Maisha na Huduma ya Yesu
Kutokea Mara ya Mwisho, na Pentekoste ya 33 W.K.
WAKATI fulani Yesu anafanya mipango ili mitume wake wote 11 wakutane naye kwenye mlima fulani katika Galilaya. Yaonekana kwamba wanafunzi wengine wanaambiwa juu ya mkutano huo, na jumla ya zaidi ya watu 500 wanakutana. Hiyo inathibitika kuwa mkusanyiko wenye furaha kama nini Yesu anapotokea na kuanza kuwafundisha!
Miongoni mwa mambo mengine, Yesu aelezea umati mkubwa kwamba Mungu amempa mamlaka mbinguni na duniani. “Basi, enendeni,” ahimiza, “mkawafanye mataifa [watu wa mataifa, NW] yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW]; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.”
Ebu fikiria hilo! Wanaume, wanawake, na watoto wote wanapokea agizo ilo hilo kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. Wapinzani watajaribu kukomesha kuhubiri na kufundisha kwao, lakini Yesu awafariji hivi: “Tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari [umalizio wa mfumo wa mambo, NW].” Yesu abaki na wafuasi wake kupitia roho takatifu, ili kuwasaidia watimize huduma yao.
Yesu ajionyesha mwenyewe hai kwa wanafunzi wake kwa muda wa siku 40 kufuata ufufuo wake. Wakati wa mitokeo hiyo, awafunza juu ya Ufalme wa Mungu, na akazia madaraka yao wakiwa wanafunzi wake. Pindi moja hata amtokea Yakobo ndugu-nusu yake na kusadikishia huyo ambaye wakati mmoja alikuwa asiyeamini kwamba Yeye kwa kweli ndiye Kristo.
Wakati mitume bado wako Galilaya, ni wazi kwamba Yesu awaagiza warudi Yerusalemu. Anapokutana nao huko, awaambia: ‘Msitoke Yerusalemu, bali mwingoje ahadi ya baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW] baada ya siku hizi chache.’
Baadaye Yesu akutana tena na mitume wake na awaongoza nje ya mji hadi Bethania, ambao uko juu ya mtelemko wa mashariki wa Mlima wa Mizeituni. Yenye kushangaza ni kwamba, yajapokuwa yale yote amesema juu ya kuondoka kwake karibuni kwenda mbinguni, wao bado wanaamini kwamba Ufalme wake utasimamishwa duniani. Kwa hiyo wanauliza hivi: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?”
Badala ya kujaribu tena kusahihisha kutofahamu kwao vema, Yesu ajibu hivi tu: “Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe.” Halafu, akikazia tena kazi ambayo lazima wafanye, asema hivi: “Mtapokea nguvu, akiisha [ikiisha, NW] kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW]; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”
Wanapokuwa bado wanatazama, Yesu aanza kuinuka kuelekea mbinguni, halafu wingu linamficha kutoka macho yao. Baada ya kuvua mwili wake wa kimnofu, apaa mbinguni akiwa mtu wa kiroho. Wale 11 wanapoendelea kutazama angani, wanaume 2 wenye mavazi meupe wanatokea karibu nao. Malaika hawa wenye kujivika miili ya kimnofu wanauliza hivi: “Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni.”
Njia ambayo Yesu ameondoka duniani hivi tu ni bila mshindo wa matarumbeta ya waziwazi na ni wafuasi waaminifu wake tu ambao wanaangalia. Kwa hiyo atarudi kwa njia iyo hiyo—bila mshindo wa matarumbeta ya waziwazi na ni wafuasi waaminifu wake tu ambao watatambua kwamba amerudi na ameanza kuwako kwake katika mamlaka ya Ufalme.
Mitume sasa wanashuka Mlima wa Mizeituni, wanavuka Bonde la Kidroni, na wanaingia Yerusalemu tena. Wanabaki huko kwa kutii amri ya Yesu. Siku kumi baadaye, katika Sikukuu ya Kiyahudi ya Pentekoste ya 33 W.K., wakati wanafunzi 120 hivi wanapokutana katika chumba cha ghorofa katika Yerusalemu, kwa ghafula uvumi kama ule wa upepo wa nguvu ukienda kasi unaijaza nyumba yote. Ndimi kama za moto zinaonekana, na mmoja unakalia kila mmoja aliye hapo, na wanafunzi wote wanaanza kusema katika lugha tofauti-tofauti. Huko ndiko kumwagwa kwa roho takatifu ambako Yesu alikuwa ameahidi! Mathayo 28:16-20; Luka 24:49-52; 1 Wakorintho 15:5-7; Matendo 1:3-15; 2:1-4.
◆ Yesu anawapa nani maagizo ya mwisho kwenye mlima mmoja katika Galilaya, na maagizo hayo ni gani?
◆ Yesu aandaa faraja gani kwa wanafunzi wake, naye atabaki nao kwa jinsi gani?
◆ Yesu anawatokea wanafunzi wake kwa muda gani baada ya ufufuo wake, naye awafundisha nini?
◆ Yesu amtokea mtu yupi, ambaye kwa wazi hakuwa mwanafunzi kabla ya kifo cha Yesu?
◆ Yesu anakuwa na mikutano gani miwili ya mwisho pamoja na mitume wake, na mambo gani yanatokea katika nyakati hizo?
◆ Yesu atarudije jinsi ile ile anavyoondoka?
◆ Ni jambo gani linalotokea kwenye Pentekoste 33 W.K.?