Mipaka ya Uhuru
“Hakuna watu walio katika utumwa usio na tumaini kama wale wanaojidanganya kwa kuamini kwamba wako huru.”—Goethe.
UHURU! Neno hilo linavuma kwa nguvu. Lakini lina maana gani kwako? Je! uhuru unamaanisha kwamba una haki kamili ya kutenda kama upendavyo, katika wakati au mahali upendapo, bila kujali watu wale wengine? Bila shaka sivyo! Mipaka inawekwa juu ya vitendo vyako na mabaraza yenye kutunga sheria ili kulinda haki na mapendezi ya watu wale wengine. Je! jambo hilo halihitajiwi kabisa wakati watu wanapoishi pamoja wakiwa jamii?
Kwa mfano, huenda ukawa na uhuru wa kusafiri, lakini unaweza kuendesha gari lako bila kuipita mipaka iliyowekwa na sheria. Mipaka hiyo, au sheria, iliimarishwa iwe ulinzi si kwa wengine tu, bali pia kwako. Basi, uhuru wa kweli haumaanishi kutokuweza kuwekewa kizuizi, kupewa nidhamu, na kujinyima; wala haumaanishi kutokuwapo kwa sheria zinazofaa na zenye kufaidi. Jambo la kupendeza ni kwamba, kamusi Black’s Law Dictionary inafafanua neno uhuru hivi:
“Hali ya kuwa huria . . . bila kuchunguzwa zaidi, kuzuiwa, au kukatazwa jambo zaidi ya kule kunakoweza kuwekwa na sheria za haki zilizo za lazima na wajibu mbalimbali wa maisha ya kijamii.”
Ili tufurahie uhuru, ni lazima tuendeshe maisha zetu kwa njia isiyoruka mipaka miwili—sheria za kiasili na za kiadili.
Sheria za Kimwili Zinawekea Mwanadamu Mipaka
Haiwezekani mwanadamu ye yote awe na uhuru wote kabisa kabisa hata kama akijitenga awe peke yake katika kisiwa kidogo sana katikati ya bahari kubwa sana. Madai ya kiasili ambayo mwili wake utafanya, na tegemeo lake juu ya mazingira, yangeweka mipaka fulani juu ya uhuru wake. Muumba, Yehova Mungu, ameimarisha mipaka hiyo ya kiasili kisha akaimarisha mingine kupitia sheria na kanuni zake.—Matendo 17:26-28.
Mungu alianzisha utendaji wa sheria za kimwili zinazodumisha ulimwengu wote katika upatani wa ajabu. Sheria hizo zinatufaidi sisi. Kwa mfano, je! wewe unajisikia ukidhulumiwa na sheria-asili ya nguvu za uvutano aliyoweka Mungu? Bila shaka sivyo! Hiyo ndiyo kani inayohitajiwa sana ambayo inafanya ulimwengu wote ushikamane na kukuzuia wewe usiruke utoke duniani.
Lakini, namna gani kama ungepuuza kwa makusudi sheria ya uvutano kisha uruke chini ukiwa kwenye genge la futi 100? Ungeanguka ufe au sivyo uumie vibaya. Matokeo: si uhuru bali ni ongezeko la mipaka ya uhuru wako. Hatuwezi kukosa kujali sheria za kimwili tusipatwe na adhabu. Hata hivyo, tunapofanya kazi bila kuruka mipaka yazo, tunavuna faida nyingi.
Sheria za Kuweka Mipaka ya Mwenendo
Karibu miaka 300 iliyopita, John Locke mwanafalsafa Mwingereza alitoa muhtasari wa mambo ambayo huenda wewe ukawa umegundua juu ya uhuru na sheria ya kibinadamu. Aliandika hivi: “Mahali pasipo na sheria hapana uhuru. Kwa maana uhuru ni kuwa bila kuwekewa kizuizi wala kutendwa jeuri na watu wale wengine, na haiwezi kuwa hivyo mahali pasipo na sheria; na kama tunavyoambiwa, huo si ‘uhuru wa kwamba kila mtu afanye anavyotaka.’ Kwa maana ni nani angeweza kuwa huru, hali anaweza kugandamizwa na kila la mapendezi ya mtu mwingine?”
Maneno hayo yanafaa kama nini yanapotumiwa kuhusu sheria za kibinadamu zinazoweka mipaka isirukwe na mwenendo wenye madhara! Kama mwanadamu anaona uhitaji wa sheria ya kusimamia mwenendo wa kijamii, je, Muumba wake pia anaweza kuwa hajauona uhitaji huo? Je, tufikiri kwamba Mungu angesababisha kuwako kwa sheria za kimwili lakini awaache wanadamu bila sheria za kuongoza mwenendo wao? Hata kidogo.—Mathayo 6:8.
Sheria za Muumba kwa wanadamu zimeandikwa na kuhifadhiwa ili tuweze kujua njia bora zaidi ya kushughulikia mambo yetu. (2 Timotheo 3:16, 17) Juu ya ubora wazo, The Bible in Living English inasema: “Maelekezo ya Yehova hayakosei, yanarudisha uzima; masomo ya Yehova yanastahili kutumainiwa, yanawaangazia nuru wajinga; maagizo Yehova yanakubalika, yanafurahisha mioyo; amri ya Yehova ni nyofu, inang’arisha macho.”—Zaburi 19:7, 8.
Mtu anayejaribu kuishi bila mipaka yo yote inayofaa ya kiadili ni kama merikebu ambayo imepoteza dira na hata usukani. Mtu huyo merikebu pia anapeperushwa-peperushwa ni lazima apate njia inayomwelekeza kwenye usalama au sivyo matokeo yatakuwa yenye msiba. Basi, jambo hilo linatokeza ulizo zito. Je! tunaweza kuongoza maisha yetu kwa usalama pasipo kumtegemea Mungu?