Sehemu ya 9
Jinsi Sisi Tujuavyo Kwamba Tumo Katika “Siku za Mwisho”
1, 2. Sisi tunaweza kujuaje kama tumo katika siku za mwisho?
SISI tunaweza kuwaje na hakika kwamba tunaishi katika wakati ambapo Ufalme wa Mungu utachukua hatua dhidi ya mfumo huu uliopo wa utawala wa kibinadamu? Tunaweza kujuaje kwamba tuko karibu sana na wakati ambapo Mungu ataleta mwisho wa uovu na kuteseka kote?
2 Wanafunzi wa Yesu Kristo walitaka kujua mambo hayo. Walimwuliza “ishara” ingekuwa nini ya kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme na ya “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, NW) Yesu alijibu kwa kuwapa mambo mengi hata yale madogomadogo juu ya matukio na hali ambazo zingeungana pamoja kuonyesha kwamba ainabinadamu ilikuwa imeingia “wakati wa mwisho,” “siku za mwisho” za huu mfumo wa mambo. (Danieli 11:40; 2 Timotheo 3:1) Je! sisi katika karne hii tumeona ishara hiyo yenye mambo mengi? Ndiyo, tumeona, kwa wingi sana!
Vita vya Ulimwengu
3, 4. Vita vya karne hii vinapatanaje na unabii wa Yesu?
3 Yesu alitabiri kwamba ‘taifa lingeinuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme.’ (Mathayo 24:7, NW) Katika 1914 ulimwengu ulipata kuhusika katika vita ambayo iliona kukusanywa na kutayarishwa kwa mataifa na falme kwa ajili ya vita kwa njia ambayo ilikuwa tofauti na vita yoyote kabla yayo. Katika kutambua uhakika huo, wanahistoria wakati huo waliiita hiyo Vita Kuu. Ilikuwa ndiyo vita ya kwanza ya aina yake katika historia, vita ya kwanza ya ulimwengu. Askari na raia wapatao 20,000,000 walipoteza maisha zao, wengi sana kuliko katika vita yoyote iliyotangulia.
4 Vita ya Ulimwengu 1 ilionyesha mwanzo wa siku za mwisho. Yesu alisema kwamba tukio hilo na mengine yangekuwa “mwanzo wa utungu.” (Mathayo 24:8) Hiyo ilithibitika kuwa kweli, kwa kuwa Vita ya Ulimwengu 2 ilikuwa yenye kufisha zaidi, askari na raia wapatao 50,000,000 wakipoteza maisha zao. Katika karne hii ya 20, watu zaidi ya 100,000,000 wameuawa katika vita, wengi zaidi ya mara nne ya waliouawa katika miaka 400 iliyotangulia wakijumlishwa pamoja! Ni lawama baya kama nini kwa utawala wa kibinadamu!
Shuhuda Nyinginezo
5-7. Ni zipi baadhi ya shuhuda nyinginezo kwamba tuko katika siku za mwisho?
5 Yesu alitia ndani mambo mengine ambayo yangeandamana na siku za mwisho: “Kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi; na njaa na tauni [mweneo mkubwa wa magonjwa] mahali mahali.” (Luka 21:11) Hiyo hupatana vizuri na matukio tangu mwaka 1914, kwa kuwa kumekuwako ongezeko kubwa sana katika dhiki kutokana na misiba hiyo.
6 Matetemeko makubwa ya nchi ni matukio ya kawaida, yakiangamiza maisha nyingi. Homa ya Kihispania pekee iliua watu wapatao 20,000,000 kufuata Vita ya Ulimwengu 1—makadirio kadhaa yakiwa 30,000,000 au zaidi. UKIMWI umeangamiza mamia ya maelfu ya maisha na ungeweza kuangamiza mamilioni zaidi katika wakati ujao ulio karibu. Kila mwaka mamilioni ya watu hufa kwa maradhi ya moyo, kansa, na magonjwa mengine. Mamilioni zaidi hufa kile kifo cha polepole cha njaa. Pasipo shaka wale ‘wapanda farasi wa Apokalipsi (Ufunuo)’ wakiwa na vituko vyao vya vita, upungufu wa chakula, na mieneo mikubwa ya magonjwa wamekuwa wakiua idadi kubwa za familia ya kibinadamu tangu 1914.—Ufunuo 6:3-8.
7 Yesu alitabiri pia ongezeko la uhalifu ambao unapata wengi katika nchi zote. Alisema: “Kwa sababu ya kuongezeka maasi, upendo wa wengi utapoa.”—Mathayo 24:12.
8. Unabii kwenye 2 Timotheo sura ya 3 unapatanaje na wakati wetu?
8 Zaidi, unabii wa Biblia ulitabiri kuharibika kwa maadili ambako kunaoonekana sana kotekote ulimwenguni leo: “[Katika] siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; . . . Watu wabaya na wadanganyaji wataendelea na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika.” (2 Timotheo 3:1-13) Yote hayo yametimia mbele hasa ya macho yetu.
Jambo Jingine
9. Kulitukia nini mbinguni wakati uleule wa kuanza kwa siku za mwisho duniani?
9 Kuna jambo jingine lenye kusababisha ongezeko kubwa mno la kuteseka katika karne hii. Wakati uleule wa mwanzo wa siku za mwisho katika mwaka 1914, jambo fulani lilitukia kuweka ainabinadamu katika hatari kubwa hata zaidi. Katika wakati huo, kama vile unabii katika kile kitabu cha mwisho cha Biblia kisimuliavyo: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli [Kristo katika mamlaka ya kimbingu] na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake [wale roho waovu]; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.”—Ufunuo 12:7-9.
10, 11. Ainakibinadamu iliathiriwaje wakati Shetani na roho waovu wake walipotupwa kwenye dunia?
10 Matokeo yalikuwa nini kwa familia ya kibinadamu? Unabii huo huendelea hivi: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” Ndiyo, Shetani ajua kwamba mfumo wake unakaribia mwisho wao, hivyo anafanya yoteyote awezayo kugeuza wanadamu dhidi ya Mungu kabla yeye na ulimwengu wake haujaondolewa mbali. (Ufunuo 12:12; 20:1-3) Viumbe hao wa roho ni wapotovu kama nini kwa sababu walitumia vibaya hiari yao! Hali duniani zimekuwa mbaya kama nini chini ya uvutano wao, hasa tangu 1914!
11 Si ajabu kwamba Yesu alitabiri juu ya wakati wetu hivi: “Duniani huzuni kuu ya mataifa, yasijue njia ya kutokea . . . Watu wakizirai kwa sababu ya woga na taraja la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa.”—Luka 21:25, 26, NW.
Mwisho wa Utawala wa Kibinadamu na wa Roho Waovu U Karibu
12. Ni nini mmojawapo unabii wa mwisho unaobaki kutimizwa kabla ya ukomo wa mfumo huu?
12 Ni unabii wa Biblia mwingi kadiri gani unaobaki kutimizwa kabla Mungu hajaharibu mfumo huu uliopo? Ni mchache sana! Mmojawapo wa mwisho uko kwenye 1 Wathesalonike 5:3, ambao hutaarifu hivi: “Wakati wanapoongea juu ya amani na usalama, mara moja msiba u juu yao.” (The New English Bible) Hiyo yaonyesha kwamba mwisho wa ulimwengu huu utaanza “wakati wanapoongea.” Bila ulimwengu kutangulia kuutazamia, uharibifu utafyatuka wakati usipotarajiwa hata kidogo, wakati fikira za wanadamu ziko juu ya amani na usalama wao wanaoutumainia.
13, 14. Ni wakati gani wa taabu alioutabiri Yesu, nao utamaliziaje?
13 Ulimwengu huu ulio chini ya uvutano wa Shetani unaishiwa na wakati. Karibuni utakuja kwenye mwisho wao katika wakati wa taabu ambao Yesu alisema juu yao: “Wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.”—Mathayo 24:21.
14 Upeo wa “dhiki kubwa” utakuwa vita ya Mungu ya Har–Magedoni. Huo ndio wakati alionena juu yao nabii Danieli wakati Mungu ‘atavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu.’ Hiyo itamaanisha mwisho wa tawala zote za kibinadamu zilizopo zenye kujitegemea bila Mungu. Ndipo utawala wa Ufalme wake kutoka mbinguni utakapochukua udhibiti kamili wa mambo yote ya kibinadamu. Danieli alitabiri kwamba mamlaka ya kutawala haitaachiwa “watu wengine” tena kamwe.—Danieli 2:44; Ufunuo 16:14-16.
15. Ni nini litakalopata uvutano wa Shetani na roho waovu wake?
15 Wakati huo uvutano wote wa kishetani na kimashetani utakoma pia. Viumbe-roho hao waasi wataondolewa mbali ili wasiweze “kuwadanganya mataifa tena.” (Ufunuo 12:9; 20:1-3) Wamehukumiwa kifo na wanangojea uharibifu. Kitakuwa kitulizo kama nini kwa ainabinadamu kuwa huru na uvutano wao wenye kupotosha!
Ni Nani Wataokoka? Ni Nani Hawataokoka?
16-18. Ni nani ambao wataokoka mwisho wa mfumo huu, na ni nani ambao hawataokoka?
16 Hukumu za Mungu zitekelezwapo dhidi ya ulimwengu huu, ni nani wataokoka? Ni nani hawataokoka? Biblia huonyesha kwamba wale ambao wanataka utawala wa Mungu watalindwa na kuokoka. Wale ambao hawataki utawala wa Mungu hawatalindwa bali wataharibiwa pamoja na ulimwengu wa Shetani.
17 Mithali 2:21, 22 husema: “Wanyofu [wale ambao hujitiisha chini ya utawala wa Mungu] watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu [wale ambao hawajitiishi chini ya utawala wa Mungu] watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”
18 Zaburi 37:10, 11 pia husema hivi: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” Mstari wa 29 huongeza: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”
19. Ni shauri gani ambalo twapaswa kuzingatia moyoni?
19 Yatupasa kuzingatia moyoni shauri la Zaburi 37:34, ambalo hutaarifu: “Wewe umngoje BWANA [Yehova, NW], ushike njia yake, naye atakutukuza urithi nchi, wasio haki watakapoharibiwa utawaona.” Mistari 37 na 38 husema hivi: “Umwangalie sana mtu mkamilifu, umtazame mtu mnyofu, maana mwisho wake mtu huyo ni amani. Wakosaji wataangamizwa pamoja, wasio haki mwisho wao wataharibiwa.”
20. Kwa nini twaweza kusema kwamba hizi ni nyakati zenye kusisimua ambamo tunaishi?
20 Inafariji kama nini, ndiyo, inatumainisha kama nini kujua kwamba Mungu ajali kweli kweli na kwamba karibuni yeye atakomesha uovu na kuteseka kote! Inasisimua kama nini kujua kwamba utimizo wa unabii huo mtukufu u karibu sana!
[Picha katika ukurasa wa 20]
Biblia ilitabiri matukio ambayo hujumuika kuwa “ishara” ya siku za mwisho
[Picha katika ukurasa wa 22]
Karibuni, kwenye Har–Magedoni, wale ambao hawajitiishi chini ya utawala wa Mungu watakatiliwa mbali. Wale ambao hujitiisha wataokoka kuingia ndani ya ulimwengu mpya wenye uadilifu