Furahia Maisha ya Familia
Familia zaweza kuwa na furaha kweli?
Hilo lawezekanaje?
Je! unajua familia zozote zilizo na umoja na furaha kama zile zinazoonekana katika trakti hii? Kila mahali familia zinavunjika. Talaka, ukosefu wa uhakika wa kazi, matatizo ya mzazi-mmoja, mfadhaiko—yote hayo huchangia tatizo. Mstadi wa maisha ya familia aliomboleza: “Kufikia sasa, matabiri ya kutoweka kwa familia yanajulikana na kila mtu.”
Kwa nini familia leo zinapatwa na matatizo mazito kama hayo? Twaweza kufurahiaje maisha ya familia?
Jinsi Familia Ilivyoanza
Ili kujibu maswali hayo, twahitaji kujua chanzo cha ndoa na familia. Kwa kuwa ikiwa vitu hivyo vilikuwa na Mwanzilishi—Muumbaji—washiriki wa familia wanapaswa wamtegemee yeye ili kupata mwongozo, kwa kuwa kwa hakika angejua vizuri zaidi jinsi tunavyoweza kufurahia maisha ya familia kwa ukamili.
Kwa kushangaza, wengi huamini kwamba mpango wa familia haukuwa na Mwanzilishi. The Encyclopedia Americana husema: “Wasomi fulani wana mwelekeo wa kuonyesha kwamba chanzo cha ndoa ni kama ilivyo mipango ya wanyama walio chini ya mwanadamu ya kutafuta kuwa wawili wawili.” Hata hivyo, Yesu Kristo alisema juu ya uumbaji wa mwanamume na mwanamke. Alinukuu kuwa mamlaka maandishi ya mapema ya Biblia na kusema: “Aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.”—Mathayo 19:4-6.
Kwa hiyo Yesu Kristo hakosei. Mungu mweledi aliumba wanadamu wa kwanza akapanga kuwe maisha ya familia yenye furaha. Mungu aliwaleta pamoja wale wawili wa kwanza katika ndoa kisha akasema kwamba mwanamume “ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:22-24) Je! basi, ingeweza kuwa kwamba matatizo ya leo ya familia yanasababishwa na kufuatilia mitindo ya maisha ambayo hukiuka viwango vilivyowekwa na Muumba katika Neno lake, Biblia?
Ni Njia Ipi ya Kufaulu?
Bila shaka kama unavyojua, ulimwengu wa kisasa huchochea kujipendeza mwenyewe na kujitimizia mambo mwenyewe. “Pupa inafaa,” mwanauchumi mmoja akaliambia darasa la chuo lenye kuhitimu katika United States. “Unaweza kuwa mwenye pupa na bado ujihisi vizuri.” Lakini kufuatia vitu vya kimwili hakuongozi kwenye kufaulu. Kwa kweli, ufuatiaji wa vitu vya kimwili, ni mojapo vitisho vikubwa kwa maisha ya familia kwa sababu huingilia mahusiano ya kibinadamu na hunyang’anya watu wakati na pesa. Kinyume cha hilo, hebu fikiria jinsi mithali mbili tu za Biblia hutusaidia kuona jambo lililo la maana ili kupata furaha.
“Afadhali kula mboga pamoja na watu unaopenda kuliko kula nyama bora penye chuki.”
“Afadhali kula ganda kavu la mkate ukiwa na amani ya akili kuliko kuwa na karamu nono katika nyumba yenye kujaa matatizo.”
Mithali 15:17; 17:1, “Today’s English Version.”
Mithali hizo ni zenye nguvu, sivyo? Hebu fikiria jinsi ulimwengu ungekuwa tofauti kama kila familia ingeshikilia kanuni hizo! Biblia pia huandaa mwongozo wenye thamani wa jinsi washiriki wa familia wanavyopaswa kutendeana wao kwa wao. Fikiria mielekezo michache tu inayotoa.
Waume: ‘Mpende mke wako kama mwili wako mwenyewe.’—Waefeso 5:28-30.
Sahili, lakini ni jambo linalowezekana! Biblia pia humwelekeza mume ‘amheshimu mke wake.’ (1 Petro 3:7) Yeye hufanya hivyo kwa kumpa uangalifu wa pekee, kutia ndani wororo, uelewevu, na uhakikishio. Pia huthamini maoni ya mke na kumsikiliza. (Linganisha Mwanzo 21:12.) Je! hukubali kwamba familia yoyote itanufaika ikiwa mume atamtendea mke wake kwa ufikirio, kama vile yeye mwenyewe angetaka atendewe?—Mathayo 7:12.
Wake: “Mke asikose kumstahi mumewe.”—Waefeso 5:33.
Mke huchangia furaha ya familia kwa kusaidia mume wake atimize madaraka yake mazito. Hilo ndilo lililokusudiwa, kwa kuwa Mungu aliandaa mke kuwa “msaidiaji kwa ajili yake, awe kikamilisho chake.” (Mwanzo 2:18, New World Translation) Je! unaweza kuwazia baraka zinazoweza kuyajia maisha ya familia wakati mke anapomwonyesha mume wake staha kwa kuunga mkono maamuzi yake na kushirikiana naye katika kutekeleza miradi ya familia?
Wenzi wa Ndoa: “Ni lazima waume na wake wawe waaminifu kwa kila mmoja na mwenzake.”—Waebrania 13:4, TEV.
Wanapokuwa waaminifu, maisha ya familia kwa hakika yatanufaika. Mara nyingi uzinzi huharibu kabisa familia. (Mithali 6:27-29, 32) Kwa hiyo, Biblia huhimiza kwa hekima: “Uwe na furaha pamoja na mke wako na uone shangwe pamoja na msichana uliyeoa . . . Kwa nini umpe mwanamke mwingine upendo wako?”—Mithali 5:18-20, TEV.
Wazazi: “Leeni [watoto] wenu katika njia iwapasayo [wao].”—Mithali 22:6.
Wazazi wanapotoa uangalifu na wakati kwa watoto, maisha ya familia bila shaka yatakuwa na maendeleo. Hivyo, Biblia huhimiza wazazi wawafundishe watoto wao kanuni zilizo sawa ‘waketipo katika nyumba zao, na watembeapo njiani, walalapo na waondokapo.’ (Kumbukumbu la Torati 11:19) Biblia pia husema wazazi wanapaswa kuonyesha wanawapenda watoto wao kwa kuwatia nidhamu.—Waefeso 6:4.
Watoto: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana.”—Waefeso 6:1.
Ni kweli katika ulimwengu huu usiofuata sheria, si rahisi sikuzote kutii wazazi wako. Hata hivyo, je! hukubali kwamba ni jambo la hekima kufanya yale ambayo Mwanzilishi wa familia anatuambia? Yeye ajua kinachofaa kabisa kufanya maisha ya familia yetu kuwa yenye furaha zaidi. Kwa hiyo jitahidi kuwatii wazazi wako. Azimia kuepuka vishawishi vingi vya ulimwengu vya kufanya mabaya.—Mithali 1:10-19.
Maisha ya familia yatanufaika kwa kadiri ambayo kila mshiriki wa familia anatumia mashauri ya Biblia. Familia itafurahia maisha bora sasa na pia itakuwa na tazamio la wakati ujao ulio mzuri ajabu katika ule ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Kwa hiyo lifanyeni kuwa zoea la familia kujifunza Biblia pamoja! Mamilioni ya familia ulimwenguni pote yameuona kuwa wenye manufaa ya kweli ule mwongozo unaopatikana katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia.
Isipokuwa iwe imeonyeshwa vingine, manukuu yote ya Biblia yametolewa katika Union Version ya Kiswahili.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]
Sifa Kwa Ajili ya Picha: Wanasimba: Hisani ya Mbuga ya Hartebeespoortdam ya Nyoka na Wanyama.