Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • dg seh. ya 5 kur. 10-12
  • Ile Zawadi Nzuri Ajabu ya Hiari

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ile Zawadi Nzuri Ajabu ya Hiari
  • Je, Kweli Mungu Anatujali?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi Ambavyo Tumeumbwa
  • Mwanzo Bora Kabisa
  • Uhuru Ndani ya Mipaka
  • Sheria za Nani?
  • Zawadi Nzuri Ajabu ya Hiari
    Amkeni!—1991
  • Mipaka ya Uhuru
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Thamini Zawadi Yako ya Uhuru wa Kuchagua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Uhuru Unaofurahiwa na Waabudu wa Yehova
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
Pata Habari Zaidi
Je, Kweli Mungu Anatujali?
dg seh. ya 5 kur. 10-12

Sehemu ya 5

Ile Zawadi Nzuri Ajabu ya Hiari

1, 2. Ni zawadi gani nzuri ajabu iliyo sehemu ya maumbile yetu?

ILI kuelewa kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka na ni jambo gani atafanya juu yako, twahitaji kuthamini jinsi alivyotufanyiza. Yeye alifanya zaidi ya kutuumba tukiwa tu na mwili na ubongo. Alituumba pia tukiwa na sifa za pekee za kiakili na kihisiamoyo.

2 Sehemu ya msingi ya maumbile yetu ya kiakili na kihisiamoyo ni hiari (uhuru wa kuchagua). Ndiyo, Mungu alikaza ndani yetu uwezo wa uhuru wa kuchagua. Ilikuwa kweli kweli zawadi nzuri ajabu kutoka kwake.

Jinsi Ambavyo Tumeumbwa

3-5. Kwa nini sisi twathamini hiari?

3 Acheni tufikirie jinsi hiari ilivyohusika katika Mungu kuruhusu kuteseka. Kwanza, fikiria hili: Je! wewe huthamini kuwa na uhuru wa kuchagua yale ambayo utafanya na kusema, kile ambacho utakula na kuvaa, ni aina gani ya kazi ambayo utafanya, na wapi na jinsi gani utaishi? Au ungetaka mtu fulani aamrishe kila neno na tendo lako kila dakika ya maisha yako?

4 Hakuna mtu aliye timamu ambaye hutaka maisha yake yachukuliwe hivyo kabisa kutoka udhibiti wake. Kwa nini? Kwa sababu ya jinsi ambavyo Mungu alituumba. Biblia hutuambia kwamba Mungu alimuumba mtu kwa ‘mfano na sura yake,’ na mmojawapo uwezo wa Mungu mwenyewe ni uhuru wa kuchagua. (Mwanzo 1:26; Kumbukumbu la Torati 7:6) Alipowaumba wanadamu, aliwapa uwezo uo huo mzuri ajabu—zawadi ya hiari. Hiyo ndiyo sababu moja kwa nini twaliona kuwa jambo lenye kukatisha tamaa sana kutumikishwa na watawala waonevu.

5 Kwa hiyo tamaa ya uhuru si aksidenti, kwani Mungu ni Mungu wa uhuru. Biblia husema: “Ilipo roho ya Yehova, pana uhuru.” (2 Wakorintho 3:17, NW) Kwa hiyo, Mungu alitupa sisi hiari ikiwa sehemu ya maumbile yetu. Kwa kuwa alijua jinsi akili na hisiamoyo zetu zingefanya kazi, yeye alijua kwamba tungekuwa na furaha zaidi tukiwa na hiari.

6. Mungu aliumbaje ubongo wetu ufanye kazi kupatana na hiari yetu?

6 Pamoja na zawadi ya hiari, Mungu alitupa sisi uwezo wa kufikiri, kukadiria mambo, kufanya maamuzi, na kujua yafaayo na yasiyofaa. (Waebrania 5:14) Hivyo, hiari ilitakiwa itegemee uchaguzi wa akili. Hatukufanyizwa kama roboti zisizo na akili bila hiari yazo zenyewe. Wala hatukuumbwa tutende kwa silika kama vile wanyama walivyoumbwa. Badala ya hivyo, ubongo wetu wenye kustaajabisha ulikusudiwa ufanye kazi kupatana na uhuru wetu wa kuchagua.

Mwanzo Bora Kabisa

7, 8. Ni mwanzo gani mzuri ambao Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza?

7 Kuonyesha jinsi Mungu alivyokuwa mwenye kujali, wazazi wetu wa kwanza Adamu na Hawa, walipewa pamoja na zawadi ya hiari kila kitu ambacho yeyote angetaka kwa kadiri inayofaa. Waliwekwa katika paradiso kubwa mfano wa bustani. Walikuwa na vitu vingi vya kimwili. Walikuwa na akili na miili mikamilifu, hivyo hawangelazimika kuzeeka au kuwa wagonjwa au kufa—wangaliweza kuishi milele. Wangalikuwa na watoto wakamilifu ambao pia wangaliweza kuwa na wakati ujao wa milele, wenye furaha. Na idadi hiyo ya watu yenye kupanuka ingalikuwa na kazi yenye kutosheleza ya kuigeuza hatimaye dunia yote iwe paradiso.—Mwanzo 1:26-30; 2:15.

8 Kuhusu yaliyoandaliwa, Biblia husimulia hivi: “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Biblia husema hivi pia kuhusu Mungu: “Kazi yake ni kamilifu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Ndiyo, Muumba aliipa familia ya kibinadamu mwanzo mkamilifu. Haungeweza kuwa bora zaidi ya hivyo. Lo, alithibitika kuwa Mungu mwenye kujali kama nini!

Uhuru Ndani ya Mipaka

9, 10. Kwa nini hiari lazima iongozwe ifaavyo?

9 Hata hivyo, je, Mungu alikusudia hiari iwe bila mipaka? Ebu wazia jiji lenye magari mengi bila sheria za kuongoza magari, ambamo mtu angeweza kuendesha gari upande wowote kwa mwendo-kasi wowote. Je! wewe ungependa kuendesha gari chini ya hali hizo? La, huo ungekua mvurugo wa magari na hakika ungetokeza aksidenti nyingi.

10 Ndivyo pia ilivyo zawadi ya hiari itokayo kwa Mungu. Uhuru usio na mipaka ungemaanisha mvurugo katika jamii. Lazima kuwe na sheria za kuelekeza utendaji wa kibinadamu. Neno la Mungu husema: “Jiendesheni kama watu huru, na msitumie kamwe uhuru wenu kuwa udhuru wa kutenda uovu.” (1 Petro 2:16, JB) Mungu hutaka hiari iongozwe kwa ajili ya mema ya wote. Yeye hakukusudia kwamba sisi tuwe na uhuru kamili, bali uhuru wa kadiri, na ule unaotii utawala wa sheria.

Sheria za Nani?

11. Sisi tulikusudiwa tutii sheria za nani?

11 Sisi tulikusudiwa tutii sheria za nani? Sehemu nyingine ya andiko kwenye 1 Petro 2:16 (JB) hutaarifu hivi: “Nyinyi ni watumwa si wa mwingine ila wa Mungu.” Hiyo haimaanishi utumwa wenye uonevu, bali, humaanisha kwamba sisi tulikusudiwa tufurahi kabisa tutiipo sheria za Mungu. (Mathayo 22:35-40) Sheria zake, kupita sheria zozote zilizotungwa na wanadamu, huandaa mwongozo bora kabisa. “Mimi ni BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”—Isaya 48:17.

12. Tuna uhuru gani wa kuchagua ndani ya mipaka ya sheria za Mungu?

12 Wakati ule ule, sheria za Mungu huruhusu uhuru mkubwa wa kuchagua ndani ya mipaka yazo. Hiyo hutokeza unamna-namna na kufanya familia ya kibinadamu ivutie. Fikiria zile aina mbalimbali za vyakula, mavazi, muziki, sanaa, na makao kotokote ulimwenguni. Hakika sisi hupendelea kuwa na uchaguzi wetu katika mambo hayo badala ya kuwa na mtu mwingine akituamulia.

13. Ni sheria gani za maumbile ambazo lazima tutii kwa manufaa yetu?

13 Hivyo tuliumbwa tufurahi kabisa tutiipo sheria za Mungu za kuongoza mwenendo wa kibinadamu. Ni kama kutii sheria za Mungu za maumbile. Mathalani, tukipuuza sheria ya nguvu za uvutano na kuruka kutoka mahali palipo juu, tutaumia au tutakufa. Tukipuuza sheria za ndani ya mwili wetu na kuacha kula chakula, kunywa maji, au kupumua hewa, tutakufa.

14. Twajuaje kwamba wanadamu hawakuumbwa wajitegemee bila Mungu?

14 Kama ilivyo kweli kwamba tuliumbwa tukiwa na uhitaji wa kutii sheria za Mungu za maumbile, ndivyo tulivyoumbwa tukiwa na uhitaji wa kutii sheria za Mungu za maadili na za kijamii. (Mathayo 4:4) Wanadamu hawakuumbwa wajitegemee bila Mfanyi wao na hata hivyo wafanikiwe. Nabii Yeremia husema hivi: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu. Ee BWANA [Yehova, NW], unirudi.” (Yeremia 10:23, 24) Kwa hiyo katika kila njia wanadamu waliumbwa waishi chini ya utawala wa Mungu, si utawala wao wenyewe.

15. Je! sheria za Mungu zingalikuwa mzigo wenye kulemea kwa Adamu na Hawa?

15 Kutii sheria za Mungu hakungalikuwa mzigo wenye kulemea kwa wazazi wetu wa kwanza. Badala ya hivyo, kungaliendeleza hali njema yao na ile ya familia yote ya kibinadamu. Kama watu wawili wa kwanza wangalikaa ndani ya mipaka ya sheria za Mungu, yote yangalikuwa sawa. Kwa kweli, sasa tungekuwa tukiishi katika paradiso nzuri ajabu ya furaha, tukiwa familia ya kibinadamu iliyoungamanika, yenye upendo! Hakungalikuwako uovu, kuteseka, na kifo.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Muumba aliwapa wanadamu mwanzo mkamilifu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Je! wewe ungependa kuendesha gari katika barabara yenye magari mengi ikiwa hakungekuwako sheria za kuongoza magari?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki