Sura 87
Andalia Wakati Ujao kwa Hekima Inayotumika
NDIPO tu Yesu amemaliza kueleza hadithi ya mwana mpotevu kwa umati unaotia ndani wanafunzi wake, wakusanya kodi wasiofuata haki na wengine wanaotambuliwa kuwa watenda dhambi, na waandishi na Mafarisayo. Sasa, akielekeza maneno yake kwa wanafunzi wake, anasimulia kielezi kimoja kuhusu mwanamume tajiri ambaye amepokea ripoti isiyofaa juu ya msimamizi, au wakili, wa nyumba yake.
Kulingana na Yesu, tajiri huyo anaita wakili wake na kumwambia kwamba atamwondoa kazini. “Nifanyeje? maana, bwana wangu ananiondolea uwakili.” Wakili huyo anashindwa la kufanya. “Kulima, siwezi; kuomba, naona haya. Najua nitakalotenda, ili nitakapotolewa katika uwakili, wanikaribishe nyumbani mwao.”
Ni nini mpango wa wakili? Yeye anaita wote walio na deni la bwana-mkubwa wake. “Wawiwani [una deni gani] na bwana wangu?” anauliza.
Yule wa kwanza anajibu, ‘Lita 2,200 za mafuta ya mzeituni.’
‘Twaa hadi ya makubaliano uketi na kuandika haraka 1,100,’ anamwambia.
Anauliza mwingine: ‘Na wewe, deni lako ni nini?’
Anasema, ‘Lita 22,000 za ngano.’
‘Twaa hati ya makubaliano na uandike 18,000.’
Wakili anapunguza pesa wanazodaiwa na bwana-mkubwa wake bila kuruka mipaka ya haki zake za kufanya hivyo, kwa kuwa yeye angali ndiye msimamizi wa mambo ya kifedha ya bwana-mkubwa wake. Kwa kupunguza kiasi hicho mbalimbali, anafanya urafiki pamoja na wale wanaoweza kumrudishia mema anapopoteza kazi yake.
Bwana-mkubwa anaposikia lililotukia, linamvutia. Kwa hakika, yeye “akasifu wakili dhalimu kwa vile alivyotenda kwa busara [hekima inayotumika, NW].” Kweli kweli, Yesu anaongeza hivi: “Wana wa ulimwengu huu [mfumo wa mambo, NW] katika kizazi chao wenyewe huwa na busara kuliko wana wa nuru.”
Sasa, Yesu akifundisha wanafunzi wake somo, anatia moyo hivi: “Jifanyieni rafiki kwa mali ya udhalimu, ili itakapokosekana wawakaribishe katika makao ya milele.”
Yesu hampongezi wakili kwa ukosefu wake wa uadilifu bali kwa uwezo wake wa kuona mbali, hekima inayotumika. Mara nyingi ‘wana wa huu mfumo wa mambo’ hutumia pesa au cheo chao kwa busara kufanya urafiki pamoja na wale wanaoweza kuwarudishia mema. Kwa hiyo watumishi wa Mungu, “wana wa nuru,” wanahitaji pia kutumia kwa hekima majaliwa yao ya kimwili, ‘mali yao ya udhalimu,’ ili kujinufaisha wenyewe.
Lakini kama asemavyo Yesu, inawapasa watumie mali hizo kufanya urafiki pamoja na wale ambao wangeweza kuwapokea “katika makao ya milele.” Kwa washiriki wa kundi dogo, makao hayo yako mbinguni; kwa “kondoo wengine,” yamo katika dunia Paradiso. Kwa kuwa Yehova Mungu na Mwana wake ndio tu wanaoweza kupokea watu katika makao hayo, inatupasa tuwe na bidii-nyendelevu kusitawisha urafiki pamoja nao kwa kutumia ‘mali yoyote ya udhalimu’ tuliyo nayo katika kutegemeza masilahi ya Ufalme. Ndipo, mali za kimiwili zikishindwa au kutoweka, kama zitakavyofanya hakika, wakati ujao wetu wa milele utakuwa na uhakikishio.
Yesu anaendelea kusema kwamba watu walio waaminifu katika kutunza hata vitu hivyo vya kimwili, au visivyo vya maana sana, watakuwa waaminifu pia katika kutunza mambo ya umaana mkubwa zaidi. “Basi,” yeye akaendelea kusema, “kama ninyi hamkuwa waaminifu katika mali ya udhalimu, ni nani atakayewapa amana mali ya kweli [yaani, masilahi ya kiroho, au ya Ufalme]? Na kama hamkuwa waaminifu katika mali ya mtu mwingine [masiliahi ya Ufalme ambayo Mungu hukabidhi watumishi wake], ni nani atakayewapa iliyo yenu wenyewe [thawabu ya uhai katika makao ya milele]?”
Hatuwezi kamwe kuwa watumishi wa kweli wa Mungu na wakati ule ule tuwe watumwa kwa mali zisizo za uadilifu, mali za kimwili, kama vile Yesu alivyokata shauri: “Hakuna mtumishi awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana, ama atamchukia huyu ama kumpenda huyu, ama atashikamana na huyu na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.” Luka 15:1, 2; 16:1-13; Yohana 10:16.
▪ Wakili katika kielezi cha Yesu anafanyaje urafiki pamoja na wale wanaoweza kumsaidia baadaye?
▪ “Mali ya udhalimu” ni nini, nasi tunaweza kufanyaje urafiki kwa kuitumia?
▪ Ni nani wanaoweza kutupokea katika “makao ya milele,” nayo ni makao gani?