Sura 131
Kutokea Mara za Mwisho, Na Pentekoste ya 33 W.K.
WAKATI fulani Yesu afanya mipango ili mitume wake wote 11 wakutane naye kwenye mlima katika Galilaya. Yaonekana kwamba wanafunzi wengine wanaambiwa juu ya mkutano huo, na jumla ya watu zaidi ya 500 wakutana. Huo wathibitika kuwa mkusanyiko wenye furaha kama nini Yesu anapotokea na kuanza kuwafundisha!
Miongoni mwa mambo mengine, Yesu aelezea umati huo mkubwa kwamba Mungu amempa mamlaka yote mbinguni na duniani. “Basi, enendeni,” ahimiza, “mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW]; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.”
Ebu fikiria jambo hilo! Wanaume, wanawake, na watoto wote wapokea utume uo huo wa kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. Wapinzani watajaribu kukomesha kuhubiri na kufundisha kwao, lakini Yesu awafariji hivi: “Tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari [umalizio wa mfumo wa mambo, NW].” Yesu aendelea kuwa pamoja na wafuasi wake kupitia roho takatifu, ili kuwasaidia watimize huduma yao.
Kwa ujumla, Yesu ajionyesha mwenyewe kwa wanafunzi wake kuwa yuko hai kwa muda wa siku 40 kufuata ufufuo wake. Wakati wa kutokea huko mbalimbali, awafundisha juu ya Ufalme wa Mungu, na kukazia madaraka yao ni nini wakiwa wanafunzi wake. Pindi moja hata amtokea Yakobo, ndugu mzazi mmoja naye na kumsadikisha huyo ambaye wakati mmoja alikuwa asiyeamini kwamba Yeye kwa kweli ndiye Kristo.
Wakati mitume wangali wako Galilaya, kwa wazi Yesu awaagiza warudi Yerusalemu. Anapokuwa amekutana nao huko, awaambia hivi: ‘Msitoke Yerusalemu, bali mwingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika roho takatifu baada ya siku hizi chache.’
Baadaye Yesu akutana na mitume wake tena na kuwaongoza nje ya jiji hadi Bethania, ambao uko kwenye mteremko wa mashariki wa Mlima wa Mizeituni. Kwa kushangaza, yajapokuwa yale yote ambayo amesema juu ya kuondoka kwake hivi karibuni kwenda mbinguni, bado wao waamini kwamba Ufalme wake utasimamishwa duniani. Kwa hiyo, wauliza hivi: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?”
Badala ya kujaribu kusahihisha tena ufahamu wao wenye kosa, Yesu ajibu tu hivi: “Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe.” Halafu, akikazia tena kazi ambayo lazima waifanye, asema hivi: “Mtapokea nguvu, akiisha [ikiisha, NW] kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW]; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”
Wakiwa wangali wanatazama, Yesu aanza kupaa kuelekea mbinguni, kisha wingu lamficha kutoka macho yao. Baada ya kuvua mwili wake wa kimnofu, apaa mbinguni akiwa mtu wa roho. Wale 11 wanapoendelea kukaza macho mbinguni, wanaume 2 wenye kuvalia mavazi meupe watokea kando yao. Malaika hao wenye kujivika miili ya kimnofu wauliza hivi: “Enyi watu wa Galilaya mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni.”
Jinsi ambayo kwayo Yesu ameondoka duniani hivi sasa tu ni ya bila kujionyesha hadharani kwa njia yenye kutazamisha na wafuasi wake waaminifu wakiwa ndio tu wanaona. Kwa hiyo atarudi jinsi iyo hiyo—bila kujionyesha hadharani kwa njia yenye kutazamisha na wafuasi wake waaminifu ndio tu watatambua kwamba amerudi na ameanza kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme.
Sasa mitume wateremka Mlima wa Mizeituni, wavuka bonde la Kidroni, na kuingia Yerusalemu tena. Wakaa huko kwa kutii amri ya Yesu. Siku kumi baadaye, katika Sikukuu ya Kiyahudi ya Pentekoste ya 33 W.K., wakati wanafunzi 120 hivi wanapokutana katika chumba cha ghorofa katika Yerusalemu, ghafula mvumo kama ule wa upepo wenye nguvu ukienda kasi waijaza nyumba yote. Ndimi kama za moto zaonekana, na mmoja wakaa juu ya kila mmoja aliyepo, na wanafunzi wote waanza kuongea katika lugha tofauti-tofauti. Huko ndiko kumiminwa kwa roho takatifu ambako Yesu alikuwa ameahidi! Mathayo 28:16-20; Luka 24:49-52; 1 Wakorintho 15:5-7; Matendo 1:3-15; 2:1-4.
▪ Yesu awapa nani maagizo ya mwisho kwenye mlima mmoja katika Galilaya, na hayo ni maagizo gani?
▪ Yesu aandaa faraja gani kwa wanafunzi wake, naye atabaki nao kwa jinsi gani?
▪ Yesu atokea wanafunzi wake kwa muda gani baada ya ufufuo wake, naye awafundisha nini?
▪ Ni mtu yupi ambaye kwa wazi hakuwa mwanafunzi kabla ya kifo cha Yesu, ambaye atokewa na Yesu?
▪ Ni mikutano gani miwili ya mwisho ambayo Yesu afanya na mitume wake, na ni mambo gani yatukia katika pindi hizo?
▪ Ni jinsi gani Yesu atarudi jinsi ile ile alivyoondoka?
▪ Ni jambo gani latukia kwenye Pentekoste 33 W.K.?