Sura 60
Mtazamo-kimbele wa Utukufu wa Ufalme wa Kristo
YESU amekuja katika sehemu za Kaisaria Filipi, naye anafundisha umati wa watu unaotia ndani mitume wake. Yeye anafanya tangazo hili la kuwagutusha: “Kwa kweli mimi nasema kwenu nyinyi kwamba pana baadhi ya wale ambao wanasimama hapa ambao hawataonja kifo hata kidogo mpaka kwanza wao waone yule Mwana wa binadamu akija katika Ufalme wake.”
‘Yesu angeweza kuwa anamaanisha nini?’ lazima wanafunzi wawe wanashangaa wakitaka kujua. Karibu juma moja baadaye, Yesu anachukua Petro, Yakobo, na Yohana pamoja naye, nao wanapanda mlima mrefu sana. Inawezekana kuwa ni wakati wa usiku, kwa kuwa wale wanafunzi ni wenye usingizi. Wakati Yesu anaposali, yeye anageuka sura mbele yao. Uso wake unaanza kung’aa kama jua, na mavazi yake yanakuwa maangavu kama nuru.
Ndipo, maumbo mawili, yanayotambulishwa kuwa “Musa na Eliya,” yanatokea na kuanza kuambia Yesu juu ya ‘mwondoko wake ambao utatukia kule Yerusalemu.’ Mwondoko huo kwa wazi unamaanisha kifo cha Yesu na ufufuo utakaofuata baada ya hapo. Hivyo, maongezi hayo yanathibitisha kwamba kifo chake chenye kutweza si jambo la kuepukwa, kama vile Petro alivyokuwa ametamani.
Sasa wakiwa wameamka kabisa, wale wanafunzi wanatazama na kusikiliza kwa mshangao mkubwa. Ingawa hii ni njozi, inaonekana kuwa halisi sana hivi kwamba Petro anaanza kushiriki katika ile tamasha, akisema: “Bwana, ni vizuri kwetu kuwa hapa. Ikiwa wewe unataka, mimi nitasimamisha mahema matatu hapa, moja kwa ajili yako wewe na moja kwa ajili ya Musa na moja kwa ajili ya Eliya.”
Wakati Petro anapokuwa akisema bado, wingu jangavu linawafunika, na sauti kutoka lile wingu inasema: “Huyu ni Mwana wangu, yule mpendwa, ambaye mimi nimekubali; sikilizeni yeye.” Kwa kusikia ile sauti, wale wanafunzi waanguka kifudifudi. Lakini Yesu anasema: “Inukeni na msiwe na hofu.” Wakati wao wanapofanya hivyo, wao hawaoni mtu isipokuwa Yesu.
Wakiwa njiani kuteremka mlima siku inayofuata, Yesu anaamuru: “Msiambie mmoja yeyote ile njozi mpaka Mwana wa binadamu ainuliwe juu kutoka kwa wafu.” Kuonekana kwa Eliya katika ile njozi kunatokeza swali katika akili za wanafunzi. “Kwa sababu gani,” wanauliza, “waandishi wasema kwamba Eliya lazima aje kwanza?”
“Eliya tayari amekwisha kuja,” Yesu asema, “nao hawakumtambua yeye.” Hata hivyo, Yesu anasema juu ya Yohana yule Mbatizaji, ambaye alitimiza fungu la kazi linalofanana na la Eliya. Yohana alitayarishia Kristo njia, kama vile Eliya alivyofanya kwa Elisha.
Njozi hiyo inathibitika kuwa yenye kutia nguvu kama nini, kwa Yesu na wanafunzi pia! Ni kana kwamba ile njozi ni mtazamo-kimbele wa maono ya utukufu wa Ufalme wa Kristo. Ni kana kwamba wanafunzi waliona “yule Mwana wa binadamu akija katika ufalme wake,” sawasawa na vile Yesu alikuwa ameahidi juma moja mapema. Baada ya kifo cha Yesu, Petro aliandika juu yao kuwa walikwisha ‘kuwa mashahidi wenye kujionea kwa macho utukufu wa adhama ya Kristo wakati wao walipokuwa pamoja naye katika ule mlima mtakatifu.’
Mafarisayo walikuwa wamedai kutoka kwa Yesu ishara ya kuthibitisha kwamba yeye alikuwa ndiye mmoja yule aliyeahidiwa katika Maandiko kuwa Mfalme mchaguliwa wa Mungu. Wao hawakupewa ishara yoyote kama hiyo. Kwa upande ule mwingine, wanafunzi wa Yesu wenye uhusiano wa ndani naye wanaruhusiwa kuona mgeuko-sura wa Yesu kama uhakikisho wa unabii wa Ufalme. Hivyo, baadaye Petro aliandika: “Kwa hiyo sisi tunalo neno la unabii lililohakikishwa zaidi.” Mathayo 16:13, 28–17:13; Marko 9:1-13; Luka 9:27-37; 2 Petro 1:16-19, NW.
▪ Kabla ya kuonja kifo, watu fulani wanaonaje Kristo akija katika Ufalme wake?
▪ Katika ile njozi, Musa na Eliya wanaongea na Yesu juu ya nini?
▪ Kwa nini njozi kama hiyo inawatia nguvu wanafunzi?