Neno la Mungu Li Hai
Namna ya Kufurahia Maisha Yenye Furaha ya Jamaa
JE! ULIJUA kwamba Neno la Mungu linaweza kukusaidia ufurahie maisha yenye furaha ya jamaa? Mashauri inayotolea washiriki wa jamaa yakifuatwa, faida zitakuwa kubwa. Je! wewe ni mume? Ikiwa ndivyo, angalia yale unayoambiwa na Neno la Mungu.
UWE MWAMINIFU KWA MKE WAKO
“Waume, pendeni wake zenu,” Biblia inahimiza. “Uwe mwenye furaha pamoja na mke wako na upate furaha yako pamoja na yule msichana uliyeoa. . . . Mbona umpe mwanamke mwingine upendo wako? Mbona upendelee madaha ya mke wa mwanamume mwingine?”—Waefeso 5:25, 28; Mithali 5:18-20, Today’s English Version.
Ikiwa mume atatii shauri hilo la Biblia, litasaidia kuletea jamaa furaha. Pia, mke wake atatiwa moyo atumie mashauri ya Biblia hata yeye. Wake wanahimizwa wafanye nini?
HESHIMU MUME WAKO
“Mke asikose kumstahi mumewe,” Neno la Mungu linasema. (Waefeso 5:33) Kukosa kwa wanawake walioolewa kutii shauri hilo ni moja ya sababu kubwa zinazofanya waume fulani waonee uchungu wake zao. Mke anaonyesha heshima kwa kuunga mkono maamuzi ya mume wake na kumwonyesha ushirikiano wa nafsi yote. Mke akitimiza daraka alilogawiwa na Biblia kuwa ‘msaidiaji na kikamilisho’ cha mumewe, anafanya iwe rahisi mumewe kumpenda.—Mwanzo 2:18, NW.
Wakati watoto wanapozaliwa ndani ya jamaa fulani, wanapasa kupewa malezi gani? Ni mashauri gani ambayo Neno la Mungu linawapa wazazi?
TUMIENI WAKATI MKISHINDA NA WATOTO NA KUWATIA NIDHAMU (ADABU)
Kwa kuwa ninyi ni wazazi, mnahitaji kuwa pamoja na watoto wenu, kushinda mkiwa nao na kuwapa mafundisho yenye mafaa kutokana na Neno la Mungu. (Kumbukumbu la Torati 11:19) Sehemu ya mafundisho hayo inapasa kuwa ya kuwatia adabu. “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto,” Biblia inaeleza, lakini “fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.” Utoaji wa nidhamu (adabu), hata kama unatia ndani kuchapa mtoto, ni ushuhuda wenye kuonyesha kwamba mzazi anapenda mtoto wake, kama vile Biblia inavyosema: “Yeye ampendaye [mwanaye] humrudi mapema.”—Mithali 22:15; 13:24; 23:13, 14; Waefeso 6:4.
Tabia za watoto zinaamuliwa sana pia na hali ya jamaa, kama ni yenye furaha au haina furaha. Neno la Mungu linawahimiza wafanye nini?
TIINI WAZAZI WENU
Biblia inasema: “Watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki.” Jambo hilo lina uzito gani? Mithali ya Biblia inaonyesha, kwa kusema: “Jicho la mtu amdhihakiye babaye, na kudharau kumtii mamaye; kunguru wa bondeni wataling’oa, na vifaranga vya tai watalila.” Kama unavyoweza kuona, kutii na kuheshimu wazazi wako ni jambo lisilo la mchezo hata kidogo mbele za Mungu.—Waefeso 6:1; Mithali 30:17.
Je! wewe kweli unataka kufurahia maisha yenye furaha ya jamaa? Unaweza kuyafurahia. Njia ya kuyapata si siri. Muumba wa jamaa alitoa mwongozo wa kufanikisha maisha ya jamaa. Ikiwa kila mshiriki wa jamaa atajifunza na kufuata mashauri ya Mungu, kwa uhakika jamaa itakuwa yenye furaha.