vya maandalizi?
▪ Baada ya kuondoka Dekapoli, ni safari gani za mashua anazofunga Yesu?
▪ Ni uelewevu gani wenye kosa walio nao wanafunzi juu ya elezo la Yesu kuhusu chachu?
▪ Yesu anamaanisha nini kwa kusema “ile chachu ya Mafarisayo na Masadukayo”?