Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • gt sura 88
  • Tajiri na Lazaro

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tajiri na Lazaro
  • Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tajiri na Lazaro Wapatwa na Badiliko
  • Tajiri na Lazaro Wapatwa na Badiliko
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Tajiri na Lazaro
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Mabadiliko Katika Hali ya Tajiri na Lazaro
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Yule Tajiri na Lazaro Walikuwa Nani?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
gt sura 88

Sura 88

Tajiri na Lazaro

YESU amekuwa akiongea na wanafunzi wake juu ya utumizi unaofaa wa mali za kimwili, akieleza kwamba hatuwezi kuwa watumwa wazo na wakati ule ule tuwe watumwa wa Mungu. Mafarisayo pia wanasikiliza, na wanaanza kucheka Yesu kwa dharau kwa sababu wao ni wapenda pesa. Kwa hiyo yeye anawaambia: “Ninyi ndinyi mnaojidai haki [uadilifu, NW] mbele ya wanadamu, lakini Mungu awajua mioyo yenu; kwa kuwa lililotukuka kwa wanadamu huwa chukizo mbele za Mungu.”

Wakati umefika mambo yawageuke watu walio matajiri katika mali za kilimwengu, mamlaka ya kisiasa, na udhibiti na uvutano wa kidini. Watapasa kushushwa cheo. Hata hivyo, wale watu wanaotambua uhitaji wao wa kiroho wanainuliwa juu. Yesu anaelekeza kwenye badiliko hilo anapoendelea kusema hivi kwa Mafarisayo:

“Torati na mabii vilikuwapo mpaka Yohana [Mbatizaji]; tangu wakati huo habari njema ya ufalme wa Mungu hutangazwa, na kila mtu hujiingiza kwa nguvu. Lakini ni vyepesi zaidi mbingu na nchi vitoweke, kuliko itanguke nukta moja ya torati.”

Waandishi na Mafarisayo wana kiburi cha kudai kwamba wao wanashika sana Sheria ya Musa. Kumbuka kwamba Yesu alipompa mtu fulani uwezo wa kuona kwa muujiza katika Yerusalemu, wao walijisifu hivi: “Sisi tu wanafunzi wa Musa. Sisi tunajua ya kuwa Mungu alisema na Musa.” Lakini sasa Sheria ya Musa imetimiza kusudi layo la kuongoza wanyenyekevu kwenye Mfalme aliyekusudiwa na Mungu, Yesu Kristo. Kwa hiyo huduma ya Yohana inapoanza, watu wa aina zote, hasa wanyenyekevu na maskini, wanajikaza ili wawe raia za Ufalme wa Mungu.

Kwa kuwa sasa Sheria ya Musa inatimizwa, wajibu wa kuishika unapasa kuondolewa. Sheria hiyo inaruhusu talaka kwa sababu mbalimbali, lakini sasa Yesu anasema: “Kila mtu atakayemwacha [atakayemtaliki, NW] mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini.” Lo, hayo matamko rasmi lazima yawaudhi Mafarisayo kama nini, hasa kwa kuwa wao huruhusu talaka kwa sababu nyingi!

Akiendelea na maneno yake kwa Mafarisayo, Yesu anasimulia kielezi kinachohusu wanaume wawili ambao cheo au hali yao inabadilishwa sana hatimaye. Je! wewe unaweza kujua ni nani wanaowakilishwa na wanaume hao na kinachomaanishwa na hali zao zilizogeuka zikawa kinyume?

“Palikuwa na mtu mmoja, tajiri, aliyevaa nguo za rangi ya zambarau na kitani safi, na kula sikuzote kwa anasa. Na maskini mmoja, jina lake Lazaro, huwekwa mlangoni pake, ana vidonda vingi, naye alikuwa akitamani kushibishwa kwa makombo yaliyoanguka katika meza ya yule tajiri; hata mbwa wakaja wakamramba vidonda vyake.”

Hapa Yesu anatumia tajiri huyo kuwakilisha viongozi wa kidini Wayahudi, kutia ndani si Mafarisayo na waandishi tu bali pia Masadukayo na wakuu wa makuhani. Wao ni matajiri katika mapendeleo na fursa za kiroho, na wanajiendesha kama yule tajiri. Nguo zao za rangi ya zambarau iliyo ya kifalme zinawakilisha cheo chao chenye upendeleo, na ile kitani nyeupe hufananisha kujiona kwao kuwa waadilifu.

Jamii hii ya tajiri mwenye kiburi inawadharau kabisa kabisa maskini wenye cheo cha kawaida tu, wakiwaita ‘am ha·’aʹrets, au watu wa dunia. Hivyo Lazaro mwombaji maskini anawakilisha watu ambao viongozi wa kidini wanawanyima ulishaji wa kiroho unaofaa na mapendeleo. Kwa sababu hiyo, kama vile Lazaro aliyejawa na vidonda, watu wa cheo cha kawaida wanadharauliwa kuwa na maradhi ya kiroho na wenye kufaa kushirikiana na mbwa tu. Hata hivyo, wale wa jamii ya Lazaro wana njaa na kiu kwa ajili ya ulishaji wa kiroho na kwa hiyo wako langoni, wakitafuta kupokea makombo yoyote haba ya chakula cha kiroho ambayo huenda yakaanguka kutoka kwenye meza ya tajiri.

Sasa Yesu anaendelea kueleza mabadiliko katika hali ya tajiri na Lazaro. Mabadiliko hayo ni gani, na yanawakilisha nini?

Tajiri na Lazaro Wapatwa na Badiliko

Tajiri anawakilisha viongozi wa kidini waliopendelewa kuwa na mapendeleo na fursa za kiroho, na Lazaro anafananisha watu wa kawaida walio na njaa ya ulishaji wa kiroho. Yesu anaendeleza hadithi yake, akieleza badiliko la kutazamisha katika hali za wanaume hao.

“Ikawa,” anasema Yesu, “yule maskini alikufa, akachukuliwa na malaika mpaka kifuani kwa Ibrahimu. Yule tajiri naye akafa, akazikwa. Basi kule kuzimu [Hadesi, NW] aliyainua macho yake, alipokuwa katika mateso, akamwona Ibrahimu kwa mbali, na Lazaro kifuani mwake.”

Kwa kuwa tajiri na Lazaro si watu halisi bali wanafananisha jamii za watu, ni jambo la kiakili kuchukua vifo vyao kuwa vya ufananisho. Vifo vyao vinafananisha au kuwakilisha nini?

Sasa tu ndipo Yesu amemaliza kuelekeza kwenye badiliko la hali kwa kusema kwamba ‘Torati na manabii vilikuwapo mpaka Yohana Mbatizaji, lakini tangu wakati huo ufalme wa Mungu unahubiriwa.’ Kwa sababu hiyo, Yohana na Yesu Kristo wafanyapo kuhubiri kwao ndipo wote wawili tajiri na Lazaro wanapokufa kuhusu hali zao za kwanza.

Wale walio wa jamii ya Lazaro mnyenyekevu mwenye kutubu wanakufa kuhusu hali yao ya kwanza ya kunyimwa ulishaji wa kiroho na wanakuja ndani ya cheo cha upendeleo wa kimungu. Ijapokuwa hapo kwanza walitegemea viongozi wa kidini kwa kiasi chochote kidogo kilichoanguka kutoka kwenye meza ya kiroho, sasa kweli za Kimaandiko zinazotolewa na Yesu zinajaza mahitaji yao. Hivyo wanaletwa ndani ya kifua, au cheo chenye upendeleo, cha Abrahamu Mkuu Zaidi, Yehova Mungu.

Kwa upande mwingine, wale wanaojumlika kuwa jamii ya tajiri wanakuja chini ya ukosefu wa upendeleo wa kimungu kwa sababu ya kukataa ujumbe wa Ufalme anaofundisha Yesu. Kwa njia hiyo wanakufa kuhusu cheo walichokuwa nacho cha kuonekana kama wenye upendeleo. Kwa hakika, wananenwa kana kwamba wamo katika mateso ya kitamathali. Sikiliza sasa, wakati tajiri anaponena:

“Ee baba Ibrahimu, nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake majini, auburudishe ulimi wangu; kwa sababu ninateswa katika moto huu.” Jumbe zenye moto za hukumu ya Mungu zilizotangazwa na wanafunzi wa Yesu ndizo zinazotesa watu mmoja mmoja wa jamii ya tajiri. Wao wanataka wanafunzi waache kutangaza jumbe hizo, hivyo wakiwaandalia kadiri fulani ya kitulizo kutoka mateso yao.

“Ibrahimu akasema, Mwanangu, kumbuka ya kwamba wewe uliyapokea mambo mema yako katika maisha yako, na Lazaro vivyo hivyo alipata mabaya; na sasa yeye yupo hapa anafarijiwa, na wewe unaumizwa. Na zaidi ya hayo, kati yetu sisi na ninyi kumewekwa shimo kubwa, ili wale watakao kutoka huku kwenda kwenu wasiweze; wala watu wa kwenu wasivuke kuja kwetu.”

Ni haki na inafaa kama nini badiliko hilo la kutazamisha litukie kati ya jamii ya Lazaro na jamii ya tajiri! Badiliko hilo la hali linatimizwa miezi michache baadaye kwenye Pentekoste 33 W.K., wakati nafasi ya agano la zamani la Sheria (Torati) inapochukuliwa na agano jipya. Ndipo inapoonekana wazi kwa njia isiyoweza kukosewa kwamba wanafunzi, wala si Mafarisayo na viongozi wengine wa kidini, wanapendelewa na Mungu. Kwa hiyo “shimo kubwa” linalotenganisha tajiri na wanafunzi wa Yesu linawakilisha hukumu ya Mungu ya uadilifu, isiyobadilika.

Ndipo tajiri anapoomba “baba” Abrahamu: “Nakuomba, umtume [Lazaro] nyumbani kwa baba yangu, kwa kuwa ninao ndugu watano.” Hivyo tajiri anakiri ana uhusiano wa karibu zaidi na baba mwingine, ambaye kwa kweli ni Shetani Ibilisi. Tajiri anaomba kwamba Lazaro apunguze nguvu ya jumbe za hukumu ya Mungu ili asitie ‘ndugu zake watano,’ wafungamani wake wa kidini, katika “mahali hapa pa mateso.”

“Ibrahimu akasema, Wanao Musa na manabii; na wawasikilize wao.” Ndiyo, ikiwa “ndugu watano” hao wangetaka kuepuka kuteseka, la kufanya tu ni kuyatii maandiko ya Musa na Manabii yanayomtambulisha Yesu kuwa Mesiya halafu wawe wanafunzi wake. Lakini tajiri anapinga: “La, baba Ibrahimu, lakini kama akiwaendea mtu atokaye kwa wafu, watatubu.”

Hata hivyo, anaambiwa: “Wasipowasikia Musa na manabii, hawatashawishwa hata mtu akifufuka katika wafu.” Mungu hataandaa ishara au miujiza maalumu kusadikisha watu. Ni lazima wasome Maandiko na kuyatumia ikiwa wangetaka kupata upendeleo wake. Luka 16:14-31; Yohana 9:28, 29; Mathayo 19:3-9; Wagalatia 3:24; Wakolosai 2:14; Yohana 8:44.

◼ Kwa nini ni lazima iwe vifo vya tajiri na Lazaro ni vya ufananisho, na vifo vyao vinafananisha nini?

◼ Huduma ya Yohana inapoanza, Yesu anaonyesha ni badiliko gani linalotukia?

◼ Ni kitu gani kitaondolewa wakati wa kifo cha Yesu, na hiyo itaathirije lile jambo la talaka?

◼ Katika kielezi cha Yesu, ni nani wanaowakilishwa na tajiri na Lazaro?

◼ Mateso yaliyompata tajiri ni nini, naye anaomba yaondolewe kwa njia gani?

◼ “Shimo kubwa” linawakilisha nini?

◼ Ni nani baba halisi wa tajiri, na ndugu zake watano ni nani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki