Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 9 kur. 108-117
  • Neno la Yehova Laendelea Kusonga Mbele Kasi (1976-1992)

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Neno la Yehova Laendelea Kusonga Mbele Kasi (1976-1992)
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Marekebisho Mapya ya Kitengenezo
  • Kutimiza Mahitaji ya Kiroho kwa Fasihi ya Biblia
  • Programu za Elimu Zapanuliwa na Kufanywa Kuwa za Namna-Namna
  • Vifaa vya Kutimiza Mahitaji ya Ukuzi
  • Kutunza Makutaniko na Kazi ya Kueneza Evanjeli
  • “Kikundi cha Watu Kilicho Chake Mwenyewe Peke Yake”
  • Kujulisha Habari Njema Bila Kuacha (1942-1975)
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Usitawi wa Muundo wa Tengenezo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 9 kur. 108-117

Sura ya 9

Neno la Yehova Laendelea Kusonga Mbele Kasi (1976-1992)

“Hatimaye, ndugu, endelezeni sala kwa ajili yetu, ili neno la Yehova liweze kuzidi kusonga mbele kasi [au, ‘liweze kuwa likikimbia’] na kuwa likitukuzwa kama kwa kweli lilivyo kwenu.” —2 The. 3:1, “Kingdom Interlinear.”

KWA maneno hayo mtume Paulo aliomba waamini wenzake katika Thesalonike wasali kwamba yeye na waandamani wake waweze kuwa na mafanikio katika kupiga mbiu ya neno la Yehova bila kizuizi. Yehova alijibu sala hiyo. Lakini hiyo haimaanishi kwamba mtume huyo hakulazimika kushughulika na matatizo. Alikabili upinzani mkali kutoka kwa ulimwengu na akalazimika kushughulika na ndugu bandia waliofanya mambo kwa udanganyifu. (2 Kor. 11:23-27; Gal. 2:4, 5) Hata hivyo, yajapokuwa hayo, baada ya miaka kumi hivi, Paulo angeweza kuandika kwamba likiwa tokeo la baraka ya Mungu, habari njema zilikuwa ‘zikizaa matunda na kukua katika ulimwengu wote.’—Kol. 1:6.

Katika hali inayofanana na hiyo katika siku zetu—lakini kwa kadiri isiyopata kamwe kuonwa—habari njema inazaa matunda. Watu zaidi wanafikiwa kwa habari njema na wanaikubali kwa moyo kuliko wakati wowote uliopita. Utimizo wa yale yaliyotabiriwa na Neno la Mungu unasonga mbele kasi, kama mkimbiaji katika mashindano ya mbio.—Isa. 60:22.

Marekebisho Mapya ya Kitengenezo

Kufikia 1976, Ndugu Knorr alikuwa amefanya kazi kwa bidii yenye kuendelea akiwa msimamizi wa Watch Tower Society kwa zaidi ya miongo mitatu ya miaka. Alikuwa amesafiri duniani pote mara nyingi tena na tena, akizuru na kutia moyo wamishonari, akifundisha na kutoa maagizo kwa wafanyakazi wa ofisi za tawi. Alikuwa na pendeleo la kuona idadi ya Mashahidi wenye bidii ikiongezeka kutoka 117,209 katika 1942 hadi 2,248,390 katika 1976.

Lakini kufikia kiangazi cha 1976, N. H. Knorr mwenye umri wa miaka 71 alikuwa ameona kwamba alikuwa na mwelekeo wa kugonga vitu apitapo. Machunguzi yaliyofuliza yalionyesha kwamba alikuwa na uvimbe ubongoni usioweza kupasuliwa. Aling’ang’ana ili aendelee kubeba mzigo wa kazi kwa miezi fulani, lakini hakukuwa na matumaini kuwa afya yake ya kimwili ingepata nafuu. Je, afya yake yenye kudhoofika ingepunguza mwendo wa kusonga mbele wa kazi?

Katika 1971 washiriki wa Baraza Linaloongoza walikuwa wamekwisha kuanza kuongezwa. Wakati wa 1975, walikuwako washiriki 17. Muda ulio mwingi katika mwaka huo, Baraza Linaloongoza lilikuwa limefikiria kwa uzito na kwa sala jinsi wangeweza kutunza vizuri zaidi yote yaliyohusika katika kazi ya kuhubiri na kufundisha duniani pote iliyoelezwa katika Neno la Mungu kwa siku zetu. (Mt. 28:19, 20) Desemba 4, 1975, Baraza Linaloongoza lilikubali kwa umoja mojayapo marekebisho mapya ya maana zaidi ya kitengenezo katika historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova.

Kuanzia Januari 1, 1976, utendaji wote wa Watch Tower Society na wa makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova duniani kote ulikuwa umeletwa chini ya uangalizi wa halmashauri sita za usimamizi wa Baraza Linaloongoza. Kupatana na mpango huo, Februari 1, 1976, mabadiliko yalikuwa yameanza kufanya kazi katika matawi yote ya Sosaiti duniani kote. Kila tawi halikusimamiwa tena na mwangalizi mmoja wa tawi, bali wanaume watatu au zaidi waliokomaa walitumikia wakiwa Halmashauri ya Tawi, mshiriki mmoja akitumikia akiwa mratibu wa kudumu.a Baada ya halmashauri hizo kuwa zimekuwa zikitenda kwa miezi kadhaa, Baraza Linaloongoza lilionelea hivi: “Limethibitika kuwa jambo lenye kunufaisha kuwa na idadi fulani ya ndugu wakishauriana pamoja kufikiria masilahi ya kazi ya Ufalme.—Mit. 11:14; 15:22; 24:6.”

Katika vuli ya 1976, ujapokuwa uhakika wa kwamba hakukuwa na matumaini ya kuwa afya yake ya kimwili ingepata nafuu, Ndugu Knorr alishiriki kutoa maagizo yaliyotolewa kwenye mikutano iliyofanywa kwenye makao makuu pamoja na washiriki wa Halmashauri za Tawi na wafanyakazi wengine wa tawi kutoka ulimwenguni pote. Kuongezea kushiriki katika mikutano wakati wa mchana, Ndugu Knorr alialika ndugu hao kwenye chumba chake jioni wakiwa vikundi vidogovidogo. Kwa njia hiyo yeye na Audrey, mke wake, walikuwa na ushirika wa karibu na wanaume hao waliomjua na kumpenda na ambao alikuwa ameshughulika nao kwa ukaribu sana kwa miaka iliyopita. Kufuata mikutano hiyo, afya ya Ndugu Knorr ilizidi kudhoofika mpaka kifo chake Juni 8, 1977.

Juni 22, 1977, majuma mawili baada ya kifo cha Ndugu Knorr, Frederick W. Franz mwenye umri wa miaka 83 alichaguliwa kuwa msimamizi wa Watch Tower Society. Kuhusu Ndugu Franz, gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Oktoba 1, 1977, lilitaarifu hivi: “Yeye ni mwenye sifa nyingi sana ya kujifunza sana Biblia na kufanya kazi bila kuchoka kwa ajili ya faida za Ufalme, na kwa sababu hiyo ametumainiwa na kuungwa mkono na Mashahidi wa Yehova kila mahali.”

Kufikia wakati huo wa badiliko, mipango mipya ya kitengenezo iliyohakikisha kusonga mbele kwa kazi ilikuwa tayari inatenda kazi.

Kutimiza Mahitaji ya Kiroho kwa Fasihi ya Biblia

Mashahidi wa Yehova walikuwa wamelishwa vizuri kabla ya 1976. Lakini uchunguzi wa yale ambayo yametokea tangu mwaka huo chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza na Halmashauri ya Uandishi yayo hufunua kwamba maji ya kweli yametiririka nje kwa kiasi kilichozidi kuongezeka na cha namnanamna zaidi.

Vingi kati ya vichapo vilivyotolewa vimetimiza mahitaji hususa ya Mashahidi wenyewe. Hangaikio la pekee lilionyeshwa kwa vijana. Ili kusaidia vijana watumie kanuni za Biblia katika hali walizokabili maishani, kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako (Kiingereza) kilitangazwa katika 1976, na Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, katika 1989. Kile kichapo chenye picha Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, kilichotayarishwa kwa kufikiria watoto, kilitolewa katika 1978. Mwaka uo huo shauri na mwongozo kwa ajili ya kuimarisha familia vilitolewa katika kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha.

Nyakati nyingine, mahitaji hususa ya watu wa Yehova yameshughulikiwa kwa njia ya shauri la wakati wake katika kurasa za Mnara wa Mlinzi. Kwa kielelezo, ripoti ya ulimwenguni pote ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova kwa miaka 1977/78 ilionyesha upungufu wa idadi ya walioshiriki katika kazi ya kuhubiri. Je, upungufu huo ulikuwa kwa sehemu angalau kwa sababu ya kukatishwa tamaa na matarajio kuhusu 1975? Labda. Lakini kulikuwa na mambo mengine yaliyokuwa na mavutano. Ni jambo gani lingeweza kufanywa?

Baraza Linaloongoza lilichukua hatua kuimarisha usadikisho miongoni mwa Mashahidi wa Yehova kwamba kulikuwa na uhitaji wa kuendelea kupiga mbiu ya Ufalme kwa bidii nyumba hadi nyumba. Gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Julai 15, 1979 lilikuwa na makala “Juhudi kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova,” “Kuhubiri Katika Ulimwengu Wenye Uasi,” “Walihubiri Nyumba Hadi Nyumba,” na “Mambo Ambayo Wengine Wamesema juu ya Kutoa Ushahidi Nyumba Hadi Nyumba.” Makala hizo na nyinginezo zilithibitisha upya kwamba kazi ya kuhubiri nyumba hadi nyumba ina msingi imara wa Kimaandiko nazo zilihimiza ushiriki wa bidii na wa moyo wote katika utendaji huu wa maana.b—Mdo. 20:20, NW; Kol. 3:23.

Hali nyingine ilihitaji uangalifu pia. Kufikia 1980, idadi ya watu ambao walikuwa wameshiriki katika utendaji wa Mashahidi wa Yehova kwa miaka fulani, kutia baadhi ya wale waliokuwa wametumikia kwa njia yenye kutokeza katika tengenezo, walikuwa wamekuwa wakijaribu kwa njia mbalimbali kusababisha migawanyiko na kupinga kazi iliyokuwa ikifanywa na Mashahidi wa Yehova. Ili kuimarisha watu wa Yehova dhidi ya mavutano hayo ya uasi-imani, gazeti Mnara wa Mlinzi lilikuwa na makala kama vile “Endeleeni ‘Kuwa Imara Katika Imani’” (Januari 15, 1981 au Agosti 1, 1980, Kiingereza), na “Kuingiza Kisiri-Siri Madhehebu Zenye Kuharibu” (Februari 15, 1984 au Septemba 15, 1983, Kiingereza), na “Kataa Uasi-Imani, Ambatana na Ile Kweli!” (Septemba 1, 1983 au Aprili 1, 1983, Kiingereza), hali kitabu “Ufalme Wako Uje” (1981) kilikazia uhakika wa kwamba Ufalme u karibu, ukiwa umekwisha kusimamishwa mbinguni katika 1914. Baraza Linaloongoza halikuruhusu jitihada za wapinzani ziwakengeushe kutoka lengo la msingi la Mashahidi wa Yehova—kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu!

Hata hivyo, namna gani uhitaji wa Mashahidi wa Yehova wa kuendelea kuongeza ujuzi wao wa kweli ya Biblia? Kwa ajili ya funzo lenye bidii la Biblia, katika 1984 chapa ya marejezo iliyosahihishwa ya New World Translation ilitolewa, ikiwa na marejezo ya pambizoni, vielezi vya chini, na nyongeza yenye habari nyingi. Miaka minne baadaye, katika 1988, watu wa Yehova walisisimuliwa kupokea (katika Kiingereza) kitabu cha maelezo cha kisasa zaidi cha mstari kwa mstari cha Ufunuo, katika kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, pia ile ensaiklopidia ya Biblia yenye mabuku mawili Insight on the Scriptures. Halafu, katika 1991, kilitangazwa kitabu chenye vielezi vizuri sana Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, funzo kamilifu la maisha na mafundisho ya Yesu Kristo.

Lakini namna gani mahitaji ya watu ambao si Mashahidi wa Yehova? Kikiwa chombo cha kutoa maagizo kwa watu wapya wenye kupendezwa, kichapo Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kilitolewa katika 1982. Kilitayarishwa ili kusaidia wanafunzi wa Biblia watimize matakwa ya Yehova kwa ajili ya uhai katika paradiso ya dunia. Ili kusaidia watu ambao huenda wakawa na maswali juu ya chanzo na kusudi la uhai duniani, kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? kiliandaliwa katika 1985. Kilifuatwa, katika 1989, na kile kitabu chenye kutia nguvu imani Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? (Kiingereza).

Watu wanyonge ambao huenda wakahitaji msaada wa pekee kwa sababu ya malezi yao ya kitamaduni au kidini walipewa uangalifu pia. Ili kufundisha kweli juu ya Ufalme wa Yehova kwa wale ambao hawajui kusoma na kuandika au ambao hawasomi vizuri sana, broshua ya kurasa 32 Furahia Milele Maisha Duniani! ilitolewa katika 1982. Kufikia 1992, nakala zaidi ya 76,000,000 zilikuwa zimechapwa, na ilikuwa ikigawanywa katika lugha 200 kote ulimwenguni, hilo likiifanya kuwa kichapo chenye kutafsiriwa zaidi ya vyote cha Watch Tower Society.

Katika 1983, vijitabu vitatu vilitokezwa kwa kusudi pekee la kusaidia Waislamu, Wabuddha, na Wahindu. Ili kufikia watu wenye malezi hayo na mengine ya kidini, inasaidia kuelewa jambo fulani juu ya dini yao—mafundisho na historia yayo. Ili kutimiza uhitaji huo, kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu (Kiingereza) kilitolewa katika 1990.

Baraza Linaloongoza lilipendezwa sana kufikia watu wengi zaidi kadiri ilivyowezekana kwa ujumbe wa Ufalme—watu “wa kila taifa, na kabila, . . . na lugha.” (Ufu. 7:9) Kwa kusudi hilo, mipango ilifanywa ya kutafsiri fasihi katika lugha nyingi zaidi. Kwa kielelezo, kutoka 1976 hadi 1992, kulikuwa ongezeko la asilimia 42 hivi katika hesabu ya lugha ambazo katika hizo gazeti Mnara wa Mlinzi lilitokezwa. Katika Oktoba 1992, hesabu hiyo ilikuwa 111. Ili kufanya iwezekane kutafsiri haraka, mwaka huohuo watafsiri zaidi ya 800 kote ulimwenguni walikuwa wakishiriki katika kazi hiyo.

Programu za Elimu Zapanuliwa na Kufanywa Kuwa za Namna-Namna

Chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza na Halmashauri ya Kufundisha yalo, programu za maagizo kwa ajili ya wafanyakazi wa makao makuu na familia za Betheli katika matawi kote ulimwenguni zilipanuliwa na kupewa unamnanamna mkubwa zaidi. Kuongezea usomaji wa Biblia na Kitabu-Mwaka ikiwa sehemu ya ibada yao ya asubuhi, kulianzishwa uchanganuzi wenye kina wa sehemu ya Biblia iliyosomwa wakati wa juma lililopita na utumizi wa habari hiyo kuwahusu wale watumikiao Betheli. Ripoti za ukawaida kutoka idara mbalimbali za Betheli pamoja na ripoti zilizotolewa mara nyingi zaidi kutoka kwa waangalizi wa kanda ya dunia zilianzishwa pia.

Ili kutimiza mahitaji ya wale wenye madaraka zaidi ndani ya tengenezo, programu zaidi za elimu zilitayarishwa na kuanza kutumiwa. Wakati wa 1977, mipango ilifanywa kwa ajili ya wazee wote wahudhurie mtaala wa saa 15 wa Shule ya Huduma ya Ufalme. (Mdo. 20:28) Tangu wakati huo, vipindi kama hivyo vya urefu tofauti vimepangwa kila miaka michache; na kuanzia 1984, watumishi wa huduma pia walipokea mazoezi katika Shule ya Huduma ya Ufalme. Katika Brooklyn kuanzia Desemba 1977, shule ya pekee ya majuma matano kwa ajili ya washiriki wa Halmashauri ya Tawi ilianza.

Hangaiko la pekee lilionyeshwa pia kwa wale waliokuwa wakijitumikisha katika huduma ya wakati wote wakiwa mapainia. Katika Desemba 1977 Shule ya Utumishi wa Painia, mtaala wa majuma mawili ya mazoezi kwa ajili ya wahudumu mapainia, ilianzishwa Marekani na hatimaye ikaenea sehemu zote za dunia. Wakati wa miaka 14 iliyofuata, idadi ya mapainia iliongezeka zaidi ya mara tano—kutoka 115,389 hadi 605,610!

Katika vuli ya 1987, shule nyingine mpya ilifunguliwa—Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Shule hiyo ilianzishwa ili kuzoeza ndugu waseja wenye kustahili waliokuwa na uzoefu fulani wakiwa wazee au watumishi wa huduma na ambao walikuwa tayari kutumikia kokote kulikokuwa na uhitaji katika shamba la ulimwenguni pote. Kufikia 1992, madarasa yalikuwa yameongozwa katika Australia, Austria, El Salvador, Hispania, Italia, Marekani, Mexico, Nigeria, Sweden, Ufaransa, Uingereza, na Ujerumani. Matokeo yamekuwa, ongezeko la idadi ya wanaume waliostahili ifaavyo kutumikia ndugu zao, wala si jamii ya watu mmoja-mmoja wanaoonwa kuwa bora kuliko wengine kutanikoni.

Ili kuongeza kazi ya duniani pote ya elimu ya Biblia, mikusanyiko ya kimataifa iliratibiwa katika majiji yaliyokuwa mahali penye kufaa—mingine katika nchi ambako Mashahidi wa Yehova walikuwa wamekuwa chini ya marufuku. Mikusanyiko hiyo ilitumika kuimarisha akina ndugu katika maeneo hayo na kutoa kichocheo imara kwa kazi ya kuhubiri habari njema katika nchi hizo.c

Vifaa vya Kutimiza Mahitaji ya Ukuzi

Kadiri ambavyo neno la Yehova lilizidi kusonga mbele kasi, maendeleo yenye kusisimua yakawa yanahitajiwa katika kujenga na kuchapa—nyanja zilizo chini ya uangalizi wa Baraza Linaloongoza na Halmashauri ya Utangazaji yalo.

Mashahidi wenye ustadi katika ujenzi walijitolea utumishi wao mbalimbali, na jitihada zao ziliunganishwa ili kusaidia kujenga vifaa vya tawi vipya na vikubwa zaidi kote ulimwenguni. Kutoka 1976 hadi 1992, kazi ya ujenzi wa vifaa vya tawi vipya kabisa ilianzishwa katika nchi kama 60. Kuongezea hayo, miradi ya kupanua vifaa vilivyokuwako ilianzishwa katika nchi 30. Namna kazi ilivyofanywa (huku wenye kujitolea wakitoka makutaniko mengi—nyakati nyingine kutoka nchi nyinginezo) ilitumika kuimarisha vifungo vya upendo na umoja miongoni mwa watu wa Yehova.d

Ili kutimiza mahitaji ya Sosaiti yenye kupanuka ya kuchapa katika lugha nyingi, Mashahidi wazoefu katika uwanja wa kompyuta waliunda mfumo wenye kuendeshwa kwa kompyuta katika zile hatua za kabla ya kuchapa uitwao MEPS (Multilanguage Electronic Phototypesetting System). Mradi huo ulikamilishwa katika 1986. Tokeo likawa, kufikia 1992, gazeti Mnara wa Mlinzi lilikuwa likichapwa sawia katika lugha 66. Idadi iliyo kubwa zaidi ya Mashahidi wa Yehova waliweza kupokea chakula cha kiroho kilekile wakati uleule.e

Kadiri vifaa vya Watch Tower Society vilivyoendelea kupanuka, watu zaidi wa kujitolea walihitajiwa kwenye makao makuu katika Brooklyn na pia katika ofisi za tawi kote ulimwenguni. Kutoka 1976 hadi 1992, familia ya Betheli ya kimataifa iliongezeka mara tatu katika ukubwa, kutoka kama 4,000 hadi zaidi ya washiriki 12,900 wakitumikia kotekote duniani. Baraza Linaloongoza na Halmashauri ya Wafanyakazi yalo imetimiza mahitaji ya kibinafsi na ya kiroho ya jeshi hili kubwa la wafanyakazi wa kujitolea wa wakati wote.

Kutunza Makutaniko na Kazi ya Kueneza Evanjeli

Kadiri neno la Yehova lilivyoendelea kusonga mbele kasi, Baraza Linaloongoza na Halmashauri ya Utumishi yalo lilielekeza nishati zalo katika kujenga makutaniko ulimwenguni pote na kupanua kazi ya duniani pote ya kueneza evanjeli.

Je, kuna mambo zaidi ambayo yangeweza kufanywa ili kusaidia wale wapya wengi waliokuwa wakibatizwa kila mwaka? Mapema katika 1977, mipango ilifanywa ili kuimarisha kiroho Mashahidi wapya. Utumishi wa Ufalme Wetu ulieleza hivi: “Twaamini kwamba watu wote wanaoingia katika kweli wapaswa kufunzwa vitabu visivyopungua viwili. . . . Kwa hiyo funzo lapaswa kuendelea baada ya ubatizo mpaka kitabu cha pili kitakapomalizwa.” Kwa njia hiyo Mashahidi wapya waliobatizwa walipewa fursa kamilifu zaidi ya kupata maarifa na uelewevu na kuwa na uthamini wenye kukua wa yale yanayomaanishwa na ubatizo. Mpango huo mpya ulitia moyo pia ushirika zaidi wa karibu kati ya hao wapya na wale Mashahidi waliowasaidia katika funzo lao la Biblia nyumbani.

Ili kutunza hao waliokuwa wakimiminika kuingia katika tengenezo la Yehova, makutaniko mapya zaidi ya 29,000 yalifanyizwa ulimwenguni pote kati ya 1976 na 1992. (Mika 4:1) Waangalizi wa mzunguko na wa wilaya zaidi waliwekwa rasmi na Baraza Linaloongoza na kutumwa nje kusaidia. Hesabu ya waangalizi hao wasafirio iliongezeka kutoka 2,600 hivi katika 1976 hadi kama 3,900 katika 1992.

Idadi ya makutaniko ilipozidi kuongezeka, kulikuwa pia na uhitaji wenye kuongezeka wa majumba zaidi ya kukutania. Je, kulikuwa na njia ya haraka zaidi ya kujenga Majumba ya Ufalme? Katika miaka ya 1970, Mashahidi wa Yehova Marekani walipanga programu ya ujenzi ambapo wafanyakazi stadi wa ujenzi kutoka sehemu jirani za nchi walialikwa kusaidia Mashahidi wenyeji kujenga Jumba la Ufalme. Mamia wakiwa wanasaidia, jumba lingeweza kukamilishwa kwa haraka—mara nyingi katika siku mbili au tatu tu. Kufikia miaka ya 1980, Majumba ya Ufalme yaliyojengwa kwa haraka yalikuwa yakijengwa katika sehemu nyingine za dunia.

Mabadiliko ya kisiasa katika Ulaya Mashariki yaliathiri Mashahidi wa Yehova pia. Ulikuwa msisimko kama nini kwa ndugu zetu katika nchi kama vile Hungaria, na iliyoitwa wakati ule Muungano wa Sovieti, Poland, Rumania, na Ujerumani Mashariki (kama ilivyojulikana wakati ule), kupata kujua kwamba walikuwa wamepewa utambuzi wa kisheria, katika visa fulani baada ya miaka 40 ya marufuku! Uhuru ulioongezeka katika nchi hizo ulifanya iwe rahisi sasa kwao kufikia watu kama 380,000,000 wakiwa na habari njema! Mashahidi wa Yehova hawakupoteza wakati katika kutumia uhuru wao uliopatikana karibuni kushiriki katika utendaji wao wa kuhubiri peupe.

Nayo matokeo yalikuwa nini? Neno la Yehova limesonga mbele kasi! Kwa kielelezo, katika Aprili 1992 idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme waliokuwa wakiripoti katika Poland ilipita 106,915. Na matarajio kwa ukuzi wa wakati ujao yalikuwa yenye kutokeza: Mwezi huohuo hudhurio kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo lilikuwa 214,218. Vivyo hivyo, katika ile iliyojulikana wakati huo kuwa Muungano wa Sovieti, jumla ya 173,473 walihudhuria Ukumbusho katika 1992, ongezeko la asilimia 60 kupita mwaka uliotangulia.

Hata hivyo, katika nchi nyinginezo mnyanyaso wenye kuendelea na misiba ya kiasili imeleta vipingamizi. Kwa kielelezo, katika 1992 utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa ungali chini ya vizuizi vya kiserikali katika nchi kama 24. Halmashauri ya Mwenyekiti ya Baraza Linaloongoza hufanya iwezekanavyo kuandaa usaidizi na kuarifu udugu wa kimataifa juu ya njia ambazo katika hizo wanaweza kusaidia Mashahidi wenzao wanaotumikia chini ya hali ngumu. (Linganisha 1 Wakorintho 12:12-26.) Wala kampeni za mnyanyaso wala misiba ya kiasili haikuweza kukomesha kuhubiriwa kwa neno la Yehova!

“Kikundi cha Watu Kilicho Chake Mwenyewe Peke Yake”

Hivyo, katika miaka ya kutoka 1976 hadi 1992, neno la Yehova limesonga mbele kasi kwelikweli. Karibu tengenezo liwe mara mbili katika ukubwa, kufikia zaidi ya wahubiri wa Ufalme 4,470,000!

Watu wa Yehova wameendelea katika kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kwa bidii, sasa ikiwa ni katika lugha nyingi zaidi kuliko ilivyopata kuwa hapo awali. Wakitumia vichapo ambavyo vimeandaliwa, wameongeza sana kina cha ujuzi wao wa Biblia na kusaidia watu wenye kupendezwa wajifunze kweli za Biblia. Wao wamenufaishwa na programu za elimu ambazo zimeanzishwa kwa ajili ya wale walio na madaraka zaidi ndani ya tengenezo. Bila shaka Yehova amebariki kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme wake.

Kutoka miaka ya 1870 hadi leo hii, wanaume fulani wamechangia kwa njia yenye kutokeza maendeleo ya kazi ya Ufalme, wanaume kama vile Charles T. Russell, Joseph F. Rutherford, Nathan H. Knorr, na Frederick W. Franz, pamoja na wengine ambao wametumikia wakiwa washiriki wa Baraza Linaloongoza. Lakini Mashahidi wa Yehova hawakupata kwa vyovyote kuwa farakano lenye kutegemea nyutu za yeyote wa wanaume hao. Badala ya hivyo, wao wana kiongozi mmoja, “Kristo.” (Mt. 23:10) Yeye ndiye Kichwa cha hao Mashahidi wa Yehova waliopangwa kitengenezo, yeye ambaye ‘amepewa mamlaka yote’ ya kuelekeza kazi hii “siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:18-20, NW) Wao wameazimia kujitiisha chini ya ukichwa wa Kristo, kuendelea kulifuata sana Neno la Mungu, na kushirikiana na mwongozo wa roho takatifu, ili waweze kuendelea kusonga mbele katika ibada ya yule Mungu pekee wa kweli na kujithibitisha wenyewe kuwa “watu walio wake mwenyewe pekee, wenye bidii kwa kazi zilizo bora.”—Tito 2:14, NW.

Lakini ni yapi baadhi ya mafundisho ya msingi na viwango vya mwenendo vinavyowatofautisha Mashahidi wa Yehova na dini nyingine zote? Walikujaje kuitwa Mashahidi wa Yehova? Utendaji wao unaendeshwaje kifedha? Kwa nini wanadumisha hali ya kujitenga sana na makanisa mengine na ulimwengu kwa ujumla? Ni kwa nini wamekuwa shabaha ya mnyanyaso mkali sana katika sehemu nyingi sana za dunia? Maswali hayo na mengine mengi yatajibiwa katika sura ambazo zitafuata.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Sura ya 15, “Usitawi wa Muundo wa Tengenezo.”

b Kutoka 1980 hadi 1985, kulikuwa na ongezeko la asilimia 33 la idadi iliyokuwa ikishiriki katika kazi ya kuhubiri, na kutoka 1985 hadi 1992, kulikuwa na ongezeko zaidi la asilimia 47.9.

c Ona Sura ya 17, “Mikusanyiko—Uthibitisho wa Udugu Wetu.”

d Ona Sura ya 20, “Kujenga Pamoja Duniani Pote.”

e Ona Sura ya 26, “Kutokeza Fasihi za Biblia ili Zitumiwe Katika Huduma.”

[Blabu katika ukurasa wa 117]

Si farakano lenye kutegemea nyutu za wanaume wowote

[Sanduku/Grafu katika ukurasa wa 110]

Kutoka 1976 hadi 1992, kulikuwa na ongezeko la asilimia 42 katika hesabu ya lugha ambazo katika hizo “Mnara wa Mlinzi” lilitokezwa

[Grafu]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

111

78

1976 1992

[Sanduku katika ukurasa wa 111]

Historia ya Maisha ya F. W. Franz

Frederick William Franz alizaliwa katika Covington, Kentucky, Marekani, Septemba 12, 1893. Katika 1899 familia ilihamia Cincinnati, ambako Frederick alihitimu shule ya sekondari katika 1911. Kisha akaenda Chuo Kikuu cha Cincinnati, akachukua mtaala katika digrii ya sanaa panuzi. Alikuwa ameamua kwamba angekuwa mhubiri Mpresbiteri, hivyo alijitahidi kwa bidii kujifunza Kigiriki cha Biblia. Humo katika chuo kikuu Frederick alichaguliwa apokee elimu kwa udhamini wa Rhodes, ikimstahilisha kukubaliwa katika Chuo Kikuu cha Oxford katika Uingereza. Hata hivyo, kabla tangazo halijatolewa, Frederick aliacha kupendezwa kote na udhamini huo wa elimu naye akaomba kwamba jina lake lifutwe katika orodha ya washindaniao.

Wakati uliotangulia, ndugu yake Albert alikuwa amempelekea kijitabu alichokuwa amepata kutoka kwa International Bible Students. Baadaye Albert alimpa mabuku matatu ya kwanza ya “Studies in the Scriptures.” Frederick alifurahishwa na yale aliyokuwa akijifunza akaamua kukata uhusiano na Kanisa la Presbiteri naye akashirikiana na kutaniko la Wanafunzi wa Biblia. Novemba 30, 1913, akabatizwa. Katika Mei 1914 aliacha masomo ya chuo kikuu, akafanya mipango mara hiyo awe kolpota (painia).

Katika Juni 1920 akawa mshiriki wa familia ya Betheli katika Brooklyn. Kufuatia kifo cha N. H. Knorr, katika Juni 1977, Ndugu Franz alichaguliwa kwenye cheo cha msimamizi wa Sosaiti. Alitumikia kwa uaminifu akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza mpaka kifo chake, Desemba 22, 1992, akiwa na umri wa miaka 99.

[Grafu katika ukurasa wa 112]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Idadi za Mapainia Zenye Kupanuka

1992

600,000

400,000

1986

200,000

1981

1976

[Grafu katika ukurasa wa 113]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Familia ya Betheli Yenye Kukua Ulimwenguni Pote

1992

12,000

9,000

1986

6,000

1981

1976

3,000

[Grafu katika ukurasa wa 114]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Makuntaniko Yenye Kuongoza

80,000

1992

60,000

1986

1981

1976

40,000

20,000

[Grafu katika ukurasa wa 115]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Ongezeko la Wapiga-Mbiu wa Ufalme

1992

4,000,000

1986

3,000,000

1981

1976

2,000,000

1,000,000

[Picha katika ukurasa wa 109]

Kila ofisi ya tawi ya Sosaiti inasimamiwa na halmashauri ya ndugu, kama hii ambayo husimamia kazi katika Nigeria

[Picha katika ukurasa wa 116]

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova Januari 1992

Carey W. Barber

John E. Barr

W. Lloyd Barry

John C. Booth

Frederick W. Franz

George D. Gangas

Milton G. Henschel

Theodore Jaracz

Karl F. Klein

Albert D. Schroeder

Lyman A. Swingle

Daniel Sydlik

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki