Sehemu ya 4
Mungu Hutujulisha Juu ya Makusudi Yake
1, 2. Sisi twajuaje kwamba Mungu huandaa majibu kwa wale waulizao kwa weupe wa moyo?
MUNGU mwenye upendo hufunua kweli kweli makusudi yake kwa wenye moyo mweupe wamtafutao. Yeye huandalia wanadamu wenye kuulizia majibu ya maswali kama vile kwa nini yeye ameruhusu kuteseka.
2 Biblia hutaarifu hivi: “Ukimtafuta, ataonekana nawe.” “Yuko Mungu mbinguni afunuaye siri.” “Bwana MUNGU [Yehova, NW] hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.”—1 Mambo ya Nyakati 28:9; Danieli 2:28; Amosi 3:7.
Majibu Yako Wapi?
3. Ni wapi tuwezapo kupata kujua kwa nini Mungu huruhusu kuteseka?
3 Majibu ya maswali kama vile kwa nini Mungu huruhusu kuteseka na jambo atakalofanya juu yako yanapatikana katika maandishi aliyoyaongoza kwa roho kwa manufaa yetu. Maandishi hayo ni Neno lake, Biblia Takatifu. “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”—2 Timotheo 3:16, 17.
4, 5. Ni nini ambacho hufanya Biblia kuwa kitabu kisicho na kifani?
4 Biblia ni kitabu kisicho na kifani kweli kweli. Ina maandishi juu ya historia ya kibinadamu yaliyo sahihi zaidi na hata yenye kurudi nyuma kupita wakati wa kuumbwa kwa wanadamu. Pia ina habari za kisasa kabisa, kwa maana unabii wayo unahusu matukio ya wakati wetu na ya wakati ujao ulio karibu pia.
5 Hakuna kitabu kinginecho chenye sifa kama hizo za usahihi wa kihistoria. Kwa mfano, kuna hati chache tu za waandikaji bora wa kale. Lakini kuna hati nyingi za Biblia, nyingine zikiwa visehemu-visehemu na nyingine zikiwa kamili: zipatazo 6,000 za Maandiko ya Kiebrania (vile vitabu 39 vya “Agano la Kale”) na zipatazo 13,000 za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (vile vitabu 27 vya “Agano Jipya”).
6. Kwa nini twaweza kuwa na hakika kwamba kwa msingi Biblia leo iko vile vile kama wakati ilipopuliziwa na Mungu?
6 Mungu Mweza Yote, aliyeipulizia Biblia, amehakikisha kwamba ukamilifu wa kimaandishi umehifadhiwa katika nakala za hati hizo. Hivyo kwa msingi Biblia zetu leo ziko sawa na maandiko ya awali yaliyopuliziwa. Jambo jingine ambalo hutusaidia tuthamini hilo ni kwamba baadhi ya nakala za hati hizo za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hurudi nyuma kufikia miaka mia moja ya wakati wa maandiko ya awali. Zile nakala chache za hati za waandikaji wa kale wa kilimwengu ambazo zingali ziko ni mara chache sana zinapokuwa na tarehe inayokaribia hata karne kadhaa za wakati wa watungaji wa awali.
Zawadi Kutoka kwa Mungu
7. Biblia imeenezwa kwa kadiri gani?
7 Biblia ndicho kitabu chenye kuenezwa zaidi katika historia. Nakala zipatazo bilioni tatu zimechapwa. Hakuna kitabu kingine kinachokaribia tarakimu hiyo. Na Biblia au sehemu zayo imetafsiriwa katika lugha zipatazo 2,000. Hivyo, inakadiriwa kwamba asilimia 98 ya idadi ya watu wa sayari yetu wangeweza kuipata Biblia.
8-10. Ni nini baadhi ya sababu kwa nini Biblia inastahili tuichunguze?
8 Hakika kitabu kinachodai kuwa chatoka kwa Mungu na ambacho kina shuhuda zote za nje na ndani za uasilia kinastahili tukichunguze.a Kinaeleza kusudi la maisha, maana ya hali za ulimwengu, na wakati ujao una nini. Hakuna kitabu kingine kinachoweza kufanya hivyo.
9 Ndiyo, Biblia ni uwasiliano wa Mungu kwa familia ya kibinadamu. Yeye alielekeza kuandikwa kwayo kwa kani yake ya utendaji, au roho takatifu kukiwa na, wanadamu wapatao 40 wakiandika. Hivyo Mungu husema nasi kupitia Neno lake, Biblia Takatifu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli.”—1 Wathesalonike 2:13.
10 Abraham Lincoln, rais wa 16 wa United States, aliiita Biblia “zawadi bora zaidi ambayo Mungu amepata kumpa binadamu . . . Kama si kwa ajili yayo hatungeweza kutofautisha yanayofaa na yasiyofaa.” Basi, zawadi hii bora kabisa hutuambia nini juu ya jinsi kuteseka kulivyoanza, na sababu kwa nini Mungu amekuruhusu, na jambo ambalo yeye atafanya juu yako?
[Maelezo ya chini]
a Kwa habari zaidi juu ya uasilia wa Biblia, ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichotangazwa katika 1989 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Biblia, ikiwa imepuliziwa na Mungu, ni uwasiliano wake kwa familia ya kibinadamu