Uaminifu Katika Kutumia “Mali ya Udhalimu”
“Jifanyieni rafiki kwa mali ya udhalimu, ili itakapokosekana wawakaribishe katika makao ya milele. Aliye mwaminifu katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia; na aliye dhalimu katika lililo dogo, huwa dhalimu katika lililo kubwa pia. Basi, kama ninyi hamkuwa waaminifu katika mali ya udhalimu, ni nani atakayewapa amana mali ya kweli?—Luka 16:9-11.
1. Kulingana na Luka 16:1-7, wakili fulani alijifanyiaje rafiki, na kwa sababu gani?
MTU mmoja alikuwa wakili, naye alikuwa na cheo kikubwa, kwa maana yeye ndiye aliyesimamia mambo ya bwana wake. Lakini mtu huyo alipata hatia ya kusimamia mambo vibaya sana hata akakaribia kuondolewa katika uwakili wake, kufukuzwa katika nyumba ya bwana wake bila kitu cha kujipatia riziki. Akiwa bado na mamlaka yake ya uwakili, alifanya haraka kujipendekeza kwa wadeni wa bwana wake kwa kuwapunguzia deni zao. Basi akajifanyia rafiki ambao wangemsaidia akiisha agizwa kwenda zake.—Luka 16:1-7.
2. (a) Maana kuu ya mfano wa Yesu juu ya wakili huyo asiye haki ilikuwa nini? (b) Huenda jambo hilo likatokeza maulizo gani?
2 Yesu Kristo aliutumia mfano wa mtu huyo mwerevu kufundisha somo la maana: “Jifanyieni rafiki kwa mali ya udhalimu, ili itakapokosekana wawakaribishe katika makao ya milele.” (Luka 16:9) Basi maulizo yanatokea: Hiyo “mali ya udhalimu” ni nini? Ni nani wenye hayo “makao ya milele”? Nasi tunawezaje kujifanya rafiki zao kwa kutumia “mali ya udhalimu”?
3. Hizo ‘mali za udhalimu’ ni nini, nayo Maandiko yanaweza kutumiwaje kuonyesha hivyo?
3 Hakuna udhalimu wo wote kuhusu mali za kiroho. Lakini haiwezi kusemwa hivyo juu ya utajiri wa kimwili. Kuwa na mali za kimwili au hata kuzitamani kunaweza kuongoza watu watende matendo ya udhalimu. Huenda matajiri wakaanza kuonea watu, kuwafanyia ukali na ukatili. Badala ya kuhurumia wenye shida, huenda wakawatumia ili kujifaidi wenyewe. Mwanafunzi Mkristo Yakobo alikumbusha waamini wenzake kwa kuwauliza: “Je! Matajiri hawawaonei ninyi na kuwavuta mbele ya viti vya hukumu? Hawalitukani jina lile zuri mliloitwa?” (Yak. 2:6, 7) Baadhi ya matajiri hao walitumia tamaa zao mbovu kufanya anasa huku wakikataa kulipa wafanya kazi wao mshahara waliostahili kupata. (Yak. 5:4, 5) Kwa sababu ya tamaa nyingi ya kupata mali, watu wengine wametumia udanganyifu. Mithali ya Biblia imesema kweli kwa habari yao: “Afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa.” (Mit. 28:20) Kwa sababu ya mabaya yote yanayohusiana sana na mali, ilifaa Yesu Kristo akazitaja kuwa ‘za udhalimu.’
4. Yesu alisema nini juu ya kudumu kwa ‘mali za udhalimu,’ nayo mambo yaliyotukia katika historia yanawezaje kuonyesha ukweli wa jambo hilo?
4 Vilevile tunastahili kuangalia kwamba Mwana wa Mungu alionyesha hizo ‘mali za udhalimu’ zingeweza kupoteza faida. Kwa mfano, pesa zinaweza kupoteza thamani bei za vitu zinapopanda au thamani yake ipunguzwapo na serikali. Vilevile, vita, mapinduzi, mafuriko ya maji, matetemeko ya nchi na misiba mingine inaweza kuacha watu katika hali ya umaskini. Basi, jinsi ulivyo ujinga mtu ye yote kutumaini mali na kuzitafuta karibu wakati wote maishani mwake!
5. Ni nani wenye “makao ya milele,” na kwa sababu gani?
5 Lengo la wanafunzi wa kweli wa Kristo linapaswa kuwa kutumia ‘mali za udhalimu’ ili kuwa rafiki za wenye “makao ya milele.” Kwa kuwa hakuna kao lo lote duniani linaloweza kutajwa kuwa la milele, ni wazi kwamba hayo “makao ya milele” ni ya mbinguni. Wenye makao hayo ni Mungu wa milele, Yehova, na Mwanawe. Yesu Kristo aliwaambia mitume wake: “Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali.”—Yohana 14:2.
6. (a) Kwa sababu gani Mungu na Kristo hawahitaji vitu vyetu vya kimwili? (b) Tunawezaje kuwa rafiki za Mungu na Kristo kwa kutumia ‘mali za udhalimu’?
6 Kwa sababu Yehova ndiye Muumba, vitu vyote ni vyake, naye Mwanawe mzaliwa wa kwanza ni mshirika katika mali hizo kwa maana ndiye mrithi wa vitu vyote. (Zab. 50:10-12; 2 Kor. 8:9; Ebr. 1:1, 2) Maana yake ni kwamba sisi wanadamu hatuna kitu cha kuwapa. Basi, kuwa rafiki za Mungu Aliye Juu Zaidi na Mwanawe kwa kutumia ‘mali za udhalimu’ maana yake ni kutumia mali hizo kwa njia yenye kutuletea ukubali Wao. Njia moja ni kuwa na maoni yanayofaa katika kutumia mali ili kufaidi watu wengine. Yesu Kristo alitoa shauri hili: “Mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume sadaka yako iwe kwa siri.” (Mt. 6:3, 4 Naye mtume Paulo aliwaandikia Wakorintho hivi: “Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu,—2 Kor. 9:7.
KUSAIDIA WENYE SHIDA
7. Yehova Mungu na Yesu Kristo wanaonaje tunapokirimu wenye shida bila choyo?
7 Tunaposaidia wenye shida halisi kwa uchangamfu na bila choyo, Yehova Mungu na Mwanawe wanaona kama kwamba wao ndio wamefanyiwa hivyo. Katika Maandiko tunasoma kwamba: “Amwoneaye maskini humsuta Muumba wake; bali yeye awahurumiaye wahitaji humheshimu. (Mit. 14:31) “Amhurumiaye maskini humkopesha [Yehova]; naye atamlipa kwa tendo lake jema.” (Mit. 19:17) Vivyo hivyo, wakati Yesu Kristo alipokuwa akionyesha jambo linalotofautisha kondoo wanaokubaliwa na mbuzi wanaolaaniwa alisema: “Kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo mlinitendea mimi.” (Mt. 25:40) “Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi.”—Mt. 25:45.
8. (a) Kufikiria maskini na wenye shida kuna ubora mwingi namna gani? (b) Watoto wana wajibu wa kufanyia wazazi, mababu na nyanya zao nini, nao wataonwaje wasipotimiza wajibu huo? (c) Ni jambo gani la maana zaidi kwa Mkristo, wajibu alio nao kwa waamini wenzake au kwa watu walio nje ya kundi?
8 Kwa hiyo, mtu anahitajiwa sana awe na nia ya kusaidia maskini na wenye shida ili kuwa mwabudu wa kweli wa Yehova. (Ayubu 29:16; 31:19-22) Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele ya Mungu Baba ndiyo hii, kwenda kuangalia yatima na wajane katika mateso yao, na kujilinda wenyewe katika machafu ya ulimwengu huu.” (Yak. 1:27, ZSB) Inampasa mtu asaidie kwanza watu wa ukoo wake mwenyewe kwa bidii, Kwa mfano, Maandiko yanawapa watoto na wajukuu wajibu wa kuangalia wazazi wao, mababu na nyanya wenye shida. (1 Tim. 5:4) Kutotimiza wajibu huo kwa makusudi ni kuikana imani ya Kikristo. (1 Tim. 5:8) Tena, kwa kuwa Wakristo wa kweli ni ushirika wa ndugu, lazima waangalie wenye shida kati yao kabla ya kwenda wakasaidie watu walio nje ya kundi. Hilo linapatana na kanuni hii: “Tukiona nafasi, tutende mema kwa watu wote, zaidi kwao walio wa nyumba ya imani.”—Gal. 6:10.
9. Ni nani wanaopaswa kuamua kama kundi litasaidia watu mmoja mmoja, na ni jambo gani linalopasa kuamua watu wanaostahili kusaidiwa hivyo?
9 Wakristo mmoja mmoja wanaweza kutoa sana vitu vya kuwapa wengine. Lakini, nyakati nyingine, huenda kundi likalazimika kutumia michango yake kuwapa washiriki fulani msaada wa pesa. Ikiwa hivyo, wazee ndio watakaoamua anayepaswa kupewa msaada wa pesa, na kiasi atakachopewa. Kama inavyoonekana katika 2 Wathesalonike 3:10 na 1 Timotheo 5:9, 10, wakati kundi linapotoa msaada, hasa kwa ukawaida, inalipasa liwape wenye shida ambao ni mifano myema katika maisha ya Kikristo.
KAZI KUBWA YA KUSAIDIA WENYE SHIDA
10. Tuna kielelezo gani cha kutuongoza jinsi ya kugawia wenye shida misaada?
10 Tena, ziko nyakati ambazo huenda ikawa lazima mipango mikubwa ya kusaidia waamini wenzetu katika makundi mengine ifanywe, labda hata katika sehemu nyingine za ulimwengu. Uchunguzi wa kazi kubwa ya kusaidia wenye shida katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza unaonyesha hasa jinsi mipango hiyo inavyopaswa kufanywa.
11. (a) Hapo kwanza ni nani walioangalia kazi ya kusaidia, wenye shida katika kundi la karne ya kwanza? (b) Baadaye ni wanaume wa namna gani waliokabidhiwa madaraka ya kazi hiyo?
11 Kwanza, mitume walikubali michango ya hiari halafu wakasimamia ugawaji wa michango hiyo kwa wenye shida. (Matendo 4:34, 35) Kundi lilipoendelea kuongezeka wingi wa watu, haikufaa tena wasimamie kazi hiyo. Baadaye, wanaume saba ‘wenye kujawa na roho na hekima’ waliwekwa kuhakikisha kwamba hakuna wajane wenye kustahili waliosahauliwa katika ugawaji wa kila siku. Wanaume hao saba walitumainiwa na waamini wenzao. (Matendo 6:1-6) Uangalifu mwingi ulifanywa kuhakikisha kwamba wale waliokuwa wakigawa michango ya kusaidia wenye shida walikuwa wanaume wenye kutumainika. Kwa habari ya wale ambao wangekuwa wakichukua michango kutoka Korintho na kuipeleka Yerusalemu, mtume Paulo aliandikia kundi la Kikristo akaliambia: “Nitawatuma wale mutakaowachagua kwa barua, wapeleke zawadi zenu hata Yerusalema.”—1 Kor. 16:3, ZSB.
12. (a) Leo pesa za kusaidia wenye shida zinapasa zitoke wapi? (b) Kuna mipango gani kati ya Mashahidi wa Yehova kuhusu jambo hilo?
12 Kupatana na mfano wa kundi la karne ya kwanza, inapasa leo kazi ya kusaidia wenye shida ipate pesa kutokana na michango ya hiari. Vilevile, usimamizi unaotumainika na uliosawazika unahitajiwa. Ili michango ya kusaidia wenye shida ishughulikiwe kwa utaratibu, makundi ya Mashahidi wa Yehova yanapelekea Watch Tower Society, 124 Columbia Heights, Brooklyn, New York michango yao, au mojawapo matawi yake. Wakati msiba utokeapo, Sosaiti au tawi la mahali linaonana na wazee wenye kuwakilisha makundi yaliyopatwa na msiba, ili kuhakikisha mahitaji yao. Ndipo misaada na pesa zinazohitajiwa zinapotolewa upesi kusaidia wenye shida, na kwa kawaida wazee wa mahali hapo ndio wanaosaidia kufanya mipango hiyo.
13. Wazee wanapaswa kufanyaje wapashwapo habari za kuaminika juu ya wenye shida ya kimwili?
13 Mara habari za kuaminika zipokewapo juu ya ndugu waliopatwa na shida halisi, wazee katika kila kundi la karibu wanaweza kutangazia ndugu pendeleo la kuchanga ili kusaidia wenye shida. Ndipo wote watakapoweza kuamua kiasi wanachoweza kutoa. Mfano wa Maandiko kuhusu jambo hilo unapatikana katika Matendo 11:27-29, ZSB, tunaposoma hivi: “Na katika siku hizi manabii walitelemuka toka Yerusalema hata Antiokia. Na mumoja wao, jina lake Agabo, akasimama, akaonyesha kwa uwezo wa [roho takatifu] ya kama njaa kubwa itakuja katika dunia nzima; nayo ilitokea katika siku za Klaudio. Na wanafunzi, kila mutu kwa kadiri ya uwezo wake, walikusudi kutuma zawadi kwa ndugu waliokaa Yudea.” Vivyo hivyo leo, ili pesa za kusaidia wenye shida ziweze kupatikana kwa matumizi ya haraka, mara kwa mara makundi mengi na watu mmoja mmoja wanapelekea afisi kuu ya Watch Tower Society katika Brooklyn au mojawapo matawi yake michango yao.
KUSAIDIA KUPANUA FAIDA ZA KIROHO
14. (a) Wajibu mkubwa zaidi wa watumishi wa Mungu leo ni nini? (b) Vitabu na magazeti vimesaidiaje kutimiza wajibu huo? (e) Pesa za kujenga viwanda vya uchapaji na kuviendeleza zimepatikanaje? (d) Pesa zilizochangwa zimetumiwa kwa makusudi gani mengine?
14 Ingawa ni jambo la maana sana kuwapa wenye shida halisi msaada wa kimwili, wajibu mkubwa zaidi wa watumishi wa Mungu ni kusaidia watu kiroho ndani na nje ya kundi. Nyakati za kisasa msaada huo wa kiroho umetolewa sana vitabuni na magazetini. Michango na mikopo ambayo watu wamepelekea Watch Tower Society na matawi yake bila kutazamia faida imewezesha kujenga na kuendeleza viwanda ambako Biblia na vitabu vinavyoeleza habari za Biblia vinaweza kuchapwa kwa bei ndogo sana kuliko ile inayotozwa na mashirika ya kibiashara. Hivyo, hata watu walio maskini sana wanaweza kupokea vitabu bure au kwa mchango mdogo. Tena, michango inatumiwa kusaidia wamisionari na wafanya kazi wengine wa wakati wote, pamoja na wazee wanaosafiri, ili wapate vitu wanavyohitaji hasa.
15. Je! Maandiko yanaonyesha inafaa kuwapa msaada wa pesa wale wanaojitoa zaidi kuangalia faida za kiroho za wengine? (1 Kor. 9:6-18; Gal. 6:6; Flp. 4:14-18)
15 Katika 1 Timotheo 5:17, 18 inaonyeshwa wazi kwamba michango ya pesa inaweza kutumiwa kusaidia wale wanaoangalia faida za kiroho za wengine: “Wazee watawalao [wasimamiao, NW] vema na wahesabiwe kustahili heshima maradufu; hasa wao wajitaabishao kwa kuhutubu na kufundisha. Kwa maana andiko lasema, Usimfunge kinywa ng’ombe apurapo nafaka. Na tena, Mtenda kazi astahili ujira wake.” Hiyo si kusema wazee wapokee mshahara kwa sababu ya kazi yao. Lakini kupatana na kanuni za Maandiko, inafaa Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova na matawi yatumie pesa zilizochangwa ili kusaidia wanaowezeshwa nazo kujitoa zaidi wafanye kazi ya kiroho.
16. Kundi linapata gharama gani, na kwa sababu gani ni jambo la maana kuzilipia?
16 Tena, makundi ya Mashahidi wa Yehova yanapata gharama kuhusiana na mahali pao pa kukutania au Majumba ya Ufalme. Zaidi ya kulipia umeme, maji, vifaa vya kuyapasha joto, kuyasafisha na kutengeneza sehemu zilizoharibika, huenda ikawapasa kutoa malipo ya kodi ya kila mwezi au kulipa rehani. Michango inahitajiwa ili kulipa gharama hizo ili kundi lisije likaleta suto juu ya jina la Mungu kwa sababu ya kushindwa kulipa pesa wanazodaiwa. Watumishi mmoja mmoja wa Yehova, na kundi lote kwa ujumla, wanapaswa kulitii onyo hili la upole: “Musiwe na deni ya mutu, ila kupendana tu.”—Rum. 13:8, ZSB.
WAJIBU WA KUTIMIZWA NA WOTE
17. Inalipasa kila kundi liwe na maoni gani juu ya kutoa michango ili kuendeleza faida za kiroho na kusaidia wenye shida?
17 Kutumia ‘mali za udhalimu’ kwa kusudi la kuendeleza faida za kiroho na kusaidia wenye shida ni jambo la maana sana ili kuwa Mkristo. Watu wote wana pendeleo la kuchanga kitu fulani, wawe wana pesa nyingi au ndogo. Kwa mfano, angalia pendekezo ambalo mtume Paulo alitolea Wakorintho: “Kila siku ya kwanza ya juma kila mmoja wenu na aweke kando kitu fulani akibani katika nyumba yake mwenyewe kadiri anavyofanikiwa.”—1 Kor. 16:2, NW.
18. (a) Ili tuweze kutoa michango ya kuendeleza faida za Ufalme, ni onyo gani la upole la Maandiko linaloweza kutusaidia? (b) Je! jambo la maana zaidi ni kiasi ambacho kimechangwa, nalo jambo hilo limeonyeshwaje katika kisa cha yule mjane maskini?
18 Kupatana na onyo hilo la upole lililoandikwa kwa uongozi wa Mungu, wakati wa juma mtu anaweza kuweka kando mapema kitu anachoweza kuchanga. Bila shaka, kiasi kinachotolewa na watu mbali-mbali kitatofautiana sana, lakini hilo silo jambo la maana zaidi. Jambo lililo la maana zaidi ni moyo wa kupenda, ile hamu ya kuchanga. Mtume Paulo alieleza jambo hilo kwa kusema: “Kama nia ipo, hukubaliwa kwa kadiri ya alivyo navyo mtu, si kwa kadiri asivyo navyo.” (2 Kor. 8:12) Nia hiyo ya kutoa kulingana na uwezo wa mtu ndilo jambo la maana zaidi machoni pa Yehova Mungu. Kwa mfano, mjane maskini aliyeonekana na Yesu Kristo alichanga lepta mbili tu Yerusalemu hekaluni. Wakati huo, mtu mwenye kiasi hicho kidogo angeweza kununua nusu-shomoro, asiweze kumshibisha hata wakaa mmoja wa chakula. Hata hivyo, mchango ambao mjane huyo alitoa kwa sababu ya kumpenda Mungu wa kweli aliyeabudiwa katika hekalu hilo ulikubalika kabisa. Kwa kulinganishwa na uwezo wake, zawadi yake ilikuwa kubwa kuliko ya matajiri waliochanga pesa nyingi kwa sababu walikuwa na za ziada.—Marko 12:42-44.
19. Tunaonyesha nini tukitumia vizuri ‘mali zetu za udhalimu,’ na kwa hiyo tunaweza kuwa na hakika ya kupata nini?
19 Basi, inatupasa kweli tuhakikishe kwamba tu rafiki za Mungu na Kristo kwa kutumia ‘mali zetu za udhalimu’ kusaidia walio na shida na kuendeleza faida za kiroho. (Mit. 3:9; Gal. 2:10) Tukiendelea kutumia ‘mali zetu za udhalimu’ vizuri, tunaonyesha kwamba tu waaminifu katika lililo dogo. Kwa hiyo, Yehova Mungu na Mwanawe wanaweza kuendelea kututumia kama mawakili wema tugawie watu mali za kiroho ambazo ndizo zenye thamani zaidi. Matendo yetu mema yatakuwa kama hazina iliyowekwa mbinguni, nayo yatatuzalia faida tupate kibali na baraka za Mungu sasa na uzima wa milele katika taratibu mpya ya “mbingu mpya na nchi mpya.”—Mt. 6:20; Luka 16:10-13; 2 Pet. 3:13.
—Kutoka The Watchtower, Sept. 1,1977.